Friday, January 8, 2016

PWANI YAPATA ZAIDI YA MILIONI 500 KWA AJILI YA ELIMU BURE

Na John Gagarini, Kibaha
MKOA wa Pwani umepokea kiasi cha shilingi milioni 579.5 kwa ajili ya utekelezaji wa dhana ya elimu bure kwa wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa fedha hizo zimetolewa na Serikali kupitia Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
Ndikilo alisema kuwa fedha hizo tayari zimetumwa kwenye akaunti za shule hizo ambapo kwa shule za Msingi zimepokea kiasi cha shilingi milioni 167,297,00 na sekondari wamepewa kiasi cha shilingi milioni 412,249,000.
“Fedha hizo ni kwa ajili ya maendeleo ya shule ikiwa ni pamoja na ada, chakula ,gharama za mitihani na gharama nyingine ambazo zimetolewa maelekezo kwa walimu wakuu,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa fedha hizo zitasimamiwa na mkoa ambapo mwalimu mkuu yoyote atakayetumia kinyume cha utaratibu kwa ubadhirifu atachukuliwa hatua kali za kisheria.
“Walimu wakuu, Wakurugenzi wa Halmashauri na wakuu wa Wilaya wanatakiwa kukiri kwa maandishi mara watakapoziona fedha hizo kwenye akaunti zao,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa kutokana na kutolewa fedha hizo walimu wakuu hawatakiwi kutoza mchango wa aina yoyotea kama vile ulinzi, maji, umeme na michango mingine kwani fedha hizo zitatumika kwenye masuala yote.
“Michango yoyote kwa wadau kama watakuwa wamekubaliana lazima wapate kibali cha Waziri wa TAMISEMI kupitia mkuu wa mkoa ili kuchangisha michango kwa wananchi ambapo mkoa wetu una jumla ya shule za msingi 553 na sekondari 108,” alisema Ndikilo.

Mwisho.   

No comments:

Post a Comment