Monday, January 12, 2015

CHALIWASA YAKANUSHA MASHINE KUUZWA KENYA NA MAGAREZA YAPONGEZWA

Na John Gagarini, Wami
MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) imekanusha uvumi kuwa mashine za uzalishaji wa maji zimeuzwa nchini Kenya hali ambayo imesababisha maji kukatika mwezi mzima.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake    Meneja wa mamlaka hiyo Injinia Christer Mchomba alisema kuwa uvumi huo si wa kweli kwani mashine zote zipo na zinatumika kama kawaida.
Injinia Mchomba alisema kuwa uvumi huo umekuja kutokana na maji kutokutoka kwa sababu ya mashine hizo kuvuta uchafu ambao umesababisha kuziba na kushindwa kupitisha maji.
“Tatizo la maji kushindwa kutoka hakutokani na mashine kuuzwa bali ni kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha kwenye mkoa wa Morogoro ambapo ndiyo chanzo cha mto Wami na kusababisha uchafu kuwa mwingi na mashine kuziba na kuharibika hivyo maji kushindwa kutoka,” alisema Injinia Mchomba.
Alisema kuwa tatizo ni tekeo ambapo kwa sasa linawekwa ambalo likikamilika litasaidia kuchuja uchafu tofauti na ilivyokuwa mwanzo kwani maji zamani yalikuwa masafi na yalikuwa hayana uchafu.
“Uchafu huo unatokana na uharibifu mkubwa wa mazingira unaofanywa na watu wanaojihusisha na uchimbaji wa madini, kuingiza mifugo kwenye vyanzo vya maji na uchafuzi wa mazingira hivyo kusababisha uchafu mwingi kuja na maji,” alisema Injinia Mchomba.
Alisema kuwa ukarabati wa mashine hizo unaendelea ambapo umefikia asilimia 85 na baada ya miezi miwili au mitatu tatizo la ukosefu wa maji Chalinze litakuwa ni historia
“Tuna mitambo 30 na mingine mipya hata hatujaifungua iweje watu waseme kuwa imeuzwa wakitaka ukweli waje hapa ili waione kuliko kusema tu bila ya kujua ukweli na waache kuvumisha vitu ambavyo havina ukweli,” alisema Injinia Mchomba.
Aidha alisema kuwa kwa sasa kuna mradi unaotekelezwa ambao utavifikia vitongoji vyote vya Jimbo la Chalinze ambapo awamu ya tatu utatumia bilioni 60 hadi kukamilika.
Mwisho.   
Na John Gagarini, Ubena
MBUNGE wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete amelipongeza Jeshi la Magereza mkoani Pwani kwa ujenzi wa madarasa mawili ya shule ya Sekondari ya Bwawani kwa gharama nafuu.
Aliyasema hayo wakati akizindua madarasa hayo kwa ajili ya wanafunzi wa kutwa wa shule hiyo ambayo inamilikiwa na Jeshi hilo la Magereza eno la Ubena.
Ridhiwani alisema kuwa Jeshi hilo limeonyesha uzalendo wa hali ya juu na kutumia vizuri rasilimali fedha kwa kujenga madarasa hayo yenye mawili thamani ya shilingi milioni 31.8.
“Haya ndiyo mambo tunayoyataka kwa kufanya ujenzi wa vitu vya umma kwa matumizi mazuri ya fedha na ujenzi bora hivyo taasisi nyingine za serikali zinapaswa kuzingatia ujenzi kama huu,” alisema Ridhiwani.
Alisema baadhi ya taasisi za umma zimekuwa zikifanya ujenzi wa kawaida kwa gharama kubwa huku ukiwa haujazingatia ubora wa ujenzi wa majengo ambayo hutumiwa kwa muda mrefu.
Aidha alizitaka halmashauri kuwatumia wataalamu wa Magereza katika ujenzi wa majengo mbalimbali ambapo ujenzi wao unazingatia ubora matumizi bora ya rasilimali fedha.
Awali akimkaribisha mbunge huyo mkuu wa Magereza mkoa wa Morogoro  Kato Lugainunula ambaye alimwakilisha mkuu wa Magereza nchini John Minja, alisema kuwa lengo la Magereza ni kuihudumia jamii katika nyanja mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoaji wa elimu.
Lugainunula alisema kuwa awali shule hiyo ilitumika kutoa elimu ya sekondari kwa watumishi wa Magereza ambao walikuwa hawajapata elimu ya sekondari lakini waliondoa utaratibu huo na kutoa elimu kwa wanafunzi kutoka sehemu mbalimbali.
Naye kaimu mkuu wa shule hiyo ya Bwawani Emanuel Lwinga alisema kuwa madarasa hayo ni kwa ajili ya wanafunzi wa kutwa ujenzi wake ulitumia muda wa miezi mitano hadi kukamilika kwake.
Lwainga alisema kuwa kila darasa lina uwezo wa kuchukua wanafunzi kati ya 40 na 45 ambapo shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 396 wakiwemo wale wa kidato cha tano na shule hiyo ni moja ya shule zinazofanya vizuri kwenye matokeo ya kidato cha nne kimkoa.

  Mwisho.

No comments:

Post a Comment