Saturday, June 7, 2014

WATAKIWA KUKABILIANA NA TABIA NCHI



WAKAZI wa wilaya za Bagamoyo mkoani Pwani na Pangani mkoani Tanga wametakiwa kulinda misitu ikiwemo ile ya Mikoko iliyopo kandokando mwa Bahari ya Hindi ili kuinusuru wilaya hiyo na athari zitokanazo na mabadiliko ya Tabia Nchi.
Hayo yalisemwa  na mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Ahmed Kipozi alipokuwa akifungua mafunzo ya juu ya namna ya kukabiliana na mabadiliko ya Tabia Nchi kwa wajumbe wa kamati za mazingira kutoka wilaya za Bagamoyo na Pangani mkoani Tanga.
Kipozi amesema kuwa watu wengi waliathirika na mvua kubwa zilizonyesha ambazo zilileta mafuriko na kusababisha madhara yakiwemo ya watu kufa, mazao yao kusombwa na maji, miundombinu ikiwemo ya barabara na madaraja zilitokana na mabadiliko hayo ya Tabia Nchi.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi mratibu wa mafunzo hayo Dk Beno Mnembuka ambaye ni mtafiti kiongozi kwenye mradi huo unaosimamiwa na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) kwa ushirikiano na Chuo Kikuu cha Ardhi, Mamlaka ya hali ya Hewa na mtafiti mmoja toka nchini Norway amesema kuwa mabadiliko ya Tabia Nchi pia yameathiri viumbe hai kama vile samaki.
Dk Mnembuka amesema kuwa viashiria vya mabadiliko ya Tabia Nchi ni pamoja na mabadiliko ya misimu ya mvua, joto, upepo mkali wa Kasi na Kusi, ukame, mafuriko ambapo hutokana na uharibifu wa mazingira ambapo ili kukabiliana na madhara hayo lazima kurejesha uoto wa asili kwa kupanda miti na kutoharibu vyanzo vya maji.
 Naye meneja wakala wa misitu Tanzania (TFS) wilaya ya wilaya Bagamoyo Charles Mwafute amesema kuwa katika kutekeleza kwa vitendo washiriki wa mafunzo hayo walipanda miti ya Mikoko eneo la ukubwa wa hekari mbili na nusu kwenye kijiji cha Kiharaka.  
Mradi huo ambao utaisha mwezi Desemba mwaka huu unatekelezwa kwenye vijiji vya Bumbwini, Kisakasaka Zanzibar, Magomeni, Kiharaka na Kondo wilayani Bagamoyo, Matakani, Kipumbwi na Pangani Mjini wilaya ya Pangani.

No comments:

Post a Comment