Sunday, January 10, 2016

WAAZIMIA KUJENGA SHULE YA SEKONDARI KWA SASA WATOTO WAO WANASOMA UMBALI WA KILOMETA ZAIDI YA 8

Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Mtaa wa Mbwate kata ya Mkuza wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuwapatia greda kwa ajili ya kuchimba visiki kwenye eneo ambalo wamelifyeka kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari.
Wametoa ombi hilo baada ya kuanza kusafisha eneo kwa ajili ya sekondari kutokana na watoto wanaokaa mtaa huo kusoma kwenye sekondari ya kata ya Nyumbu ambayo iko umbali wa kilometa zaidi ya 8 hali ambayo inawafaya wanafunzi wanaotoka kwenye mtaa huo na jirani kukumbuna na changamoto nyingi hivyo kushindwa kumaliza shule.
Akizungumza na waandishi wa habari mkazi wa mtaa huo Alex Mathias alisema kuwa wamefikia hatua hiyo ya kujenga sekondari ili kuwapunguzia adha watoto wao kusoma mbali hivyo kushindwa kusoma kwa ufanisi hivyo wakipatiwa greda litasaidia kusafisha eneo hilo.
“Kule ni mbali sana kama mzazi huna fedha za kumlipia pikpiki kila siku kiasi cha shilingi 2,000 kwenda na kurudi basi mwanafunzi anakutana na mitihani mingi ambapo wengine wanakuwa hawafiki shule na kufikia hatua ya kuacha shule huku kwa upande wa wale wa kike wamekuwa kijiingiza kwenye vishawishi na kudanganywa na waendesha pikipiki na kujikuta wakiambulia kupata mimba,” alisema Mathias.
Kwa upande wa Salama Rajab alisema kuwa wanafunzi wamekuwa wakipata taabu ya kufika na kurudi kutoka shule kwani umbali wanaposoma kunawapunguzia ari ya kusoma.
Rajab alisema kuwa ujenzi wa shule hiyo itakuwa mkombozi kwa watoto wao hali ambayo itawafanya wafanye vizuri kwenye masomo yao kwani watakuwa na mazingira mazuri ya kusomea tofauti na ilivyo sasa.
Naye mwenyekiti wa mtaa huo Abdala Mtandio alisema kuwa kutokana na eneo hilo na maeneo jirani kukosa shule ya sekondari walifikia maamuzi ya kuanzisha wazo la kujenga shule ili kuwapunguzia watoto wao kero ya kusoma mbali.
Mtandio alisema kuwa wanalishukuru Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kambi ya Nyumbu kwa kuwapatia eneo lenye ukubwa wa hekari 10 kwa ajili ya ujenzi wa huduma za jamii ambapo ndo wamenza na maandalizi ya shule ya sekondari.
“Tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze kutusaidia kuweza kuanza ujenzi wa shule yetu ya sekondari kwani kwa sasa tunasafisha eneo letu ambapo kila Jumamosi tunalifyeka kwa ajili ya ujenzi huo,” alisema Mtandio.
Alisema kuwa wameazimia kuwa ifikapo 2017 wanafunzi waanze kusoma hapo ambapo watakuwa wamekamilisha angalau madarasa matatu kwa kuanzia ambapo kila kaya inajitolea kufyeka ambapo kuna kaya 554 zenye wakazi 2,863.

Mwisho.  

No comments:

Post a Comment