Saturday, April 11, 2015

PWANI YAINGIZA MABILIONI KUPITIA MISITU

Na John Gagarini, Bagamoyo
MKOA wa Pwani umefanikiwa kukusanya kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni nane kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika kipindi cha mwaka 2013/2014.
Hayo yalisemwa juzi wilayani Bagamoyo na Ofisa Misitu wa mkoa huo Daniel Isara, wakati wa maadhimisho ya upandaji miti kimkoa iliyofanyika kwenye eneo la la Gareza la Kigongoni ambapo ilipandwa zaidi ya miti 3,000.
Isara alisema kuwa fedha hizo zimetokana na kukabiliana na uharibifu wa rasilimali misitu na mazingira ambapo doria ziliimarishwa na ukusanyaji wa mapato kufikia kiasi hicho.
Alisema kuwa hadi kufikia mwezi Januari 2014/2015 makusanyo yalifikia kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni sita baada ya wakala hao kuongeza watumishi kwenye ngazi za wilaya.
“Mbali ya mafanikio ya ukusanyaji wa mapato hayo ya Serikali pia mkoa umehamasisha na mwamko umekuwa mkubwa na kuongeza uanzishwaji wa vitalu vya miche na upandaji wa miti kwe taasisi za serikali na zisizo za serikali na watu binafsi kutoka miche ya miti milioni 2,253,136 mwaka 2013/2014 na kufikia milioni 2,663,202 mwaka 2014/2015,” alisema Isara.
Aidha alisema kuwa pia wakala imeweza kuwaondoa wavamizi kwenye misitu ya Ruvu Kaskazini, Ruvu Kusini, Kiloka, Kazimzumbwi na wavuvi kwenye Delta ya Rufiji pia kuweka mipaka ya misitu ya hifadhi kiasi cha kilometa 640 katika hekta 10,704.
“Changamoto zinazoikabili rasilimali ya misitu ni pamoja na ongezeko kwa wakazi wa mkoa wa Dar es Salaam ambalo huongeza mahitaji ya mkaa na kuni hivyo kuongezeka kwa ukataji na ufyekaji wa misitu na mapori,” alisema Isara.
Alibainisha kuwa kuna wafanyabiashara 320 waliosajiliwa kufanyabiashara ya kuvuna mazao ya misitu mkoani Pwani kwa  mwaka 2013/2014 na 336 mwaka 2014/2015 na zaidi ya asilimia 90 wanatoka nje ya mkoa.
Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Pwani  Evarist Ndikilo ambaye aliwakilishwa na mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga alisema kuwa taasisi zinazotumia kuni kwa wingi kwa ajili ya kupikia na shughuli nyingine zinapaswa kupanda miti kwa wingi.
Ndikilo alisema kuwa zinapaswa kutumia majiko sanifu yanayotumia kuni au mkaa kidogo ili iwe sehemu ya ubunifu wa kupunguza matumizi makubwa ya nishati ya miti.
Aliwataka wananchi kila mtu kupanda miti ili kulinda mazingira pia mamalaka za serikali za mitaa kuomba vibali vya kuajiri watumishi kwa ajili ya kuimarisha usimamizi wa rasilimali misitu na misitu iliyohifadhiwa inatunzwa na kuzuia wavamizi wanaoingiza mifugo, uchimbaji wa mchanga, kilimo na makazi kwenye misitu.
Mkoa wa Pwani una misitu 34 ya hifadhi yenye jumla ya hekta 335,712 iliyohifadhiwa kisheria na hekta milioni 2.2 ya misitu kwenye ardhi huria ambayo hutegemewa na mikoa ya Pwani na Dar es Salaam kwa ajili ya matumizi ya nishati za magogo, mbao, samani na matumizi mengine.
Mwisho.      


 MKUU wa wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani Majid Mwanga akipanda mti kwaniaba ya mkuu wa wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo kama ishara ya maadhimisho ya siku ya kupanda miti kimkoa kwenye eneo la Gereza la Kigongoni 

Sunday, April 5, 2015

PIMENI MAENEO YA SHULE NA WAKRISTO WAOMBEENI POLISI

Na John Gagarini, Chalinze
VIONGOZI wa Vijiji na Vitongoji kwenye Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo  mkoani Pwani wametakiwa kupima maeneo yao ya shule ili kupata hati miliki na kuepuka uvamizi wa maeneo hayo.
Hayo yamesemwa na Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete wakati wa uzinduzi wa shule ya Msingi ya Happy Lukwambe kwenye kijiji cha Visakazi.
Ridhiwani alisema kuwa baadhi ya shule Jimboni humo maeneo yake hayajapimwa hivyo kufanay baadhi ya watu kuvamia maeneo ya shule.
“Kwa kuwa eneo lenu la shule liko kwenye mazingira mazuri na mmefanya uhifadhi wa misitu ni vema mkalipima eneo lenu ili muwe na hati ya umiliki wa ardhi muweze kukabiliana na wavamizi wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shule,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa kwa kuwa shule hiyo imejengwa kisasa ni moja ya shule za msingi ambazo ni za mfano katika wilaya ya Bagamoyo na hata nchi nzima lazima mazingira yake yalindwe.
“Isije ikawa baada ya muda si mrefu mkaja kwangu kulalamika kuwa eneo lenu limevamiwa nawashauri pimeni eneo lenu kupitia uongozi wa shule na Kijiji ili kufanikisha zoezi hilo,” alisema Ridhiwani.
Kwa upande wake moja ya wafadhili wa ujenzi wa shule hiyo Happy Frank kutoka nchini Uingereza alisema kuwa ameridhishwa na ujenzi huo na kusema kuwa kukamilika kwa shule hiyo japo ni madarasa matatu lakini ni mafanikio na ni kumbukumbu nzuri kwa familia yake.
Naye msimamizi wa ujenzi huo Remigius Mshenga alisema kuwa shule hiyo imejengwa kutokana na eneo hilo kutokuwa na shule ambapo wanafunzi walikuwa wakienda kilometa 17 kwenye shule ya Msingi Bwawani.
Mshenga alisema kuwa watoto wengi wa eneo hilo walikuwa wakishindwa kwenda shule kutokana na umbali ambapo wengine waliacha shule na sasa inaanza na wanafunzi 55 ambapo gharama za ujenzi ni shilingi milioni 60 pamoja na madawati na ujenzi wake ulianza mwaka 2013 wa madarasa matatu.
Naye ofisa elimu wa wilaya ya Bagamoyo Abdul Buheti alisema kuwa wataendelea kuisaidia shule hiyo kwa kuhakikisha wanapeleka walimu wenye sifa pamoja na vitabu vya ziada na kiada na kwa kuitambua shule hiyo tayari wameshapeleka walimu wawili wanaofundisha watoto hao wa darasa la kwanza hadi la tatu.
Shule hiyo imekengwa kwa ufadhili wa Happy Bricks Foundation ya nchini Uingereza na kusimamiwa na taasisi ya Ngerengere River Eco Camp.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
WAKRISTO nchini wametakiwa wakati wakiadhimisha sikukuu ya kufufuka Yesu Kristo  (Pasaka)  waliombee Jeshi la Polisi lisendelee kufanyiwa vitendo vya kinyama na baadhi ya watu wenye nia mbaya na nchi.
Siku za hivi karibuni kuwamekuwa na matukio ya uvamizi wa vituo vya polisi na kuwaua askari kisha kupora silaha ambazo hazifahamiki huwa zinapelekwa wapi.
Akizungumza kwenye ibaada ya Pasaka kwenye Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania KKKT Jimbo la Magharibi Usharika wa Maili Moja, Mchungaji wa kanisa hilo Isai Ntele alisema kuwa hali hiyo inahatarisha amani ya nchi.
Mch Ntele alisema kuwa hali hiyo ya uvamizi wa vituo vya polisi na kuwaua kisha kuchukua silaha havipaswi kuachwa kuendelea kwani haifahamiki silaha zinazoibiwa zinatumika vipi.
“Hali hii si ya kuifumbia macho hata sisi wakristo wakati tunasherehekea sikukuu hii ya kufufuka Yesu Kristo lazima tuiombee amani ya nchi kwani walinda amani wanashambuliwa sasa na kuuwawa sisi tutakuwa salama,” aliuliza Mch Ntele.
Aidha alisema kuwa watu hao wanaofanya vitendo hivyo wanaweza wakawa wanafanya uhalifu kwa kutumia silaha hizo hivyo wananchi wakawa hawawezi tena kuishi kwa amani na kuwajengea hofu.
“Watu hawa ni wabaya kwani wakiingia mtaani na hizo silaha tutakuwa hatuna amani tena kwani vitendo vya uhalifu vitaongezeka hivyo lazima tufanya maombi ya kuwaombea askari wetu ili wawe salama waweze kutulinda na sisi,” alisema Mch Ntele.
Aliwataka wakristo kuadhimisha sikukuu hiyo kwa upendo na mshakamano na kuacha vitendo ambavyo vitaleta athari ndani ya jamii ili kudumisha amani ya nchi yetu.
Mwisho.


Friday, April 3, 2015

HABARI MPYA ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo amewataka wadau wa mchezo wa bao kuwafundisha vijana ili kuendeleza mchezo huo ambao ulipendwa na wapigania uhuru wa nchi akiwemo Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
Alitoa rai hiyo mjini Kibaha alipokuwa akizungumza na viongozi wa Jumuiya ya Wazazi ya Kibaha Mjini wakati wa juma la jumuiya hiyo lililoadhimishwa kwa shughuli mbalimbali ikiwemo mchezo wa bao uliodhaminiwa na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka ili kumuenzi Baba wa Taifa aliyekuwa akiupenda mchezo huo.
Ndikilo alisema kuwa kwa sasa mchezo huo unachezwa zaidi na wazee kuliko vijana hivyo kuna umuhimu wa kuwafundisha vijana ili waupende mchezo huo na kuuendeleza.
“Tunampongeza mbunge kudhamini mashindano ya bao ambayo yalishirikisha timu kutoka mitaa yote ya kata 11 za Kibaha Mjini na kuwashirikisha wazee huku vijana wakiwa ni wachache,”alisema Ndikilo.
Alisema kuwa ili kumujenzi Baba wa Taifa wadau mbalimbali wa mchezo huo wanapaswa kuwaweke mazingira mazuri ya kushiriki mchezo huo ambao ni maarufu kwa wakazi wa mikoa ya Pwani.
Kwa upande wake Koka alisema kuwa lengo la kudhamini mashindano ni kuuhamasisha mchezo huo ili usipotee na kuwafanya wazee nao wapate kushiriki michezo.
Koka alisema kuwa ataendelea kuhamasisha mchezo huo hasa kwa vijana ili uweze kupendwa na kuwavutia wengi kuliko kungangania baadhi ya michezo kwani hata huo una nafasi yake.
Katika mashindano hayo timu ya Kata ya maili Moja ilifanikiwa kuwa bingwa na kujinyakulia kiasi cha shilingi 300,000 huku kata ya Kibaha wakijinyakulia 200,000 na kata za Mkuza, Mbwawa, Misugusugu, Tumbi, Visiga, Pangani, Kongowe na Picha ya Ndege zilijinyakulia 100,000 kila moja kwa ushiriki wao.
Aidha mashindano ya kukuna nazi wanawake Zuhura Rashid alijinyakulia 70,000, akifuatiwa na Sara Alfred aliyejipatia 50,000 huku Zuhura Ally akipata 30,000 huku washiriki wengine wakijinyakulia 20,000 kila mmoja kwa ushiriki wao.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MBUNGE wa Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani amemwomba mkuu wa mkoa wa Pwani kuzihimiza Halmashauri kuwawezesha wajasiriamali wanawake na vijana kupata asilimia 10 ya mikopo kwa ajili yao.
Aliyasema hayo mjini Kibaha mbele ya mkuu wa mkoa huo Evarist Ndikilo alipokuwa akiongea na viongozi wa Jumuiya ya Wazazi ya Mji wa Kibaha wakati wa maadhimisho ya juma la Wazazi.
Koka alisema kuwa upatikanaji wa fedha hizo toka halmashauri ni changamoto kwa makundi hayo hali inayowafanya walalamike kutopatiwa fedha hizo ambazo zimetengwa kwa ajili ya vikundi vya ujasiriamali.
“Mkuu wa mkoa naomba usaidie uwaandikie barua wakurugenzi wa Halmashauri za wilaya za mkoa huu kuhakikisha zinawapatia fedha hizo makundi ya akinamama na vijana ili waweze kujikwamua kiuchumi kwa kuendeleza shughuli zao za ujasirimali,” alisema Koka.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Kibaha Mjini Dk Athuman Mokiwa alisema kuwa moja ya changamoto ianyowakabili ni ukosefu wa fedha kwa ajili ya kupima kiwanja chao kilichopo Simbani.
Dk Mokiwa alisema wanaomba Halmashauri iwapimie kiwanja chao ili waweze kuwa hati ya umiliki na kuweza kuweka wawekezaji ili Jumuiya iweze kujiongezea kipato.
Naye mkuu wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo alisema kuwa maombi yote yaliyotolewa na Jumuiya ya Wazazi yapelekwe kwa maandishi ofisini kwake ili aweze kuwafikishia ujumbe wahusika.
Ndikilo aliipongeza Jumuiya hiyo na kusema ndiyo Jumuiya kiongozi kwani imeyabeba makundi yote ya chama wakiwemo vijana, akinamama na wazee hivyo lazima iwe mfano wa kuwa muhimili wa chama.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kisarawe
IMEELEZWA kuwa uanzishwaji wa Masjala za Ardhi kutasaidia kukabiliana na migogoro na kupandisha thamani ya ardhi kwa ajili ya uwekezaji kwenye vijiji mkoani Pwani.
Akizungumza na wakazi wa Kijiji cha Chakenge wilayani Kisarawe wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo alipotembelea Masjala ya Kijiji hicho, kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo Cheyo Nkelege alisema kuwa uanzishwaji wa Masjala hizo huwafanya wanakijiji kuwa na hati za umiliki za kimila.
Nkelege alisema kuwa Masjala hizo zina faida kubwa hususani kwa wananchi wa vijijini kwani wanaweza kuwa na hati miliki za mashamba yao ambazo zinaweza kuwasaidia katika mambo mbalimbali ikiwemo dhamana na rehani.
“Faida za kuanzishwa Masjala hizi kwanza inasaidia kupata hati za umiliki za kimila, kurasimisha ardhi kwa wawekezaji, kuongeza thamani ya ardhi, kuhifadhi nyaraka za ardhi na kupunguza migogoro ya mipaka ambayo imesababisha hadi vifo,” alisema Nkelege.
Alisema kuwa faida nyingine ni kuwa na mipaka inayoeleweka na kupunguza migogoro ya ardhi ambayo imekithiri baina ya wananchi na Vijiji kwa Vijiji hivyo ni mpango mzuri unaopaswa kuigwa sehemu mbalimbali nchini.
Kwa upande wake mkuu wa mkoa Ndikilo alisema kuwa Masjala hiyo ni kichocheo cha maendeleo kwani itatunza kumbukumbu mbalimbali za ardhi na itawaondolea umaskini.
Ndikilo alisema kuwa jambo jema kwani hati miliki hizo zitatambulika kisheria na zitaweza kutumika kwa ajili ya mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuweka dhamana kwa ajili ya kukopa fedha kwa ajili ya shughuli za maendeleo.
Akisoma risala juu ya ujenzi huo Belina Denisa alisema kuwa ujenzi huo umekamilika ambao umegharimu kiasi cha shilingi milioni 40 bila ya samani za ndani ambayo ni fidia iliyotolewa na kampuni ya Sun Bio Fuel kwa kijiji hicho baada ya kuchukua shamba kijijini hapo. Kutokana na ubora wa Masjala hiyo mkuu wa mkoa huyo aliahidi kuwapatia 500,000 na 500,000 zitatolewa na mbunge wa Jimbo la Kisarawe Hussein Jaffo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MBUNGE wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka ametumia kiasi cha zaidi ya milioni 400 kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali waliojiunga kwenye vikundi 150.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati wa kongamano la wajasiriamali wa Jimbo hilo na kusema kuwa lengo ni kuwafikia wajasiriamali woete kwenye mitaa na kata hasa wale waliojiunga kwenye vikundi.
Koka alisema kuwa vikundi hivyo vinajishughulisha na shughuli mbalimbali za ujasairiamali ikiwemo biashara pamoja na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali ambazo huziuza kwenye masoko mkoani humo na nje ya mkoa.
“Tumedhamiria kuwawawezesha wajasiriamali kiuchumi kwa kuwapatia fedha kwa ajili ya kuendesha shughuli zao za kiuchumi za kuweza kujiongezea kipato na kuinua uchumi wa familia,” alisema Koka.
Alisema kuwa wajasiriamali wana uwezo wa kuinua kipato cha jamii kwani ndiyo shughuli za kiuchumi zinazoweza kuwawezesha kumudu maisha kuliko ajira za kuajiriwa ambazo ni chache.
“Kama mnavyojua ujasiriamali umechukua nafasi kubwa ya kiuchumi na umewasaidia watu wengi kujiajiri hususani vijana na akinamama hivyo kuacha kuwa tegemezi,” alisema Koka.
Kwa upande wa mke wa Mbunge huyo Selina Koka ambaye ni mlezi wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) CCM Kibaha Mjini amekuwa akiwapatia mafunzo ya ujasiriamali alisema kuwa kwa sasa wanawake wengi wameamka na kuendesha familia kupitia shughuli hizo.
Selina alisema kuwa wajasirimali wanachotakiwa ni kuhakikisha wanajiunga kwenye vikundi ili waweze kupata misaada ya fedha kwa ajili ya kuendeshea shughuli zao.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kisarawe           
HOSPITALI ya Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani imekamilisha ujenzi wa chumba kipya cha kuhifadhia maiti kwenye hospitali ya wilaya hiyo ambayo ilikuwa inakabiliwa na changamoto ya kuwa na chumba kidogo hali iliyokuwa ikiwafanya kupeleka kuhifadhi maiti hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Akisoma risala mbele ya mkuu wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo aliyetembelea hospitali hiyo ya wilaya, mganga mkuu wa wilaya Dk Happiness Ndosi alisema kuwa hali hiyo ilikuwa changamoto kubwa.
Dk Ndosi alisema kuwa ndugu wa marehemu walikuwa wakipata taabu kuhifadhi maiti na kuzipeleka Jijini Dar es Salaam hivyo kutumia gharama kubwa hadi wakati wa mazishi.
“Chumba cha maiti cha zamani kilikuwa na uwezo wa kuhifadhi maiti wawili tu na kilijengwa miaka ya 1950 hivyo kushindwa kukidhi mahitaji ya kuhifadhi miili ya marehemu ambapo huwabidi kuipeleka Muhimbili,” alisema Dk Ndosi.
Alisema kuwa chumba hicho cha sasa hivi kitakuwa na uwezo wa kuhifadhi miili 36 kwa wakati mmoja endapo itatumika vizuri hivyo kuondoa changamoto hiyo.
“Mradi huu umegharimu kiasi cha shilingi milioni 102 ambazo zimetoka serikali kuu ikiwa ni maombi maalumu ambapo umekamilika kwa asilimia 99 na kwa sasa imebaki kuingiza umeme pekee na utaingia muda wowote kuanzia sasa na mafundi wanaendelea na kazi,” alisema Dk Ndosi.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kisarawe Subira Mgalu alisema wanaishukuru serikali kwa kutoa fedha za ujenzi wa chumba hicho kwani imewaondolea mzigo wa kuhifadhi maiti.
“Ilikuwa ni shida mtu akifa apelekwe Muhimbili halafua arudishwe gharama zilikuwa ni kubwa sana hivyo imesaidia kupunguza usumbufu hivyo watu wataweza kujipanga kuandaa shughuli za mazishi kwa nafasi,” alisema Mgalu.
Mgalu alisema kuwa kukamilika kwa mradi huo ambao umefanywa na serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma karibu na kwa gharama nafuu kwani sasa hawatapata usumbufu tena wa kuhifadhi maiti.
Naye mkuu wa mkoa Ndikilo alisema kuwa utu wa binadamu utalindwa kwani kipindi cha nyuma mwili ulikuwa unazikwa harakahara kwani ukikaa muda hata siku mbili una haribika hivyo kutoitendea haki maiti na utawapunguzia gharama.
Ndikilo alisema watapata muda mzuri wa kuweza kuandaa mipango ya mazishi kwa ajili ya kuwahifadhi wapendwa wao ambapo nyuma walikuwa wakikosa muda wa kuweka mipango mizuri.
Mwisho.
 

         

Wednesday, April 1, 2015

HABARI LEO

Na John Gagarini, Kibaha
KITUO cha Afya cha Mkoani wilayani Kibaha mkoani Pwani kinakabiliwa changamoto ukosefu wa vitanda  40 kwenye wodi ya wajawazito hali inayosababisha kitanda kimoja kulaliwa na akinamama wanne.
Hayo yalibainika wakati wa ziara ya Jumuiya ya Wazazi ya Kibaha Mjini na kwenye kituo hicho kilichopo mjini Kibaha kwenye maadhimisho ya wiki ya Jumuiya hiyo.
Ziara hiyo ya kutembelea kituo hicho iliongozwa na mlezi wa Jumuiya ya Wazazi Selina Koka ikiwa ni sehemu ya maadhimisho hayo ambayo huambatana na shughuli mbalimbali za Kijamaii.
Ofisa Muuguzi wa Kituo hicho Prisca Nyambo alisema kuwa changamoto hiyo ni kubwa sana kwani vitanda vilivyopo ni nane.
“Kama mnavyoona vitanda viko nane tu kwa ajili ya mama wajawazito lakini idadi ya wajawazito wanaokuja kwa mwezi ni 250 hadi 300 ambapo idadi hiyo ni kubwa sana kwa kituo chetu,” alisema Nyambo.
Nyambo alisema kuwa idadi ya wajawazito waliojifungua mwezi Januari walikuwa 342 na Februari walikuwa 344 ambapo hadi Machi 31 mama wajawazito 300 walikuwa tayari wameshajifungua.
“Idadi ya mama wajawazito wanaohudumiwa hapa ni wengi sana na tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze kuchangia vitanda na magodoro yake ili tukabiliane na changamoto hii,” alisema Nyambo.
Aidha alisema kuwa vifo vya watoto kwa mwezi Januari ilikuwa ni tisa na mwezi Februari vilikuwa vifo saba ambavyo vinatokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na akinamama hao kwenda wakiwa katika hatua za mwisho kabisa pamoja na matumizi ya dawa za kienyeji za kuongeza uchungu.
Kwa upande wake mlezi huyo wa Jumuiya ya Wazazi Selina Koka alisema kuwa anaguswa na hali hiyo ambapo alitoa vitu mbalimbali vikiwemo vifaa vya kujifungulia zikiwemo dawa, pamba na vifaa vy kukatia vitovu.
Selina alisema kuwa changamoto zingine atazifanyia kazi kwa kushirikiana na mbunge wa Jimbo hilo Silvestry Koka ili kuwaondoa adha wanayoipata akianamama wajawazito wanaokwenda kujifungua kituoni hapo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MTOTO Joel Roman (3) wa mtaa wa Ungindoni wilayani Kibaha mkoani Pwani amefariki dunia baada ya kutumbukia kwenye kisima cha maji alipokuwa akicheza.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa huo Geofrid Nombo alisema kuwa mtoto huyo aliondoka nyumbani na kuelekea kisimani akiwa peke yake.
Nombo alisema kuw atukio hilo lilitokea Machi 30 mwaka huu majira ya saa 4 asubuhi baada ya mtoto huyo kuondoka bila ya mama yake Marry Ngowi kujua.
“Alipoondoka mama yake alimtafuta bila ya mafanikio ndipo alipowaambia majirani wenzake kisha kuanza kumtafuta na ndipo walipokuta ndala zake zikiwa nje ya kisima huku yeye akiwa amedumbukia kwenye kisiama hicho,” alisema Nombo.
Aidha alisema kuwa mtoto huyo alikuwa akienda na mama yake kisimani hapo hivyo akawa amekariri eneo hilo ambalo si mbali na nyumba waliyokuwa wakiishi.
“Kisima hicho cha maji ni kirefu unaokaribia kufika futi tano na hutumiwa na watu wa eneo hilo kwa ajili ya matumizi ya kufulia na kuogea wakati wa kiangazi lakini kwa bahati mbaya kilikuwa wazi na hakikuzibwa juu,” alisema Nombo.
Aliongeza kuwa kutokana na tukio hilo alimwamuru mmiliki wa kisima hicho ambaye alimtaja kwa jina moja la Frank akifunike au akifukie ili kuepusha matukio kama hayo yasiweze kutokea. Jeshi la polisi limethibitisha kutokea kwa tukio hilo. 
Mwisho.
Na John Gagarini, Chalinze
KIJIJI cha Wafugaji cha Mindutulieni kata ya Lugoba wilayani Bagamoyo kinapoteza ngombe zaidi ya 600 wanaokufa kutokana na ugonjwa wa Ndigana unaosababisha hasara ya shilingi milioni 200 kila mwaka.
Akisoma risala ya wanakijiji hao ofisa mtendaji Meisi Sokoroti kwa Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete wakati wa ziara yake alisema kuwa ugonjwa huo umekuwa unawatia hasara kubwa.
Sokoroti alisema kuwa vifo vingi vinatokana na baadhi ya magonjwa ukiwemo huo ambao unawaletea ngombe homa kali na kusababisha vifo .
“Hata hivyo baadhi ya dawa zimekuwa na gharama kubwa ambapo dawa kama Butalex inauzwa kwa bei ya shilingi 50,000 hali ambayo inawasababisha baadhi ya wafugaji kushindwa kumudu gharama hiyo,” alisema Sokoroti.
Alisema kuwa tatizo hilo la ngombe kufa kwa wingi lmedumu kwa kipindi cha miaka minne sasa ambapo dawa mbalimbali za mifugo zimekuwa zikiuzwa kwa gharama kubwa sana.
“Ili kukabiliana na changamoto hii tunaomba serikali ituletee dawa za mifugo zenye ruzuku ya serikali ili kupunguza hasara hiyo,” alisema Sokoroti.
Aidha alisema kuwa ni vyema serikali ikavitumia vyama vya wafugaji katika kuwapatia ruzuku ya dawa kwani kwa sasa wauzaji wa dawa hizo wanawauzia kwa gharama kubwa mno.
Kwa upande wake alisema kuwa kutokuwa na madawa ya ruzuku kumetokana na ufinyu wa bajeti toka halmashauri lakini mara bajeti itakapokuwa nzuri wataweka ruzuku kwenye dawa hizo.
Ridhiwani alisema kuwa changamoto kubwa ni ukosefu wa fedha ndiyo unachangia changamoto hiyo na kuwa serikali inafanyia kazi suala hilo.
Mwisho.  

 Na John Gagarini, Kibaha
IMEELEZWA kuwa mabaraza ya wafanyakazi katika sehemu za kazi ni vyombo muhimu katika kuongeza ufanisi wa kazi ikiwa ni pamoja kufanya maamuzi mbalimbali yanayohusu maslahi ya wafanyakazi taasisi na Taifa kwa ujumla.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki mjini Kibaha na mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo wakati akifungua mkutano wa Baraza la Wafanyakzi wa Ofisi ya Rais Tume ya Mipango.
Ndikilo alisema kuwa wajibu wa mabaraza haya kama vyombo vya ushauri na usimamizi ni kuhakikisha kuwa waajiri na watumishi wanatambua wajibu wao na haki zao na wanazingatia maadili ya utumishi wao ili kuleta matokeo makubwa ya utendaji kazi wenye tija, staha na upendo.
“Hata kama kutakuwa na sera, sheria na kanuni nzuri za kazi kama hakuna malenbgo ya pamoja na ushirikiano baina ya mwajiri na mwajiriwa ni vigumu taasisi hiyo kuwa na tija hivyo mabaraza yana wajibu wa kumshauri mwajiri ili kuleta tija na mashikamano wa pamoja,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa si vizuri kwa watumishi kutumia muda mwingi katika kudai maslahi mazuri zaidi kuliko kupima kiwango cha utekelezaji wa wajibu wao wa kazi hivyo viongozi  wa mabaraza wana wajibu wa kuwahimiza wafanyakazi kutimiza wajibu wao ili kufikia malengo.
“Nyie mmepewa majukumu makubwa kitaifa kama vile kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Taifa  na kufanya mapitio ya utekelezaji wa mpango wa maendeleo wa miaka mitano kuandaa mwongozo wa usimamizi wa utekelezaji wa umma na kukamilisha tafiti mbalimbali zinazoharakisha maendeleo ya uchumi wan chi yetu na mahitaji ya kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya maendeleo mwaka 2015,” alisema Ndikilo.
Kw upande wake mwenyekiti wa baraza hilo Florence Mwanri alisema kuwa tume imeendelea kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa fedha katika kutekeleza majukumu yake pamoja na kupata wataalamu wenye weledi.
Mwanri ambaye pia ni Naibu Katibu Mtendaji anayesimamia klasta ya huduma za jamii na idadi ya watu alisema kuwa katika kuhakikisha watumishi wanafanya kazi iapasavyo wamekuwa wakiwajengea uwezo kupitia mafunzo ya muda mrefu na mfupi ndani na nje ya nchi ili kuwaongezea ufanisi katika utendaji kazi wao.
Mwisho.     

Na John Gagarini, Kibaha
MKE wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Selina Koka anatarajia kuanzisha mfuko wa kutoa mikopo isiyokuwa na riba kwa wajasiriamali wa jimbo hilo utakaojulikana kama Chap Chap wa kuwasaidia waweze kuinua uchumi wao.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati wa mkutano na wajasiriamali wanawake ambao wamewezeshwa mafunzo ya utengenezaji wa bidhaa mbalimbali.
Selina alisema kuwa ameamua kufanya hivyo kwa lengo la kuwapunguzia mzigo wajasiriamali kwani taasisinyingi za kifedha zinaweka riba kubwa kwenye mikopo.
“Wajasiriamali wengi wanashindwa kuendeleza shughuli zao kutokana na riba kubwa wanazotozwa ambazo haziwezi kuwakomboa kiuchumi lakini mfuko huu utakuwa hauwatozi riba yoyote,” alisema Selina.
Alisema kuwa mkopo huo utaanzia kiasi cha shilingi 50 hadi 200,000 lakini lengo ni kwa wale wenye biashara ndogo kabisa.
“Tunatarajia kuwakopesha watu mmoja mmoja na vikundi kwa kupitia kwa mabalozi, wenyeviti wa mitaa na madiwani kwenye kata zote 11 za Kibaha Mjini bila ya kujali itikadi ya chama lengo ni kuwainua wajasiriamali,” alisema Selina.
Aidha alisema hadi sasa tayari hadi sasa wamevifikia vikundi 150 na kutumia gharama ya kiasi cha shilingi milioni 150.
Alibainisha kuwa mfuko huo unatrajia kuanza kukopesha kabla ya mwishoni mwa mwaka huu na kusema kwa sasa wako kwenye taratibu za kuandaa namna ya kutoa mikopo hiyo kisheria na kuwataka wale watakaokopeshwa wawe waaminifu katika kurejesha.
Kwa upande wake Mbunge huyo alisema kuwa anampongeza mkewe kwa kuweza kumsaidiaa katika kuwawezesha wajasiriamali hususani wanawake.
Koka alisema kuwa yeye kwa kushirikiana na mke wake watahakikisha malengo ya kuanzishwa mfuko huo yanafikiwa ili kuwakwamua wanakibaha.
Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha
VIONGOZI wa dini wametakiwa kuacha kujiingiza kwenye siasa badala yake wawahudumie waumini wao katika masuala ya kiroho.
Hayo yalisemwa na Mwangalizi mkuu wa Kituo cha Maandiko cha (PMC) kilichopo Kibaha mkoani Pwani, Mchungaji Gervase Masanja alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Mch Masanja alisema kuwa viongozi wa dini kazi yao kubwa ni kuwaelekeza mambo muhimu ya kumjua Mungu pamoja na kuishi kwa amani baina ya mtu na mtu na taifa kwa taifa.
“Viongozi wa dini tuna kazi kubwa kwani waumini wanahitaji huduma kubwa za kiroho hivyo haipendezi kujiingiza kwenye siasa na tudumishe amani iliyopo hapa nchini,” alisema Mch Masanja.
Alisema kuwa kazi ya siasa ni vema ikaendeshwa na wanasiasa wenyewe huku viongozi wa dini wakiwa ni wapatanishi na walinda amani ya nchi.
“Pia tusisahau kushiriki kwenye masuala makubwa yaliyopo mbele yetu yakiwemo kujiandikisha kwenye Daftari la wapiga kura, kura za maoni ya katiba inayopendekezwa na kushiriki kwenye uchaguzi mkuu mwezi Oktoba,” alisema Mch Masanja.
Aidha alisema anawaomba wakristo na wananchi kujitokeza kwa wingi katika upigaji wa kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na si kususia.
“Kuipigia kura katiba inayopendekezwa ni haki yako ya msingi hivyo mwananchi hupaswi kuisusia na kura utakayopiga ni siri yako lakini si vema kutopiga kura hiyo kwa mustakbali wan chi yetu,” alisema Mch Masanja.
Mwisho.
    














Wednesday, March 25, 2015

ABAKA WANAE KWA MIAKA MIWILI MFULULIZO

Na Mwandishi Wetu, Kibaha

MKAZI wa Miembe Saba wilayani Kibaha mkoani Pwani Said Kundum (52) anatuhumiwa kuwabaka watoto wake wawili wa kike kwa kipindi cha miaka miwili na kuwasababishia maumivu makali.

Akizungumza na waandishi wa habari mtoto mkubwa wa mtuhumiwa ambaye anasoma darasa la saba katika Shule ya Msingi ya Miembe Saba jina limehifadhiwa (15) alisema kuwa baba yake alikuwa akimbaka yeye na mdogo wake kwa nyakati tofauti.

Alisema kuwa baba yake alianza kumbaka tangu mwaka 2013 ambapo kwa kipindi chote hicho alipokuwa akiwafanyia vitendo hivyo aliwatishia kuwa atawaua endapo watasema kwa mtu yoyote.

“Baba alikuwa akitubaka kwa nyakati tofauti wakati mama akiwa anaenda sokoni Kariakoo kuuza mboga huku akituacha na baba nyumbani na kutufanyia vietendo hivyo mimi na mdogo wangu ambaye anasoma darasa la tatu shule ya Msingi Tandau akiwa na miaka (12),” alisema Mwanafunzi huyo.

Aidha alisema kuwa wakati wakifanyiwa vitendo hivyo walikuwa wakisikia maumivu makali lakini aliwaambia kuwa wajikaze kwani baadaye watazoea na hawata sikia tena maumivu.

“Tulivumilia kwa kipindi choete hicho lakini Jumamosi Machi 21 ilibidi ni mwambie mama na kusema potelea mbali liwalo na liwe kama ataniua basi lakini hatuwezi kuvumilia vitendo hivyo,” alisema mwanafunzi huyo.

Alibainisha baada ya kumwambia mama yao ilibidi atoe taarifa kwa viongozi wa serikali ya mtaa wa Miembe Saba ambao nao waliwataarifu polisi ambao walimkamata baba yake.

Naye mama mzazi wa watoto hao Rahima  Mshamu alisema kuwa yeye hakujua kinachoendelea kati ya mume wake na watoto wake kwani alikuwa akimuacha na watoto na hakutegemea kama angeweza kuwafanyia watoto wake vitendo hivyo vya ukatili.

Mshamu alisema tangu alipoona na mume wake amekuwa akifanya biashara ya kuuza mboga za majani ambazo huzikusanya nyakati za jioni hadi usiku kisha kuzipeleka sokoni Kariakoo Jijini Dar es Salaam.

“Mume wangu nilikuwa nikimuamini kama baba na sikutegemea kama angeweza kufanya hivyo na huwa nakusanya mboga kwenye maeneo mbalimbali huko mashambani majira ya saa 12 jioni baada ya hapo tunazisafirisha usiku kwenda Kariakoo ambapo kule huwa tunazifikisha usiku wa manane na ifikapo saa 11 alfajiri tunakuwa tumemaliza na tunaanza safari ya kurudi nyumbani,” alisema Mshamu.

Alisema kuwa hayo ndiyo maisha waliyokuwa wakiishi tangu walipohamia kutokea Kibamba mwaka 2012 ambapo kwa kiasi kikubwa yeye amekuwa akiiendesha familia hiyo kwani mume wake hana kazi maalumu.
“Roho inaniuma sana kwani nimekuwa nikihangaika kuhakikisha kuwa familia yangu haipati shida watoto wanakwenda shule na ana mtoto wake ambaye sijazaa naye yuko sekondari namlipia ada na michango mingine na mahitaji yote lakini mume wangu yeye haangaiki kwa chochote tukio hili limeniuma sana nashindwa hata kujizuia,” alisema huku akilia kwa uchungu.

Aidha alisema kuwa kutokana na kumpenda mume wake alimnunulia pikipiki kwa ajili ya kuongeza kipato cha familia lakini aliuza pikipiki hiyo jambo ambalo lilimfanya ashindwe kumwelewa kuwa ana tatizo gani lakini alishangazwa na afya za watoto wake kuumwa magonjwa UTI kila mara.

“Mimi na yeye hatukuwa na ugomvi wowote ambapo hivi karibuni alijaribu kuuza sehemu ya eneo letu na nilipomuuliza alikataa hadi yule mnunuzi alipokuja na kutaka kumalizia fedha zilizobaki ndipo niligundua kuwa aliuza eneo hilo kwa nguvu bila ridhaa yangu na kusema kuwa aliwabaka watoto kuwa tuna ugomvi wa eneo hilo si kweli kwani suala la eneo ni la mwezi Machi huku yeye akiwabaka watoto miaka miwili iliyopita,” alisema Mshamu.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa huo Hamis Shomary alisema kuwa baada ya kumhoji mtuhumiwa alikiri kufanya matukio hayo na kusema kuwa aliamua kufanya hivyo kutokana na ugomvi aliokuwa nao na mke wake na kuwa alikuwa akimnyima unyumba.

Shomary alisema kuwa mtuhumiwa alifikishwa polisi kwenye kituo cha Kongowe ambako anashikiliwa kwa hatua zaidi za kisheria ikiwa ni pamoja na kusubiri kupelekwa mahakamani.

Mwalimu mkuu wa shule ya Miembe Saba anayosoma mwanafunzi huyo Rajab Chalamila alisema kuwa mwanafunzi huyo alikuwa anaonekana mnyonge na mawazo mengi.

Chalamila alisema kuwa kutokana na hali ya mwanafunzi huyo alimwita baba mzazi zaidi ya mara mbili na kumwambia kuwa ampeleke hospitali mwanae na alisema alimpeleka na kukutwa na malaria lakini hali bado ilikuwa inajirudia na kuonekana kuwa ameathirika kisaikolojia. Jeshi la polisi limethibitisha kutokea kwa tukio hilo.  


Mwisho.

Wednesday, March 18, 2015

RIDHIWANI AENDELEA NA ZIARA JIMBONI CHALINZE

Mbunge wa Chalinze Ridhiwani Kikwete kwenye kijiji cha Mkange wakati wa ziara yake kutembelea shughuli za maendeleo, kushoto ni katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo na kulia mwenyekiti wa Kijiji hicho Said Mgaya. 

Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani akiweka udongo kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya cha Kijiji cha Mkange wakati wa ziara yake kutembelea jimbo hilo kuona shughuli za maendeleo. 

Katibu wa chama cha mapinduzi CCM wilaya ya Bagamoyo Kombo Kamote akizungumza na wajumbe wa halmashauri ya Kijiji cha Matipwili juu ya uwajibijaki kwa wananchi wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete jimboni humo. 

 Baadhi ya Wazee wa Kijiji cha Matipwili wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete hayupo pichani alipokuwa akiwahutubia wakazi hao kwenye mkutano wa hadhara wakati wa ziara ya kutembelea shughuli za maendeleo jimboni humo.

Baadhi ya akina mama wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete hayupo pichani  alipokuwa akiwahutubia wakazi wa Kijiji cha Matipwili wakati wa ziara yake ya kutembelea shughuli za maendeleo kwenye jimbo hilo.

 Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya Matipwli wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alipotembelea shule hiyo wakati wa ziara yake jimbo humo kuangalia shughuli za maendeleo

Mzee Halfana Mgobanya wa kijiji cha Gongo akichota maji ya mvua kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kijiji hicho ni moja ya vijiji vya jimbo hilo vinavyokabiliwa na tatizo la uhaba wa maji.

 Baadhi ya akinamama wa kijiji cha Mkange wakiwa wanachota maji huku kukiwa na foleni kubwa ya madumu ya maji eneo hilo nalo linakabilia na tatizo la maji ambayo yamekuwa yakitoka mara chache.


 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akifyetua tofali wakati akiwa kwenye ziara ya kukagua shughuli za maendeleo kwenye jimbo hilo