Sunday, December 7, 2014

OUT KUTUMIA MAMILIONI KUFUNDISHA WALIMU WA MASOMO YA SAYANSI



Na John Gagarini, Kibaha
CHUO Kikuu Huria Tanzania (OUT) kimepata fedha kiasi cha dola za Kimarekani milioni 50 kutoka benki ya dunia kwa ajili ya kuwajengea uwezo walimu wa masomo ya Sayansi na Hisabati hapa nchini.
Aidha fedha hizo pia zitatumika kwa ajili ya kujenga maabara mchanganyiko, mabweni na ofisi za walimu kwa lengo la kuboresha ufundishaji wa masomo chuoni hapo.
Hayo yalibainishwa na mgeni rasmi kwenye mahafali ya kwanza ya OUT kituo cha mkoa wa Pwani, Naibu Makamu Mkuu wa chuo hicho kitengo cha Teknolojia za Kujifunzia na Huduma za Mikoa Profesa Modest Varisanga.
Prof. Varisanga alisema kuwa kuna uhaba mkubwa wa walimu wa masomo hayo hivyo wameamua kuwekeza kwenye masomo hayo kwani ndiyo msingi wa kupata wataalamu mbalimbali.
“Chuo kinaendelea kujiimarisha kwenye maeneo mbalimbali pamoja na kuhakikisha tunazalisha wataalamu na msingi ni masomo ya Sayansi ndiyo sababu ya kuweka mkakati wa makusudi wa kuwawezesha na kuwajengea uwezo walimu hao wanaosoma kwenye chuo chetu,” alisema Prof Varisanga.
Alisema kuwa fedha hizo pia zitatumika kujenga maabara mabweni na ofisi za walimu ili kuboresha utoaji elimu kwa wanachuo ambao hupata masomo yao kwa elimu ya masafa.
Katika hatua nyingine alisema kuwa wameiomba serikali kuvibadili vyuo hivyo kutoka vituo hadi kuwa vyuo vya mikoa ambapo maombi hayo yamefikishwa kwenye baraza la Mawaziri na yamekubaliwa huku kwa sasa mchakato ukiwa unaendelea.
Kwa upande wake mkurugenzi wa kituo cha mkoa wa Pwani Abdala Alli alisema kuwa elimu ya masafa ambayo inatolewa na chuo hicho imekuwa suluhisho la elimu hapa nchini wakiwemo wanawake.
Alli alisema kuwa elimu ya masafa ndiyo elimu bora kwa sasa kwani inatolewa huku kwa wale watumishi wakiendelea kufanyakazi bila ya kuathiri utendaji kazi tofauti na elimu ya moja kwa moja ambayo humtaka mwanachuo kukaa darasani pamoja na kuwa kwenye bweni ambapo gharama zake ni kubwa.
Akisoma risala ya wahitimu Stella Mapunda alisema kuwa kituo chao kinakabiliwa na uhaba wa walimu pamoja na kumbi za mikutano na mihadhara kwa ajili ywa wanachuo kujadiliana na kujifunzia.
Mapunda alisema kwa sasa wanatumia majengo ya Shirika la Elimu Kibaha ambayo hayatoshelezi mahitaji ya wanachuo ambapo kumekuwa na ongezeko la udahili wa wanachuo wapya kila mwaka.
Jumla ya wahitimu 98 toka kituo cha mkoa wa Pwani walihitimu na kutunukiwa vyeti ngazi mbalimbali kwenye mahafali ya Kitaifa yaliyofanyika kwenye makao makuu ya chuo hicho yaliyopo Bungo wilayani Kibaha wiki iliyopita.
Mwisho.       

No comments:

Post a Comment