Friday, September 8, 2023

WATAKA HATUA ZAIDI KUONGEZA MATUMIZI YA GESI

IMEELEZWA kuwa matumizi ya nishati ya gesi kwa ajili ya kupikia ni asilimia moja tu huku matumizi ya kuni na mkaa ikiwa ni asilimia 98.9 hapa nchini huku ikihitajika hatua za makusudi za kuzuia matumizi hayo ya miti ili kupunguza athari kubwa za kimazingira.

Aidha serikali imeombwa kuweka bei ya juu ya
upatikanaji wa vibali vya ukataji wa miti ili kupunguza matumizi ya mkaa na kuhamasisha matumizi ya gesi majumbani.

Hayo yamesemwa Jijini Dar es Salaam na ofisa Mahusiano wa kampuni ya Taifa Gesi Ambwene Mwakalinga alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali waliotembelea eneo la ujazaji wa gesi ya (LPG) kwenye ghala lililopo Kigamboni.

Mwakalinga amesema kuwa matumizi ya kuni na mkaa ni makubwa sana hivyo kuna haja ya serikali kuweka jitihada za makusudi za kukabiliana na hali hiyo ili kusitokee mabadiliko ya Tabianchi ambayo yanasababisha athari ikiwemo ukosefu wa mvua na uharibifu wa mazingira.

Naye meneja wa ghala hilo la Kigamboni Juma Masese amesema kuwa Taifa Gesi ndiyo kampuni ya hifadhi kubwa ya gesi hapa nchini ambayo inamilikiwa na mzawa ambapo kwa sasa inahifadhi ujazo wa metriki tani 7,400 ambapo inatarajia kuwa kampuni ya kwanza Afrika kwa kuwa na hifadhi kubwa ya nishati hiyo ambayo huletwa na meli kutoka nchi zinazozalisha gesi duniani.

Kwa upande wake ofisa usalama wa kampuni hiyo Albert Bungayela amesema kuwa wanatoa elimu kwa mawakala ili nao watoe elimu kwa watumiaji kuwa makini katika matumizi ili kuepuka madhara yatokanayo na matumizi mabaya ya gesi.


Thursday, September 7, 2023

JUMUIYA YA WAFANYABIASHARA TANZANIA WACHARUKA MKOANI MBEYA

 



WAFANYABIASHARA mkoani Mbeya waiomba Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Mbeya kufanya marekebisho ya baadhi ya mifumo na Sheria za Kodi zinachochea rushwa .


Hayo yamesemwa na wafanyabiashara wa mkoani hapo wakati wa kupokea kero, maoni na changamoto za wafanyabiashara katika mkutano uliofanyika eneo la soko jipya la Mwanjelwa chini ya Rais wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania Hamis Livembe.

Wamesema kuwa TRA mkoani hapo imekuwa ikitumia mifumo hiyo kama chanzo cha mapato binafsi na si kuwasaidia kukuza biashara  za wafanyabiashara hao.

Aidha wameitaka serikali kutambua kuwa uchumi wa Watanzania wengi unajengwa kupitia biashara hivyo wanaiomba serikali ipunguze ututiri wa kodi .

Awali Mwenyekiti wa  Jumuiya wafanyabiashara Tanzania Hamis Livembe amesema kuwa moja ya sababu ya kufanya ziara mkoani hapo ni kukusanya changamoto , kero na maoni ili kuyatafutia ufumbuzi kwa mamlaka husika.

Livembe amesema kuwa zipo changamoto zinazowakumba wafanyabiashara hivyo kama kiongozi wa Jumuiya ya wafanyabiashara atahakikisha kero  zote zimetafutiwa ufumbuzi.

Naye katibu wa Jumuiya ya wafanyabiashara Tanzania Abdall Salim amesema kuwa wafanyabiashara wote Tanzania wanatakiwa kuungana kwa pamoja ili kukomboa biashara zao hivyo wanapaswa kujisajili na Jumuiya hiyo.

Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania ni Taasisi inayosimamiwa na wafanyabiashara wenyewe wenye lengo la kuhakikisha wanatatua changamoto za kibiashara.

Wednesday, September 6, 2023

JAMII YAFUNDISHWA USAWA WA KIJINSIA KULETA MAENDELEO JUMUISHI


HALMASHAURI ya Mji Kibaha imedhamiria kuhakikisha inafikia asilimia 50 ya usawa wa kijinsia ili kuleta maendeleo jumuishi kwa wananchi.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na ofisa maendeleo ya jamii kitengo cha jinsia wa Halmashauri ya Mji Kibaha Maria Nkangali wakati wa mafunzo kwa watu maarufu kwenye jamii kupitia mradi wa uongozi wa wanawake na haki za kiuchumi (WLER).

Nkangali alisema kuwa hadi sasa wamefikia asilimia 20 kwenye mradi huo wa miaka mitano kuanzia 2021 hadi 2026 ambapo hadi sasa wako kwenye kata tatu za Visiga, Mkuza na Pangani.

"Lengo la mradi huu ni kuwa na usawa wa kijinsia kwenye masuala mbalimbali ikiwemo uongozi, uchumi, umiliki wa ardhi na kupata huduma za kijamii,"alisema Nkangali.

Kwa upande wake wakili wa serikali kutoka Halmashauri ya Mji Kibaha Elizabeth Lukumay  alisema kuwa baadhi ya ndoa zinakuwa ni batili kutokana na kutofuata taratibu za kisheria hivyo inapotokea zinavunjika mwanamke na watoto wanakosa haki.

Naye mwenyekiti wa wazee kata ya Mkuza Anangisye Mwakapande alisema kuwa changamoto za ndoa na ardhi ni kubwa sana kutokana na kutokuwa usawa wa kijinsia.



Tuesday, September 5, 2023

MBUNGE MUHARAMI MKENGE AKUTANA NA NAIBU WAZIRI MKUU DK DOTTO BITEKO NA WAZIRI MSTAAFU WA MALIASILI WA KENYA NAJIB BALALA

MBUNGE wa Jimbo la Bagamoyo Muharami Shabani Mkenge, Leo tarehe 5 mwezi wa 9 alipata  wasaa wa kuwa na mazungumzo na Naibu waziri mkuu na waziri wa Nishati  Mhe Dotto Biteko,  pamoja na waziri wa maliasili mstaafu wa Kenya Mhe Najib Balala  ofisini kwa Naibu  waziri  mkuu 

Wakijadili uwekezaji  katika sekta ya chumvi, pamoja na upatikanaji wa umeme wa uhakika katika Jimbo la Bagamoyo.

IMETOLEWA NA OFISI YA MBUNGE JIMBO LA BAGAMOYO🇹🇿

WAFANYABIASHARA WA PEMBEJEO NJOMBE WAMSHUKURU RAIS KWA RUZUKU YA MBOLEA

Na Mwandishi Wetu, Makambako

WAFANYABIASHARA wa pembejeo Soko Kuu la Mji wa Makambako, mkoani Njombe, wamemshukuru na kumpongeza Rais Samia kwa kuweka ruzuku ya mbolea iliyorahisisha shughuli za kilimo na upatikanaji mazao ya kutosha kwa wakulima mkoani humo.

Wizara ya Kilimo mwaka 2023/24, kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), inaendelea kuratibu upatikanaji wa mbolea nchini  kutoa ruzuku kwa wakulima hadi mwaka 2025/26 ili kuongeza matumizi ya mbolea kutoka kilo 19 hadi kilo 50 kwa hekta, kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza upatikanaji wa mazao.

Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Pembejeo za Kilimo mkoani Njombe, Abdusalim Mangoma alitoa pongezi hizo kwa niaba ya wenzake wakati akizungumza kwenye mkutano wa viongozi wa Jumuiya ya Wafanyabishara Tanzania (JWT), katika ofisi za jumuiya hiyo zilizopo Mji Mdogo wa Makambako.

Vìongozi hao wakiongozwa na Mwenyekiti wake Hamis Luvembe, wanafanya ziara ya kutembelea wafanyabishara wa mikoa ya Njombe, Mbeya na Songwe kwa ajili ya kusikiliza kero zinazowakabili ili kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu na kusajili wanachama  wake.

 Sanga alisema hatua ya serikali kutoa ruzuku ya mbolea kwa wakulima imeonesha matokeo chanya kwenye uzalishaji mazao katika mkoa huo.

"Wakulima sasa wananunua mbolea kwa utaratibu maalum, tofauti na awali hawakuwa wanaunua mbolea kwa sababu bei zilikuwa siyo rafiki kwao hivyo kushindwa kupata mazao ya kutosha," alisema.

Naye Katibu wa wafanyabiashara hao, Mhema Wakala, alisema mfumo wa usajili wakulima umesaidia kutambulika maeneo walipo na mashamba yao.

"Hii imetusaidia wasambazaji wa mbolea kuwatambua wakulima na kuwafikia kwa urahisi hadi waliopo vijijini," alisema Wakala.

Mwenyekiti wa Wafanyabiashara Mkoa wa Njombe na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Sifael Msigala, alisema wafanyabiashara wa mikoa hiyo wanatekeleza majukumu yao kikamilifu kutokana na kupata ushirikiano mkubwa kutoka kwa viongozi wa serikali ikiwamo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Katibu wa JWT, Abdallah Salim, aliwasihi wafanyabishara kutekeleza vyema majukumu yao kwa kufuata taratibu na kanuni za serikali kwa sababu Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anasikiliza na kuzifanyia kazi kero zinazowakabili.

"Endeleeni kufanyabiashara huku mkitembea kifua mbele kwa sababu Rais Dkt. Samia tunaendelea kumfikishia kero zenu na kuzifanyia ufumbuzi, lengo ni wafanyabishara kuwa na ustawi kwenye taifa latu," alisema.

Naye Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Mkoa wa Tanga na Mjumbe wa JWT, Ismail Masoud,  alisema Rais Dkt. Samia ni kiongozi wa mfano kwa sababu amegusa moja kwa moja matatizo ya wafanyabiashara nchini.

Kwa mujibu wa Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, akizungumza Agosti 8, 2023 kwenye kilele cha Maonesho ya Kimataifa ya Nane Nane, jijini Mbeya, alisema eneo la uzalishaji kabla ya ruzuku ya mbolea lilikuwa ekari 10,440,000  mwaka 2021/2022 hadi kufikia hekta 11,137,874.

Aidha, matumizi ya mbolea yameongezeka kutoka hekta 363,599 mwaka 2021/22 hadi tani 580,529 5085,590 mwaka 2022/23

Uzalishaji wa chakula umeongezeka kutoka tani. 17,148,290 mwaka 2021/22 hadi tani 20,42,014 mwaka 2022/23 sawa na ongezeko la tani 3,000,000.

Aidha, mbolea zitakazohusika kwenye ruzuku ni mbolea za kupandia na kukuzia ambapo DAP kwaajili ya kupandia na Urea kwaajili ya kukuzia ambazo ni takribani asilimia 50 ya matumizi ya mbolea nchini.

Mbolea za kupandia na kukuzia za aina zingine zinahusika kwenye ruzuku kulingana na mahitaji ya soko.

Monday, September 4, 2023

WAHAMIAJI HARAMU WAKAMATWA

 

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani limewakamata wahamiaji haramu watatu toka nchi mbalimbali kwa kuingia nchini bila ya kibali.
 
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na kaimu kamanda wa polisi mkoani Pwani ACP Muhudhwari Msuya imesema kuwa watuhumiwa hao wamekabidhiwa Uhamiaji kwa hatua za kisheria.

Msuya amesema kuwa watuhumiwa hao ni kutoka nchi za Ethiopia mmoja, Kenya mmoja na Uganda mmoja.

Amesema kwenye matukio mengine jeshi hilo limekamata jumla ya Pikipiki 111 za aina mbalimbali Haoujue 23, Boxer 30, Fekon 10, SanLg 16, Sinray 1, Kinglion, Senke 01, bajaji 4 na Tvs 23 mali zidhaniwazo kuwa za wizi na watuhumiwa 97 walikamatwa.

Pia kwenye matukio mengine jeshi limefanikiwa kukamata Bhangi viroba 7, Puli 60, Kete 791 na Mbegu za Bangi kilogramu 5, Mirungi Kilogramu 5, Bunda 3 za mirungi ambapo umla ya watuhumiwa 114 wamekamatwa katika makosa hayo.


POLISI PWANI WAKAMATA WATUHUMIWA NYAMA YA SWALA NA MAGAMBA 11 YA KAKAKUONA

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani kwa kushirikiana na askari wa wanyama pori limefanikiwa kukamata watubuhumiwa 14 wakiwa na nyama ya swala na magamba 11 ya mnyama Kakakuona.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani humo ACP Muhudhwari Msuya amesema kuwa baadhi ya watuhumiwa walifikishwa mahakamani.

Msuya amesema kuwa kukamatwa watuhumiwa hao 14 ni mafanikio ya jeshi hilo ambapo kati ya hao watuhumiwa watatu wamefikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.

Amesema kuwa watu watatu wamehukumiwa vifungo tofuati kutokana na kukutwa na makosa ya ubakaji na ulawiti.

Amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Salim Issa ambaye amehukumiwa kifungo cha maisha baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kulawiti mwingine ni Albino Anthony amehukumiwa kifungo cha miaka 30 baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kubaka.

"Mazoea Salum amehukumiwa kifungo cha miaka 30 baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kubaka huku Hamisi Idd amehukumiwa kifungo cha miaka 20 baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kupatikana na nyara za Serikali,"amesema Msuya.

Aidha amesema kuwa Yusuph Athuman naye  amehukumiwa kifungo cha maisha baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kupatikana na nyara za Serikali.

"Katika kipindi cha mwezi Agosti jumla ya kesi zilizoshinda mahakamani zilikuwa 75 zikiwemo hizo za watuhumiwa ambao walihukumiwa jela maisha na wengine jela miaka 30 kwa kosa la kulawiti na kubaka watuhumiwa waliotiwa hatiani katika mahakama za Mkoa wa Pwani na kwenda jela kwa baadhi ya kesi,"amesema Msuya.