Tuesday, July 7, 2015

RAIS KIKWETE AJIANDIKISHA DAFTARI LA KUDUMU ATAKA WANANCHI WAJITOKEZE KWA WINGI

Na John Gagarini, Msoga
RAIS Dk Jakaya Kikwete amewataka Watanzania kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Mpiga Kura kwani ni haki ya  Kikatiba kwa kila mwananchi mwenye sifa.
Aliyasema hayo jana kwenye Kijiji cha Msoga kata ya Msoga wilaya Bagamoyo mkoani Pwani wakati alipojiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Mpiga kura na kusema kuwa amefurahi kutimiza haki yake.
Dk Kikwete alisema kuwa kwa kujiandikisha huko kutamsaidia mwananchi kuchagua kiongozi anayempenda na si baadaye kulalamika kuwa kiongozi fulani hafai.
“Mimi tayari nimeshapata kitambulisho cha kuweza kumchagua Rais wangu, Mbunge wangu na Diwani wangu kama mtu humtaki mnyime kura kwa kumpigia umtakaye,” alisema Dk Kikwete.
Aidha aliipongeza Tume ya Uchaguzi kwa kuendelea kupambana kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa licha ya kuwa na maneno mengi kazi yenu ni nzuri na tunaithamini.
“Chapeni kazi changamoto ni kawaida na ni sehemu ya maisha na mtakaposhindwa tuambieni kwani kazi yenu ni nzuri na tunaithamini sana chapeni kazi,” alisema Dk Kikwete.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi nchini Damian Lubuva alisema kuwa licha ya changamoto zilizojitokeza lakini zoezi linakwenda vizuri na matarajio ni makubwa ya kulifanikisha.
Lubuva alisema kuwa hadi sasa mikoa 13 tayari imeshakamilisha zoezi hilo ambapo changamoto inatokana na mfumo mpya wa BVR na tayari watu zaidi ya m 11 wameshaandikishwa.
“Malengo ni kuandikisha watu m 21 hadi 23 mara litakapokamilika mwishoni mwa Julai au Agosti mwanzoni kama mambo yatakwenda vizuri,” alisema Lubuva.
Mkoa wa Pwani una jumla ya vituo 1,752 na mashine za BVR 932 ambapo kata ya Msoga kuna jumla ya vituo 17 zoezi hilo kwa mkoa wa Pwani lilianza jana na litamalizika Julai 20.   
Mwisho.


Friday, June 26, 2015

MAJAMBAZI YAUA ASKARI YATOKOMEA NA FEDHA

Na John Gagarini, Kibaha
WATU zaidi ya watano wanaosadikiwa kuwa ni majambazi wamevamia benki ya NMB tawi la Mkuranga,mkoani Pwani na kufanikiwa kuua askari mmoja na kujeruhi watu watatu kisha kupora fedha kiasi ambacho hakijafahamika.
Majambazi hayo walifanikiwa kumuua askari huyo aliyekuwa kavaa kirai kwa kumpiga risasi kichwani baada ya mapambano ya kurushiana risasi.
Askari aliyefariki dunia alitajwa kwa jina la PC Alfred ambaye hakuwa kazini bali alikwenda katika benki hiyo kufuata huduma na kati ya waliojeruhiwa ni pamoja na PC James.
Tukio hilo limetokea mapema leo, baada ya watu hao kufika katika benki hiyo na kuanza kuwashambulia askari wanaolinda katika benki hiyo.
Kwa mujibu wa mashuhuda walielezea kuwa baadaye watu hao walihamia katika gari lililokuwa linapeleka fedha benki na kuchukua fedha zote kisha kuchukua silaha mbili aina ya SMG na kutokomea kusikojulikana.
Aidha inasadikiwa watu hao walifika katika benki hiyo wakiwa na pikipiki tatu aina ya boksa wakiwa wamebebana mshikaki na walipofanikisha tukio hilo waliondoka.
"Majambazi hayo yalipofika eneo la tukio walianza kufanya mashambulizi kwa askari ambapo walifanikiwa kuwadhibiti askari waliokuwepo kwa kuanza kuwashambulia na kupiga risasi hewani"alisema mmoja wa mashuhuda hao.
Alielezea kuwa  askari waliokuwepo eneo la tukio walikimbia na kumuacha mmoja kupambana nao ambapo alizidiwa.
Aidha alieleza kuwa dakika chache baada ya mashambulizi hayo liliingia gari lililobeba fedha ambapo walivamia gari hilo bila kuwepo kwa mtu yeyote na kufanikiwa kubeba  fedha zote.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani,ACP Jafari Ibrahim alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuahidi kutoa taarifa kamili mara atakapopata taarifa hizo.

Mwisho

Tuesday, June 9, 2015

REJESHENI HESHIMA YA RIADHA BALOZI ALI IDD

Na John Gagarini, Kibaha
WANARIADHA wa Tanzania wametakiwa kujiandaa kimataifa zaidi ili kuiletea heshima nchi kama ilivyokuwa miaka ya 70 ambapo Tanzania ilikuwa ikitamba kimataifa na kuipeperusha vema bendera ya Taifa.
Hayo yalisemwa juzi mjini Kibaha na makamu wa pili wa Rais Zanzibar Balozi Seif Ali Idd wakati akifunga mashindano ya riadha ya Taifa ya 54 kwenye viwanja vya Filbert Bayi na kusema kuwa kwa sasa mchezo huo umedorora.
Balozi Idd alisema kuwa wanariadha hao wanapaswa kuweka malengo ya kushindana kimataifa na si kuridhika na kukimbia hapahapa nchini kwani nafasi ya kufanya vizuri kimatiafa bado ipo kinachotakiwa ni kuwekwa mipango mizuri.
“Miaka ya nyuma kulikuwa na wakimbiaji wengi wazuri ambao walikuwa wakikimbia kimataifa na kuiletea sifa nchi yetu na sasa tunapaswa kulenga kimataifa zaidi kwani inasiadia kuitangaza nchi yetu kama ilivyo kwa wenzetu ambao ni majirani zetu Kenya ambao kwa sasa wanatamba kwenye mchezo huo,” alisema Balozi Idd.
Alisema miaka ile kulikuwa na akina Filbert Bayi, Suleiman Nyambui, Juma Ikangaa na wengi waliweka historia ya nchi duniani kwa kufanya vyema kwenye mashindano ya kimataifa hata wakati huu bado nafasi ipo ya kufanya hivyo.
“ Fanyieni kazi Kisayansi mapungufu yaliyojitokeza hadi kusababisha tushindwe kufanya vema katika mashindano ya kimataifa pia wekeni malengo ya muda mfupi na muda mrefu hasa kwa mashindano ya Kimataifa yajayo ili kuweza kurejesha heshima ya mchezo huo kwa Taifa letu,” alisema Idd.
Aidha alisema kuwa serikali zote zimekuwa zikifanya kazi kubwa ya kuwekeza kwenye michezo ambapo hali hiyo imefanya Muungano uendelee kudumu na kujenga mshikamano baina ya Watanzania na zitaendelea kusaidia sekta hiyo ya michezo.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania RT Antony Mtaka alisema kuwa moja ya changamoto inayowakabilini na kukosa mdhamini wa moja kwa moja hali ambayo inasababisha maandalizi ya mashindano kuwa mabaya.
Mtaka ameiomba serikali kuwasaidia wanariadha wa zamani wanaoanzisha shule za Michezo ili waweze kufungua shule nyingi kwa lengo la kuinua michezo hapa nchini kwnai uwekezaji unapaswa kuanzia ngazi ya chini.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
NAIBU Waziri wa Habari Vijana Utamaduni na Michezo Juma Nkamia amewataka viongozi wa timu mbalimbali kuhakikisha wanapeleka wanamichezo kwenye mashindano badala ya kupeleka viongozi jambo ambalo linafanya timu hizo zisiweze kufanya vizuri.
Waziri Nkamia aliyasema hayo juzi mjini Kibaha wakati wa kufunga michezo ya Taifa ya Riadha ya 54 kwenye viwanja vya shule ya Filbert Bayi na kusema kuwa baadhi ya timu zilipeleka viongozi badala ya wachezaji.
Alisema kuwa ni vema wachezaji wakapewa nafasi zaidi kwani wao ndiyo wanaokwenda kushindana na viongozi wao wanasimamia masuala ya kiutawala lakini fursa kubwa iwe kwa wachezaji ili kutimiza malengo yao.
“Hapa kwenye mashindano hayo tumesikia kuna timu wamekuja viongozi ni vema nafasi hiyo wakapewa wachezaji ili washindane na si kuleta viongozi ambao hawatashiriki kwa hiyo ushiriki wa timu hiyo haupo,” alisema Waziri Nkamia.
Aidha alisema kuwa mchezo huo unapaswa kuwekewa mikakati ya kuboreshwa ili uweze kurudia kwenye hadhi yake ya zamani ambapo Tanzania ilikuwa ikitamba vilivyo na kuiletea sifa kubwa nchi lakini kwa sasa hali ni tofauti.
Aliwataka wanariadha kuongeza jitihada ili waweze kufikia viwango vitakavyowafanya waweze kushiriki mashindano ya Kimataifa na kuleta medali kama walivyofanya wanariadha wakongwe ambao rekodi za kimataifa hadi leo zimedumu.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI imeombwa kupunguza ushuru wa vifaa vya michezo ili kusaidia malengo ya uanzishwaji wa shule na vituo vya michezo kuinua vipaji vya vijana wadogo ili waje kuwa wachezaji watakaotegemewa na Taifa.
Akizungumza wakati wa ufungaji wa michezo ya Riadha ya Taifa mjini Kibaha mkurugenzi wa shule za Filbert Bayi Ana Bayi alisema kuwa ushuru wa vifaa hivyo vya michezo ni mkubwa sana hivyo azma ya kukuza vipaji kushindwa kufikiwa.
Bayi alisema kuwa uwekezaji kwenye michezo hususani kwa vijana wadogo wakiwemo wanafunzi ndiyo chimbuko la wanamichezo tofauti na sasa ambapo wachezaji wengi hawajaanzia kwenye shule au vituo vya michezo.
“Wachezaji wote wanaotamba sehemu mbalimbali duniani walianzia kwneye shule au vituo vya michezo hivyo ili na sisi tuweze kufanikiwa lazima tuwekeze kwa watoto ili wakue kwenye michezo na si kuanza kuwafundisha ukubwani lakini tunakwazwa na ushuru mkubwa wa vifaa vya michezo ,” alisema Bayi.
Alisema kuwa wao kama wanamichezo waliamua kuwekeza kwa kujenga viwanja vya kisasa vya michezo yote nab ado wanendelea na ujenzi lakini vifaa vinavyotumiwa na wanamichezo vina ushuru mkubwa ambapo hata baadhi ya wanamichezo wamekuwa wakishiriki peku peku.
“Tunapokwenda kwenye michezo mbalimbali hasa kwenye nchi zilizojuu kimichezo tunaumia sana kwani wenzetu wamewekeza kwa vijana wadogo na mafanikio ya uwekezaji huo yanaonekana kwani wanafanya vizuri sana,” alisema Bayi.
Aidha alisema kuwa fedha wanazotumia kwa ajili ya ujenzi wa viwanja ni mikopo hivyo serikali iangalie namna ya kupunguza ushuru ili waweze kuweka vifaa ambavyo ni vya kisasa ambavyo vitawafanya wachezaji kutoshangaa wanapokwenda kwenye michuano ya kimataifa kwani wataona vifaa hivyo na mazingira ya viwanja ni ya kawaida.
Akijibu suala hilo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Seif Ali Idd alisema kuwa ataongea na Waziri wa Fedha ili kuangalia namna ya kuwawasidia wanamichezo ili kuwapunguzua gharama kubwa za ushuru wa vifaa hivyo vya michezo.
Makamu wa Rais alimpongeza Filbert Bayi kwa kuanzisha shule ya michezo ambayo itajibu tatizo kubw ala kuandaa vijana kwa ajili ya kuwa wachezaji wazuri watakaorudhisha hadhi ya michezo hapa nchini ikiwemo riadha.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
IMEELEZWA kuwa uwekezaji kwenye sekta ya michezo kwa michezo ya mchezaji mmoja mmoja inaweza kuinua sekta hiyo kwa haraka tofauti na michezo inayoshirikisha wachezaji wengi.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na msiadizi wa mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka, Method Mselewa wakati wa tamasha la mchezo wa Karate lililoandaliwa na klabu ya KAMBOJI ya wilayani Kibaha na kushirikisha wachezaji toka mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro na Pwani.
Mselewa alisema kuwa wachezaji wanaocheza michezo ya mchezaji mmoja wana uwezo wa kufanya vyema endapo wataandaliwa vizuri kushiriki michezo hiyo kama ilivyo kwa michezo kama ya ngumi, kareti, riadha, tenisi, michezo ya mitupo na michezo mingine ambayo inashirikisha mchezaji mmoja.
“Hatusemi kuwa michezo inayoshirikisha wachezaji wengi haina nafasi ya kufanya vizuri bali kuna haja ya michezo ya mtu mmoja mmoja nayo kupewa nafasi kwani inaonyesha kuwa ndiyo iliyowahi kufanya vema kimataifa,” alisema Mselewa.
Alisema kuwa mfano wa michezo ya ngumi na riadha kwa miaka ya nyuma ilifanya Tanzania itambuliwe duniani ambapo wachezaji wake walifanikiwa kutwaa medali mbalimbali kwenye michuano kama ile ya Jumuiya ya Madola, Olimpiki na michezo ya kimataifa.
“Tunapaswa kueiendeleza michezo yote lakini pia kuwekeza kwenye michezo kama hii itasaidia nchi kuwa kwenye ramani ya michezo ambapo tumeona uwekezaji kwenye michezo ya watu wengi licha ya kusaidiwa lakini bado mafanikio hayajaonekana,” alisema Mselewa.
Kwa upande wake mwenyekiti wa klabu hiyo ya Kamboji Kachingwe Kaslenge alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutokuwa na ofisi pamoja na sehemu yao binafsi ya kufanyia mazoezi ambapo kwa sasa wanaomba.
Kaselenge alisema kuwa changamoto nyingine ni ukosefu wa vifaa kutoakana na vifaa kuuzwa kwa gharama kubwa hivyo wachezaji wengi kushindwa kuvinunua kutokana na bei kuwa juu ambapo wakati mwingine mchezjai hujikuta na kifaa kimoja kwa ajili ya mazoezi na mashindano.
Mwisho.

HABARI MPYA

Na John Gagarini, Kibaha
ZOEZI la kuandikisha wananchi kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura mkoani Pwani linatarajiwa kuanza Juni 14 mwaka huu kwa watu wenye sifa wakiwemo wale waliokuwa na umri chini ya miaka 18 wakati zoezi hilo lilipofanyika miaka ya nyuma.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha mchambuzi wa mfumo wa kompyuta wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Mariam Rajab alisema kuwa zoezi hilo litadumu kwa kipindi cha siku 28 kwenye maeneo yote ya mkoa huo.
Rajab alisema kuwa zoezi hilo ni kwa watu wote wenye sifa wakiwemo wale wenye umri kuanzia miaka 18 na kuendelea ambao ni raia wa kuzaliwa au kuandikishwa kisheria.
“Zoezi hili ni muhimu kwa wananchi hivyo wanapaswa kujitokeza kwa wingi ili waweze kujiandikisha kwa lengo la kupata fursa ya kupiga kura kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka huu,” alisema Rajab.
Alisema kuwa zoezi hili litawahusisha hata wale ambao walijiandikisha kwenye daftari hilo kabla ya uchaguzi mkuu uliopita kwani vitambulisho hivyo havitatumika tena ambapo uchaguzi huu utatumia vitambulisho vipya.
“Tunawashauri wananchi wajitokeze kwa wingi kwenye uandikishaji huu kwani endapo hawataandikishwa watakosa fursa ya kupiga kura ambayo ni haki yao ya msingi,” alisema Rajab.
Aidha alisema Tume imeshaleta vifaa kwa ajili ya zoezi hilo na hakutakuwa na tatizo la vifaa kwa ajili ya kujiandikisha kama ilivyotokea kwa baadhi ya mikoa kuwa na upungufu wa vifaa.
“Changamoto mbalimbali ambazo tulizipata wakati wa zoezi hili kwenye ile mikoa ya awali tayari zimefanyiwa kazi hivyo wananchi wasiwe na wasiwasi juu ya vifaa kikubwa ni kushiriki kwa wingi,” alisema Rajab.
Alisema kuwa tayari maofisa wa uchaguzi kwenye mkoa huo wameshapatiwa mafunzo kwa ajili ya kutumia mashine zitakazotumika kuandikishia BVR na kinachosubiriwa ni muda kufika.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kisarawe
SHIRIKA la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) limeanzisha mitandao kwa ajili ya ulinzi wa misitu hiyo ili kukabiliana na uharibifu unaofanywa na watu wanaotumia mazao ya misitu kwa ajili ya kujipatia kipato.
Hayo yalisemwa wilayani Kisarawe na mratibu wa shirika hilo Yahaya Mtonda wakati wa sherehe za kuwapa zawadi washindi wa Insha juu ya umuhimu wa misitu zilizoambatana na siku ya mazingira duniani.
Mtonda alisema kuwa TFCG imehamasisha kuanzishwa kwa mitandao ipatayo 93 ijulikanayo kwa kifupi (MJUMITA).
“Mbali ya mitandao hii kulinda misitu hiyo pia tumewawezesha wananchi wanaozunguka misitu hiyo kuanzisha vyama vya kuweka na kukopa (Vicoba) ili waweze kukopeshana ili kufanya shughuli nyingine za kujiongezea kipato badala ya kutegemea misitu kama chanzo chao cha mapato,” alisema Mtonda.
Mtonda alisema kuwa pia wamewapatia mafunzo walimu wanaofundisha masomo yahusuyo utunzaji wa mazingira ili kuwa na uelewa juu ya masuala ya kuhifadhi mazingira ili wawafundishe wanafunzi wa shule za msingi.
“Tunatoa mafunzo kwa walimu wa shule za msingi ili kuwarithisha wanafunzi tangu wakiwa wadogo waweze kuona umuhimu wa tangu wakiwa wadogo misitu ili waweze kuitunza na kuhamasisha jamii kupanda miti,” alisema Mtonda.
Aidha alisema kuwa lengo la kuwafundisha ni kuwafanya wawe mabalozi wazuri wa kulinda misitu na kutunza mazingira ambayo yamekuwa yakiharibiwa kwa kasi na waharibifu wa mazingira.
Juu ya Insha alisema ilikuwa ni kuataka kujua uelewa wa wanafunzi kutoka shule nane kutoka wilaya za Ilala, Temeke, Kinondoni, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini na Kisarawe ambapo Januari Eric wa Shule Msingi Mtamba alijinyakulia 100,000, Catherine Mbelwa wa Kongowe 70,000 na Prisca Joseph wa Soga 50,000.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kisarawe
WAKALA wa Misitu Tanzania (TFS) wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani unatarajia kubadilisha sehemu ya msitu wa Pugu kuwa sehemu ya Utalii na kuwa hifadhi asilia kutokana na vivutio vilivyopo kwenye msitu huo ambavyo baadhi havipo sehemu yoyote duniani.
Hayo yalisemwa na meneja wa (TFS) wilaya ya Kisarawe Andrew Mwenuo alipozungumza na mwandishi wa habari hizi wilayani humo.
Mwenuo alisema kuwa kwa sasa tayari wameshaweka baadhi ya maeneo kwa ajili ya watu kupumzika na njia za kutembea kwa miguu na baiskeli ili watu waweze kuutembelea msitu huo na kuona mandhari na vivutio vilivyopo.
“Kuna wanyama wadogo wadogo akiwemo aina ya nyani mwenye aibu kwani amuonapo mtu huficha uso wake kwa aibu na hawapatikani sehemu nyingine yoyote duniani zaidi ya hapa,” alisema Mwenuo.
Alisema kuwa mbali ya nyani huyo pia kuna aina ya tembo mdogo ambao sehemu nyingine hapatikani zaidi ya kwenye msitu huu pia kuna wanyama wengine, ndege, wadudu kama vipepeo na wengine ambao ni vivutio.
“Hii itakuwa fursa kwa Watanzania na raia wan je ambao wanataka kupumzika na kuona mazingira mazuri ya msitu wakiwemo wasafiri wanaotumia njia ya ndege wanaweza kuja hapa na kupumzika wakisubiri muda wa kuondoka kwa njia ya anga kwani ni jirani na uwanja wa ndege,” alisema Mwenuo.
Aidha alisema kuwa watu wataruhusiwa kuweka mahema na kupumzika na kujipumzisha huku wakila vyakula pamoja na vinywaji ambapo kiingilio kitakuwa kwa wageni ni dola 10 huku kwa Watanzania ni 1,500 huku wanafunzi wakitozwa 500.
Mwisho.
  




Sunday, May 31, 2015

PWANI WAANZISHA WILAYA MPYA YA KIBITI NA MAJIMBO MAPYA


Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani umepitisha mapendekezo ya kugawanywa kwa Wilaya ya Rufiji kuwa wilaya mbili za Rufiji na Kibiti na kuligawa Jimbo la Chalinze kuwa majimbo mawili ya Chalinze na Saadani.

Mbali ya kupitisha wilaya mpya ya Kibiti na Jimbo la Saadani umepitisha mapendekezo yaliyowasilishwa na Halmashauri ya Kibaha Mji ya kugawa Tarafa ya Kibaha na kuwa na  Tarafa mpya ya Kongowe.

Maamuzi hayo yalifanywa mjini Kibaha kwenye Kiko cha Usahauri cha Mkoa (RCC) kilichokaa mwishoni mwa wiki chini ya kaimu mkuu wa mkoa wa Pwani ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba
Kihemba alisema kuwa mapendekezo hayo yamefuata sheria na taratibu zinazostahili kwa upande wa wilaya na Jimbo ni pamoja na Jimbo kuwa ndani ya wilaya moja ama Halmashauri moja, idadi kubwa ya watu ,upatikanaji wa mawasiliano ikiwemo mitandao ya simu, barabara, huduma za kiuchumi na jiografia ya eneo husika.
Naye Mkuu wa wilaya ya Rufiji Nurdin Babu alisema kuwa anpongeza kikao hicho kuweza kupitisha uanzishwaji wa wilaya mpya ya Kibiti kwani itawasogezea huduma mbalimbali za kijamii karibu.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Majid Mwanga alisema kugawanywa kwa Jimbo la Chalinze ni mchakato wa wilaya ya Bagamoyo kugawanywa katika wilaya mbili

Mwanga alisema kuwa endapo utaratibu huo utakuwa umekamilika wilaya hiyo itakuwa na majimbo matatu ya uchaguzi ambayo ni Bagamoyo,Saadani na Chalinze kutokana na ukubwa wa wilaya hiyo.

Jimbo la Bagamoyo litakuwa na kata za Dunda,Magomeni,Nia Njema ,Kisutu, Makurunge, Kiromo,Zinga ,Kerege, Mapinga, Yombo na Fukayosi ambayo itatolewa kutoka jimbo la Chalinze.

Huku Jimbo la Chalinze likiwa na kata za Vigwaza ambayo imeondolewa katika Jimbo la Bagamoyo, Kiwangwa, Msata, Lugoba,Talawanda, Ubena, Pera, Bwiringu na Msoga na Jimbo jipya la Saadani makao makuu yatakuwa Miono na Jimbo hilo likiwa na kata za Kibindu, Mbwewe, Kimange, Mandela, Miono na Mkange.


Mwisho

Friday, May 29, 2015

UMISSETA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
WACHEZAJI wa michezo ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA) mkoa wa Pwani wametakiwa kushindana na si kushiriki kwenye michuano hiyo ngazi ya Kanda ili mkoa utoe wachezaji wengi.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na ofisa elimu wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani Benjamini Majoya wakati wa ufungaji wa michezo hiyo ngazi ya mkoa kwenye viwanja vya Filbert Bayi na kusema kuwa ushindani ndiyo unaotakiwa na si ushiriki.
Majoya alisema kuwa mashindano ya Kanda ambayo yatafanyika mkoani Morogoro mwezi ujao ili kupata timu itakayounda kanda ya Mashariki inayoundwa na mikoa ya Pwani na Morogoro kwa ajili ya timu itakayokwenda mkoani Mwanza kwenye mashindano ya Taifa.
“Michezo ni sehemu ya kuendeleza taaluma hivyo lazima mcheze ip[asavyo na si muende kwa ajili ya kushiriki tu lazima mpambane na kuonyesha vipaji vyenu ili muwakilishe vyema mkoa na kutoa wachezaji wengi kuwakilisha kanda ya Mashariki,” alisema Majoya.
Aidha aliwataka wanamichezo hao kuonyesha nidhamu wakati wanacheza michezo kwani nidhamu ndiyo mafanikio ya michezo kwani bila ya kuwa na nidhamu itakuwa vigumu kufanikiwa.
Kwa upande wake ofisa michezo wa mkoa wa Pwani Grace Bureta alisema kuwa michezo hiyo ilihusisha wilaya sita za mkoa huo ambapo jumla ya wachezaji 136 wa michezo mbalimbali walichaguliwa kwa ajili ya kuunda timu ya mkoa.
Bureta alisema kuwa timu hiyo itaingia kambini kwa muda wa siku nne hadi Mei 31 ambapo Juni Mosi wataelekea mkoani Morogoro kwa ajili ya mashindano ya kanda ya Mashariki.
Alisema kuwa wachezaji waliochaguliwa ni wazuri na anategemea watafanya vizuri kwa kutoa wachezaji wengi kuunda timu ya Kanda na kufanikiwa kutetea ubingwa wa jumla wa mashindano hayo kitaifa mjini Mwanza.

Mwisho.Na John Gagarini, Kibaha
MKOA wa Pwani umechagua jumla ya wanamichezo 136 wa michezo mbalimbali kwa ajili ya kuunda timu ya mkoa ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA) kwa ajili ya kushiriki michezo ya Kanda ya Mashariki.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Ofisa Michezo wa mkoa wa Pwani Grace Bureta wakati wa ufungaji wa michezo hiyo ngazi ya wilaya iliyofanyika kwenye viwanja vya shule ya Filbert Bayi.
Bureta alisema kuwa mashindano hayo ambayo yaliwahusisha wachezaji toka kwenye shule za sekondari za wilaya sita za mkoa huo ambazo ni Mafia, Rufiji, Kibaha Mjini na Vijijini, Kisarawe, Mkuranga na Bagamoyo walifanikiwa kupata wachezaji ambao walifanya vizuri.
“Mara baada ya michezo kukamilika na kuchaguliwa wachezaji hao timu itaingia kambini kwa muda wa siku nne hadi Mei 31 ambapo Juni Mosi wataelekea mkoani Morogoro kwa ajili ya mashindano ya kanda ya Mashariki,” alisema Bureta.
Alisema kuwa wachezaji waliochaguliwa ni wazuri na anategemea watafanya vizuri kwa kutoa wachezaji wengi kuunda timu ya Kanda na kufanikiwa kutetea ubingwa wa jumla wa mashindano hayo kitaifa mjini Mwanza.
Benjamini Majoya aliwataka wanamichezo wa mkoa huo kushindana na si kushiriki kwenye michuano hiyo ngazi ya Kanda ili mkoa utoe wachezaji wengi watakaounda kanada hiyo.
Majoya alisema kuwa mashindano ya Kanda ambayo yatafanyika mkoani Morogoro mwezi ujao ili kupata timu itakayounda kanda ya Mashariki inayoundwa na mikoa ya Pwani na Morogoro kwa ajili ya timu itakayokwenda mkoani Mwanza kwenye mashindano ya Taifa.
“Michezo ni sehemu ya kuendeleza taaluma hivyo lazima mcheze ip[asavyo na si muende kwa ajili ya kushiriki tu lazima mpambane na kuonyesha vipaji vyenu ili muwakilishe vyema mkoa na kutoa wachezaji wengi kuwakilisha kanda ya Mashariki,” alisema Majoya.
Aidha aliwataka wanamichezo hao kuonyesha nidhamu wakati wanacheza michezo kwani nidhamu ndiyo mafanikio ya michezo kwani bila ya kuwa na nidhamu itakuwa vigumu kufanikiwa, michezo iliyoshindaniwa ni pamoja na soka, pete, wavu, kikapu, riadha na bao.
Mwisho.

 Na John Gagarini, Kibaha
MKOA wa Pwani umechagua jumla ya wanamichezo 136 wa michezo mbalimbali kwa ajili ya kuunda timu ya mkoa ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA) kwa ajili ya kushiriki michezo ya Kanda ya Mashariki.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Ofisa Michezo wa mkoa wa Pwani Grace Bureta wakati wa ufungaji wa michezo hiyo ngazi ya wilaya iliyofanyika kwenye viwanja vya shule ya Filbert Bayi.
Bureta alisema kuwa mashindano hayo ambayo yaliwahusisha wachezaji toka kwenye shule za sekondari za wilaya sita za mkoa huo ambazo ni Mafia, Rufiji, Kibaha Mjini na Vijijini, Kisarawe, Mkuranga na Bagamoyo walifanikiwa kupata wachezaji ambao walifanya vizuri.
“Mara baada ya michezo kukamilika na kuchaguliwa wachezaji hao timu itaingia kambini kwa muda wa siku nne hadi Mei 31 ambapo Juni Mosi wataelekea mkoani Morogoro kwa ajili ya mashindano ya kanda ya Mashariki,” alisema Bureta.
Alisema kuwa wachezaji waliochaguliwa ni wazuri na anategemea watafanya vizuri kwa kutoa wachezaji wengi kuunda timu ya Kanda na kufanikiwa kutetea ubingwa wa jumla wa mashindano hayo kitaifa mjini Mwanza.
Benjamini Majoya aliwataka wanamichezo wa mkoa huo kushindana na si kushiriki kwenye michuano hiyo ngazi ya Kanda ili mkoa utoe wachezaji wengi watakaounda kanada hiyo.
Majoya alisema kuwa mashindano ya Kanda ambayo yatafanyika mkoani Morogoro mwezi ujao ili kupata timu itakayounda kanda ya Mashariki inayoundwa na mikoa ya Pwani na Morogoro kwa ajili ya timu itakayokwenda mkoani Mwanza kwenye mashindano ya Taifa.
“Michezo ni sehemu ya kuendeleza taaluma hivyo lazima mcheze ip[asavyo na si muende kwa ajili ya kushiriki tu lazima mpambane na kuonyesha vipaji vyenu ili muwakilishe vyema mkoa na kutoa wachezaji wengi kuwakilisha kanda ya Mashariki,” alisema Majoya.
Aidha aliwataka wanamichezo hao kuonyesha nidhamu wakati wanacheza michezo kwani nidhamu ndiyo mafanikio ya michezo kwani bila ya kuwa na nidhamu itakuwa vigumu kufanikiwa, michezo iliyoshindaniwa ni pamoja na soka, pete, wavu, kikapu, riadha na bao.
Mwisho.














Friday, May 22, 2015

SHULE HATARINI KUANGUKA


WANANCHI wa Kijiji cha Mkoko wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wameiomba Halmashauri kubomoa baadhi ya madarasa ya  shule ya Msingi Mkoko ambayo yananyufa na yako hatarini kuanguka hivyo kufanya wanafunzi kusoma kwa hofu.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo hivi karibuni Muhsin Mkumbi alisema kuwa majengo hayo yako kwenye hali mbaya na wakati wowote yanaweza kuanguka na kuleta madhara.
Mkumbi alisema kuwa madarasa hayo ni mabovu sana na hayastahili kutumika kutokana na ubovu wake hivyo ni vema Halmashauri ikayabomoa na kuyajenga upya ili kuepuka madhara ambayo yanaweza kutokea.
“Madarasa hayo yameharibika sana na yataanguka wakati wowote hivyo tunaiomba halmashauri iyabomoe kwani ni hatari kwa wanafunzi na walimu wanaofundisha shule hiyo, hali ni mbaya sana tunaomba hatua madhubuti zichukuliwe,” alisema Mkumbi.
Alisema kuwa hata baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakiogopa kwenda shule kutokana na hali hiyo ya ubovu wa madarasa hayo ambayo yamewekewa na miti kuyazuia ili yasianguke na tunawasiwasi kwani yakianguka yataleta tatizo.
Kwa upande wake ofisa elimu wa kata ya Msata Rajab Msakam alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kusema kuwa madarasa mengi yana nyufa kutokana na ardhi ya eneo hilo ujenzi wake kuwa mgumu kwani inapasuka na kusababisha nyufa.
Msakamali alisema kuwa talipeleka jambo hilo sehemu husika ili kuangalia namna ya kuikabili hali hiyo ambayo inahatarisha usalama wa wanafunzi pamoja na walimu wanaofundisha madarasa hayo yenye nyufa.
Naye Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete alisema kuwa tayari suala hilo limepelekwa halmashauri na kinachosubiriwa ni kibali kwa Kijiji kwa ajili ya kuvunja madarasa hayo ambayo yanahatarisha usalama wa wanafunzi na walimu.
Mwisho.