Tuesday, January 5, 2016

HALMASHAURI YASAKA MILIONI 16 KUKARABATI TAA ZA STENDI AMBAZO HAZIWAKI MIEZI 10 ILIYOPITA

Na John Gagarini, KibahaHUKU watumiaji wa stendi kuu ya mabasi ya Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wakilalamika kukosekana kwa taa kwenye stendi hiyo kwa kipindi cha miezi 10 Halmashauri ya Mji wa Kibaha imesema kuwa iko katika harakati za kutafuta fedha kiasi cha shilingi milioni 16 kwa ajili ya kukarabati taa hizo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha Mhandisi wa Halmashauri ya Mji huo Dismas Marango alisema kuwa baadhi ya taa kwenye stendi hiyo zimeungua hali inayofanya stendi hiyo kuwa gizani kwa kipindi chote hicho.
Marango alisema kuwa mara baada ya baadhi ya taa hizo kuungua waliwasiliana na Temesa ambao ndiyo wanaohusika na ukarabati wa umeme na magari ya serikali walifuatilia juu ya tataizo hilo na kugundua kuungua kwa baadhi ya taa hizo ambazo ziko zaidi ya 10.
“Waligundua kuungua kwa taa hizo huku nyingine zikiwa hazina mwanga mkali ambapo gharama ya kukarabati ni shilingi milioni 16 ili huduma hiyo iweze kurejea katika hali yake ya kawaida na kuondoa adha ya watumiaji wa stendi hiyo kuwa gizani,” alisema Marango.
Alisema kuwa gharama hizo ni kubwa sana hali ambayo inawafanya washindwe kurejesha huduma ahiyo ya taa kwa muda sasa lakini hata hivyo wanaendelea na michakato ya kutafuta fedha hizo ili kurejesha huduma hiyo.
“Suala hili ni la ghafla hivyo hata bajeti yake haikuwepo lakini tunaendelea na michakato mbalimbali ili kupata fedha hizo ili kuhakikisha taa zinawaka na kuondoa usumbufu kwa watumiaji wa stendi wakiwemo abiria na wale wanaofanyabiashara kwenye stendi yetu,” alisema Marango.
Aliwataka watumiaji wa stendi hiyo kuwa na uvumilivu wakati Halmashauri ikihangaika kupata fedha kwa ajili ya kurudisha huduma ya taa kwani hata wao wanachukizwa na hali hiyo lakini mipango inafanywa kurudisha hali ya kawaida.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment