Tuesday, February 6, 2024

JINSI SERIKALI ILIVYOBORESHA SHULE YA SEKONDARI MWANALUGALI YAPELEKA MAMILIONI

MTAA wa Mwanalugali B Wilaya ya Kibaha umepokea kiasi cha shilingi milioni 452.6 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni mawili madarasa saba na bwalo la chakula kwenye Shule ya Sekondari ya Mwanalugali.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake Mwenyekiti wa Mtaa huo ilipo shule hiyo Deodatus Rwekaza amesema kuwa wanaishukuru serikali kwa kutoa fedha hizo ili wanafunzi wasome kwenye mazingira mazuri.

Rwekaza amesema kuwa fedha kiasi cha shilingi milioni 240 kwa ajili ya bweni moja ilitolewa na limekamilika linatumika, bweni la pili ilitolewa fedha kiasi cha shilingi milioni 120 zimetolewa na ujenzi umefikia hatua ya kupaua.

"Fedha nyingine ni kiasi cha shilingi milioni 88 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa saba ambapo sita yamekamilika moja likiwa bado tunaishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wetu Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha sekta ya elimu,"amesema Rwekaza.

Amesema kuwa fedha kiasi cha shilingi milioni 100 zometolewa kwa ajili ya ujenzi wa bwalo la wanafunzi ambalo ujenzi wake umefikia hatua ya linta.

"Shule hii pia imechimbiwa kisima kirefu kutoka kwa wafadhili kutoka taasisi ya Ishik Education and Medical Foundation ya nchi ya Uturuki tunawashukuru sana kwa msaada huo ili kukabiliana na changamoto ya maji,"amesema Rwekaza.

Monday, February 5, 2024

NYUMBU YAITAMBIA AFRICAN LYON

Ofisa Michezo Mkoa wa Pwani katika aliyevaa tisheti ya bluu Grace Bureta akiwa na baadhi ya viongozi wa Chama Cha Soka Mkoa wa Pwani (COREFA)  wakifuatilia mchezo wa First League Nyumbu 3-2 African Lyon Fc.

MWENDAPOLE B KUJENGA SHULE YA MSINGI


MTAA wa Mwendapole B Wilayani Kibaha uko kwenye hatua za mwisho katika kupata eneo kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Msingi ili kuwapunguzia changamoto watoto wa mtaa huo kugongwa na magari wakivuka kwenda shule iliyoko mtaa jirani.

Aidha wanafunzi wanaotoka mtaa huo hutembea umbali wa kilometa mbili kwenda na kurudi hivyo kuwa na uhitaji wa shule ili kuwapunguzia umbali mrefu kwenda shule.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha Mwenyekiti wa Mtaa huo Abubakary Matumla amesema kuwa mtaa huo una shule za msingi na sekondari za watu binafsi ambazo ni wazazi wachache wenye uwezo wa kuwapeleka watoto wao kusoma hapo.

"Tayari eneo limepatikana lina ukubwa wa hekari nne ambalo ni la mtu binafsi ambaye inabidi alipwe ndipo aliachie hivyo kuna makubaliano na Halmashauri ya Mji wampatie eneo lingine ili apishe hapo tuko hatua za mwisho za mabadilishano,"amesema Matumla.

Matumla amesema kuwa tayari wana tofali zaidi ya 4,000 kwa ajili ya ujenzi huo hivyo wanasubiri tu Halmashauri wampatie eneo lingine ili waanze ujenzi wa shule hiyo ambayo itawaondolea changamoto ya kugongwa au kusoma mbali.

"Wananchi wameshachanga fedha kiasi cha shilingi milioni 1.6 ambapo tunashirikiana na diwani ili kufanikisha kupata eneo hilo na matumaini ni makubwa,"amesema Matumla.

LATRA YACHUKUA HATUA KWA DALADALA ZINAZOKIUKA TARATIBU ZA USAFIRISHAJI/KUKATISHA RUTI

MAMLAKA ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) Mkoa wa Pwani imeyachukulia hatua za kisheria mabasi madogo Daladala 53 kutokana na makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na kukatisha safari.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na ofisa leseni na usajili wa Mamlaka hiyo Geofrey Mashishi alipozungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake.

Mashishi amesema kuwa hatua hizo zimechukuliwa kwa kipindi cha miezi miwili iliyopita Desemba mwaka jana na Januari mwaka huu kwa Daladala zinazofanya safari ndani ya Mkoa huo.

"Hatua hizo tumezichukuwa kwa wasafirishaji hao kwa sababu ya kukiuka masharti ya leseni zao kwa makosa mbalimbali mengine yakiwa ni kutotoa tiketi, kuzidisha nauli na mengine ambayo ni kinyume na taratibu za usafirishaji,"amesema Mashishi.

Amesema kuwa ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa wasafirishaji wanaokiuka masharti ya leseni zao kunahitajika ushirikiano baina yao na wadau wakiwemo abiria.

"Sekta ya usafirishaji ina changamoto nyingi na tumekuwa tukifanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa kwashirikiana na Jeshi la Polisi ili kuhakikisha wasafirishaji wanafuata kanuni, sheria na taratibu za usafirishaji ili kuondoa malalamiko,"amesema Mashishi.

Aidha amesema kuwa wamekuwa wakitoa elimu kwa abiria ili kujua haki zao na wasafirishaji kujua wajibu wao wanapotekeleza majukumu yao kupitia vyombo vya habari.

"Ukaguzi wa kufuatilia ni endelevu hivyo ni vema wasafirishaji wakazingatia masharti ya leseni zao ili kuondoa changamoto zisizo za lazima kwa wadau wa usafiri,"amesema Mashishi.




Sunday, February 4, 2024

LIKUNJA CUP ROBO FAINALI KUTIMUA VUMBI FEBRUARI 7


 MAashindano ya Likunja Cup hatua ya Robo Fainali yataanza kutimua vumbi Februari 7 uwanja wa Shule ya Msingi Zegereni kwa kuzikutanisha Misugusugu Fc na Veterani Fc kwa mujibu wa Rashid Likunja 

ATAKA MIKOPO ASILIMIA 10 YA HALMASHAURI IKOPESHE VIJANA WALIOACHA MATUMIZI DAWA ZA KULEVYA

HUKU Serikali ikiendelea na mchakato wa namna ya utoaji mikopo ya asilimia 10 za Halmashauri imeombwa kuangalia namna ya kuvikopesha vikundi vya waraibu wa dawa za kulevya ili wafanye shughuli za ujasiriamali.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Yohana Kilonzo Mkurugenzi wa Taasisi ya (OYARB) inayowahudumia watu waliokuwa wakitumia dawa za kulevya na kuacha na sasa wanatumia dawa za Methadoni zinazosaidia kuwarudisha katika hali yao ya kawaida ambapo kituo hicho kina vijana 500.

Kilonzo amesema kuwa watumiaji hao wanapokuwa hawana shughuli ya kufanya ni rahisi kurudia kutumia dawa za kulevya hivyo kuna haja ya kuwapatia shughuli za kufanya ili waweze kujipatia kipato.

"Wakati wakiendelea na tiba tunawafundisha shughuli za ujasiriamali ambapo wana mradi wa uuzaji wa sabuni za maji lengo wakitoka hatua hii wawe na uwezo wa kujitegemea ndiyo sababu tunaona nao wafikiriwe kwenye hiyo mikopo wapewe upendeleo,"amesema Kilonzo

Amesema kuwa kwa baadhi ya waliofuzu tiba hiyo baada ya kutumia Methadoni kwa kipindi cha miaka miwili ambazo wanapewa Hospitali ya Mkoa ya Rufaa ya Tumbi wamewachukua na kazi yao ni kufundisha juu ya athari na kuachana na matumizi ya dawa hizo. 

"Na hawa wana kikundi chao wanafanya shughuli zao hivyo hata wakikopeshwa wana uwezo mzuri wa kurudisha kwani kikundi chao kiko makini na wanajitambua kwani baadhi yao ni wasomi wazuri na wana uwezo mkubwa wanashindwa kukopesheka kama vijana kwani wengi wana umri mkubwa,"amesema Kilonzo.


HOSPITALI YA BENJAMIN MKAPA YAIKOSHA KAMATI YA BUNGE KWA UBORA WA HUDUMA

 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Maswala ya UKIMWI imeipongeza menejimenti na uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamin Mkapa kwa ubora wa Huduma na kuwatia moyo kwa  kuendelea kuwahudumia wananchi .

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Afya na Maswala ya UKIMWI, Mhe. Stanslaus Nyongo baada ya kupokea taarifa ya Huduma za kibingwa na bingwa bobezi zinazotolewa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamin Mkapa iliyopo Jijini Dodoma.

Mhe. Nyongo amesema kuwa Hospitali hiyo imekuwa ya mfano katika utoaji wa Huduma bora na  usafi wa mazingira na kuleta ufanisi sahihi wa uwekezaji mkubwa ulofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Sluhu Hassan.

“Hongereni kwa kazi nzuri mnayofanya ya kuwahudumia watanzania lakini pia Mkurugenzi husisite kutuma kutuma vijana wako kuendelea kujifunza ili Tanzania tuzidi kuwa kivutio cha tiba Utalii Afrika mashariki na Afrika nzima kwa ujumla”, Amesema Mhe. Nyongo.

Vile vile ametoa wito kwa uongozi huo kwendelea kuwa wabunifu katika kuongeza mapato ya hospitali hiyo ili kujiimarisha zaidi kiuchumi na kuacha kuwa tegemezi kwa serikali kuu.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamin Mkapa, Dkt. Alphonce Chandika ameishukuru serikali chini ya uongozi imara wa Rais Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa alioufanya katika Hospitali hiyo hususani katika vifaa tiba na vitendanishi, kusomesha wataalamu na upatikanaji wa dawa kwa wakati.