Thursday, January 14, 2016

ARDHI KUPIMWA KWA NJIA YA KILETRONIKI KWA MAJARIBIO MIKOA MITATU HATI KUPATIKANA KWA SIKU MOJA

Na John Gagarini, Kibaha

WIZARA ya Ardhi na Makazi iko kwenye mpango wa kupima maeneo yote hapa nchi kupitia mpango wa majaribio wa kutoa hati za kumiliki ardhi kwa njia ya Kieletroniki ndani ya siku moja ili kila mwananchi aweze kumiliki ardhi kisheria.
Hayo yalisemwa  hivi karibuni mjini Kibaha na Waziri wa Ardhi na Makazi Wiliam Lukuvi wakati alipofanya zaiara ya siku moja wilayani Kibaha kuangalia changamoto zinazoikabili idara ya ardhi kwenye mkoa huo.
Lukuvi alisema kuwa utoaji hati za kumiliki ardhi kwa haraka itasaidia kupunguza migogoro ambayo imejitokeza kutokana na kuchelewa kutolewa kwa hati hizo ambapo watu wamekuwa wakivamia maeneo yaliyowazi.
“Upatikanaji wa hati unasaidia kuepusha migogoro pia uvamizi kwani kutokana na uchelewaji wa kupatikana hati kunasababisha mtu kushindwa kumiliki kihalali eneo lake hivyo tunataka tuondokane na ucheleweshaji huo,” alisema Lukuvi.
Alisema kuwa majaribio hayo yataanza kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Morogoro kupitia mfumo wa Kieletroniki ambapo mfumo huo endapo utafanikiwa utasamabazwa nchi nzima na kuweza kufikia malengo ya kupima ardhi ya nchi nzima.
“Utashangaa mfumo huu wa sasa kuna baadhi ya watu wamekuwa kwenye mchakato wa kupatiwa hati kwa muda mrefu tangu mwaka 2013 lakini wamekuwa wakitumia ofa pekee jambo ambalo hatulitaki tena,” alisema Lukuvi.
Aidha alisema ametoa hadi mwisho wa mwezi huu Halmashauri kuhakikisha unawapatia hati watu wote walioomba hati kwani ofa hazitatambuliwa tena hivyo wanatakiwa kufanikisha zoezi hilo ili kuondoa kero kwa wananchi.
“Tunataka tuondokane na kero ya kucheleweshwa kupatikana kwa hati kwani mbali ya maeneo kuvamiwa na changamoto nyingine pia watu wanaweza kuzitumia hati zao katika kukopa kwenye mabenki au taasisi za kifedha kwa  ajili ya shughuli zao za maenedeleo,” alisema Lukuvi.
Mwisho.    


No comments:

Post a Comment