Saturday, January 2, 2016

DEREVA BODABODA ACHOMWA KISU AFA WALIKUWA WAKIGOMBEA MWANAMKE

Na John Gagarini, Kibaha
DEREVA Bodaboda Ally Kasimu (23) mkazi wa Kilimahewa wilayani Kibaha mkoani Pwani amefariki dunia kwa kuchomwa kisu na waendesha pikipiki wenzake wakati wakigombea mwakanamke.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa wa Mtakuja kata ya Pangani, Ramadhan Mwaya alisema kuwa marehemu alikufa wakati wa mkesha wa kukaribisha mwaka mpaya wa 2016 na kuaga mwaka 2015.
Mwaya alisema kuwa marehemu alikutwa na umauti huo akiwa amekaa pembeni na pikipiki yake huku wenzake wakimgombea mwanamke kisha kumchoma yeye kutokana na ugomvi wa wenzake waliokuwa wakigombana.
“Madereva hao pamoja na watu wengine walikuwa kwenye sherehe hizo ambazo ziliandaliwa na Halima Kitwana ambazo ziliambatana na muziki maarufu Kigodoro ulianza majira ya saa 2 usiku na baada ya muziki kwisha baada ya saa sita kamili waliondoka lakini baadaye walionekana kumgombea mwanamke ndipo walipomchoma mwenzao,” alisema Mwaya.
Alisema kuwa marehemu alichomwa kisu sehemu ya tumboni na kujeruhiwa vibaya ambapo walijaribu kumkimbiza hospitali ya Rufaa ya Mkoa  ya Tumbi kwa ajili ya matibabu lakini alifariki wakiwa njiani.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoani Pwani Bonventura Mushongi alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa watu waliohusika na tukio hilo walikimbia na wanaendelea kutafutwa kujibu tuhuma za mauaji.
Mushongi aliwataka wananchi wa mkoa huo kuwa makini katika kipindi hichi cha sherehe za kusherehekea kuukaribisha mwaka mpya kwa kutotumia vilevi kupita kiasi ili kuepukana na matukio ya uvunjifu wa amani.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment