Saturday, January 2, 2016

MKULIMA AOKOTA BOMU LA KUTUPWA KWA MKONO

Na John Gagarini, Kibaha
MKULIMA wa Mtaa wa Sagare wilayani Kibaha mkoani Pwani Hassan Omary ameokota bomu la kutupwa kwa mkono  ambalo lilisahaulika wakati wa Operesheni Tokomeza iliyofanyika nchini Julai mwaka 2015.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha kamanda wa polisi mkoani Pwani Bonventura Mushongi alisema bomu hilo lilisahaulika wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo la kukamata wahalifu mbalimbali waliokuwa wakiiba Maliasili za nchi.
Mushongi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Desemba 31 mwaka 2015 majira ya saa 5 asubuhi wakati mke wa Omary alipokuwa akilima aligonga kitu kigumu cha chuma na alipokitoa aliona kitu kama bomu na kumwita mumewe aliye waita watu wakiwemo viongozi wa mtaa huo.
“Baada ya kuona hivyo Omary alitoa taarifa polisi na kusema kuwa wameona bomu ndipo polisi walipofika na kubaini kuwa ni bomu la kutupwa kwa mkono ambalo fuse yake ili haribika,” alisema Mushongi.
“Halikuweza kulipuka lakini endapo lingepata joto kali mfano joto la moto lingeweza kulipuka lakini hata hivyo tumeshukuru Mungu kuwa halikuweza kulipuka kwa muda wote huo kwnai endapo lingelipuka lingeweza kuleta madhara,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa baadaye ilibainika kuwa inawezekana bomu hilo la kutupwa kwa mkono liliachwa kwa bahati mbaya  wakati wa Operesheni Tokomeza iliyofanyika Julai mwaka jana.
“Kwa kushirikiana na jeshi letu tutalipelekwa kwa wataalamu wa mabomu ambao ni Jeshi la wananchi (JWTZ) kwa ajili ya kujua zaidi kuhusiana na bomu hilo ikiwa ni pamoja na kuliharibu ili lisiweze kuleta madhara,” alisema Mushongi.
Awali mwenyekiti wa mtaa wa Sagale Bernego alisema kuwa mama huyo alikuwa akisafisha shamba kwenye eneo la Omary ambalo limekuwa likichimbwa vitu vilivyoachwa zamani na watawala wa Kijerumani na Kiarabu maarufu kama Tunu.
Bernego alisema kuwa machimbo hayo ya Tunu yalikuwa yakifanywa na mmiliki huyo ambapo eneo hilo lilizua utata miaka michache iliyopita kwani kumekuwa na mambo ya miujiza yamekuwa yakitokea kwenye machimbo hayo.
Mwisho.        


No comments:

Post a Comment