Thursday, January 14, 2016

OFISA ARDHI AWEKWA KITI MOTO LUKUVIA AMTAKA AWALIPE WANANCHI

Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA baadhi ya wakazi wa Mtaa wa Mwanalugali wilayani Kibaha mkoani Pwani kulalamika mbele ya Waziri wa Ardhi na Makazi Wiliam Lukuvi juu ya kushindwa kulipwa fidia ya viwanja vyao vilivyochukuliwa na Halmashauri kwa zaidi ya miaka 18 iliyopita wakazi hao sasa watalipwa ifikapo Machi mwaka huu.
Ahadi hiyo ilitolewa na Halmashauri mbele ya Waziri Lukuvi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja wilayani hapa kujua kero mbalimbali zitokanazo na masuala ya ardhi na kusema kuwa ofisa ardhi wa Mji huo endapo atashindwa kutekeleza hilo basi atakuwa amejifukuzisha kazi mwenyewe.
Akitoa ahadi hiyo ofisa ardhi wa halmashauri ya Mji wa Kibaha Edward Mbala baada ya kubanwa na wananchi hao ambao walisema kuwa wamekuwa wakizungushwa kwa kipindi hicho huku wakiwa hawajui hatma yao.
Moja ya wakazi hao aliyejitambulisha kwa jina la Merry Yohana alisema kuwa maeneo yao yalichukuliwa na Halmashauri kipindi hicho na kuahidiwa kuwa wangelipwa fidia na wengine wangepewa viwanja katika maeneo hayo lakini hakuna utekelezaji wowote uliofanyika licha ya kuwa viwanja hivyo tayari walishaviuza kwa watu wengine.
“Tunapata shida sana kwani walichukua maeneo yote licha ya kuwa ni jambo zuri la maendeleo lakini kwa kipindi cha miaka 18 tumekuw atukifuatilia bila ya mafanikio kwani tunazungushwa tu na hakuna majibu ya uhakika kuwa  ni lini tutalipwa kwenye eneo la Kitalu E,” alisemaYohana.
Kufuatia malalamiko hayo Waziri Lukuvi alimwita ofisa ardhi ili atoe majibu ambapo alisema kuwa ni kweli watu hao wamekuwa wakidai kwa kipindi hicho lakini Hlamashauri iko kwenye utaratibu wa kuwalipa majibu ambayo hayakumridhisha waziri.
“Mkuu ni kweli kuna watu wanadai fidia na wengine wanadai viwanja na huu ulikuwa ni mradi lakini tuko kwenye utaratibu wa kuwalipa na tutawalipa wakati wowote mara taratibu zitakapokamilika kwani tunahangaika kuhakikisha madai yao yanapata majibu,” alisema Mbala.
Hata hivyo waziri alimwambia atoe ahadi kuwa ni lini watakuwa wamekamilisha zoezi hilo ambapo alisema kuwa baada ya miezi miwili kutoka sasa fedha hizo zitakuwa zimepatikana kiasi cha shilingi bilioni 1.4 pamoja na kuwapatia viwanja wengine.
Kwa upande wake Waziri Lukuvi alisema kuwa haipendezi wananchi kukaa muda mrefu bila ya kulipwa fidia ya maeneo yao ambayo yalichukuliwa na Halmashauri kwani kuchelewesha kulipa kunasababisha migogoro isiyo ya lazima.
“Wananchi ofisa ardhi ameahidi hapa mbele yangu na ninyi hivyo msiwe na wasiwasi Bw Ardhi kwa kuwa umeahidi mwenywe muda mtkaowalipa hawa wananchi endapo utashindwa utakuwa umejifukuzisha kazi mwenyewe,” alisema Lukuvi.
Lukuvi aliwataka wananchi hao kukubali muda huo wa miezi miwili kwani walishakaa muda wa miaka 18 hivyo atahakiki wanaodai fidia na wale wanaodai viwanja kwani muda umekuwa mrefu sana na watu wanataka wafanye maendeleo yao.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment