Tuesday, January 5, 2016

WALIOTELEKEZA VIWANJA VYA KITOVU CHA MJI WAPEWA MIEZI SITA KUVIENDELEZA

Na John Gagarini, Kibaha
HALMASHAURI ya Mji wa Kibaha imetoa muda wa miezi sita kwa watu walionunua viwanja kwenye kitovu cha mji kujenga kama sheria za ujenzi vinavyoonyesha na kwa sasa hawatakuwa tena na majadiliano kwa watakaoshindwa kujenga watanyanganywa viuwanja hivyo.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na hatua ambazo watachukua kwa watu walioshndwa kuendeleza viwanja hivyo tangu walipovinunua mwaka 2010 ofisa ardhi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Edward Mbala alisema kuwa watu hao walipew ahadi mwaka 2015 wawe wamejenga.
Mbala alisema kuwa licha ya kupewa muda wote huo lakini watu hao wameshindwa kujenga hadi sasa licha ya kuwa na maongezi ya mara kwa mara kati ya Halmashauri na wawekezaji hao mara kwa mara lakini hadi sasa wameshindwa kuyaendeleza maeneo hayo.
“Mara ya mwisho tuliwaita Aprili mwaka jana lakini walisema kuwa tatizo kubwa lililowafanya washindwe kuanza ujenzi kwenye viwanja hivyo ni hadi pale Halmashauri itakapokuwa imefanya ujenzi wa Stendi na Soko jambao ambalo tuliwaambia kuwa wao waendelee na ujenzi huku sisi tukitafuta wabia kwa ajili ya ujenzi wa vitu hivyo,” alisema Mbala.
Alisema tayari wameshapata benki ambayo itawakopesha kwa ajili ya ujenzi wa soko pamoja na stendi ambapo zaidi ya bilioni 20 zinatarajiwa kutumika kujenga miuondombinu hiyo hivyo wale walionunua viwanja waanze ujenzi.
“Tumesha waambia wayaendeleze maeneo hayo na tayari tumewapa miezi  sita kuhakikisha wanakamilisha ujenzi huo na endapo watashindwa kujenga sheria itachukua mkondo wake kwa kuwanyanganya na kuwapa wengine,” alisema Mbala.
Aidha alisema kuwa tayari wameshatoa matangazo sehemu mbalimbali na kwa wamiliki hao ili waendeleze maeneo yao ambayo ndiyo yanaonyesha sura ya mji  wa Kibaha lakini kwa sasa maeneo hayo bado ni vichaka.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment