Monday, January 26, 2015

HALMASHAURI YA MJI KUJENGA SOKO NA STENDI VYA KISASA

Na John Gagarini, Kibaha
HALMASHAURI ya Mji wa Kibaha inatarajia kuanza mradi mkubwa wa ujenzi wa Soko la kisasa pamoja na Stendi utakaogharimu kiasi zaidi ya shilingi bilioni 20 kuanzia Februari mwaka huu.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Adhu Mkomambo alipozungumza na mwandishi wa habari hizi na kusema kuwa taratibu za mwisho zinakamilika kuanza ujenzi huo.
Mkomambo alisema kuwa ujenzi huo wa soko na setndi vitakuwa mkombozi kwa wananchi wa Kibaha na mkoa mzima wa Pwani kutokana na kukosa vitu hivyo kwa muda mrefu.
“Pale kuna soko na stendi lakini havina hadhi ya Mji hivyo kupitia benki ya uwekezaji (TIB) tutajenga vitu hivi kwa lengo la kuboresha mji na kuleta maendeleo kwa wananchi wa wilaya ya Kibaha,” alisema Mkomambo.
Aidha alisema kuwa vitu hivyo ni moja ya vyanzo vya mapato ya Halmashauri hivyo ujenzi wake utazingatia ubora na viwango ili kuwa na hadhi kwani soko lililopo halina ubora kulingana na mji wa Kibaha
“Mbali ya miradi hiyo ambayo itaanza kwa pamoja pia Halmashauri itaendelea na miradi yake ya ujenzi wa barabara na uboreshaji wa sekta mbalimbali za jamii ili huduma ziweze kuwa bora,” alisema Mkomambo.
Alibainisha kuwa wataendeleza ushirikiano kati ya Halmashauri yake wananchi pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kuendelea kuuboresha mji huo unaoelekea kuwa Manispaa.
Mwisho.  




  

Friday, January 23, 2015

ASKARI ALIYEUAWA AAGWA

Na John Gagarini, Kibaha
KONSTEBO wa Polisi aliyeuwawa na majambazi waliovamia kituo cha Polisi cha Ikwiriri wilayani Rufiji mkoani Pwani Judith Timoth (32) juzi aliagwa mjini Kibaha na mamia ya watu wakiwemo askari wenzake aliowahi kufanya nao kazi kabla ya kuhamia Rufiji.
Mwili huo uliagwa kwenye hospitali ya Polisi mkoa na kuongozwa na ofisa wa jeshi hilo Thabita Makaranga, kwa safari ya kuelekea mkoani Mbeya kwa ajili ya mazishi  na kuliibua simanzi kubwa kwa watu waliohudhuria tukio hilo na kuvuta hisia na vilio kutoka kwa waombolezaji.
Akiongoza kwenye ibaada ya kumwaga marehemu mwinjilisti wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Maili Moja alikokuwa akisali kabla ya kuhamia wilayani Rufiji, Josephine Urio alisema kuwa watu wanapaswa kujiandaa kwa kusali muda wote kwani hawajui siku wala wakati watatwaliwa.
“Wanadamu wanapaswa kuacha roho za mauaji kama hao waliofanya mauaji hayo kwani hawako salama kama wanavofikiri Mungu atawapa pigo kama walivyotoa roho za watu wasiokuwa na hatia na watu wenye uovu waache njia hizo,” alisema Urio.
Akisoma wasifu wa marehemu moja ya wafanyakazi wenzake Robert Munisi alisema kuwa jeshi hilo litapambana na watu wote waliohusika na tukio hilo na kuliomba kanisa lilisaidie polisi kukabiliana na wahalifu hao na watasimamia amri kumi za Mungu.
Munisi alisema marehemu alizaliwa mkoani Mbeya na kupata elimu ya Msingi na Sekondari na kupata mafunzo ya sheria mkoani Mbeya kisha kujiunga na Chuo cha Mafunzo ya Polisi huko Moshi kuanzia Oktoba 30 mwaka 2004 na kuhitimu Fabruari 25 mwaka 2005 pia alipata mafunzo mbalimbali yakiwemo ya Upelelezi.
Aidha amesema marehemu kabla ya umauti alikuwa akisoma masomo ya Sociology mwaka wa pili Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) ameacha mtoto mmoja wa kiume aitwaye Bryan.Marehemu alivamiwa juzi akiwa kazini na mwenzake majira ya saa 8 usiku na kushambuliwa na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi waliokuwa na silaha na kufariki dunia yeye na mwenzake Koplo Edger Milinga.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAZAZI wa shule ya Msingi Juhudi kata ya Visiga wilayani Kibaha wameulalamikia uongozi wa shule hiyo kwa kuwarudisha watoto wao wanaojiunga darasa la kwanza kwa kushindwa kulipa kiasi cha shilingi 15,000 kwa ajili ya kuwaandikisha.
Moja ya wazazi hao Mabeka Mabeka akizungumza kwenye kikao cha wazazi alisema kuwa wanashangazwa na taratibu za kuwatoza kiasi hicho licha ya kuwa serikali imekataza michango hiyo na kusababisha wazazi kuwa kwenye wakati mgumu kupata fedha hizo.
Mabeka alisema kuwa wanaushangaa uongozi wa shule hiyo kwa  kuwaandikisha wanafunzi wa darasa la kwanza kwa kututoza fedha hizo jambo ambalo ni kinyume cha sheria kwani serikali ilitamka kuondoa michango kwa wanafunzi wanaoanza ili kuondoa kero kwa wazazi.
