Thursday, June 5, 2014

WABUNGE WA KATIBA WATAKIWA KUREJEA BUNGENI




WABUNGE wa Bunge Maalumu la Katiba ambao walisusia vikao vya bunge hilo Mjini Dodoma wametakiwa kurejea kwenye mjadala wa marekebisho ya katiba kwani kuendelea kususia ni sawa na kufanya uasi na usaliti kwa wananchi.
Wanapaswa kuheshimu mamalaka iliyopo kwa kulimaliza tatizo lililopo kwa kutumia busara kwa kukaa chini kwa pamoja na kukubaliana na si kwa kulalamika kwa kupiga kelele nje ya Bunge hilo ili suluhu ipatikane.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha Nabii Jofrey John wa Huduma ya HAKI Ministry ya Kongowe Kibaha mkoani Pwani amesema kuwa endapo wabunge hao wataendelea kususia bunge lijalo kama walivyosusa ni kwamba watakuwa wanaihujumu nchi.
Nabii John amesema kususa na kulalamika nje ya bunge hilo ni sawa na kuasi hali ambayo inaweza kujenga chuki na matokeo yake ni kuleta mafarakano ambayo mwisho wake ni mbaya kwani urithi walionao Watanzania ni amani na si vurugu
Nabii John amesema kuwa kusiwe na kundi ambalo linasusia mchakato wa kuunda katiba hiyo mpya kwani ni moja ya njia ambayo inaweza kusababisha kuvurugika kwa amani na litajenga roho za kuona kuwa wanaonewa.
Amesema kuwa haitapendeza kuona kuwa kuna wabunge wamekwenda kwenye bunge hilo kwa ajili ya kuhujumu mchakato huo kwani watasababisha kuvunja amani iliyopo ambayo imedumu kwa maiaka 50 tangu tulipopata uhuru hivyo haipaswi kuvunjwa na kundi la watu.
Amesema kiongozi yoyote awe wa chama au sehemu yoyote amechaguliwa na Mungu hivyo hapaswi kudharau mamlaka iliyopo madarakani ambayo hata Mungu anaitambua.
Aidha amesema kuwa anaamini kuwa wabunge waliochaguliwa kwenye bunge hilo la katiba ni wasomi hivyo wasijishushie heshima ya usomi wao kwani wako pale kwa niaba ya wananchi na si kwa maslahi yao binafsi bali kwa maslahi ya wananchi.
Amewataka waumini wa dini zote kufunga na kuomba kwa ajili ya amani ya nchi ili Mungu aepushe roho ya umauti katika nchi yetu ambayo inanyemelea  kutokana na sababu ambazo zinaweza kuzuilika za kumaliza tofauti ndogo ndogo zilizopo.
Ameiomba serikali kuwatumia viongozi wa dini kama sehemu ya kudumisha amani ya nchi kwa kuwafanyia maombi viongozi waliopo madarakani ili waweze kuongoza kwa kutumia hekima za Mungu kwani bila ya kuwa na maombi hayo shetani anaweza kuleta roho ya uchonganishi na kusababisha amani kutoweka.
Amebainisha kuwa kwa kipindi chote cha mwezi huu hadi ujao watakuwa na kongamano kubwa la kuiombea amani ya nchi ambapo halitakuwa na itikadi ya dini yoyote bali ni madhehebu yote hivyo kuwataka watu kujitokeza kufanya maombi hayo.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment