Thursday, November 16, 2017

UINGIZAJI MIFUGO TOKA NJE YA NCHI SERIKALI YASHAURIWA






Na John Gagarini, Kibaha

SERIKALI imetakiwa iendee kudhibiti uingizaji mifugo kutoka nje ya nchi ili kuepuka magonjwa ambayo yakiingia yataathiri soko la nje ambalo linapato kubwa.

Hayo yalisemwa wilayani Kibaha na Mwenyekiti wa Chama Cha Waganga Wasaidizi wa Mifugo Tanzania (TAVEPA) Salim Mselem wakati wa mkutano wa kamati kuu ya chama hicho na kusema kuwa lazima kuwe na udhibiti wa magonjwa.

Mselem alisema kuwa suala la udhibiti wa magonjwa ni mgumu sana lakini serikali kwa kushirirkrana na wataalamu wake wanapaswa kudhibiti uingizwaji wa mifugo hapa nchini.

“Hivi karibuni serikali ilivichoma moto vifaranga ambavyo viliingizwa kwenye mpaka wa Namanga ambapo wahusika hawakufuata taratibu za uingizaji mifugo na hizo ndiyo sheria hata kwenye mataifa mengine,” alisema Mselem.

Alisema kuwa ili kudhibiti magonjwa lazima mifugo inayoingia nchini lazima ikaguliwe ili kuangalia kama imepata chanjo na kama haijapata chanjo lazima uharibiwe.

“Magonjwa mengine ni ya hatari sana licha ya kuathiri soko la nje ambapo endapo itabainika mifugo yetu ina maganjwa haitaruhusiwa kwenye nchi za nje hata kwa afya za walaji pia ni hatari sana na hatutakubali nchi yetu kuwa sehemu ya kuuzwa vitu vibaya,” alisema Mselem.

Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa TAVEPA Ephrahim Masawe alisema kuwa kitengo cha ukaguzi wa uingizwaji mifugo kinapaswa kuwa makini ili kuepuka uingizwaji wa mifugo ambayo haijachanjwa.



Masawe alisema kuwa mifugo inayo ingizwa bila ya kuchanjwa ina hatari ya kuingiza magonjwa ambayo ni ya hatari kwa mifugo pamoja na afya za walaji.

Mwisho.




Friday, October 27, 2017

MIILI MIWILI YA WATU WALIOSOMBWA NA MAJI YAPATIKANA


Na John Gagarini, Kibaha

WATU wawili wamefariki dunia kufutaia mvua iliyonyesha juzi mkoani Pwani ambapo miili yao imeweza kugundulika baada ya maji kupungua kwenye mto Mpiji unaotenganisha mikoa ya Pwani na Dar es Salaam.

Akithibitisha kuokotwa kwa miili hiyo kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Pwani Blasius Chatanda alisema kuwa miili hiyo ilikutwa kando kando ya mto huo ambao ulikuwa umejaa kutokana na mvua kubwa zilizonyesha maeneo mbalimbali ya nchi.

Chatanda alisema kuwa miili hiyo ilokotwa maeneo tofauti ambapo mwili wa kwanza ulipatikana majira ya saa 2:30 eneo la Muheza kata ya Pangani alitambuliwa kwa jina la Simon Ramadhan mwenye umri kati ya miaka (25) na (30) uliokotwa eneo la mto Mpiji na marehemu alikufa alipokuwa akijaribu kuvuka.

“Mwili wa pili wa Issa Ally (28) ambaye ni mgambo uliokotwa eneo la Kiluvya na inadaiwa kuwa marehemu alisombwa na maji alipokuwa akijaribu kumwokoa mtoto aliyetaka kusombwa na maji na kukutwa kilometa nne toka sehemu aliyozama,” alisema Chatanda.

Alisema kuwa miili yote ya marehemu imehifadhiwa kwenye hospitali ya Rufaa ya Tumbi kwa ajili ya kusubiri ndugu kwa ajili ya mazishi.

“Nawaomba wananchi kuwa makini wakati wa kuvuka kwenye mito kuwa na subira ili maji yapungue waweze kuvuka na kuendelea na safari zao kwani wasidaharu maji kama ni madogo ambapo yanaweza kuwaletea madhara,” alisema Chatanda.

Mwisho.   
  


SABA WASOMBWA NA MAJI WANUSURIKA


Daraja linalounganisha mikoa ya Pwani na Dar es Salaam likiwa limejaa maji

 Baadhi ya wananchi wakifuatilia zoezi la uokoaji watu waliosombwa na maji ambao walipanda kwenye miti

 Moja ya kijana aliyenusurika Silas Moshi baada ya kusombwa na maji mara baada ya kuokolowa

 Dada ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja baada ya kuokolewa akiwa amepoteza fahamu akipakiwa kwenye gari la polisi kwa ajili ya huduma ya kwanza.



 Kijana Mohamed Kitindi aliyenusurika baada ya kusombwa na maji 

 Furaha Mwaipopo moja ya watu walionusurika baada ya kusombwa na maji na kupanda kwenye mti


 Moja ya watu walionusurika akihojiwa na polisi baada ya kunusurika 

 Kened Meshaki ambaye alishika nguzo ya bango huku mwili wake ukiwa ndani ya maji kwa zaidi ya masaa matatu akiwa ameshikwa mkono na polisi kwa ajili ya kwenda kupatiwa huduma ya kwanza


Na John Gagarini,Kibaha

WATU saba wamenusurika kifo baada ya kusombwa na maji walipokuwa wakijaribu kuvuka huku wakiwa wameshikana mikono ambapo walijinusuru kwa kupanda kwenye miti kabla ya kuokolewa na kikosi cha Zimamoto na Uokoaji kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi mkoa wa Pwani.

Aidha kati ya watu hao mmoja alikuwa akininginia kwa kujishika kwenye bomba la bango la matangazo huku mwili wake ukiwa ndani ya maji kwa masaa zaidi ya huku akiwa anaomba msaada wa kuokolewa bila mafanikio.

Watu walionusurika ni pamoja na Kened Meshaki, Mohamed Kitindi, Silas Moshi Henry Francis na mwanamke mmoj ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja ambao wote walikimbizwa hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Pwani.

Tukio hilo lilitokea jana eneo la Maili Moja wilayani Kibaha kwenye daraja linalotenganisha kati ya mkoa wa Dar es Salaam na mkoa wa Pwani na kusababisha daraja kujaa maji na kusababisha magari na watu kushindwa kuvuka upande wa pili.

Daraja hilo ambalo linapita kwenye mto Mpiji lilikuwa halipitiki na kusababisha watu na abiria kushindwa kuvuka upande wa pili kutoka Maili Moja wilayani Kibaha na upande mwingine Kiluvya wilaya ya Ubungo.

Kutokana na daraja hilo kushindwa kupitika abiria wa mabasi wameshindwa kuendelea na safari zao za kwenda mikoani na maeneo mengine yanayopita kwenye barabara ya Morogoro.

Akizungumza na gazeti hili kwenye eneo la tukio hilo ofisa habari na uhusiano wa Jeshi la uokoaji Harison Mkonyi alisema kuwa zoezi la ukoaji limefanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani wameweza kuwaokoa watu hao wakiwa salama.

Mkonyi alisema kuwa wamefanikiwa kuwaokoa watu hao kwa kushirikiana na wadau wengine ambao walijitosa kwenye maji hayo ambayo yalikuwa mengi na kulifunika kabisa daraja hilo na kusababisha kushindwa kupitika.

“Tunawashukuru wadau mbalimbali vikiwemo vikosi vya majeshi ya Polisi, Magereza, JWTZ na wananchi ambao walionyesha ushirikiano wa hali ya juu kuwanusuru watu hao akiwemo mwanamke mmoja,” alisema Mkonyi.

Mwisho.

Thursday, October 19, 2017

MBUNGE KIBAHA MJINI AKABIDHI VYEREHANI KWA WATU WENYE ULEMAVU


Na John Gagarini, Kibaha

MBUNGE wa Jimbo la Kibaha mkoani Pwani Silvestry Koka ametoa vyerehani vinnne kwa Shirikisho la Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) wilaya ya Kibaha kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao za ujasiriamali.

Akikabidhi vyerehani hivyo kwa uongozi wa shirikisho hilo Katibbu wa Mbunge huyo Method Mselewa alisema kuwa mbunge huyo katoa vyerehani hivyo kufuatia ombi lao.

Mselewa alisema kuwa watu wenye ulemavu nao wanapaswa kusaidiwa kama wanavyosaidiwa watu wa makundi mengine yanavyosaidiwa ili kujiendeleza kiuchumi.

“Kuwa na ulemavu siyo mwisho wa maisha kwani nguvu mnazo na mnauwezo kama watu wasiokuwa na ulemavu na tutaendelea kuwasaidia ili nanyi mjikwamue kwa kujiongezea kipato chenu na cha familia zenu,” alisema Mselewa.

Alisema kuwa kutokana na kuungana kwao kutasaidia kuwafikia kwa urahisi kuliko kila mtu angekuwa anaomba peke yake ingekuwa ngumu lakini kwa kuwa pamoja imekuwa rahisi.

“Hizi mashine mnapaswa kuzitunza kwani mbali ya kuwapatia ujuzi kia zitawapatia kipato ambacho kitaweza kuwafanya muwe na mapato kuliko kuomba jambo ambalo halifurahishi,” alisema Mselewa.

Kwa upande wake mwenyekiti wa SHIVYAWATA Ally Mlanga alisema kuwa wanshukuru msaada huo kwani kwao huo ni kama mtaji ambao watahakikisha wnaauendeleza.

Mlanga alisema kuwa wao hawataki fedha ila wanachotaka ni kupewa vitu ambavyo vitawasaidia kuliko fedha ambazo zinaweza kupotea kwa urahisi.

Naye ofisa Maendeleo wa Kata ya Kibaha Regina Lazaro alisema kuwa kupatiwa vyerehani hivyo vitawasaidia kujiongezea kipato kwani moja ya shughuli zake ni kuhamasisha ujasiriamali.

Lazaro alisema kuwa wamekuwa wakishirikiana na shirikisho hilo ikiwa ni njia mojawapo ya kuwasaidia kupata huduma mbalimbali zinazotolewa na serikali au wadau toka sekta binafsi.


Mwisho.

WAWILI WASHIKILIWA NA POLISI KWA KUKUTWA NA MAGUNIA SABA YA BHANGI



Na John Gagarini, Kibaha


WATU wawili wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Pwani kwa tuhuma za kukutwa na magunia saba ya dawa za kulevya aina ya bhangi yenye uzito wa kilogramu 7,500.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha kamanda wa Polisi mkoani humo Jonathan Shana alisema kuwa watuhumiwa hao waligundulika baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali.

Shana alisema kuwa tukio hilo lilitokea huko Kwa Mathias wilaya ya Kibaha baada ya askari waliokuwa doria kupata taarifa juu ya ajali ya gari.

“Watuhumiwa hao walikuwa kwenye gari namba T847DHT aina ya IST ambalo lilipata ajali kwenye eneo hilo na baada ya kufika walianza kuwaokoa na ndipo walipokuta na gunia saba za bhangi hiyo ikiwa kwenye hilo gari ikiwa imehifadhiwa kwenye magunia ya salfeti,” alisema Shana.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Kundaeli Mbowe (24) ambaye ni dereva wa gari hilo na mkazi wa Kiwalani Jijini Dar es Salaam na Ally Mtena (28) mfanyabiashara na makazi wa Gongolamboto.

Aidha alisema kuwa watuhumiwa hao wanashikiliwa ili kuweza kuchukuliwa hatua za kisheria na kujua bhangi hiyo waliitowa wapi na walikuwa wakiipeleka wapi.


Mwisho.

AMUUA MWENZAKE KWA KUMCHONA NA VISU


Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la Polisi Mkoani Pwani linamsaka Niniyay Silongoy kwa tuhuma za kumwua kwa kumchoma kisu Lemandra Kishwakwi (35) wote wa Kijiji cha Chamakweza wilaya ya Kipolisi Chalinze-Bagamoyo.
Kwa mujibu wa kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani Jonathan Shana alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikimbia kusikojulikana baada ya tukio hilo.

Shana alisema kuwa tukio hilo lilitokea Oktoba 18 mwaka huu majira ya saa 11:30 jioni Kijijini hapo baada ya kuchomwa kisu hicho kwenye kwapa la kushoto na mtuhumiwa.

 “Mbali ya kuchomwa kwapani pia mtuhumiwa alimchoma kisu shingoni na mkono wa kulia na mtuhumiwa baada ya kutekeleza azma yake alikimbia na anatafutwa na jeshi hilo kufuatia tukio hilo,” alisema Shana.

Alisema kuwa chanzo cha mauaji hayo ni ulevi ndipo mtuhumiwa alipofanya mauaji hayo ya kusikitisha ambayo haikujulikana kwanini mtuhumiwa alifikia hatua hiyo ya kumchoma mwenzake kisu.

Aidha alisema kuwa mwili wa marehemu ulikabidhiwa ndugu kwa ajili ya mazishi baada ya uchunguzi wa daktari huku juhudi za kumtafuta mtuhumiwa zikiendelea.

Mwisho.

Thursday, October 12, 2017

ULEGA AMWAGA CHECHE

NAIBU Waziri mpya  wa wizara ya  Mifugo na Uvuvi Abdalah  Ulega amesema hawezi kulifumbia macho hata kidogo suala la baadhi ya viongozi na watendaji ambao wamekuwa na tabia ya kufanya kazi kwa mazoea kwa kukaa tu ofisini bila ya kutimiza majukumu yao   ipasavyo na kuwaagiza kuchapa kazi kwa bidii bila ya kutegeana kwa kuvitembelea vikundi  vyote vya  uvuvi na ufuga   ili kuweza kusikiliza kero na kubaini  changamoto  zinazowakabili katika kutekeleza majukumu yao.

Ulega alitoa  kauli hiyo wakati alipofanya ziara yake ya kikazi ya siku moja kwa viongozi  mbali mbali wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, ambapo  amesema kuna baadhi ya watumishi wengine  wamekuwa ni wazembe na kusababisha kukwamisha juhudi za serikali katika kuleta  chachu ya maendeleo  hivyo ameahidi kulivalia njuga suala hilo kwa lengo la kuweza kuboresha sekta ya uvuvi na ufugaji.

Aidha Naibu Waziri huyo aliwataka maafisa uvuvi na mifugo  kuwa wazalendo na nchi yao na kuhakikisha wanazilinda  na kuzitunza rasilimali zilizopo  pamoja na   kuweka mipango  endelevu ya kutenga maeneo  maalumu kwa ajili  ya kufanyia kazi zao sambamba na kuviwezesha vikundi hivyo  katika mambo mbali mbali ikiwemo kujenga,malambo, majosho pamoja  na kuwapatia vitendea kazi.

Pia Ulega alisema kwamba  kwa sasa kipaumbele chake kikubwa ni kuhakikisha kwamba anavisaidia kwa hali na mali  kwa kuviwezesha vikundi mbali mbali  vya wafugaji na uvuvi  pamoja na kuweka mipango madhubuti ambayo itaweza kusaidia kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo katika sekta hiyo aliyopewa dhamana na Rais Dk. John Pombe Magufuli.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Filbeto Sanga akizungumzia kuhusiana na suala la ardhi alisema kuwa kumeibuka kikundi cha baadhi ya  madalali ambao ni matapeli wanachukua hela za watu na kuamua kuuza  maeneo ya mashamba  ambayo tayari yana hati miliki  bila ya kufuata taratibu zozote na  kupelekea  wananchi  wenyewe  kujikuta wanakosa maeneo  kwa ajili ya kuendeshea shughuli zao za kimaendeleo.

Katika hatua nyingine Mkugenzi mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Mkurunga Mshamu Munde akizungumza katika kikao cha dharura na waandishi wa habari ofisini kwake amekanusha uvumi wa taarifa zinazotolewa na  wananchi kuhusiana na shamba  linalomilikiwa na  mwekezaji wa kampuni ya Soap Allied Industry .

Mkurugenzi huyo alifafanua kuwa  eneo hilo  ambalo linalalamikiwa na wananchi hao lina ukumbwa wa hekari 1750 na kuongeza kuwa kwa sasa linamilikiwa kihalali na mwekezaji huo  tangu mwaka 1988, na kupiga marufuku  wananchi wanaovamia maeneo  ya watu kiholela bila ya kuzingatia taratibu.

“Mimi kwa kweli nina shangaa sana  huu uvumi unaotokwa kwa baadhi ya wananchi kuhusiana na eneo hili, ndugu zangu waandishi eneo hili linamilikiwa kihalali, hivyo mimi ninachowaomba watu wanaolalamika kufika ofisi za mkurugenzi ili niwape ufafanuzi zaidi na sio kuanza kusababisha migogoro ambayo haina faida  hata kidogo katika Wilaya yetu ya Mkuranga nah ii tabia kwa kweli mimi siwezi kuivumilia hata kigogo nitahakikisha kwamba maeneo yote yanatolewa kwa utaratibu unaotakiwa,”alisema Mkurugenzi huyo.

Pia Mkurugenzi huyo alisema  katikia kumuunga juhudi mkono Rais wa awamu ya tano Dk. John Pombe Magufuli katika kuwa na Tanzania yenye uchumi wa viwanda wameshatenga maeneo mbali mbali kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda ambavyo vitaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kukuza sekta ya viwanda na kuleta maendeleo kwa wananchi pamoja na upatikanaji wa fursa za ajira kwa vijana.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa halmashauri hiyo ya Mkuranga Juma Abed na Diwani wa kata ya Makamba  Hssan Dunda hapa wanazungumzia kuhusiana na sakata hilo la mgogoro wa shamba la mwekezaji huo na  malalamiko yanayotolewa na wananchi.

Walisema kuwa kwa sasa shamba hilo linamilikiwa kihalali na mwekezaji huyo kwani alishakabidhiwa na halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga baada ya kufuata taratibu zote zinazostahili hivyo wananchi wanatakiwa kuachana na tabia ya kuvamia maeneo mengine ambayo sio yao.

VITENDO vya uvamizi wa maeneo ya mashamba pamoja na viwanja  vinavyofanywa na baadhi ya viongozi wa  na wenyeviti wa vijiji kwa kushirikiana na madalali ambao ni matapeli kwa kuvamia maeneo ambayo sio yao na kuamua kuuza  kinyemela kinyume na taratibu katika Wilaya ya Mkuranga Mkoani Pwani vinachangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa migogoro kila kukicha.
      MWISHO