Monday, December 15, 2014

SOKA WANAWAKE PWANI WAINGIA KAMBINI KUJIANDAA TAIFA CUP

Na John Gagarini, Kibaha
TIMU ya soka ya wanawake ya mkoa wa Pwani imeingia kambini kwenye shule ya sekondari ya Baden Powell iliyopo wilayani Bagamoyo kujiandaa na mchezo wake na timu ya mkoa wa Morogoro utakaochezwa Desemba 28 mwaka huu.
Mchezo huo ambao utapigwa kwenye uwanja wa Mabatini Mlandizi wilayani Kibaha wa kuwania kombe la Taifa kwa wanawake.
Akizungumza na gazeti hili mjini Kibaha, katibu wa chama cha soka la Wanawake (TWFA) mkoa wa Pwani Florence Ambonisye alisema kuwa maandalizi ya mchezo huo yanaendelea vizuri.
Ambonisye alisema kuwa timu hiyo inanolewa na mchezaji wa timu ya Taifa ya Wanawake Hilda Masanche iliingia kambini wiki iliyopita.
“Timu inatarajiwa kurejea Desemba 26 wilayani Kibaha ambapo itaingia kambini kwenye kambi ya Ruvu JKT Mlandizi siku mbili kabla ya mchezo huo,” alisema Ambonisye.
Aidha alisema kuwa timu hiyo itaongezewa wachezaji wanne mara itakaporudi Kibaha ili kuipa nguvu timu hiyo inayoundwa na wachezaji wengi vijana ambao ni wanafunzi shule za sekondari.
“Changamoto kubwa inayoikabili timu hiyo ni ukosefu wa vifaa kwani wachezaji wanatumia vifaa vyao binafsi walivyoendanavyo kambini,” alisema Ambonisye.
Alibainisha kuwa wanatarajia kushinda mchezo huo kwani timu yao imejiandaa vyema na mchezo huo licha ya kuwa wapinzani wao nao wako vizuri na wana uhakika wa kuingia 16 bora.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment