Friday, June 20, 2014

WATATU WADAKWA NA SILAHA NA SARE ZA JESHI

Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani limefanikiwa kuwakamata watu watatu akiwemo mtu Daniel Mtalisi mkazi wa Kisemvule wilaya ya Mkuranga ambaye alipitia mafunzo ya kijeshi kwa tuhuma za kufanya tukio la uhalifu wa kupora silaha na vitu mbalimbali.
Mtuhumiwa huyo ambayealiwahi kupata mafunzo ya kijeshi kwenye Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kikosi namba 833 Oljoro Arusha na namba yake ni MT. 95150.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kwa waandishi wa habari mjini Kibaha, kamanda wa Polisi mkoani humo Kamishna Mwandamizi Msaidizi wa Polisi (SACP) Ulrich Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea Juni 17 mwaka huu majira ya saa 2 usiku huko Kijiji cha Kisemvule kata ya Vikindu kata ya Mkuranga wilaya ya Mkuranga.
Kamanda Matei alisema kuwa watuhumiwa hao wengine wakiwa ni Khalfan Abas (25) mkazi wa Mwanambaya na Mashaka Masanja (24) mkazi wa Mwongozo Kigamboni Jijini Dar es Salaam walikamatwa baada ya polisi kufanya msako mkali na kumkuta mtuhumiwa huyo akiwa na silaha hiyo ambayo walimpora Musa Kambangwa ambaye ni mfanyabiashara wa Mwanambaya.
“Watu hao walimvamia mlalamikaji ambaye alikuwa akirejea nyumbani kutoa kwenye biashara zake walimteka kisha kumpiga na walimwamuru awapeleke nyumbani kwake na kuichukua silaha hiyo bastola yenye namba A 569542 aina ya Browning, Carriber 7.65 mm, magazine 2 na risasi 23, chaja 1 ambavyo alikuwa amehifadhi nyumbani kwake,” alisema Kamanda Matei.
Aidha Kamanda Matei alisema kuwa kabla ya kukamatwa watuhumiwa hao walifanya tukio hilo Juni 11 mwaka huu huko Kijiji cha Mwanambaya ambapo walimvamia mlalamikaji akiwa na mke wake.
“Walimjeruhi kwa kutumia silaha mbalimbali za jadi na kumsababishia maumivu makali kisha kumtaka awape funguo ya nyumba yake ili waingie ndani lakini alikataa wakaendelea kumpiga hadi alipopoteza fahamu na kuichukua funguo na kuingia ndani na kuchuakua silaha hiyo na simu 2 aina ya Nokia, Inveta , deki 1 ya Dvd  na viatu pea moja kisha kutoweka na ndipo walipokuja kukamatwa Juni 17,” alisema Kamanda Matei.
Alisema kuwa baada ya tukio hilo ndipo walipofanya msako na kufanikiwa kuvikuta vitu hivyo ambapo mtuhumiwa wa kwanza alikutwa na sare za Jeshi.
Alibainisha kuwa mlalamikaji anaendelea vizuri na kuwataka watu kutoa taarifa za uhalifu ili kuzuia matukio hayo ambayo yameanza kuibuka kwa wingi na watuhumiwa hao wanatarajiwa kufikishwa mahakamani mara upelelezi wa tukio hilo utakapokamilika.
Mwisho      

Monday, June 16, 2014

WANAJESHI WAWILI WAFA AJALINI



Na John Gagarini, Kibaha
WATU wawili wamefariki dunia huku mmoja akijeruhiwa baada ya magari waliyokuwa wakisafiria kugongana uso kwa uso.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa Polisi mkoani Pwani, kamishna Msaidizi mwandamizi wa polisi (SACP) Ulrich Matei amesema kuwa ajali hiyo ilihusisha lori na gari dogo.
Kamanda Matei alisema kuwa ajali hiyo ilitokea Juni 16 mwaka huu majira saa 1:15 usiku eneo la Chamakweza kata ya Pera tarafa ya Chalinze wilayani Bagamoyo.
Alisema ajali hiyo ilihusisha lori aina ya Scania lenye namba za usajili T 164 AUS na tela namba T 498 AZ likiendeshwa na Hassan Shaban mkazi wa Dar es Salaam ambaye aligongana na gari aina ya Isuzu Carry lenye namba za usajili Z 190 DR likitokea mkoani Morogoro.
“Waliokufa ni  dereva wa gari dogo Meja Edward Mosi ambaye ni ofisa wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kikosi cha Kinonko na mkaguzi Msaidizi wa Polisi wa wilaya ya Korogwe mkoani Tanga Johnson Zakaria,” alisema Matei.
Aidha alisema katika ajali hiyo mtu mmoja alijeruhiwa na kukimbizwa hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani Tumbi kwa ajili ya matibabu huku miili hiyo nayo ikiwa hospitalini hapo kusubiri ndugu kwa ajili ya mazishi.
“Kutokana na ajali hiyo jeshi la polisi linamtafuta dereva wa lori ambaye alikimbia mara baada ya tukio hilo, ili aweze kufikishwa kwenye vyombo vya sheria,” alisema Matei.
Mwisho.    

Tuesday, June 10, 2014

WAFANYABIASHARA WATAKIWA KUPIMA AFYA ZAO



Na John Gagarini, Kibaha
IDARA ya Afya ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani imeanza uhakiki wa wafanyabiashara mbalimbali kama wamepima afya zao kwa mujibu wa sheria ili watoe huduma hizo wakiwa na afya njema na endapo watashindwa kufanya hivyo watafungiwa biashara zao.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake jana  mjini Kibaha ofisa afya wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha David Vuo alisema kuwa wafanyabiashara hao pamoja na wamiliki wa viwanda wanapaswa kuhakikisha watoa huduma wao wanapima afya zao.
“Utaratibu huu ni wa kisheria kwani hata wafanyakazi wa serikali kabla ya kuanza kazi wanapaswa kupima afya zao na hii ni sheria ya afya ya mwaka 2009 namba 169 kifungu namba 17ambapo kwa sasa maofisa afya wa kata wanafanya uhakiki kuona zoezi hilo ili taratibu stahiki zichukuliwe kwa wale watakaoshindwa kutekeleza agizo hilo ,” alisema Vuo.
Alisema kuwa jambo hilo si geni kwani liko kisheria na linawagusa wafanyabiashara wote na shughuli mbalimbali za wajasiriamali ambao wanapaswa kufuata taratibu za kiafya.
“Lengo la kupima afya na kuhakikisha kuwa wahudumu hao wanahudumia wateja wakiwa na afya njema na kama kuna atakayegundulika anapaswa kutibiwa kwanza hadi atakapopona ndipo aendelee kutoa huduma na kutakuwa na fomu maalumu itakayokuwa kwenye eneo la shughuli ili kuwatambua waliofanya hivyo na wale watakaoshindwa hawataruhusiwa kuhudumiwa watu,” alisema Vuo.
Aidha alitaja magonjwa ambayo yanapimwa kuwa ni Taifodi, Kuhara, Mkojo, magonjwa ya Kaswende, Gono, Kifua, magonjwa ya ngozi kama vile upele na mengineyo.
“Suala la kupima virusi vya ugonjwa wa UKIMWI ni hiyari ambapo upimaji wa magonjwa haya hayahusiani na kupima ugonjwa huo labda mhusika atake mwenyewe ambapo upimaji huu utafanyika kwenye hospitali ya wilaya ya Mkoani na kituo cha afya Kongowe,” alisema Vuo.
Ofisa afya huyo wa halmashauri ya Mji wa Kibaha alissema kuwa kuhusiana na uchangiaji wa vipimo hivyo kila mhusika anapaswa kutoa kiasi cha shilingi 5,000 kwenye ofisi ya kata kisha atapewa fomu kwa ajili ya kwenda kupima ambapo alisema elimu ilishatolewa.
Alitaja biashara ambazo watumishi wake wanatakiwa kupima afya zao kuwa ni mama na baba lishe, bekari, migahawa, hoteli, baa, nyumba za kulala wageni, mashine za kusaga nafaka, maduka ya vyakula, mabucha, machinjio, saluni, dobi, viwanda, wachoma chipsi, vilabu vya pombe za kienyeji, wafanyakazi wa kampuni na vikundi vya ujasiriamali.

Saturday, June 7, 2014

WATAKIWA KUKABILIANA NA TABIA NCHI



WAKAZI wa wilaya za Bagamoyo mkoani Pwani na Pangani mkoani Tanga wametakiwa kulinda misitu ikiwemo ile ya Mikoko iliyopo kandokando mwa Bahari ya Hindi ili kuinusuru wilaya hiyo na athari zitokanazo na mabadiliko ya Tabia Nchi.
Hayo yalisemwa  na mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Ahmed Kipozi alipokuwa akifungua mafunzo ya juu ya namna ya kukabiliana na mabadiliko ya Tabia Nchi kwa wajumbe wa kamati za mazingira kutoka wilaya za Bagamoyo na Pangani mkoani Tanga.
Kipozi amesema kuwa watu wengi waliathirika na mvua kubwa zilizonyesha ambazo zilileta mafuriko na kusababisha madhara yakiwemo ya watu kufa, mazao yao kusombwa na maji, miundombinu ikiwemo ya barabara na madaraja zilitokana na mabadiliko hayo ya Tabia Nchi.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi mratibu wa mafunzo hayo Dk Beno Mnembuka ambaye ni mtafiti kiongozi kwenye mradi huo unaosimamiwa na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) kwa ushirikiano na Chuo Kikuu cha Ardhi, Mamlaka ya hali ya Hewa na mtafiti mmoja toka nchini Norway amesema kuwa mabadiliko ya Tabia Nchi pia yameathiri viumbe hai kama vile samaki.
Dk Mnembuka amesema kuwa viashiria vya mabadiliko ya Tabia Nchi ni pamoja na mabadiliko ya misimu ya mvua, joto, upepo mkali wa Kasi na Kusi, ukame, mafuriko ambapo hutokana na uharibifu wa mazingira ambapo ili kukabiliana na madhara hayo lazima kurejesha uoto wa asili kwa kupanda miti na kutoharibu vyanzo vya maji.
 Naye meneja wakala wa misitu Tanzania (TFS) wilaya ya wilaya Bagamoyo Charles Mwafute amesema kuwa katika kutekeleza kwa vitendo washiriki wa mafunzo hayo walipanda miti ya Mikoko eneo la ukubwa wa hekari mbili na nusu kwenye kijiji cha Kiharaka.  
Mradi huo ambao utaisha mwezi Desemba mwaka huu unatekelezwa kwenye vijiji vya Bumbwini, Kisakasaka Zanzibar, Magomeni, Kiharaka na Kondo wilayani Bagamoyo, Matakani, Kipumbwi na Pangani Mjini wilaya ya Pangani.

Thursday, June 5, 2014

WABUNGE WA KATIBA WATAKIWA KUREJEA BUNGENI




WABUNGE wa Bunge Maalumu la Katiba ambao walisusia vikao vya bunge hilo Mjini Dodoma wametakiwa kurejea kwenye mjadala wa marekebisho ya katiba kwani kuendelea kususia ni sawa na kufanya uasi na usaliti kwa wananchi.
Wanapaswa kuheshimu mamalaka iliyopo kwa kulimaliza tatizo lililopo kwa kutumia busara kwa kukaa chini kwa pamoja na kukubaliana na si kwa kulalamika kwa kupiga kelele nje ya Bunge hilo ili suluhu ipatikane.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha Nabii Jofrey John wa Huduma ya HAKI Ministry ya Kongowe Kibaha mkoani Pwani amesema kuwa endapo wabunge hao wataendelea kususia bunge lijalo kama walivyosusa ni kwamba watakuwa wanaihujumu nchi.
Nabii John amesema kususa na kulalamika nje ya bunge hilo ni sawa na kuasi hali ambayo inaweza kujenga chuki na matokeo yake ni kuleta mafarakano ambayo mwisho wake ni mbaya kwani urithi walionao Watanzania ni amani na si vurugu
Nabii John amesema kuwa kusiwe na kundi ambalo linasusia mchakato wa kuunda katiba hiyo mpya kwani ni moja ya njia ambayo inaweza kusababisha kuvurugika kwa amani na litajenga roho za kuona kuwa wanaonewa.
Amesema kuwa haitapendeza kuona kuwa kuna wabunge wamekwenda kwenye bunge hilo kwa ajili ya kuhujumu mchakato huo kwani watasababisha kuvunja amani iliyopo ambayo imedumu kwa maiaka 50 tangu tulipopata uhuru hivyo haipaswi kuvunjwa na kundi la watu.
Amesema kiongozi yoyote awe wa chama au sehemu yoyote amechaguliwa na Mungu hivyo hapaswi kudharau mamlaka iliyopo madarakani ambayo hata Mungu anaitambua.
Aidha amesema kuwa anaamini kuwa wabunge waliochaguliwa kwenye bunge hilo la katiba ni wasomi hivyo wasijishushie heshima ya usomi wao kwani wako pale kwa niaba ya wananchi na si kwa maslahi yao binafsi bali kwa maslahi ya wananchi.
Amewataka waumini wa dini zote kufunga na kuomba kwa ajili ya amani ya nchi ili Mungu aepushe roho ya umauti katika nchi yetu ambayo inanyemelea  kutokana na sababu ambazo zinaweza kuzuilika za kumaliza tofauti ndogo ndogo zilizopo.
Ameiomba serikali kuwatumia viongozi wa dini kama sehemu ya kudumisha amani ya nchi kwa kuwafanyia maombi viongozi waliopo madarakani ili waweze kuongoza kwa kutumia hekima za Mungu kwani bila ya kuwa na maombi hayo shetani anaweza kuleta roho ya uchonganishi na kusababisha amani kutoweka.
Amebainisha kuwa kwa kipindi chote cha mwezi huu hadi ujao watakuwa na kongamano kubwa la kuiombea amani ya nchi ambapo halitakuwa na itikadi ya dini yoyote bali ni madhehebu yote hivyo kuwataka watu kujitokeza kufanya maombi hayo.
Mwisho.

Saturday, May 31, 2014

BILALI AZINDUA MFUKO WA ELIMU ACHANGIA MILIONI 10



Na John Gagarini, Kibaha
MAKAMU wa Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Mohamed Gharib Bilali ameuchangia mfuko wa elimu wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani kiasi cha shilingi milioni 10.
Alichangia fedha hizo jana wakati wa uzinduzi wa mfuko wa elimu wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha uliofanyika kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja wilayani hapa.
Alisema kuwa katika kufikia malengo ya Matokeo Makubwa Sasa (BRN) kwenye sekta ya elimu lazima kuwe mikakati maalumu ya kuweza kufikia malengo kwa kukabiliana na changamoto zilizopo kwenye sekta hiyo.
“Nawapongeza kwa kuanzisha mfuko huu na serikali itawaunga mkono kwa hali na mali na mimi nawachangia milioni 10 kwa ajili ya kukabiliana na changamoto kwenye sekta ya elimu katika mji wa Kibaha wilaya na mkoa mzima wa Pwani.
“Ningependa suala la choo kuwa historia kwani hii ni aibu na si changamoto ya kudumu na inapaswa kufanyiwa kazi mara moja na kuiondoa kabisa kwani ni jambo lisilo pendeza na changamoto nyingine zilizopo kama vile za upungufu wa madawati kwa shule za msingi, ukosefu wa maabara kwa shule za sekondari, upungufu wa nyumba za walimu, matundu ya vyoo, vyumba vya madarasa na maktaba kupitia mfuko huo utasaidia kukabiliana na hali hiyo,” alisema Dk Bilali.
Aidha alisema kuwa amefurahi kusikia kuwa fedha hizo zitatumika kujenga maabara tatu katika sekondari za Pangani, Visiga na Miembe Saba na kununua madawati 1,500 kwa ajili ya shule za msingi za Tandau, Lulanzi, Misugusugu, Zogowale, Msangani, Viziwaziwa, Vikawe, Mwanalugali, Mkuza na Kidimu.
Alizitaka halmahauri hapa nchini kuiga mfano wa Halmashauri hiyo ya Mji wa Kibaha kwa kuanzisha mifuko kama hii kwa ajili ya kutatua changamoto za elimu badala ya kuisubiri serikali kwani ni mgao inaoutoa ni mdogo na elimu na mafunzo bora ni mkakati wa kipaumbele katika kufikia malengo ya mipango ya maendeleo ya Taifa ya 2025 na kutumia Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza umaskini MKUKUTA na malengo ya milenia.
Awali Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Kasimu Majaliwa alisema kuwa ubunifu wa kupata fedha kwa ajili ya Halmashauri 167 hapa nchini ni mzuri kwnai utasaidia kukabiliana na changamoto zilizopo kwenye sekta ya elimu.
Majaliwa alisema kuwa uboreshaji wa elimu unapaswa kusimamiwa na watu wote wakiongozwa na madiwani na wananchi wote wanapaswa kujitokeza kuuchangia na wizara yake itachangia kiasi cha shilingi milioni tano.
Kwa upande wake mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka alisema kuwa amefurahishwa na uzinduzi huo ambapo alisema kuwa moja ya ndoto zake za kukabiliana na changamoto za elimu.
“Ili kuwa na elimu bora ni pamoja na kuwa na miundombinu mizuri na watu wa kuiboresha ni wazazi pamoja na wadau wote ndani ya Halmashauri licha ya kuwa wananchi wanachangamoto kubwa ya kuchangia hata hivyo wameonyesha nia ya kuchangia kwa kujitolea na mimi nawaunga mkono kwa kutoa kiasi cha shilingi milioni 16,” alisema Koka.
Awali mwenyekiti wa mfuko huo Anna Bayi alisema kuwa lengo la kuanzishwa mfuko huo ni kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia ambapo hadi sasa mfuko huo una kiasi cha shilingi milioni 210 na ahadi ni shilingi milioni 34 huku malengo yakiwa ni kukusanya kiasi cha shilingi milioni 300.
“Tunatarajia kati ya fedha hizo zitajenga maabara tatu katika shule ya sekondari Nyumbu, Miembe Saba na shule ya wasichana Kibaha ambapo tumejiwekea mikakati mbalimbali ikiwa ni pamoja na kujiunga na mfuko wa elimu nchini kwa lengo la kupata ruzuku ya miundombinu, samani, vifaa vya kufundishia na kujifunzia,” alisema Bayi.
Mwisho.