Wednesday, December 31, 2014

WAZEE ZAIDI YA 300 WAPATIWA MATIBABU MAALUMU

Na John Gagarini, Kibaha
JUMLA ya Wazee zaidi ya 300 kati ya wazee 2,500 kwenye kata ya Kibaha katika halmashauri ya mji wa Kibaha mkoani Pwani wamepatiwa matibabu ya maradhi mbalimbali.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkurugenzi wa Shirika lisilo la Kiserikali la Msamaria Mwema Huduma za Jamii (GSSST), Elisha Sibale alipozungumza na waandishi wa habari juu ya huduma walizotoa kwa wazee.
Sibale alisema kuwa wazee hao ambao wanahudumiwa na shirika lake ni wale wenye umri kuanzia miaka 60 walitibiwa magonjwa mbalimbali kama vile Kisukari, Macho, Wingi wa damu, Uoni hafifu na ugonjwa wa Ukimwi.
“Lengo la mradi huu ni kuwawezesha wazee kupata matibabu kwa wakati kwani wengi wao wamekuwa hawapati huduma hizo kutokana na jamii kutowathamini hivyo kujikuta wakiwa na changamoto za kuumwa maradhi mengi,” alisema Sibale.
Naye mtaalamu wa maabara kwenye zahanati ya Mwendapole Hans Amon alisema kuwa wazee hao wameanza kujiamini kwenda kupata matibabu ambapo awali walikuwa na woga kutokana na jamii kutowapeleka hospitali na kuwaacha.  
Kwa upande wake moja ya wazee walionufaika na mradi huo Hadija Mbwambo alisema kuwa wameweza kujua afya zao na kujitambua na kuona umuhimu wa kuwahi kupata matibabu.
 Mradi huo wa miaka miwili unatekelezwa kwenye mitaa ya Kwa Mfipa, Simbani, Mwendapole A na B kwa Kibaha Mjini na Kibaha Vijijini Mwanabwito na Kikongo na matibabu hayo yalifadhiliwa na shirika hilo kwa kushirikiana na Help Age International na Pfizer Pharmaceuticals kuanzia Oktoba Mosi siku ya wazee duniani hadi Desemba mwaka jana na litakuwa endelevu.

Mwisho.  

AFA KWA KUJINYONGA KISA KUUGUA MUDA MREFU

Na John Gagarini, Kibaha
HUKU leo ikiwa ndiyo siku ya kwanza ya mwaka mpya wa 2015 ikiwa imeanza fundi wa kuchomelea Michael Mpondo (36) mkazi wa Machinjioni wilayani Kibaha mkoani Pwani ameamua kukatisha uhai kwa kujinyonga.
Imeelezwa kuwa chanzo cha fundi huyo kuamua kuchukua maamuzi hayo magumu ya kuamua kujiua kunatokana na kuugua kwa muda mrefu.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa wa Machinjioni Evarist Kamugisha alisema kuwa marehemu alijinyonga jirani na nyumba laiyokuwa akiishi.
Akielezea kwa kina tukio hilo Kamugisha alisema kuwa tukio hilo lilitokea Desemba 30 mwaka huu majaira ya saa 4:30 asubuhi baada ya mwili wake kukutwa ukininginia kwenye mti umbali wa mita 60 na alipokuwa akiishi.
“Marehemu usiku wa majira ya saa 2:30 kabla ya kifo chake alikula chakula na ndugu zake lakini aliondoka na jitihada za kumtafuta zilifanyika bila ya mafanikio lakini asubuhi yake ndipo watu walipouona mwili wake ukinginginia,” alisema Kamugisha.
Kamugisha alisema kuwa marahemu alikuwa akiumwa ambapo baada ya chumba chake kupelkuliwa kulikutwa dawa aina ya Panadoli pamoja na Amoxilini ambazo inasemekana alikuwa akizitumia.
“Marehemu alijinyonga kwa kutumia kamba ya nguo ya jeshi ambayo aliikata na kuwa kama kamba na kujinyonga nayo na hakuacha ujumbe wowote juu ya kifo chake,” alisema Kamugisha.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alithibitisha kutokea tukio hilo na kusema kuwa chanzo cha kifo hicho ni marehemu kuugua muda mrefu na kukata tamaa ya maisha.

Mwisho.   

Sunday, December 28, 2014

MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA YAWA TISHIO NA WAZEE WAFURAHIA HUDUMA ZA AFYA

Na John Gagarini, Bagamoyo
WATANZANIA wametakiwa kuzingatia ulaji wa vyakula na ufanyaji wa mazoezi ili kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza ambayo kwa sasa yanasababisha vifo vya watu wengi hapa nchini.
Hayo yamesemwa hivi karibu kwenye Kijiji cha Msoga wilayani Bagamoyo mkoani Pwani na katibu mkuu wa Wizara ya Afya Dk Donan Mmbando alipotembelea kukagua ujenzi wa kituo cha afya cha kisasa cha Kijiji hicho.
Dk Mmbando amesema kuwa kwa sasa kumekuwa na ushindani mkubwa wa magonjwa yasiyoambukiza na yale yanayoambukiza katika kusababisha vifo hivyo jamii inapaswa kuangalia njia za kujikinga na magonjwa hayo.
Amesema kuwa magonjwa yasiyoambukiza kama vile kisukari, magonjwa ya moyo na presha na mengineyo ya namna hiyo yanasababisha vifo vingi hapa nchini kwa sasa ambapo serikali imekuwa ikitumia gharama kubwa kuyadhibiti
Ametoa mfano wa baadhi ya nchi zilizoendelea zimekuwa zikitenga hadi kufikia asilimia 15 ya bajeti katika kukabiliana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza ili kupunguza vifo.
Amebainisha baadhi ya vitu vinavyochangia magonjwa hayo kuongezeka ni pamoja na uvutaji wa sigara, unywaji wa pombe na kutofanya mazoezi ni baadhi ya mambo yanayochangia kuongezeka kwa magonjwa hayo. 
Aidha amesema kuwa wao kama wizara wanasisistiza kinga zaidi ili kukabilina na magonjwa hayo na ndiyo maana wamekuwa wakitoa chanjo za kinga za magonjwa mbalimbali hasa kwa watoto ili kukabiliana na magonjwa mbalimbali.
Katibu mkkuu huyo wa wizara ya Afya amesema wamekuwa wakihamasisha ulaji wa chakula kwa mpangilio kwani chakula nacho kimekuwa ni changamoto ya ongezeko la magonjwa hayo kutokana na ulaji usiofaa, na wamekuwa wakikabili magonjwa hayo kwa kuzingatia taratibu za afya kupunguza vifo.
Amewataka wananchi kupata tiba sahihi ya magonjwa ili kupunguza madhara yatokanayo na magonjwa kuwa sugu pia wajiunge na mifuko ya afya ili kupunguza mzigo wa malipo kwa ajili ya matibabu.

