Tuesday, January 27, 2015

ZAKIA MEGHJI SHEREHE ZA CCM PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MLEZI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Pwani Zakia Meghji anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye sherehe za (CCM) kutimiza miaka 38 zitakazofanyika Kata ya Visiga wilayani Kibaha.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana mjini Kibaha katibu wa CCM Kibaha Mjini Abdala Mdimu alisema kuwa sherehe hizo zitaadhimishwa kwa shughuli mbalimbali za kuimarisha chama ambazo tayari zilishaanza tangu Januari 26 kwenye kata ya Mkuza.
Mdimu alisema kuwa Meghji ambaye ni Mbunge na Mjumbe wa Halmashauri Kuu (MNEC) atahitimisha sherehe hizo Februari Mosi kwenye kata hiyo ambayo imepewa upendeleo kutokana na chama hicho kuchukua mitaa yote saba kwenye uchaguzi wa wenyeviti wa Mitaa uliofanyika hivi karibuni.
“Wakati wa sherehe hizi kutakuwa na shughuli mbalimbali kama vile kukagua uhai wa chama ngazi ya mashina, matawi, kata wilaya pamoja na uhakiki wa daftari la uanachama ili kuwa na takwimu sahihi za wanachama,” alisema Mdimu.
Aidha alisema kuwa kazi nyingine ni kufanya mikutano ya kuhamasisha wanachama kujitokeza kujiandikisha katika daftarai la wapiga kura msisitizo ukiwa ni kwa wananchi wote wenye sifa kujiandikisha upya hata wale wenye vitambulisho vya kupiga kura miaka iliyopita.
“Tunatarajia Halmashauri kuu za kata zitafanyika kwenye kata hizo za Kibaha Mjini ambazo ni 14 ambapo wajumbe wa mkoa watasambaa kwenye kata hizo kabla ya mkutano mkubwa wa hadhara wa kuhitimisha sherehe hizo ambapo Meghji ndiye atakayefunga akiwa ndiyo mgeni rasmi,” alisema Mdimu.
Aliwataka wanaccm kujitokeza kwa wingi siku hiyo ili kwenda kumsikiliza mlezi wa chama siku hiyo ili waweze kuimarisha chama katika maeneo yao pia kujiandaa na uchaguzi mkuu wa mwaka huu ili kuhakikisha chama kinapata ushindi mkubwa wa kishindo huku kaulimbiu ya mwaka huu ikisema Umoja ni Ushindi (Katiba Yetu, Taifa Letu).
Mwisho.

  

No comments:

Post a Comment