Thursday, January 14, 2016

PANGANI YAPIGA MARUFUKU MUZIKI WA VIGODORO

Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA vijana wawili kuchomwa moto na mmoja kujeruhiwa mwishoni mwanzoni mwa wiki hii kwenye mtaa wa Vikawe kata ya Pangani wilayani Kibaha mkoani Pwani kamati ya ulinzi na usalama ya kata imepiga marufuku muziki wa vigodoro ili kuepusha mauaji kama hayo.
Marufuku hiyo inakuja baada ya tukio la kufa vijana hao ambao ni Alex Kapungu (18), Godfrey Ernest huku Omary Mohamed akijeruhiwa kwenye tukio lililotokea januari 10 mwaka huu majira ya saa 2:50 usiku kwenye mtaa huo, baada ya vijana hao kutuhumiwa kuwa ni wezi baada ya kuibuka kwa vurugu zilizosababisha baadhi ya vijana waliokuwa kwenye mziko huo kufanya uporaji kwenye maduka.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana diwani wa kata ya Pangani Agustino Mdachi alisema kuwa kamati ya ulinzi na usalama ilifikia hatua hiyo baada ya kujiridhisha kuwa muziki huo umekuwa chanzo cha vurugu ambazo zimesababisha vifo pamoja na wizi kwenye maeneo unakopigwa muziki huo.   
Mdachi alisema kuwa hilo ni tukio la pili la mauaji ambayo yametokeo kwenye muzikio huo ambao unatumiwa sana na waendesha pikipiki ambapo imebainika kuwa waendesha bodaboda hao hasa wale wanaofanya biashara nyakati za usiku maarufu kama Mapopo wengi wao ni wezi na hujificha kwenye mgongo wa kazi hiyo.
“Uchunguzi umebaini kuwa wengi wa wa mapopo hao hujihusisha na vitendo vya wizi kwani wakati muziki unaendelea huanzisha vurugu na na kuwaibia watu ambapo wengi wao huwa na mapanga wanapokwenda kwenye muziki huo ambao unatamba kwa sasa,” alisema Mdachi.
Alisema kuwa kutokana na kubaini kuwa muziki huo umekuwa ukichangia vitendo vya uhalifu katika kata ya Pangani waliamua kwa pamoja kuzuia upigwaji wa muziki huo kwa kipindi kisichojulikana ili kuepukana na vitendo hivyo vya uhalifu pamoja na mauaji.
“Kwa ujumla Kigodoro mara nyingi hakiishi salama kwani mara nyingi vurugu zimekuwa zikitokea na vijana wanauana kutokana na muziki huu hivyo tumeamua kusitisha muziki huu ili kupunguza wimbi hili la uhalifu na mauaji,” alisema Mdachi.
Aidha alisema kuwa kwa sasa wameamua kufanya doria kwa muda wote kwa kushirikiana na vyombo vya dola ili kukabiliana na matukio hayo ya kihalifu ambayo mengi yanafanywa na waendesha pikipiki.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment