Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Mtaa wa Mbwate kata ya Mkuza wilayani Kibaha mkoani
Pwani wameiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuwapatia greda kwa ajili ya
kuchimba visiki kwenye eneo ambalo wamelifyeka kwa ajili ya ujenzi wa shule ya
sekondari.
Wametoa ombi hilo baada ya kuanza kusafisha eneo kwa ajili ya
sekondari kutokana na watoto wanaokaa mtaa huo kusoma kwenye sekondari ya kata
ya Nyumbu ambayo iko umbali wa kilometa zaidi ya 8 hali ambayo inawafaya
wanafunzi wanaotoka kwenye mtaa huo na jirani kukumbuna na changamoto nyingi
hivyo kushindwa kumaliza shule.
Akizungumza na waandishi wa habari mkazi wa mtaa huo Alex
Mathias alisema kuwa wamefikia hatua hiyo ya kujenga sekondari ili kuwapunguzia
adha watoto wao kusoma mbali hivyo kushindwa kusoma kwa ufanisi hivyo
wakipatiwa greda litasaidia kusafisha eneo hilo.
“Kule ni mbali sana kama mzazi huna fedha za kumlipia pikpiki
kila siku kiasi cha shilingi 2,000 kwenda na kurudi basi mwanafunzi anakutana
na mitihani mingi ambapo wengine wanakuwa hawafiki shule na kufikia hatua ya
kuacha shule huku kwa upande wa wale wa kike wamekuwa kijiingiza kwenye
vishawishi na kudanganywa na waendesha pikipiki na kujikuta wakiambulia kupata
mimba,” alisema Mathias.
Kwa upande wa Salama Rajab alisema kuwa wanafunzi wamekuwa
wakipata taabu ya kufika na kurudi kutoka shule kwani umbali wanaposoma
kunawapunguzia ari ya kusoma.
Rajab alisema kuwa ujenzi wa shule hiyo itakuwa mkombozi kwa
watoto wao hali ambayo itawafanya wafanye vizuri kwenye masomo yao kwani
watakuwa na mazingira mazuri ya kusomea tofauti na ilivyo sasa.
Naye mwenyekiti wa mtaa huo Abdala Mtandio alisema kuwa
kutokana na eneo hilo na maeneo jirani kukosa shule ya sekondari walifikia
maamuzi ya kuanzisha wazo la kujenga shule ili kuwapunguzia watoto wao kero ya
kusoma mbali.
Mtandio alisema kuwa wanalishukuru Jeshi la Wananchi wa
Tanzania (JWTZ) kambi ya Nyumbu kwa kuwapatia eneo lenye ukubwa wa hekari 10
kwa ajili ya ujenzi wa huduma za jamii ambapo ndo wamenza na maandalizi ya
shule ya sekondari.
“Tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze kutusaidia kuweza
kuanza ujenzi wa shule yetu ya sekondari kwani kwa sasa tunasafisha eneo letu
ambapo kila Jumamosi tunalifyeka kwa ajili ya ujenzi huo,” alisema Mtandio.
Alisema kuwa wameazimia kuwa ifikapo 2017 wanafunzi waanze
kusoma hapo ambapo watakuwa wamekamilisha angalau madarasa matatu kwa kuanzia
ambapo kila kaya inajitolea kufyeka ambapo kuna kaya 554 zenye wakazi 2,863.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment