Tuesday, December 23, 2014

AMWUA MWANAE KWA KUMNYONGA ADAKWA NA HEROIN

Na John Gagarini, Kibaha
ESTER Endrew (23) mkulima mkazi wa Tabata Jijini Dar es Salaam anashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Pwani kwa tuhuma za kumwua mwanae Marko Elibariki (2) kwa kumnyonga kwa kutumia mikono.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha, kamanda wa polisi mkoani hapa Ulrich Matei alisema kuwa tukio hilo linahusishwa na wivu wa kimapenzi.
Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea saa 2 asubuhi eneo la Wipas mtaa wa mkoani B kata ya Tumbi wilayani Kibaha.
“Mtuhumiwa baada ya kutekeleza tukio hilo naye alijichoma tumboni kwa kisu hali iliyosababisha apate majeraha,” alisema Kamanda Matei.
Alisema kuwa mtuhumiwa huyo baada ya tukio baadhi ya majirani waligundua kutokana na kulalamika huku damu zikimtoka.
“Alijijeruhi tumboni kwa kisu akitaka kujiua lakini hata hivyo licha ya kujichoma hakufa na kuanza kupiga kelele ndipo majirani walipotoa taarifa polisi na mtuhumiwa kuja kuchukuliwa ambapo ilibainika kuwa alikuwa akimlaumu mumewe kuwa na mke mwingine,” alisema Kamanda Matei.
Aidha alisema mtuhumiwa amelazwa kwenye hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Tumbi kwa matibabu huku akiwa chini ya ulinzi.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SHAMBA Malela (20) mkazi wa Nianjema wilayani Bagamoyo mkoani Pwani anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kupatikana na kete 136 za dawa aina ya Heroin.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa na polisi waliokuwa doria.
Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea Desemba 22 mwaka huu majira ya saa 7:45 mchana huko Nianjema kata ya Magomeni wilaya ya Bagamoyo.
“Mtuhumiwa baada ya kutiliwa mashaka alikwenda kupekuliwa nyumbani kwake na kukutwa na dawa hizo ambazo zinadhaniwa kuwa ni za Heroin ambapo hata hivyo thamanai yake haikuweza kufahamika mara moja.
Alisema kuwa jeshi hilo linafanya doria kwenye maeneo mbalimbali ya wilaya za mkoa huo ili kukabiliana na matukio mbalimbali ya uhalifu.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment