Tuesday, January 5, 2016

HALMASHAURI KUTOA HUDUMA KADRI YA UWEZO WAKE

Na John Gagarini, KibahaKATIKA kukabiliana na changamoto mbalimbali za utoaji huduma kwa wananchi Halmashauri ya Mji wa Kibaha imesema kuwa itatatua kero hizo kadiri ya uwezo wa fedha za miradi ya maenedeleo zinavyopatikana.
Hayo yalisemwa na mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Gladys Dyamvunye alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake na kusema kuwa kuna changamoto za utoaji huduma kwani kila mwananchi anataka maendeleo.
Dyamvunye alisema kuwa changamoto ni nyingi kwani ili kuondoa kero lazima huduma ziboreke lakini kutokana na mahitaji ya huduma kuongezeka kutokana na ongezeko la idadi ya watu kila wakati.
“Kadiri maendeleo yanavyokuja mahitaji ya huduma nayo yanaongezeka hivyo kuonekana kama huduma ni kidogo lakini tutaendelea kutoa huduma kadiri ya uwezo wetu ili kuwaondolea changamoto wananchi,” alisema Dyamvunye.
Alisema kuwa halmashuri itahakikisha huduma zinazotolewa kwa wananchi zinaboreshwa ili kuondoa malalamiko yasiyo ya msingi kwani lengo ni kuboresha utoaji huduma ambayo ndiyo kazi ya Halmashauri.
“Bajeti ya fedha inaweza kuwa ni tatizo hivyo baadhi ya huduma zinaonekana kama hazitolewi kiufasaha lakini si lengo la Halmashauri yetu kwani matazamio yetu ni huduma bora kwa wananchi ili waipende serikali yao,” alisema Dyamvunye.
Aliwataka wananchi kushirikiana na halmashauri yao ili iweze kutoa huduma ambazo zitakabili changamoto zilizopo kwa wananchi na kusema wataendelea kuhudumia wananchi kadiri ya uwezo wao.

Mwisho.      

No comments:

Post a Comment