Monday, December 8, 2014

CHADEMA WATISHIA KUANDAMANA

CHAMA Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani kimetoa siku mbili hadi Desemba 10 kwa Katibu Tawala wa Wilaya (DAS) Kibaha kuwarejesha wagombea wa nafasi mbalimbali kupitia chama hicho na endapo hatawarejesha watafanya maandamano kushinikiza warudishwe kuwania nafasi hizo.
Jumla ya wagombea 16 wa chama hicho wameondolewa kwenye kinyanganyiro cha kuwania nafasi za uongozi kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Deemba 14 mwaka huu, wakiwemo wenyeviti na wajumbe, kutokana na sababu mbalimbali za kukiuka sheria za uchaguzi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha mwenyekiti wa chama hicho Jimbo la Kibaha Mjini Mohamed Mnembwe alisema kuwa wametoa siku mbili Jumatatu na Jumanne ambapo Jumatano wataandamana kama endapo DAS hatawarejesha wagombea hao kwenye kinyanganyiro hicho.
Mnembwe alisema kuwa maandamano hayo watayafanya kuanzia kwenye ofisi za chama kwenda kwa DAS kudai haki za wagombea wao.
“Kuandamana ni haki ya kikatiba na si kuvunja sheria ni kutaka wagombea wetu warejeshwe kwani wameondolewa kwa uonevu na hawakutendewa haki kwani sababu zenyewe za kuwaengua si za halali,” alisema Mnembwe.
Alisema wagombea wao hawakupewa nafasi ya kupeleka ushahidi kwani wengi walienguliwa kwa madai kuwa si wakazi wa maeneo waliyoomba uongozi na kukosea kujaza fomu ikiwa ni pamoja na mtaa na mahali wanapoishi.
“Wengi waliwekewa pingamizi kuwa si wakazi wa maeneo hayo lakini wangethibitisha kwa kuwaita wahusika wakiwemo wenye nyumba kwani kusema kuwa balozi hamtambui si sawa kwani sisi pia tuna mabalozi wetu kikubwa wangepata ushahidi kama kweli si wakazi wa maeneo hayo, kwa upande wa ujazaji wa fomu ni mahali unapoishi na mtaa ndiyo walivyokosea na majina yao kuondolewa,” alisema Mnembwe.
Aidha alisema kuwa wao wanachotaka ni wagombea wao kurejeshwa kwenye nafasi za kuwania nafasi hizo na endapo DAS atafanya hivyo hawatafanya maandamano kwani wanataka uchaguzi huo ufanyike kwa amani na utulivu.
“Tunajua muda umeisha ila wakirejeshwa tunauhakika wa kushinda kwenye uchaguzi huo na tutatoa taarifa polisi ili kuomba ulinzi kwani maandamano yetu ni ya amani na hatuna nia ya kufanya vurugu kikubwa tunachotaka ni haki kutendeka,” alisema Mnembwe.
Mwenyekiti huyo wa CHADEMA Jimbo la Kibaha alitaja maeneo ambako wagombea wake wameondolewa kuwa ni Maili Moja 2, Kongowe 6, Visiga 3, Vikawe Shuleni 1,Miswe Chini 1 na Miwaleni 3.
Hivi karibuni DAS Sozi Ngate alipoulizwa kuhusiana na malalamiko hayo alisema kuwa kama wanaona wameonewa waende mahakamani kudai haki yao.
Mwisho.


















No comments:

Post a Comment