Na John Gagarini, Kibaha
WAZEE wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha mkoani Pwani wameipongeza serikali kwa kuwatengea kitengo maalumu kwa ajili ya kuwahudumia.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha mwenyikiti wa wazee Mlandizi Mohamed Pongwe wakati wa mafunzo ya kuwahudumia wazee majumbani alisema kuwa kwa sasa huduma zao zimeboreshwa tofauti na ilivyokuwa mwanzo.
Pongwe alisema kuwa huduma kwa wazee kwenye kituo cha Afya cha Mlandizi na sehemu nyingine za huduma za afya zilikuwa ni mbaya kutokana na wazee kutopewa kipaumbele wakati wa kupata matibabu.
“Kwa sasa tunaishukuru serikali ya wilaya kwa kutuwekea kitengo chetu dirisha malumu kwa ajili ya kuwapatiwa huduma za matibabu kwenye kituo hicho cha afya cha Mlandizi kwani tunahudumiwa vizuri,” alisema Pongwe.
Alisema kuwa kama unavyojua wazee wana matatizo mengi hasa ya kiafya lakini walikuwa wakipuuzwa kwenye suala la afya hali iliyokuwa ikisababisha waishi katika hali mbaya za kiafya.
“Tunakwenda hospitali tukiwa hautna wasiwasi wa matibabu kwani tuna dirisha letu maaalumu tunapata huduma kwa upendo kutoka kwa wahudumu wa afya kwa kweli hata afya zetu zinaridhisha,” alisema Pongwe.
Kwa upande wake mwezeshaji wa mafunzo hayo Elizabeth Sekaya ambaye ni muuguzi wagonjwa majumbani na huduma kwa wazee kutoka halmashauri ya wilaya alisema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wazee waweze kuwasaidia wenzao kwenye huduma za afya wakiwa majumbani.
“Tumekuwa tukiwapatia mafunzo haya mara kwa mara na tumeona mafanikio kwani sasa wameweza kuyakabili baadhi ya magonjwa wakiwa nyumbani ikiwa ni pamoja na ufanyaji wa mazoezi na lishe bora,” alisema Sekaya.
Sekaya alsiema kuwa wazee wanachangamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na maumivu ya mwili na kingine ni ususaji wa chakula endapo wanaudhiwa hivyo tunawajengea uwezo wa kujiamini na kukabilina na changamoto mbalimbali.
Mwisho.

  


Wednesday, December 24, 2014

PWANIYAONGEZA UFAULU DARASA LA SABA

Na John Gagarini, Kibaha
MKOA wa Pwani umeongeza ufaulu kwa wanafunzi waliofanya mtihani wa darasa la saba ambapo jumla wanafunzi 13,242 wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza kwenye shule mbalimbali za sekondari.
Akitangaza matokeo hayo mjini Kibaha katibu tawala wa mkoa huo Mgeni Baruani na kusema kuwa wanafunzi wote waliofaulu wamepata nafasi ya kujiunga na shule za sekondari.
Mgeni alisema kuwa Idadi hiyo ni kati ya wanafunzi 23,562 waliofanya mtihani wa darasa la saba mwaka huu, ambapo idadi ya waliofaulu wasichana walikuwa ni 6,851 na wavulana ni 6,391 huku idadi ya wanafunzi wasichana ikionekana kuwa juu.
“Kwa mwaka huu mkoa umeweza kuongeza kiwango cha ufaulu kwa asilimia 56.2 kutoka asilimia 54 ya mwaka 2013 hivyo kushika nafasi ya 13 kitaifa na kuwa moja ya mikoa iliyofanya vizuri,” alisema Mgeni.
Aidha alisema kuwa kupatikana kwa nafasi kwa wanafunzi hao kumetokana na mpango madhubuti uliowekwa na sekretarieti ya mkoa kwa kushirikiana na halmashauri mpango wa kuongeza vyumba vya madarasa katika shule zote za sekondari.
“Shule mpya zimejengwa ambazo zilisaidia kuondoa tatizo la wanafunzi kukosa nafasi katika shule za serikali na tunawaomba wazazi na walezi ambao watoto wao wameichaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza, kutoa ushirikiano kwa kuhakikisha wanawaandikisha watoto hao na kuhudhuria shuleni pasipo visingizio mbalimbali hali inayosababisha kuwakosesha haki yao ya msingi kielimu,” alisema Mgeni.
Kwa upande wake ofisa elimu mkoa wa Pwani Yusuph Kipengele alisema changamoto kubwa inayojitokeza kwa sasa ni baadhi ya wanafunzi wanaosoma shule za binafsi kutokwenda kuripoti katika shule wanazopangiwa.
“Wanafunzi hao wanaosoma shule za binafsi unakuta wanapata nafasi za juu lakini wanaokwenda kuripoti shule za sekondari wanzochaguliwa ni wachache labda wakipangiwa shule za sekondari za  Kibaha zinazomilikiwa na shirika la elimu Kibaha hivyo kuipa shida sana idara yetu”alisema Kipengele.
Kipengele alieleza kuwa wanafunzi hao wasioripoti katika shule za sekondari wanazopangiwa wanawanyima nafasi wanafunzi wengine ambao wangepata fursa ya kwenda kwenye shule hizo.
Mwisho

BEI ZA BIDHAA ZA VYAKULA HAZIJAPANDA X-MASS

Na John Gagarini, Kibaha
HUKU leo ikiwa ni sikukukuu ya kumbukumbu ya kuzaliwa Yesu Kristo X-MASS ikiwa inaadhimishwa duniani kote wakazi wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani wanasherehekea kwa furaha kutokana na bei za bidhaa za vyakula zikiwa hazijapanda kama inavyokuwa miaka ya nyuma.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa bei za bidhaa za vyakula hazijapanda kama miaka ya nyuma kwani nyingi ziko vilevile hali amabyo imefurahiwa na wananchi wengi.
Akizungumza na gazeti hili mjini Kibaha mkazi wa Maili Moja Kibena Mtoro alisema kuwa wanasherehekea sikukuu hii huku bei za bidhaa za vyakula zikiwa ni za kawaida.
“Miaka ya nyuma beiza bidhaa za vyakula zilikuwa zinapanda mara dufu lakini mwaka huu tunamshukuru Mungu kwani bei ni zilezile,” alisema Mtoro.
Mtoro alisema kipindi cha nyuma baadhi ya watu wenye kipato cha chini walikuwa hawaifurahii sikukuu kutokana na bei kuwa juu.
“Kutokana na hali ya kiuchumi kuwa mabaya na bei kuwa za kawaida ni dhahiri tunasherehekea sikuku hii kwa furaha kwani kila mtu anamudu kununua chakula,” alisema Mtoro.
Kwa upande wake katibu wa soko kuu la wilaya ya Kibaha Maili Moja, Muhsin Abdu alisema kuwa kwa mwaka huu bei hazijapanda kabisa.
Abdu alisema kuwa bei ya ndizi pekee ndiyo iliyopanda ambapo mkungu umepanda bei kutoka shilingi 20, 000 hadi 35,000 kwa mkungu pamoja na tanagawizi toka shilingi 3,000 kwa kilo hadi 4,500.
“Bei haijapanda kwa sababu mojawapo ni wakulima wengi kuleta bidhaa toka mashambani na kuja kuziuza mjini tofauti na kipindi cha nyuma ambapo wafanyabiashara walikuwa wakileta bidhaa na kuuza kwa bei kubwa,” alisema Muhsin.
Alisema kuwa wafanyabiashara ndiyo walikuwa wakipandisha bei kwa kuficha bidhaa ili wauze kwa bei kubwa wakitoa visingizio mbalimbali.
“Kipindi kile bei zilikuwa juu na zinakuwa adimu lakini safari hii vyakula vingi na bado vinakuja kwa wingi hata sisi tunafurahia hali kwani bei zikiwa juu hata uuzaji unakuwa mgumu,” alisema Abdu.
Mwisho.

BIDHAA ZA VYAKULA HAZIJAPANDA X-MASS 2014

Na John Gagarini, Kibaha
HUKU leo ikiwa ni sikukukuu ya kumbukumbu ya kuzaliwa Yesu Kristo X-MASS ikiwa inaadhimishwa duniani kote wakazi wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani wanasherehekea kwa furaha kutokana na bei za bidhaa za vyakula zikiwa hazijapanda kama inavyokuwa miaka ya nyuma.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa bei za bidhaa za vyakula hazijapanda kama miaka ya nyuma kwani nyingi ziko vilevile hali amabyo imefurahiwa na wananchi wengi.
Akizungumza na gazeti hili mjini Kibaha mkazi wa Maili Moja Kibena Mtoro alisema kuwa wanasherehekea sikukuu hii huku bei za bidhaa za vyakula zikiwa ni za kawaida.
“Miaka ya nyuma beiza bidhaa za vyakula zilikuwa zinapanda mara dufu lakini mwaka huu tunamshukuru Mungu kwani bei ni zilezile,” alisema Mtoro.
Mtoro alisema kipindi cha nyuma baadhi ya watu wenye kipato cha chini walikuwa hawaifurahii sikukuu kutokana na bei kuwa juu.
“Kutokana na hali ya kiuchumi kuwa mabaya na bei kuwa za kawaida ni dhahiri tunasherehekea sikuku hii kwa furaha kwani kila mtu anamudu kununua chakula,” alisema Mtoro.
Kwa upande wake katibu wa soko kuu la wilaya ya Kibaha Maili Moja, Muhsin Abdu alisema kuwa kwa mwaka huu bei hazijapanda kabisa.
Abdu alisema kuwa bei ya ndizi pekee ndiyo iliyopanda ambapo mkungu umepanda bei kutoka shilingi 20, 000 hadi 35,000 kwa mkungu pamoja na tanagawizi toka shilingi 3,000 kwa kilo hadi 4,500.
“Bei haijapanda kwa sababu mojawapo ni wakulima wengi kuleta bidhaa toka mashambani na kuja kuziuza mjini tofauti na kipindi cha nyuma ambapo wafanyabiashara walikuwa wakileta bidhaa na kuuza kwa bei kubwa,” alisema Muhsin.
Alisema kuwa wafanyabiashara ndiyo walikuwa wakipandisha bei kwa kuficha bidhaa ili wauze kwa bei kubwa wakitoa visingizio mbalimbali.
“Kipindi kile bei zilikuwa juu na zinakuwa adimu lakini safari hii vyakula vingi na bado vinakuja kwa wingi hata sisi tunafurahia hali kwani bei zikiwa juu hata uuzaji unakuwa mgumu,” alisema Abdu.
Mwisho.

POLISI KUWEKA ULINZI MKALI SIKUKUU ZA X-MASS NA MWAKA MPAYA

Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani limewataka wananchi kutumia vikundi vya ulinzi shirikishi ili kukabiliana na uhalifu katika kipindi hichi cha sikukuu za X-Mass na mwaka mpya.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha, kamanda wa Polisi mkoani hapa Ulrich Matei alisema kuwa wamejipanga vyema kudhibiti vitendo viovu kwa kushirikiana na wananchi.
Matei alisema kuwa katika kukabiliana na matukio ya uhalifu kipindi cha sikukuu kwa kutumia ulinzi shirikishi, ulinzi jirani na mgambo.
“Tutashirikiana na wananchi katika ulinzi ili washerehekee kwa amani na utulivu na tutakaowabaini wanaofanya matukio ya uhalifu,” alisema Matei.
Alisema kuwa katika ulinzi jirani wananchi wanatakiwa kuacha tabia ya kuondoka nyumbani bila ya kuacha mtu au hata kama wanatoka wawajulishe majirani zao.
“Baadhi ya vitendo viovu vinavyofanyika ni pamoja na uchomaji matairi ni kinyume cha sheria na hairuhusiwi kufanya hivyo,” alisema Matei.
Aidha alisema kuwa wazazi wanapaswa kutowaacha watoto wao kwenda kwenye maeneo ya starehe peke yao kwani ni hatari.
Aliwataka madereva kuhakikisha wanaendesha magari wakiwa hawajalewa ili kuepukana na ajali pia watawapima ulevi madereva hao kwani vifaa vya kupimia sasa wanavyo vya kutosha.
Mwisho.

Tuesday, December 23, 2014

AMWUA MWANAE KWA KUMNYONGA ADAKWA NA HEROIN

Na John Gagarini, Kibaha
ESTER Endrew (23) mkulima mkazi wa Tabata Jijini Dar es Salaam anashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Pwani kwa tuhuma za kumwua mwanae Marko Elibariki (2) kwa kumnyonga kwa kutumia mikono.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha, kamanda wa polisi mkoani hapa Ulrich Matei alisema kuwa tukio hilo linahusishwa na wivu wa kimapenzi.
Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea saa 2 asubuhi eneo la Wipas mtaa wa mkoani B kata ya Tumbi wilayani Kibaha.
“Mtuhumiwa baada ya kutekeleza tukio hilo naye alijichoma tumboni kwa kisu hali iliyosababisha apate majeraha,” alisema Kamanda Matei.
Alisema kuwa mtuhumiwa huyo baada ya tukio baadhi ya majirani waligundua kutokana na kulalamika huku damu zikimtoka.
“Alijijeruhi tumboni kwa kisu akitaka kujiua lakini hata hivyo licha ya kujichoma hakufa na kuanza kupiga kelele ndipo majirani walipotoa taarifa polisi na mtuhumiwa kuja kuchukuliwa ambapo ilibainika kuwa alikuwa akimlaumu mumewe kuwa na mke mwingine,” alisema Kamanda Matei.
Aidha alisema mtuhumiwa amelazwa kwenye hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Tumbi kwa matibabu huku akiwa chini ya ulinzi.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SHAMBA Malela (20) mkazi wa Nianjema wilayani Bagamoyo mkoani Pwani anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kupatikana na kete 136 za dawa aina ya Heroin.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa na polisi waliokuwa doria.
Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea Desemba 22 mwaka huu majira ya saa 7:45 mchana huko Nianjema kata ya Magomeni wilaya ya Bagamoyo.
“Mtuhumiwa baada ya kutiliwa mashaka alikwenda kupekuliwa nyumbani kwake na kukutwa na dawa hizo ambazo zinadhaniwa kuwa ni za Heroin ambapo hata hivyo thamanai yake haikuweza kufahamika mara moja.
Alisema kuwa jeshi hilo linafanya doria kwenye maeneo mbalimbali ya wilaya za mkoa huo ili kukabiliana na matukio mbalimbali ya uhalifu.
Mwisho.

Sunday, December 21, 2014

Saturday, December 20, 2014

RIDHIWANI AKARIBISHWA KIJIJINI MSOGA KWA SHEREHE ZA JADI

Na John Gagarini, Chalinze

MBUNGE wa Jimbo la Chalinze Wilayani Bagamoyo mkoani Pwani  Ridhiwani Kikwete juzi alifanyiwa sherehe za jadi za kabila la Kikwere kama kiongozi baada ya kuchaguliwa kuwa mbunge.

Sherehe hizo za jadi ambazo zilifanyika kijijini kwao Msoga ziliambatana na kukabidhiwa vitu mbalimbali vya kijadi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Baadhi ya vitu alivyoakabidhiwa na mzee wa kabila hilo Zaidi Rufunga ni pamoja na fimbo kama kiongozi, kitanda cha kamba, msuli, kigoda na kinu pamoja na vitu mbalimbali.


Sherehe hizo za kijadi ziliamabatana na ngoma ya Kikwere na ulaji wa chakula kiitwacho Bambiko ambacho hutumiwa na kabila hilo. 

 Mzee Zaidi Rufunga kulia akimkabidhi vyungu mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete wakati wa sherehe za jadi za kumkaribisha nyumbani zilizofanyika juzi kijiji cha Msoga. 




 Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani  akielekezwa jambo na mzee Zaidi Rufunga  kabla ya kula chakula cha jadi cha kabila la Wakwere kiitwacho Bambiko baada ya kukaribishwa nyumbani na kufanyiwa sherehe za jadi za kikabila zilizofanyika kwenye Kijiji cha Msoga.




Baadhi ya akina mama wakila chakula mcha jadi cha kabila la Kikwere kiitwacho Bambiko mara baada ya kumkaribisha nyumbani Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani

 Baadhi ya akina mama wakila chakula mcha jadi cha kabila la Kikwere kiitwacho Bambiko mara baada ya kumkaribisha nyumbani Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani

Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kushoto na katikati diwani wa kata ya Msoga Mohamed Mzimba na baadhi ya wageni wakila chakula cha jadi kiitwacho Bambiko mara baada ya sherehe za jadi za kumkaribisha nyumbani kwenye Kijiji cha Msoga .


Friday, December 19, 2014

HABARI ZA PWANI

Na John Gagarini, Chalinze
KATIKA kutekeleza mpango wa Matokeo ya haraka (BRN) Wizara ya Afya imesema kuwa iko katika maongeza na wafadhili kwa ajili ya kujenga viwanda vya kuzalisha dawa kwa ajili ya kutibu magonjwa mbalimbali badala ya kutegemea kuagiza dawa kutoka nje ya nchi.
Asilimia 80 ya dawa zinaotumika zinaagizwa toka nje ya nchi na kuifanya nchi kutumia gharama kubwa kwa ajili ya kuagiza dawa hizo ambapo endapo kutakuwa na viwanda vingi kutasaidia kupunguza gharama.
Hayo yalisemwa na katibu mkuu wa Wizara ya Afya Donan Mmbando, kwenye Kijiji cha Msoga alipotembelea ujenzi wa kituo cha afya cha kijiji hicho na kusema kuwa dawa bado ni changamoto kubwa.
“Mpango huu kama ulivyo kwenye sekta nyingine utatupima kwa kipindi cha miaka mitatu kutuona je temeweza kufikia malengo ambapo kati ya malengo hayo ni kuhakikisha upatikanaji wa dawa, upatikanaji wa vifaa tiba na mambo mengine,” alisema Mmbando.
Alisema BRN itafanikiwa endapo kutakuwa hakuna tatizo la upatikanaji wa dawa pamoja na vifaa tiba ambavyo vimeonekana kuwa ni changamoto kubwa.
“Mbali ya changamoto ya upatikanaji wa dawa pia kuna baadhi ya watumishi wanaojihusisha na wizi wa dawa hawa sasa tutawakamata na kuwatangaza kwenye vyombo vya habari,” alisema Mmbando.
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa ujenzi wa Kituo hicho cha afya ambacho ni cha kisasa ni ukombozi kwa watu wa Jimbo hilo ambao hutegemea kuwapeleka wagonjwa kwenye hospitali ya Tumbi.
Ridhiwani alisema kuwa pia majeruhi wa ajali ambao walikuwa wakipelekwa Tumbi sasa watapata huduma hapo ambapo wanatarajia kituo hicho kufunguliwa mwezi Machi mwakani.
Naye diwani wa kata ya Msoga Hussein Mzimba alisema kuwa kituo hicho kinajengwa kwa nguvu ya wananchi, serikali pamoja na wadau wa maendeleo wa kata na wilaya hiyo.
Mwisho.

19,Des
Na John Gagarinii, Chalinze
KITUO cha Afya cha Chalinze wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani kinakabiliwa na ukosefu wa gari la kubebea wagonjwa kwa kipindi cha miezi mine jambo ambalo linasababisha wagonjwa kukodisha magari kwa ajili ya kupelekwa kwenye hospitali kubwa ikiwemo ya Tumbi.
Hayo yalisemwa na Mganga mkuu mfawidhi wa kituo hicho, Dk Victor Bamba wakati wa ziara ya mbunge wa jimbo la Chalinze,Ridhiwani Kikwete alipotembelea kituo hicho na kuangalia changamoto zinazoikabili sekta ya afya.
“Changamoto hii imetokana na imetokana na gari la wagonjwa lililopo kuwa kwenye matengenezo kwa muda wote huo,” alisema Dk Bamba.
Kwa upande wake Ridhiwani alisema kuwa tayari kuna mkakati wa kuhakikisha kunakuwepo na magari ya kubebea wagonjwa matatu mkakati utakaotekelezwa mapema mwaka ujao.
“Magari hayo yatagawiwa katika kituo cha afya Chalinze, Miono na kituo cha afya Msoga ambacho kinatarajia kukamilika hivi karibuni,” alisema Ridhiwani.
Kituo cha afya Chalinze kinakabiliwa na changamotombalimbali ikiwa ni pamoja na uhaba wa madawa, chumba cha kuhifadhia maiti, vifaa vya kujifungulia mama wajawazito ambapo kwa miezi 12 sasa havijasambazwa katika kituo hicho.
Mwisho.


Na John Gagarini, Kibaha
IMEELEZWA kuwa ajali kwa sasa zinaonekana kama ugonjwa usioambukiza ambao unaua watu wengi kwa sasa hapa nchini.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na mkurugenzi wa Elimu Mafunzo na Uenezi wa kamati ya usalama Barabarani Taifa Henry Bantu, wakati wa kilele cha siku ya usalama barabarani mkoani Pwani.
Alisema kuwa ajali kwa sasa zinaelekea kuwa ugonjwa unaoua kuliko magonjwa mengine kwani mwelekeo ndiyo unaoonekana.
“Endapo jitihada za kuzuia ajali hazitafanyika ajali ndiyo zitakuwa ni ugonjwa usioambukiza unaoua watu wengi nchini kwa sasa lakini hata hivyo baraza linajitahidi kuhakikisha ajali zinapungua,” alisema Bantu.
Bantu alisema kuwa madereva wanapaswa kuwa makini katika uendeshaji wa magari ili kupunguza ajali zisizo za lazima.
“Ajali nyingi siyo bahati mbaya kama wanavyosema watu bali ajali zinatokana na uzembe na si mpango wa Mungu hivyo umakini unatakiwa kuwepo,” alisema Bantu.
Awali akisoma risala ya kamati ya usalama barabarani mkoa Shaban Nkindwa alisema kuwa katika kipindi cha Januari Mosi hadi Novemba 30 jumla ya watu 556 walifariki dunia.
Nkindwa alisema kuwa ajali kwa jumla zilikuwa 1,859 za vifo zilikuwa 424 huku zilizojeruhi zikiwa 1,126 na watu waliojeruhiwa walikuwa 2,601.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani limekusanya kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni mbili kutokana na makosa madogo madogo ya usalama barabarani yaliyotokea kwa kipindi cha Januari hadi Novemba mwaka huu.
Akisoma risala ya kamati ya usalama barabarani mkoa wa Pwani, wakati wa kilele cha siku ya usalama barabarani zilizofanyika jana mjini Kibaha, Shaban Nkwinda alisema kuwa fedha hizo zilitokana na makosa yaliyotokana na makosa yaliyofanywa na madereva.
Nkwinda alisema kuwa makosa yaliyokamatwa yalikuwa 80,786 ambapo ni ongezeko la ajali 23,839 sawa na asilimia 41.8 ikilinganishwa na mwaka jana.
“Makosa yaliyolipiwa yalikuwa 80,259 ikiwa ni ongezeko la ajali 24,293 sawa na asilimia 43.4 ikilinganishwa na mwaka jana,” alisema Nkwinda.
Alisema kuwa kwa kipindi cha mwaka jana mkoa uliweza kukusanya kiasi cha shilingi zaidi ya bilioni moja kutokana na makosa 56,946 kutokana na makosa yaliyolipiwa na 55,966.
Mwisho.


Tuesday, December 16, 2014

TATIZO LA MAJI CHALINZE KUWA HISTORIA NA KIBAHA YAENDELEA KUKIMBIZANA NA MAABARA

Na John Gagarini, Kibaha
CHANGAMOTO ya maji wilayani Bagamoyo mkoani Pwani huenda ikawa historia baada ya serikali ya India kutoa kiasi cha bilioni 800 kwa ajili ya mradi wa maji wa Wami Chalinze.
Akizungumza na waandishi wa habari mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa fedha hizo zitasaidia kukabiliana na tatizo hilo ambalo limekuwa likiwasumbua wananchi wa wilaya hiyo.
Ridhiwani alisema kuwa fedha hizo ambazo ni sehemu ya mkopo baada ya ziara ya Waziri Mkuu wa nchi ya India alipotembelea nchini hivi karibuni.
“Fedha hizi zitasaidia kwa kiasi kikubwa kukamilisha mradi huo ambao umekwama kwa baadhi ya maeneo kutokana na mkandarasi aliyepewa kazi hiyo kutotengeneza miundombinu kwa kiwango kinachotakiwa,” alisema Ridhiwani.
Alisema mbali ya kujenga miuondombinu ya kufika kwenye vijiji mbalimbali pia fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kujenga mabwawa ya muda kwa ajili ya kuhifadhi maji na kuchujia maji.
“Wakati mwingine maji yamekuwa yakitoka machafu kutokana na maji kuingiwa na tope hasa pale mvua inaponyesha hivyo tunatarajia kuwe na matanki ambayo yatachuja maji kwani yaliyopo ni machache,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisema pia kutajengwa vioski na matenki kwenye vitongoji na vijiji 20 kwani baadhi viko umbali mdogo  kwenye baadhi ya matenki lakini havipati maji.
Alibainisha kuwa Jimbo la Chalinze baada ya muda mfupi itaepukana na adha ya maji kwani watakuwa na uhakika wa kupata maji safi na salama kupitia mradi huo kama baadhi ya maeneo.
Na John Gagarini, Kibaha
WILAYA ya Kibaha mkoani Pwani imefikia asilimia 80 ya ujenzi wa maabara kwenye shule za sekondari na inatarajia kukamilisha ujenzi huo mwishoni mwa mwezi huu.
Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba alisema kuwa wilaya hiyo imeweza kujenga maabara 53 katika kipindi cha miezi miwili cha agizo la Rais Dk Jakaya Kikwete.
Kihemba alisema kuwa kulikuwa na changamoto kubwa ambazo zimechangia ujenzi huo kushindwa kukamilika kwa asilimia 100 ambapo kwa sasa zimebakia maabara 10.
“Changamoto kubwa ilikuwa ni wenyeviti wa mitaa na viji kujiuzulu kabla ya uchaguzi kwani wao ndiyo wahamasishaji wakuu wa kukusanya michango pia mwitikio wa wananchi kuchangia kuwa mdogo na suala la akaunti ya Tegeta Escrow kushusha uchangiaji kutokana na wapinzani kutumia sababu ya wananchi wasichangie,” alisema Kihemba.
Alisema kuwa wilaya yetu ina jumla ya shule 21 ambapo kila shule inatakiwa kujenga maabara 3 hivyo kufanya wilaya kuhitaji maabara 63 na thamani ya kila maabara ni shilingi milioni 60.
“Tunawashukuru wadau wetu mbalimbali wa maendeleo na wananchi ambao walitusaidia fedha kwa ajili ya kufanikisha ujenzi wa maabara hizi na tunaendelea kuwaomba watusaidie ili tuweze kukamilisha ujenzi huo kama tulivyopanga,” alisema Kihemba.
Mkuu huyo wa wilaya ya Kibaha alisema kuwa anamshukuru Rais kwa kuwapa msukumo wa ujenzi wa maabara kwani kwa kipindi kifupi maabara nyingi zimejengwa ambazo zitakuwa na manufaa makubwa kwa wanafunzi.

Mwisho.

Monday, December 15, 2014

SOKA WANAWAKE PWANI WAINGIA KAMBINI KUJIANDAA TAIFA CUP

Na John Gagarini, Kibaha
TIMU ya soka ya wanawake ya mkoa wa Pwani imeingia kambini kwenye shule ya sekondari ya Baden Powell iliyopo wilayani Bagamoyo kujiandaa na mchezo wake na timu ya mkoa wa Morogoro utakaochezwa Desemba 28 mwaka huu.
Mchezo huo ambao utapigwa kwenye uwanja wa Mabatini Mlandizi wilayani Kibaha wa kuwania kombe la Taifa kwa wanawake.
Akizungumza na gazeti hili mjini Kibaha, katibu wa chama cha soka la Wanawake (TWFA) mkoa wa Pwani Florence Ambonisye alisema kuwa maandalizi ya mchezo huo yanaendelea vizuri.
Ambonisye alisema kuwa timu hiyo inanolewa na mchezaji wa timu ya Taifa ya Wanawake Hilda Masanche iliingia kambini wiki iliyopita.
“Timu inatarajiwa kurejea Desemba 26 wilayani Kibaha ambapo itaingia kambini kwenye kambi ya Ruvu JKT Mlandizi siku mbili kabla ya mchezo huo,” alisema Ambonisye.
Aidha alisema kuwa timu hiyo itaongezewa wachezaji wanne mara itakaporudi Kibaha ili kuipa nguvu timu hiyo inayoundwa na wachezaji wengi vijana ambao ni wanafunzi shule za sekondari.
“Changamoto kubwa inayoikabili timu hiyo ni ukosefu wa vifaa kwani wachezaji wanatumia vifaa vyao binafsi walivyoendanavyo kambini,” alisema Ambonisye.
Alibainisha kuwa wanatarajia kushinda mchezo huo kwani timu yao imejiandaa vyema na mchezo huo licha ya kuwa wapinzani wao nao wako vizuri na wana uhakika wa kuingia 16 bora.
Mwisho.

CCM YAONGOZA MATOKEO YA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA, VITONGOJI NA VIJIJI

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Pwani kimeonyesha kufanya vizuri kwenye uchaguzi wa serikali za Mitaa, Vitongoji na Vijiji ambapo kwenye matokeo ya awali kimeonekana kushinda maeneo mengi.
Katika Jimbo la Mafia CCM ilishinda vitongoji  96 kati ya 136 sawa na asilimia 70 Chama Cha Wananchi CUF asilimia 40 sawa na asilimia 29,katika vijiji  CCM ilishinda vijiji 19 kati ya 23 sawa na asilimia 82.6 CUF vijiji 4 sawa na asilimia 17.3.
Katika Jimbo la Kibaha Mjini kati ya mitaa iliyopo 73 ,CCM imeshinda mitaa 62 sawa na asilimia 84.9, huku wapinzani wao Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wakishinda kwenye mitaa 10 sawa na asimilia 13.7.
Katika Jimbo Kibaha  Vijijini kwenye Vijini 32 CCM ilishinda mitaa 31 , ambapo kwenye mitaa 10 ilishinda bila kupingwa sawa na asimilia 96.9 ,upinzani ilishinda kijiji kimoja sawa na asimilia 13.1, kati ya vitongoji 106 CCM ilishinda vitongoji 98 sawa na asilimia 92.5,upinzani vitongoji 4 sawa na asilimia 3.8.
Katika Wilaya ya Bagamoyo vijiji vilivyopo ni 75 CCM ilishinda vijiji 67 sawa na asilimia 90.5 na vijiji 8 havijafanya uchaguzi, kati ya vitongoji  610 CCM ilishinda 540 sawa na asilimia 88.5 na vitongoji 45 havijafanya uchaguzi ambapo wapinzani walishinda vitongoji sawa na  asilimia 4.1.
Wilaya ya Bagamoyo haijafanya uchaguzi katika vijiji 8 na vitongoji 45 kutokana na uhaba wa vifaa ikiwemo katasi husika za viti maalum na kuchanga majina ya wananchi na nembo za vyama vya siasa.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Bagamoyo Ibrahim Matovu alithibitisha kutokea kwa mabadiliko ya uchaguzi katika maeneo hayo ambapo alisema uchaguzi huo baadhi ya maeneo ulifanyika jana na kwingine utafanyika leo desemba 16.

Mwisho

ZAIDI YA 500 WASHINDWA KUPIGA KURA UCHAGUZI WAHAIRISHWA

Na John Gagarini, Bagamoyo
HUKU uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji ukiwa umefanyika juzi na matokeo yakiendelea kutoka wananchi 514 wa Kijiji cha Mwetemo Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo wameshindwa kupiga kura kutokana na uhaba wa karatasi za kupigia kura.
Uchaguzi huo ulishindwa kufanyika kutokana na karatasi za kupigia kura kuwa chache hivyo watu wengine kushindwa kupiga kura ambapo watafanya uchaguzi huo Desemba 19.
Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kitongoji hicho kuangalia zoezi hilo la upigaji kura wa kuchagua viongozi akiwemo mwenyekiti na wajumbe watano msimamizi msaidizi wa uchaguzi Thomas Madega alisema kuwa wamekubaliana uchaguzi huo kufanyika siku hiyo.
“Karatasi za kupigia kura kwanza zilichelewa kwani zilifika kituoni saa 10 kasoro jioni na pia zilikuwa chache hivyo watu wachache walipiga kura na wengine walishindwa kupiga kabisa,” alisema Madega.
Madega alisema kuwa walikaa na viongozi wa vyama vyote na kukubaliana kusogezwa mbele zoezi la upigaji kura.
“Tumekubaliana na vyama vyote kusogeza uchaguzi huo hadi Ijumaa na wamekubali tumewaambia wawatangazie wafuasi wao juu ya hili,” alisema Madega.
Juu ya kuahirisha kwa muda mrefu tofauti na maeneo mengine ambayo yalikuwa na matatizo na uchaguzi kufanyika jana alisema kuwa wametoa muda mrefu ili waandaliwe vifaa vya upigaji kura kwa uhakika.
Kwa upande wake mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete alisema kuwa muda huo ni mrefu sana kwani maeneo mengine yalifanya uchaguzi kesho yake.
“Nadhani suala la siku ya kupiga kura lirudishwe nyuma kwani Ijumaa ni mbali sana hivyo kuna haja ya wahusika kuliangalia hilo ili wasipishane na wengine,” alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alishauri zoezi la namna ya kupiga kura washirikishwe zaidi wananchi kwani wale wanaowachagua ni viongozi wao hivyo wao ndiyo wenye nafasi kubwa ya kushauri na si viongozi wa vyama vya siasa.
Baadhi ya vijiji na vitongoji ambavyo vilifanya uchaguzi wao jana Jumatatu badala ya Jumapili ni Kijiji cha Changarikwa, Vitongoji vya Kwamkula, Mkambala A na B, Kwaluguru A na B, Pugwe, Migola na Kwadivumo kwenye kata ya Mbwewe.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo Ibrahim Matovu alipoulizwa juu ya baadhi ya maeneo kushindwa kupiga kura alisema kuwa bado hajapata takwimu sahihi ndiyo anafuatilia kujua changamoto hizo.
Uchuguzi mdogo uliofanywa na mwandishi wa habari hizi ulibaini zoezi la upigaji kura ulikumbwa na changamoto kadhaa ikiwemo ukosefu wa vifaa vya upigaji kura kama vile upungufu wa karatasi, picha za wagombea kuwekwa kwenye nembo ya chama kisichohusika na kukosekana kwa  fomu za wagombea wa nafasi ya ujumbe.

Mwisho.


Picha no 3942 msimamizi msaidizi wa kituo cha kupigia kura Kitongoji cha Mkwajuni kwenye Kijiji cha Miono wilaya ya Bagamoyo Faustina Oforo  akisubiria wapiga kura wa uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa. 


Picha no 3940 Msimamizi msaidizi wa uchaguzi kitongoji cha Msikitini kwenye Kijiji cha Mbwewe wilaya ya Bagamoyo Said Mlinde kulia akiongea na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kushoto alipotembela kituo hicho kushuhudia zoezi la upigaji kura.
 

Monday, December 8, 2014

CHADEMA WATISHIA KUANDAMANA

CHAMA Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani kimetoa siku mbili hadi Desemba 10 kwa Katibu Tawala wa Wilaya (DAS) Kibaha kuwarejesha wagombea wa nafasi mbalimbali kupitia chama hicho na endapo hatawarejesha watafanya maandamano kushinikiza warudishwe kuwania nafasi hizo.
Jumla ya wagombea 16 wa chama hicho wameondolewa kwenye kinyanganyiro cha kuwania nafasi za uongozi kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Deemba 14 mwaka huu, wakiwemo wenyeviti na wajumbe, kutokana na sababu mbalimbali za kukiuka sheria za uchaguzi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha mwenyekiti wa chama hicho Jimbo la Kibaha Mjini Mohamed Mnembwe alisema kuwa wametoa siku mbili Jumatatu na Jumanne ambapo Jumatano wataandamana kama endapo DAS hatawarejesha wagombea hao kwenye kinyanganyiro hicho.
Mnembwe alisema kuwa maandamano hayo watayafanya kuanzia kwenye ofisi za chama kwenda kwa DAS kudai haki za wagombea wao.
“Kuandamana ni haki ya kikatiba na si kuvunja sheria ni kutaka wagombea wetu warejeshwe kwani wameondolewa kwa uonevu na hawakutendewa haki kwani sababu zenyewe za kuwaengua si za halali,” alisema Mnembwe.
Alisema wagombea wao hawakupewa nafasi ya kupeleka ushahidi kwani wengi walienguliwa kwa madai kuwa si wakazi wa maeneo waliyoomba uongozi na kukosea kujaza fomu ikiwa ni pamoja na mtaa na mahali wanapoishi.
“Wengi waliwekewa pingamizi kuwa si wakazi wa maeneo hayo lakini wangethibitisha kwa kuwaita wahusika wakiwemo wenye nyumba kwani kusema kuwa balozi hamtambui si sawa kwani sisi pia tuna mabalozi wetu kikubwa wangepata ushahidi kama kweli si wakazi wa maeneo hayo, kwa upande wa ujazaji wa fomu ni mahali unapoishi na mtaa ndiyo walivyokosea na majina yao kuondolewa,” alisema Mnembwe.
Aidha alisema kuwa wao wanachotaka ni wagombea wao kurejeshwa kwenye nafasi za kuwania nafasi hizo na endapo DAS atafanya hivyo hawatafanya maandamano kwani wanataka uchaguzi huo ufanyike kwa amani na utulivu.
“Tunajua muda umeisha ila wakirejeshwa tunauhakika wa kushinda kwenye uchaguzi huo na tutatoa taarifa polisi ili kuomba ulinzi kwani maandamano yetu ni ya amani na hatuna nia ya kufanya vurugu kikubwa tunachotaka ni haki kutendeka,” alisema Mnembwe.
Mwenyekiti huyo wa CHADEMA Jimbo la Kibaha alitaja maeneo ambako wagombea wake wameondolewa kuwa ni Maili Moja 2, Kongowe 6, Visiga 3, Vikawe Shuleni 1,Miswe Chini 1 na Miwaleni 3.
Hivi karibuni DAS Sozi Ngate alipoulizwa kuhusiana na malalamiko hayo alisema kuwa kama wanaona wameonewa waende mahakamani kudai haki yao.
Mwisho.


















AFA KWA KUCHOMWA KISU NA WATU WASIOFAHAMIKA

Na John Gagarini, Kibaha
MTU mmoja aliyefahamika kwa jina la Juma Abdala (65) mkulima wa Kitongoji cha Kwa Mwaleni kijiji cha Mbwewe kata ya Mbwewe wilayani Bagamoyo mkoani Pwani amekufa kwa kuchomwa kwa visu na watu wasiofahamika.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo walisema kuwa mzee huyo aliitwa na vijana wawili waliofika nyumbani kwake na kumwita pembezoni mwa nyumba yake kisha kumshambulia na kumwua.
Akizungumza kwa njia ya simu na mwandishi wa habari hizi ofisa mtendaji wa kijiji cha Mbwewe Ramadhan Mwanaagonile alisema kuwa tukio hilo lilitokea Novemba 6 mwaka huu majira ya saa 1:30 usiku Kitongojini hapo.
Mwanaagonile alisema kuwa siku ya tukio vijana hao ambao hawafahamiki walifika nyumbani kwa marehemu na kumtaka waongee naye wakati huo marehemu alikwenda kwenye kibanda jirani kwa ajili ya kunywa kahawa.
“Watu hao walipomuulizia marehemu walijibiwa kuwa hayupo walitaka aitwe ili waongee naye ndipo alipoitwa na kumtaka wakazungumze pembeni na ndipo walipokwenda kwenye ua wa nyumba yake na kuanza kuongea,” alisema Mwanaagonile.
Alisema baada ya muda walisikia marehemu akipiga kelele kuomba msaada huku akisema kuwa anakufa na walipokwenda walikutwa kachomwa kisu kitovuni na kifuani na mkononi.
“Marehemu alijaribu kukimbia kwenda waliko watu lakini alishindwa na kuanguka na watu walipofika walimkuta akiwa anatokwa na damu nyingi ambazo zilisababisha kifo chake huku wale watu wakiwa hawaonekani kwani walikimbia kusikojulikana,” alisema Mwanaagonile.
Aidha alisema taarifa zilitolewa kituo cha Polisi cha Mbwewe ambao walifika na kuuchukua mwili wa marehemu na baadaye mwili ulichunguzwa na daktari kisha kukabidhiwa ndugu kwa ajili ya mazishi.
“Tulijaribu kuwatafuta vijana hao bila ya mafanikio na hatukukuta chochote pale palikotokea tukio watu hao hawakumchukulia kitu chochote kwnai alikuwa na simu na vitu vingine lakini waliviacha,” alisema Mwanaagonile.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo alisema bado halijafikishwa ofisini kwake na kusema kuwa atafuatilia na kulitolea taarifa.
Mwisho.



Sunday, December 7, 2014

OUT KUTUMIA MAMILIONI KUFUNDISHA WALIMU WA MASOMO YA SAYANSI



Na John Gagarini, Kibaha
CHUO Kikuu Huria Tanzania (OUT) kimepata fedha kiasi cha dola za Kimarekani milioni 50 kutoka benki ya dunia kwa ajili ya kuwajengea uwezo walimu wa masomo ya Sayansi na Hisabati hapa nchini.
Aidha fedha hizo pia zitatumika kwa ajili ya kujenga maabara mchanganyiko, mabweni na ofisi za walimu kwa lengo la kuboresha ufundishaji wa masomo chuoni hapo.
Hayo yalibainishwa na mgeni rasmi kwenye mahafali ya kwanza ya OUT kituo cha mkoa wa Pwani, Naibu Makamu Mkuu wa chuo hicho kitengo cha Teknolojia za Kujifunzia na Huduma za Mikoa Profesa Modest Varisanga.
Prof. Varisanga alisema kuwa kuna uhaba mkubwa wa walimu wa masomo hayo hivyo wameamua kuwekeza kwenye masomo hayo kwani ndiyo msingi wa kupata wataalamu mbalimbali.
“Chuo kinaendelea kujiimarisha kwenye maeneo mbalimbali pamoja na kuhakikisha tunazalisha wataalamu na msingi ni masomo ya Sayansi ndiyo sababu ya kuweka mkakati wa makusudi wa kuwawezesha na kuwajengea uwezo walimu hao wanaosoma kwenye chuo chetu,” alisema Prof Varisanga.
Alisema kuwa fedha hizo pia zitatumika kujenga maabara mabweni na ofisi za walimu ili kuboresha utoaji elimu kwa wanachuo ambao hupata masomo yao kwa elimu ya masafa.
Katika hatua nyingine alisema kuwa wameiomba serikali kuvibadili vyuo hivyo kutoka vituo hadi kuwa vyuo vya mikoa ambapo maombi hayo yamefikishwa kwenye baraza la Mawaziri na yamekubaliwa huku kwa sasa mchakato ukiwa unaendelea.
Kwa upande wake mkurugenzi wa kituo cha mkoa wa Pwani Abdala Alli alisema kuwa elimu ya masafa ambayo inatolewa na chuo hicho imekuwa suluhisho la elimu hapa nchini wakiwemo wanawake.
Alli alisema kuwa elimu ya masafa ndiyo elimu bora kwa sasa kwani inatolewa huku kwa wale watumishi wakiendelea kufanyakazi bila ya kuathiri utendaji kazi tofauti na elimu ya moja kwa moja ambayo humtaka mwanachuo kukaa darasani pamoja na kuwa kwenye bweni ambapo gharama zake ni kubwa.
Akisoma risala ya wahitimu Stella Mapunda alisema kuwa kituo chao kinakabiliwa na uhaba wa walimu pamoja na kumbi za mikutano na mihadhara kwa ajili ywa wanachuo kujadiliana na kujifunzia.
Mapunda alisema kwa sasa wanatumia majengo ya Shirika la Elimu Kibaha ambayo hayatoshelezi mahitaji ya wanachuo ambapo kumekuwa na ongezeko la udahili wa wanachuo wapya kila mwaka.
Jumla ya wahitimu 98 toka kituo cha mkoa wa Pwani walihitimu na kutunukiwa vyeti ngazi mbalimbali kwenye mahafali ya Kitaifa yaliyofanyika kwenye makao makuu ya chuo hicho yaliyopo Bungo wilayani Kibaha wiki iliyopita.
Mwisho.