“Michango hii ni kikwazo kwa wazazi kuwapeleka watoto shule huku serikali ikitaka watoto wote waliofikia umri wa kwenda shule waandikishwe ili waweze kupata elimu ya msingi,” alisema Mabeka.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo Theobad Rwegalulila alikiri kuwepo kwa jambo hilo na kusema kuwa limekuwa changamoto kubwa kwa wazazi ambao wamekuwa wakilalamika kupinga malipo hayo ili watoto waweze kupata fursa ya kujiunga na darasa la kwanza.
Naye mwalimu mkuu wa shule hiyo Hawa Mgogolo alikiri kuwepo kwa michango hiyo na kusema kuwa walikubaliana na wazazi kwenye kikao cha wazazi mwaka 2012 lakini anashangaa wazazi hao kuanza kulalamika wakati wao wenyewe walikubali mchango huo.
Mgololo alisema kuwa ni kweli walikuwa wakiwatoza fedha hizo kwa ajili ya matumizi mbalimbali na fedha hizo zinatumika kununulia vitu mbalimbali kama vile chaki, madaftari ya maendeleo na vifaa mbalimbali kwa ajili ya wanafunzi hao.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SHULE ya Msingi ya Maili Moja iliyopo wilayani Kibaha inakabiliwa na ubovu wa madarasa ambayo yanaweza kuanguka wakati wowote hali ambayo inahatarisha usalama wa wanafunzi na walimu kwenye shule hiyo.
Kutokana na ubovu huo madarasa matano kati ya 11 ndiyo yanayotumika ambapo wanafunzi wanasoma zaidi ya wanafunzi 150 hadi 200 kwenye darasa moja.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kikoa cha dharura cha wazazi kuzungumzia ubovu wa madarasa hayo, mwalimu mkuu wa shule hiyo Reginald Fanuel alisema kuwa madarasa hayo yamebomoka vibaya.
“Madarasa hayo yako kwenye hali mbaya na wakati wowote yanaweza kuanguka na kusababisha maafa kwa wanafunzi na walimu endapo hazitachukuliwa hatua za haraka za kunusuru hali hiyo ambayo sasa imefikia hatu mbaya,” alisema Fanuel.
Fanuel alisema kuwa kutokana na hali hiyo wanaomba msaada wa kusaidiwa ujenzi ili kunusuru hali hiyo ambayo ni hatari kwa wanafunzi na walimu wanaotumia madarasa hayo pia mlundikano kwenye madarasa mazima ni mkubwa sana.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya shule Said Chitenje alisema kuwa tatizo hilo lilianza muda mrefu ambapo wamekuwa wakiakabiliana na hali hiyo kwa kuchangisha michango wazazi lakini michango imekuwa ikisusua.
“Kweli hali ni mbaya na kutokanana hali kuzidi kuwa mbaya tumekubaliana na wazazi kuwa kila mzazi ambaye ana mwanafunzi shuleni hapa atoe kiasi cha shilingi 5,000 kwa ajili ya kufanya ujenzi wa madarasa hayo,” alisema Chitenje.
Naye diwani wa kata ya Maili Moja Andrew Lugano alisema kuwa kwa sasa wanaendelea na mchakato wa kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya ujenzi wa madarasa hayo yaliyoharibika ili kuwanusuru wanafunzi hao.
Lugano alisema kuwa wazazi hao waliomba wakutane na mkurugenzi wa halmashauri ya Mji ili wazungumzie suala hilo na namna ya kuwez akukabiliana na tatizo hilo na kuwaomba watu na wafadhilimbalimbali kujitokeza kusaidia ujenzi wa majengo hayo.

Mwisho.  

Wednesday, January 21, 2015

MAJAMBAZI YAUA ASKARI WAWILI

Na John Gagarini, Kibaha

ASKARI wawili wa Jeshi la Polisi Kituo cha Ikwiriri wilayani Rufiji mkoani Pwani wamekufa baada ya watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kuwashambulia kwa silaha baada ya kuvamia kituo hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari kwa njia ya simu toka eneo la tukio Ikwiri wilayani Rufiji Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alisema kuwa majambazi hao walitumia silha kuwaua askari hao.

Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 8 kwenye kituo hicho cha Polisi cha Ikwiriri. Aliwataja askari waliokufa kuwa ni usiku Askari waliokufa ni namba E 8732 CPL Edger Milinga na WP 5558 PC Judith Timoth.

Alisema kuwa licha ya kufanya mauaji hayo pia walifanikiwa kupora silaha aina mbalimbali zikiwemo SMG 2, SAR 3, Ant Riot 1, mali ya serikali na S/Gun Protector mali ya kampuni ya Sigara Tanzania.

Aidha alisema kuwa pia watu hao waliharibu kwa kulipiga risasi gari la polisi la kituo  hicho lenye namba za usajili PT 1965.


Mwisho.

Wednesday, January 14, 2015

MRADI WAMI CHALINZE KUNUFAISHA 271,000

Na John Gagarini, Chalinze

MRADI wa Maji wa Wami Chalinze awamu ya tatu  mara utakapokamilika unaratajia kuwafikia wananchi 271,000 wa Jimbo la Chalinze wilaya ya Bagamoyo mkoa wa Pwani.

 Aidha mradi huo wenye thamani ya shilingi bilioni 60 unatarajia kuanza mwezi Machi mwaka huu utapunguza tatizo la upatikanaji wa maji kwa wakazi wa Chalinze ambao wanahudumiwa na mradi huo.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Meneja wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) Mhandisi Christer Mchomba alisema katika awamu hiyo itaongeza mitandao ya maji kwenye vitongoji 210 kutoka kwenye vijiji 47 ambavyo vilifikiwa kwenye utekelezaji wa awamu ya pili iliyoanza mwaka 2008.

 “Katika awamu ya tatu ya mradi huu yatajengwa pia matenki ya kuhifadhia maji kwenye vijiji 20 vya awamu ya kwanza kikiwamo kijiji cha Bwiringu, Msata, Lugoba, Msoga, Mandela na vingine ambavyo havikujengewa matenki,” alisema Mhandisi Mchomba.

Mhandisi Mchomba alisema kwa sasa awamu ya pili ,wizara inakamilisha ujenzi wa nyongeza ya chujio la maji ambalo litaongeza wingi wa maji yanayosafishwa na kuzalishwa.

Alisema kuwa watajenga tanki kubwa eneo la Mazizi lenye uwezo wa kuhifadhi maji yenye ujazo wa lita 200,000 pamoja na vituo vya maji kwenye vijiji na vitongoji vyote kwenye Jimbo hilo.

“Kwa sasa wanazalisha maji kwa asilimia 85 tu kutokana na mashine kushindwa kufanya kazi kikamilifu ambapo kwa siku ni mita za ujazo 2,000 badala ya 5,000 kwa siku,” alisema Mhandisi Mchomba.  

Kwa upande wake ofisa maabara wa mradi huo Riziki Kacheche alisema  kuwa maji ghafi yanapokuwa machafu zaidi tope huziba na kuzuia maji kuchukuliwa katika kiwango kinachotakiwa kwenda kusafishwa na hivyo kusabababisha uwezo wa kuzalisha maji na kuyasafisha kuwa mdogo.

Mwisho

Tuesday, January 13, 2015

VIONGOZI WA SERIKALI ZA MITAA NA VIJIJI WAASWA NA WANANCHI WAHAKIKISHIWA KUPATA UMEME


 Na John Gagarini, Bagamoyo
VIONGOZI wa serikali za mitaa na vijiji wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani waliochaguliwa hivi karibuni wametakiwa kusoma mapato na matumizi ili kuepuka kuenguliwa kwenye nafasi zao kama baadhi yao waliopita kukataliwa na wananchi.
Moja ya changamoto zilizosababisha viongozi hao waliopita baadhi yao walienguliwa na wananchi huku wengine wakishindwa kurudishwa kwenye kura za kuteuliwa kuwani uongozi kwenye uchaguzi uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana.
Hayo yalisemwa Bagamoyo na katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kombo Kamoto alipozungumza na wananchi wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo Ridhiwani Kikwete kwenye  vijiji vya kata za Kibindu, Mbwewe, Mdaula, Bwiringu, Fukayosi, Miono na Kiwangwa.
Kamote alisema kuwa viongozi hao waliochaguliwa na wananchi hasa wale wanaotoka chama hicho kwani hawana budi kuwatumikia wananchi ipasavyo kwa lengo la kuwatatulia changamoto ambazo zinawakabili katika nyanja mbalimbali kwenye huduma za kijamii.
“Mmechaguliwa na wananchi kwa heshima ya chama chetu, hususani kusoma mapato na matumizi hivyo niwasihi mchape kazi kama sheria na taratibu zinavyowaongoza, sitopenda kusikia wananchi wakilalamikia kuhusu utendaji wenu, mtambue mwaka huu mmeapishwa na mahakimu tofauti na miaka yote, hivyo yeyote atayekiuka kiapo hicho ataondolewa kwenye nafasi yake,” alisema Kamote.
Alisema kuwa viongozi hao watatakiwa kuitisha mikutano na kusoma mapato na matumizi kwa wananchi ili waweze kujua yanayofanyika kwenye maeneo yao.
Viongozi hao pia waliaswa kutokuwa madalali wa kuuza ardhi kiholela na kuwakandamiza wananchi ambao wakati mwingine hawajui haki zao za msingi.
“Baadhi waliondolewa kutokana na kushindwa kuitisha mikutano ikiwa ni pamoja na kushindwa kusoma mapato na matumizi hali iliyowafanya waondolewa madarakani au kushindwa kwenye uteuzi wa kuwania nafasi hizo, alisema Kamote.
Aidha alisema kuwa inashangaza kuona baadhi ya viongozi wanakuwa vinara wa kuuza maeneo na kama yupo kiongozi aliyekuwa anafanya hivyo wanapaswa kuacha na kuwa waadilifu ili kulinda nafasi walizopata.
“Viongozi huu si muda wa kuanza majigambo ama kujivunia nafasi mlizoshika  bali mnatakiwa kutimiza wajibu wenu kwa kusimamia ilani ya chama cha mapinduzi ili kuleta maendeleo kwa wananchi,” alisema Kamote.
Kwa upande wake Ridhiwani Kikwete aliwaomba viongozi hao kufanya kazi kwa bidii ili chama kiendelee kuaminika na kushika dola .
“Fanyeni kazi bila kubagua watu ,watumikieni pasipo kujali itikadi za kisiasa na hiyo ndio sifa pekee ya kiongozi wa sasa asiyejali udini,ukabila wala chama alichopo,”alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alisema kuwa yeye akiwa mbunge ataendelea kuwatumika ipasavyo katika kuwaondolea changamoto zinazowakabili.
mwisho.
Na John Gagarini,Chalinze
KILIO cha baadhi ya wananchi wa Jimbo la Chalinze kukosa umeme huenda kikaisha baada ya kuhakikishiwa kuwa watapata huduma hiyo kuanzia m,waka huu kupitia miradi ya umeme vijijini kupitia wakala wa umeme Vijijini (REA).
Changamoto hiyo itapungua kwenye maeneo mbalimbali ya Jimbo hilo katika vijiji ambavyo vipo kwenye awamu ya awamu ya tatu inayotarajiwa kuanza mwezi Juni mwaka huu kupitia miradi hiyo ya REA.
Akiwahutubia wananchi wa vijiji vya Kibindu, Mbwewe, Mdaula, Bwilingu, Fukayosi, Kiwangwa na Chalinze mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa serikali ya CCM imejipanga kuikabilia changamoto hiyo.
“Kila maeneo niliyopita nimekutana na malalamiko  kutoka kwa wananchi juu ya kukosa umeme wakati vijiji vingine vya kata hizo vikiwa vimepata umeme na kuhoji huku wao wakiona kwa macho umeme umepita juu na kwenda maeneo jirani,” alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alise kuwa anatambua umuhimu wa umeme hivyo amekuwa akifanya jitihada za kufuatilia na ndio maana amelazimika kufuatana na meneja wa miradi ya umemem mkoani Pwani Leo Mwakatobe ambaye anatolea ufafanuzi suala hilo.
“Mfano eneo la Kiwangwa halikuwepo katika umeme unaosambazwa na REA lakini baada ya kufanya juhudi hizo fedha zimepatikana hivyo utakuwa wa REA ambapo tanesco imetoa sh.milioni 420 na REA sh.milioni 800,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisema kuwa fedha hizo tayari ziko na kazi ya kuanza kusambaza umeme itaanza wakati wowote, kwani anajua umuhimu wa umeme lakini wananchi na kuwaomba wananchi wafahamu juhudi za serikali.
Kwa upande wake  mhandisi wa Tanesco mkoa wa Pwani, Mhandisi Leo Mwakatobe, alisema wanaendelea kumalizia utekelezaji wa awamu ya pili wa mradi wa REA na kazi iliyobaki ni mkandarasi kuanza kazi wakati wowote kuanzia mwezi huu.
Mwakatobe fedha kwa ajili ya mradi wa kusambaza umeme zimepatikana, hivyo wananchi wenye kuhitaji waanze kuchukua fomu.kinachotakiwa wawe na picha mbili na kitambulisho cha aina yoyote.
Mwisho




Monday, January 12, 2015

CHALIWASA YAKANUSHA MASHINE KUUZWA KENYA NA MAGAREZA YAPONGEZWA

Na John Gagarini, Wami
MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) imekanusha uvumi kuwa mashine za uzalishaji wa maji zimeuzwa nchini Kenya hali ambayo imesababisha maji kukatika mwezi mzima.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake    Meneja wa mamlaka hiyo Injinia Christer Mchomba alisema kuwa uvumi huo si wa kweli kwani mashine zote zipo na zinatumika kama kawaida.
Injinia Mchomba alisema kuwa uvumi huo umekuja kutokana na maji kutokutoka kwa sababu ya mashine hizo kuvuta uchafu ambao umesababisha kuziba na kushindwa kupitisha maji.
“Tatizo la maji kushindwa kutoka hakutokani na mashine kuuzwa bali ni kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha kwenye mkoa wa Morogoro ambapo ndiyo chanzo cha mto Wami na kusababisha uchafu kuwa mwingi na mashine kuziba na kuharibika hivyo maji kushindwa kutoka,” alisema Injinia Mchomba.
Alisema kuwa tatizo ni tekeo ambapo kwa sasa linawekwa ambalo likikamilika litasaidia kuchuja uchafu tofauti na ilivyokuwa mwanzo kwani maji zamani yalikuwa masafi na yalikuwa hayana uchafu.
“Uchafu huo unatokana na uharibifu mkubwa wa mazingira unaofanywa na watu wanaojihusisha na uchimbaji wa madini, kuingiza mifugo kwenye vyanzo vya maji na uchafuzi wa mazingira hivyo kusababisha uchafu mwingi kuja na maji,” alisema Injinia Mchomba.
Alisema kuwa ukarabati wa mashine hizo unaendelea ambapo umefikia asilimia 85 na baada ya miezi miwili au mitatu tatizo la ukosefu wa maji Chalinze litakuwa ni historia
“Tuna mitambo 30 na mingine mipya hata hatujaifungua iweje watu waseme kuwa imeuzwa wakitaka ukweli waje hapa ili waione kuliko kusema tu bila ya kujua ukweli na waache kuvumisha vitu ambavyo havina ukweli,” alisema Injinia Mchomba.
Aidha alisema kuwa kwa sasa kuna mradi unaotekelezwa ambao utavifikia vitongoji vyote vya Jimbo la Chalinze ambapo awamu ya tatu utatumia bilioni 60 hadi kukamilika.
Mwisho.   
Na John Gagarini, Ubena
MBUNGE wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete amelipongeza Jeshi la Magereza mkoani Pwani kwa ujenzi wa madarasa mawili ya shule ya Sekondari ya Bwawani kwa gharama nafuu.
Aliyasema hayo wakati akizindua madarasa hayo kwa ajili ya wanafunzi wa kutwa wa shule hiyo ambayo inamilikiwa na Jeshi hilo la Magereza eno la Ubena.
Ridhiwani alisema kuwa Jeshi hilo limeonyesha uzalendo wa hali ya juu na kutumia vizuri rasilimali fedha kwa kujenga madarasa hayo yenye mawili thamani ya shilingi milioni 31.8.
“Haya ndiyo mambo tunayoyataka kwa kufanya ujenzi wa vitu vya umma kwa matumizi mazuri ya fedha na ujenzi bora hivyo taasisi nyingine za serikali zinapaswa kuzingatia ujenzi kama huu,” alisema Ridhiwani.
Alisema baadhi ya taasisi za umma zimekuwa zikifanya ujenzi wa kawaida kwa gharama kubwa huku ukiwa haujazingatia ubora wa ujenzi wa majengo ambayo hutumiwa kwa muda mrefu.
Aidha alizitaka halmashauri kuwatumia wataalamu wa Magereza katika ujenzi wa majengo mbalimbali ambapo ujenzi wao unazingatia ubora matumizi bora ya rasilimali fedha.
Awali akimkaribisha mbunge huyo mkuu wa Magereza mkoa wa Morogoro  Kato Lugainunula ambaye alimwakilisha mkuu wa Magereza nchini John Minja, alisema kuwa lengo la Magereza ni kuihudumia jamii katika nyanja mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoaji wa elimu.
Lugainunula alisema kuwa awali shule hiyo ilitumika kutoa elimu ya sekondari kwa watumishi wa Magereza ambao walikuwa hawajapata elimu ya sekondari lakini waliondoa utaratibu huo na kutoa elimu kwa wanafunzi kutoka sehemu mbalimbali.
Naye kaimu mkuu wa shule hiyo ya Bwawani Emanuel Lwinga alisema kuwa madarasa hayo ni kwa ajili ya wanafunzi wa kutwa ujenzi wake ulitumia muda wa miezi mitano hadi kukamilika kwake.
Lwainga alisema kuwa kila darasa lina uwezo wa kuchukua wanafunzi kati ya 40 na 45 ambapo shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 396 wakiwemo wale wa kidato cha tano na shule hiyo ni moja ya shule zinazofanya vizuri kwenye matokeo ya kidato cha nne kimkoa.

  Mwisho.