Monday, January 5, 2015

MCHAKATO WA MAMLAKA YA MJI MDOGO CHALINZE CHANGAMOTO KUBWA, MAJAMBAZI WATUMIA MSITU WA MWIDU

Na John Gagarini, Ubena
MCHAKATO wa kuifanya Chalinze kuwa mamlaka ya Mji Mdogo umekumbwa na changamoto kubwa baada ya makundi mawili ya wakulima na wafugaji kupinga mpango huo.
Makundi hayo ambayo ndiyo makubwa katika Jimbo la Chalinze yameonekana kutoupokea mpango huo kwa madai kuwa utawasababisha kushindwa kufanya shughuli za ambazo ndizo zinazowafanya waweze kuishi.
Changamoto za kupinga mchakato huo zimebainika wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete kutembelea shughuli za maendeleo.
Akizungumzia changamoto hizo Ridhiwani alisema Jimbo hilo lilitenga maeneo kwa ajili ya wafugaji na wakulima katika mpango bora wa matumizi ya ardhi ambapo kila kundi linakaa kwenye eneo lake.
“Changamoto hizi zinakuja kutokana na hali halisi kuwa endapo mamlaka hiyo itakubalika ina maana kutakuwa na sheria ya kuzuia ufugaji wa mifugo pamoja na kuzuia kilimo huku makundi hayo yakitegemea shughuli hizo kuendeshea maisha yao,” alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alitoa mfano kwenye maeneo ya wafugaji ya Vijiji vya Chamakweza ambao wana mifugo zaidi ya 18,000, Lukenge wana mifugo zaidi ya 10,000 na Matuli mifugo zaidi ya 8,000.
“Wafugaji wamesema kuwa endapo Mamlaka hiyo itapitishwa mifugo yao wataipeleka wapi na wao ufugaji ndiyo maisha yao kwa ajili ya chakula pamoja na uchumi,” alisema Ridhiwani.
Alisema pia kwa wakulima nao hawataruhusiwa kulima je wataishije wakati kilimo ndiyo shughuli yao ya kuendeshea maisha yao ikiwa ni pamoja na uchumi wao na hawana kitu kingine wanachoweza kukifanya.
“Changamoto hizi katika kueleka Mji Mdogo zimekuwa ni kubwa na ukiangalia zina uzito hivyo mchakato huu umesitishwa huku serikali ikiwa inaangalia namna bora ya kufanya ili kutoathiri maisha ya wananchi,” alisema Ridhiwani.
Aliongeza hata hivyo wananchi wanapaswa kujiandaa na mabadiliko kwani kila jambo lina wakati wake ambapo mipango kama hiyo ina lengo la kuwasogezea huduma karibu wananchi.
Mwisho.
Na John Gagarini, Ubena
WANANCHI wa Kata ya Ubena Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani wameuomba uongozi wa Gereza la Ubena kuwaruhusu kulitumia eneo la pori la Mwidu kwenye barabara ya Morogoro Chalinze ambalo limekuwa likitumiwa na majambazi kujificha kwa ajili ya kuteka magari nyakati za usiku.
Ombi hilo lilitolewa na diwani wa kata hiyo Mrisho Choka mbele ya Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete ambaye yuko kwenye ziara kutembelea Jimbo hilo kukagua shughuli za maendeleo.
Choka alisema kuwa kuwa pori hilo limekuwa likitumiwa na majambazi ambao hujificha kisha kutega magogo barabarani na kusababisha ajali kisha kufanya uhalifu kwa kutumia silaha mbalimbali.
“Eneo hili limekuwa hatarishi kwa magari hasa nyakati za usiku ambapo kumekuwa na matukio mengi ya utekwaji wa magari ambayo kabla ya kutekwa husababishiwa ajali kwa kuwekewa magogo hivyo tunauomba uongozi wa gereza kuturuhusu tutumie eneo hilo ili kuzuia vitendo hivyo,” alisema Choka.
Alisema kuwa endapo wananchi watalitumia eneo hilo itasaidia kupunguza vitendo hivyo kwani kwa ambapo kwa sasa majambazi hao wanafanya wanavyotaka kutokana na eneo hilo kuwa pori.
Aidha alisema kuwa wiki iliyopita magari manne yalitekwa na katika kukabiliana na uhalifu katika eneo hilo wamekuwa wakifanya doria na askari polisi lakini hata hivyo majambazi hao wamekuwa wakiwategea na kutekeleza uhalifu.
Kwa upande wake Ridhiwani Kikwete alisema kuwa ombi lao atalipeleka kwenye vyombo husika ili lifanyiwe kazi ili kuondokana na vitendo hivyo ambavyo vimekithiri katika eneo hilo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment