Thursday, February 29, 2024

BMH YAENDELEA KUPANDIKIZA BETRI KWENYE MOYO



Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) ya jijini Dodoma imefanya upandikiza betri kwenye moyo kwa watu watatu.

Upandikizaji wa betri kwenye moyo ambao kitaalamu unaitwa _pacemakers_  _implantation_ unafanyika kwa watu wenye matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo na kusababisha mapigo ya moyo kuwa chini ya kiwango kinachotakiwa kwa mtu wa kawaida ambayo ni 60-100 kwa dakika.Wengi wao huwa ni chini ya 40.

Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Moyo wa BMH, Daktari Bingwa wa Moyo, Happiness Kusima, amesema leo kuwa BMH imefikisha upandikizaji kwa watu 18 toka huduma ianzishwe mwaka 2021.

"Jana tumepandikiza watu watatu (3), leo tumepandikiza watu wawili," amesema Daktari huyo Bingwa wa Moyo.

Dkt Happiness amesema upandikizaji huu umefanyika kwenye kambi ya Madaktari Bingwa wa Moyo wa BMH kwa kujengewa uwezo na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) ya jijini Dar es Salaam.

ZEGERENI FC MABINGWA LIKUNJA CUP


TIMU ya soka ya Zegereni Fc imetwaa ubingwa wa Likunja Cup baada ya kuifunga Visiga Veterans kwa mabao 2-0

Mchezo huo ulifanyika kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Zegereni ulihudhuriwa na mashabiki wengi licha ya mvua kubwa kunyesha.

Washindi walipata seti ya jezi na mpira mmoja huku mshindi wa pili akijinyakulia jezi seti moja ambapo zawadi hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa CCM Kibaha Mjini Mwajuma Nyamka.

Nyamka amesema kuwa michezo ni ajira hivyo mashindano hayo ni moja ya utekelezaji wa ilani ya CCM hivyo kuwataka wadau wa michezo kuandaa michezo mingi.

Amesema kuwa mbali ya michezo kuwa ajira pia ni afya hivyo wananchi washiriki michezo na wahakikishe wanadumisha ulinzi na kuwaondoa vijana kwenye matumizi ya dawa za kulevya.

Naye mwandaaji wa mashindano hayo Rashid Likunja ambaye ni mwenyekiti wa serikali ua mtaa wa Zegereni amesema kuwa jumla ya timu 12 zilishiriki mashindano hayo.

Likunja amesema mashindano hayo kwa mwaka huu ni mwaka wa 10 kuyaandaa ambapo mwakani zawadi zitaongezwa ili kuleta msisimko.

Wednesday, February 28, 2024

Taasis ya Digital Agenda for Tanzania Initiatives yasisitiza haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi Nchini.*


Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Wataalamu kutoka Taasisi ya Digital Agenda for Tanzania Initiative imekutanaa pamoja na wadau kutoka Wizara ya habari, mawasiliano na teknolojia ya habari  wamekutana Jijini Dodoma kujadiliana kuhusu utetezi wa haki kidigitali.

Lengo la kikao hicho ni kutoa matokeo ya ripoti mbili zilizofanywa na Taasisi ya Digital Agenda Tanzania Initiative kuhusu utambuzi Kwa kutumia taarifa za kibayometriki,usajili wa laini za simu unaofanywa na Makampuni ya simu nchini.

Tafiti  imebainisha kuwa makampuni  ya simu nchini licha ya kufanya vizuri katika kutoa huduma lakini bado kuna mapungufu  katika kulinda haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi zonazowahusu wateja wao.

Akibainisha mapungufu hayo mkurugenzi mtendaji wa taasisi hiyo Peter Mmbando amesema kuwa ulinzi wa data, uhuru wa kujieleza pamoja na uendeshaji wake vilibainika kuwa ni moja kati ya mapungufu ya mitandao hiyo.

Mmbando amesema kuwa, elimu zaidi Kwa wananchi inapaswa ku ndelea kutolewa ili kuhakikisha taarifa zao zinakuwa salama pamoja na kuhakikisha wanaepukana na makosa ya kimtandao ambayo yamekuwa yakifanyika.

Kwa upande wake  Mtaalamu wa ulinzi wa taarifa binafsi Nchini Tanzania,Mrisho Swetu ameitaka jamii kuamka na kuwa mstari wa mbele katika kulinda taarifa zao. Amesisitiza kuwa taarifa binafsi nyeti za kibayometriki mfano alama za vidole zina athari kubwa endapo zitatumika vibaya.

Pia ameendelea kuhimiza wadhibiti na wachakataji wa taarifa binafsi Nchini kuboresha viwango vya ulinzi wa taarifa binafsi pamoja  na kuendelea kutoa elimu ya ulinzi wa taarifa binafsi kwa mujibu wa sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi,2022. Wadhibiti na wachakataji wanapaswa kuheshimu haki ya faragha na hyo itasaidia kuongeza uaminifu na wateja wao.

Kwa upande wa Jamii amesema,wadau wa serikali na sekta binafsi waendelee kutoa elimu kwa umma kuhusu haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi.Jamii inapaswa kupewa elimu ya kutosha kuhusu ulinzi wa taarifa binafsi pamoja na haki zao kama haki ya kuomba kufutwa kwa taarifa zako,haki ya kurekebisha,haki ya kupata fidia pale itakapotokea misingi ya sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi imekiukwa.

Aidha,ameendelea kusema, mafunzo hayo wamelenga kuyafikia makundi yote katika jamii, mikoa yote ambapo kwa upande wa watu wenye ulemavu wa kuona na kusikia wapo kwenye mpango wa kukutana na wataalamu wa lugha ya alama ili  kujua elimu hiyo itawafikiaje jamii hiyo ya watu wenye ulemavu. 

"Lengo ni kuikumbusha jamii matumizi sahihi  ya taarifa  binafsi,kujua haki zao ,lakini ni muhimu wafahamu kuwa taarifa zao binafsi zikitumika vibaya zinaweza kuleta madhara,lakini wafahamu kuwa endapo kutatokea  uvunjifu wa sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi basi ni wapi wanaweza kupeleka malalamiko yao" amesema Mrisho Swetu 

Naye, Afisa Mwandamizi Tume ya Haki za binadamu za Utawara Saidi Zuberi amesema mafunzo hayo yatakwenda  kumasaidia mwananchi kuweza kulinda  taarifa zake na kutambua haki za faragha. 

Pia ametoa wito kwa watoa elimu wa tume ya ulinzi wa data kuwa na miongozo itayoweza kutoa elimu ya haki ya faragha katika jamii .

WATANZANIA WATAKIWA KUENZI FALSAFA ZA MWALIMU JULIUS KAMBARAGE NYERERE






WATANZANIA wametakiwa kuenzi falsafa za Mwalimu Julius Kambarage Nyerere za Ujamaa na Kujitegemea kwani siyo umaskini bali ni kuwafanya wananchi kuwa na umoja ili kujiletea maendeleo.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Taifa Paul Kimiti wakati wa Kongamano la Maadili lililofanyika kwenye Shirika la (TATC) Nyumbu Kibaha.

Kimiti alisema kuwa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema kuwa taasisi hiyo ilianzishwa ili kuyaenzi yale aliyoyafanya hasa katika kujitegemea.

"Sisi ambao tunajua alichokuwa akikitaka Nyerere kuhusu uzalendo na kujitegemea na kudumisha umoja na amani lazima tuwakumbushe viongozi na vijana ili wazingatie falsafa hizo ili kuleta maendeleo,"alisema Kimiti. 

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Kikosi cha Nyumbu na Mkurugenzi wa Nyumbu Kanali Charles Kalambo alisema Shirika hilo ambalo ni maono ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere limepata mafanikio ikiwa ni pamoja na kubuni gari aina ya Nyumbu.

Kalambo alisema kuwa wanamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kulipatia Shirika la Nyumbu fedha kwa ajili ya kufanya shughuli zake mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuendeleza miradi ya kiufundi.

Naye Kanali Ngemela Lubinga katibu mkuu mstaafu (NEC-CCM) siasa na uhusiano wa kimataifa akifundisha somo la uzalendo, itifaki na uadilifu alisema kuwa viongozi wanapaswa kuwa na moyo wa kujituma kwani ndiyo msingi wa kujenga jamii bora na yenye uzalendo.

Lubinga alisema kuwa viongozi wanapaswa kuwa na uadilifu ili kujenga jamii bora pia wawe wabunifu, moyo wa kujituma ili kuleta maendeleo kwa wananchi na awajali ili kuwa na mipango ya pamoja.

Balozi Mstaafu Meja Jenerali Anselm Bahati alisema kuwa ili kuwa na usalama mahali pa kazi kwa wafanyakazi lazima wafanyakazi wapate mafunzo ya namna ya kujilinda na kujikinga.

Bahati alisema kuwa wafanyakazi wakiwa na mazingira salama watakuwa na uwezo wa kuzalisha pia maslahi yao kuangaliwa ili kuepukana na afya ya akili inayotokana na msongo wa mawazo.

Naibu Katibu Mkuu wa Taasisi hiyo Neema Mkwachu alisema malengo ni kutoa elimu kwa wanafunzi kuanzia ngazi ya shule za msingi hadi vyuo juu ya falsafa za Nyerere ikiwemo uzalendo wa nchi.

Mkwachu alisema kuwa pia ni kuwa na klabu za Mwalimu Nyerere ambazo zitakuwa zinatakuwa pia na uwezo wa kutunza mazingira ambayo ni moja ya vitu alivyohimiza Hayati Nyerere 

Katibu wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Mkoa wa Pwani Abdul Punzi alisema kuwa ili kuenzi falsafa za Nyerere kwa kufungua Klabu ya Mwalimu Nyerere Nyumbu.

Punzi alisema kuwa uzalendo unapaswa kuanzia chini kabisa ili wananchi watambue misingi mizuri iliyoasisiwa na Nyerere na kuifanya Tanzania kuwa na umoja na mshikamano ambapo kongamano hilo lilidhaminiwa na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Benki ya CRDB na NSSF.


Monday, February 26, 2024

*HISTORIA YAANDIKWA; JNHPP YAINGIZA MEGAWATI 235 GRIDI YA TAIFA*

📌 *Serikali yatekeleza ahadi kabla ya siku tatu*

📌 *Megawati 235 nyingine kuingizwa Machi, 2024*

📌 *Uzinduzi rasmi kufanyika mwezi Machi mwaka huu*

📌 *Dkt. Biteko asema hakuna kulala; vyanzo vipya kutekelezwa*

📌 *Mkandarasi apongeza usimamizi wa Dkt.Biteko*

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa, mradi wa umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) wenye uwezo wa megawati  2,115  umeanza kazi na kuingiza  megawati 235 katika gridi ya Taifa kupitia mtambo Namba 9. 

Hatua hii ni utekelezaji wa ahadi ya Serikali kuwa mtambo huo ungeanza kuzalisha umeme tarehe 25 Februari 2024, ahadi iliyotimizwa siku tatu kabla kuanzia tarehe 22 Februari 2024  mtambo huo ulipoanza uzalishaji.

Dkt. Biteko amesema hayo tarehe 25 Februari 2024 wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kwa baadhi ya wakuu wa vyombo vya Habari na Wahariri katika eneo la mradi wilayani Rufiji mkoani Pwani ambapo wahariri hao walipata fursa ya kutembelea maeneo mbalimbali ikiwemo Bwawa la kuhifadhi maji yatakayozalisha umeme, Tuta Kuu na mitambo ya umeme.

Ameeleza kuwa, kuingia kwa megawati 235 kwenye Gridi ya Taifa  kumeboresha hali ya upatikanaji umeme nchini na kupunguza upungufu wa umeme kwa zaidi ya asilimia 85.

Ameongeza kuwa, utekelezaji wa mradi wa Julius Nyerere unaendelea na ifikapo mwezi  Machi 2024 megawati nyingine 235 zitaingia katika gridi kupitia mtambo namba 8 na kufanya JNHPP kuingiza megawati 470 kwenye gridi na hivyo kupelekea nchi kuwa na ziada ya umeme ya megawati 70.

Amesema utekelezaji wa mradi huo ni jitihada za Rais, Dkt.Samia Suluhu Hassan ambaye alikuta mradi huo ukiwa na aslimia 33 na sasa  mradi huo unafikia mwisho.

Amesema, Dkt. Samia anaijali nchi kwa dhati na sasa mipango yake ya maendeleo haiangalii kipindi cha sasa tu bali miaka 30 hadi 40 ijayo na ndio maana ameshaagiza uendelezaji wa vyanzo vipya vya umeme ikiwemo Gesi, Maji na Nishati Jadidifu inayojumuisha Jua, Upepo na Jotoardhi.

Dkt. Biteko pia amepongeza juhudi za Serikali ya  Awamu ya Tano chini ya Hayati, Dkt. John Pombe Magufuli kwa uamuzi wa kutekeleza mradi huo ambao ulianza kutekelezwa mwaka 2018.

Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko ameeleza kuwa, utekelezaji wa JNHPP hauifanyi Wizara ya Nishati na Taasisi zake kubweteka na kutegemea umeme kutoka mradi huo pekee bali kasi ya utekelezaji wa miradi mingine mipya inaendelea ikiwemo mradi wa Rumakali (222MW), Ruhudji (358) na miradi ya Jotoardhi ya Ngozi na Kiejo-Mbaka pamoja na mradi wa umeme Jua wa Kishapu (150MW).

Kuhusu utunzaji wa mazingira, Dkt. Biteko ametoa wito kwa Wahariri wa Vyombo vya Habari kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa utunzaji wa mazingira ambao ndio unasababisha mabwawa ya umeme kuwa na maji ya kutosheleza kuzalisha umeme na pia kutoa elimu kuhusu athari za kuharibu vyanzo vya maji vinavyopeleka maji pia katika mabwawa ya umeme.

Kwa wananchi wanaozunguka maeneo  yenye mitambo ya kuzalisha umeme, Dkt. Biteko amesisitizaTANESCO ihakikishe hawapati changamoto ya umeme kwani hao ndio walinzi wa maeneo hayo na mradi unapofika katika eneo lolote lazima ubadilishe hali ya wananchi katika eneo husika kwa namna mbalimbali ikiwemo uboreshaji wa huduma za kijamii.

Dkt. Biteko ameipongeza TANESCO na  kampuni ya usimamizi wa mradi ya TECU kwa utekelezaji na usimamizi madhubuti wa mradi ambao umewezesha kuingiza megawati 235 kwenye gridi.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso amesema kuwa, ujazo wa maji unaohitajika katika Bwawa la umeme la JNHPP ni mita za ujazo bilioni 32.7 na sasa kuna mita za ujazo bilioni 28 hivyo bado mita nne tu Bwawa hilo kujaa kabisa.

Amesema kuwa, makadirio ni kuwa mita nne zilizobaki zitajaa mwezi huu kupitia usimamizi madhubuti wa Bonde la Maji la Rufiji.

Ametoa wito kwa wananchi kutunza vyanzo vya maji na kutofanya uharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji pia wasichepushe maji kiholela.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge amesema kuwa, mradi huo ni muhimu katika kutekeleza dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuifanya Pwani kuwa Mkoa wa kimkakati kwa kujenga viwanda vingi zaidi ambavyo kufanya kwake kazi kunategemea nishati ya umeme ya uhakika.

Amesema kuwa, mahitaji ya umeme mkoani Pwani ni megawati 130 lakini bado hayatoshelezi mahitaji hivyo mradi wa JNHPP kupitia kituo cha umeme cha Chalinze kitawezesha Mkoa huo kupata umeme wa uhakika ambao utachochea wawekezaji wapya.

Ameongeza kuwa, kwa sasa Mkoa wa Pwani una viwanda 1,533 ambapo  katika Serikali ya Awamu ya Sita viwanda 30 vinajengwa huku 17 vikiwa ukingoni kumalizika hivyo mradi wa JNHPP ni muhimu katika kufanya viwanda hivyo kufanya uzalishaji.

Meneja Mradi kutoka kampuni zinazotekeleza mradi huo (Arab Contractors na Elsewedy Electric) Mohamed Zaky, amesema kuwa kampuni hiyo inaona fahari kufikia hatua hiyo ya uzalishaji na kwamba nia yao ni kutimiza ndoto ya Tanzania kuzalisha megawati 2115 kupitia mradi wa JNHPP.

Aidha, amempongeza Dkt. Doto Biteko kwa msukumo anaoutoa kwa wakandarasi hao ili kutekeleza mradi kwa wakati na pia kwa kuusimamia kwa karibu mradi husika.

Viongozi wengine walioambatana na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati ni  Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Meja Edward Gowele, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba, Naibu Katibu Mkuu Mteule Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio, Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga,  Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Dkt. Rhimo Nyansaho na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Gissima Nyamo-Hanga.

Sunday, February 25, 2024

TAASISI YA KUMBUKUMBU YA MWALIMU JULIUS KAMBARAGE YATOA MAFUNZO ITIFAKI, UZALENDO NA USALAMA MAHALI PA KAZI KWA CWT KIBITINYERERE







TAASISI ya kumbukumbu ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Mkoa wa Pwani imetoa mafunzo ya Itifaki, Uzalendo na Usalama Mahali pa kazi kwa viongozi wa walimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti na kuzindua Club ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Wilaya ya Kibiti.

Mafunzo hayo yalitolewa Februari 24, 2024 Wilayani Kibiti kwa viongozi walimu hao kutoka Chama Cha Walimu (CWT) Wilaya ya Kibiti wapokea mafunzo ya ya Itifaki, Uzalendo na Usalama yalifunguliwa na Bi Nelea Nyanguye  ofisa Usalama mahali pa kazi wa Chama Cha Walimu (CWT) Taifa.

Katibu wa Taasisi hiyo ya Kumbukumbu ya Mwalimu Julius Nyerere Mkoa wa Pwani Ndugu Omary Punzi alifundisha mada ya Itifaki na Uzalendo na kuwaelekeza misingi ya Kiitifaki na kuwa Mzalendo wa Taifa la Tanzania.

Sadick Mchama alifundisha Usalama Mahali pa kazi ambapo mgeni rasmi Ndugu Salumu Mzanganya ofisa Tarafa Kibiti ambaye  alimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kibiti Mheshimiwa Kanali Joseph Kolombo, alitoa nasaha kwa wahitimu kuwa baada ya Mafunzo hayo kuwa wanatakiwa wawe wazalendo na kuisidia Wilaya, Mkoa na Taifa kwa ujumla kisha alizindua Club ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Wilaya ya Kibiti.

Kwa Upande wa Mwenyekiti wa CWT  Wilaya ya Kibiti Ndugu Hamdani Juma na Katibu Wake Bi Crencencia Ditrick walipongeza na kushukuru kuletewa mafunzo ambapo jumla ya washiriki 130 waliopatiwa vyeti vya mafunzo na  hayo.

NEC YATOA VIBALI VYA ELMU YA MPIGA KURA NA WATAZAMAJI WA UCHAGUZI MDOGO WA UDIWANI KATA 23.

 

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) katika kikao chake cha tarehe 24 Februari, 2024, kilichofanyika katika Ofisi za Tume Jijini Dodoma imetoa vibali vya kutoa elimu ya mpiga kura wakati wa uchaguzi mdogo wa Udiwani katika kata 23 za Tanzania Bara utakaofanyika tarehe 20 Machi, 2024 kwa asasi za kiraia 11.

Kwa Mujibu wa Taarifa kwa Vyombo vya Habari iliyosainiwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi Kailima, R. K imeainisha Asasi za kiraia 11 ambazo zimekidhi vigezo na kupewa vibali vya kutoa elimu ya mpiga kura pamoja na kata walizoomba kutoa elimu  hiyo kuwa ni Mbogwe Legal Aid Organization (MBOLAO) Isebya iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe, Sustainable Hub for Policy Initiatives (SHPI) Mshikamano iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Musoma.

Asasi zingine ni Promotion and Women Development Association (PWDA) Kasingirima iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma/Ujiji, Bagamoyo Community Capacity Empowerment and Education (BCCEE) Fukayosi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Action for Democratic Governance (A4DG) Kimbiji iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni.

Asasi zingine ni Vanessa Foundation ambayo itatoa elimu katika kata ya Nkokwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, Tanzania Centre for Disability Development Initiatives (TCDDI) Nkokwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, Safe Society Platform Tanzania (SSPT) Busegwe iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Butiama na Isebya iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe

Asasi zingine za kiraia zilizopata kibali ni Youth Against Aids and Poverty Association (YAAPA) ambayo itatoa elmu katika kata ya Kasingirima iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma/Ujiji, Musoma Municipal Paralegal Organisation (MMPO) Mshikamano iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Musoma.

Asasi nyingine iliyopata kibali ni Shirika la Elimu ya Uraia na Uzalendo “Civic Education and Patriotism Association” iliyoomba kutoa Elimu katika kata za Kimbiji iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni, Msangani iliyopo katika Halmashauri ya Mji Kibaha, Fukayosi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Mlanzi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti na Kibata iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa.

Wakati huo huo, Tume pia imetoa kibali kwa asasi za kiraia tatu ambazo zimekidhi vigezo ili ziweze kutazama uchaguzi mdogo wa Udiwani katika Kata 23 za Tanzania Bara.

Asasi hizo tatu zitakazoenda kutazama uchaguzi Mdogo wa udiwani siku ya Jumatano tarehe 20 Machi, 2024 ni Tanzania Alliance for Disability Development Initiatives itakayokuwa katika kata ya Mhande iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba, Bridge Development Trust Organisation itakuwa katika kata ya Buzilasoga iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema na Promotion and Women Development Association itayokuwa katika Kata ya Kasingirima iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma/Ujiji.

Aidha, katika kikao hicho, Tume imezitaka asasi za kiraia zilizopata kibali cha kutoa elimu ya mpiga kura, kuzingatia Mwongozo wa Elimu ya Mpiga Kura wa Mwaka 2020 katika kipindi chote cha kutoa elimu hiyo katika uchaguzi mdogo.

MAMA KOKA AFANYE KWELI AGAWA DOTI ZA VITENGE KUELEKEA SIKU YA MWANAMKE DUNIANI

 

NA MWANDISHI WETU

Mke wa Mbunge wa  Jimbo la Kibaha Mjini Selina Koka  amegawa doti za  sare 125 za vitenge  kwa ajili ya sherehe za maadhimisho ya siku ya  Mwanamke Duniani zilizogharimu kiasi cha shilingi milioni 2.

Sare hizo ambazo zimegawiwa katikka makundi mbali mbali ikiwemo Jumuiya ya wazazi, Wajumbe wa Baraza la UWT Kibaha Mjini, Wajumbe Wanawake wa Baraza la Wazazi la Wilaya, Wajumbe wanawake wa Baraza la UVCCM Kibaha Mjini Pamoja na Wajumbe Wanawake wa Halmashauri kuu ya CCM Wilaya Kibaha Mjini. 

Akikabidhi sare hizo kwa niaba ya Mama Selina Koka Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha mji Method Mselewa  amesema huu ni Utaratibu wa Ofisi ya Mbunge kupitia kwa Mama Koka kugawa sare kwa wanawake kila mwaka na kila zinapofika Sherehe hizo pamoja na Makongamano mbalimbali. 

Kwa Upande wake Mama Selina Koka akizungumza katika mahojiano maalumu kwa njia ya simu alisema kwamba ameamua kutoa sare hizo kwa lengo la kuungana na wanawake wenzake katika kusherekea kwa pamoja siku hiyo.

"Nimetoa sare zipatazo 125 kwa ajili ya  makundi mbali mbali ya wanawake,ikiwemo kundi la Uwt,Uvccm,Wazazi,pamoja na chama chenyewe cha Ccm  ambapo wao ndio watawakilisha wanawake wengine wote wa Jimbo la Kibaha mjini,"alisema Selina Koka.

Mama Koka alisema kwamba amekuwa akishirikiana bega kwa bega na wanawake wenzake katika mambo mbali mbali ya kijamii ambayo yamekuwa yakifanyika ikiwemo hili la kuelekea maadhimisho ya siku ya wanawake duniani.

Pia aliahidi kuendelea kushirikiana kwa dhati na wanawake wenzake na kuwatakia kila la kheri katika sherehe hizo ambazo kiwilaya zinatarajiiwa kufanyika machi 5 mwaka huu mjini Kibaha.

Mama Koka  alifafanua kwamba ameamua kutumia jumuiya  hizo ikiwa kama wawakilishi wa wanawake wengine wote wa Jimbo zima  la Kibaha mjini kwani sio rahisi kwa kila mmoja kupata sare hiyo kwa ajili ya sherehe hizo.

Katika hatua nyingine amesema kwamba anawapenda wanawake wote na kwamba wajitokeze kwa wingi siku hiyo kwa ajili ya kusherekea siku yao ambayo ni muhimu kwa ajili ya kuonana na kubadilishana mawazo.

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Wilaya ya Kibaha Mjini Elina Mgonja amemshukuru kwa dhati Mama Koka pamoja na  Mbunge kwa kujali wanawake wa Kibaha na kwamba tunapaswa kumtia moyo.

Mgonja alisema kwamba wanawake wa Kibaha wamepata Mama ambaye amekuwa ni mstari wa mbele katika kusaidia mambo mbali mbali ya kijamii pamoja hivyo anastahili sifa  na kumthamini.

"Kwa kweli  tumefarijika sana kupokea sare hizi za vitenge kiukweli mama Selina koka ni mfano wa kuigwa kutokana na kuonyesha mashirikiano na mahusiano mema katika kila jambo,"alisema Mgonja.

Aidha Mwenyekiti Mgonja alisema kwamba Mama koka amekuwa ni kichocheo kikubwa katika kila nyanja ikiwepo sambamba na kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuwapatia mitaji na fedha.

Naye Katibu wa UWT Cecilia Ndalu amesema kuwa kitendo cha Mama Koka kujali wanawake ni kitendo cha kipekee sana  kwani kuwa mke wa Mbunge hawajibik kwa wanawake moja kwa moja lakini amejigusa na kujali sana. 

Wajumbe wengi waliopokea sare hizo wameendelea kuishukuru familia ya Mhe Koka kwa kujitoa na wameahidi kuendelea kumuunga mkono Mhe Koka katika kuhakikisha shughuli zake za utekelezaji wa ilani unaenda vyema. 

Sherehe za Mwanamke zinaadhimishwa Duniani kote na kwa upande wa  Kibaha Mjini kilele kitakuwa siku ya tarehe 05/03/2024 katika viwanja vya Mailimoja. 



        MWISHO

Saturday, February 24, 2024

SHULE YA EL-SHADDAI YAWASHIKA MKONO WATHIRIKA WA MAAFA HANANG.

 

NA MWANDISHI WETU, DODOMA

UONGOZI wa shule ya Msingi  El shaddai  iliyopo Dodoma umekabidhi misaada ya kibinadamu ikiwemo mchele, unga, maharagwe, nguo, dawa za meno na vyombo mbalimbali vya kupikia kwa ajili ya waathirika wa maafa ya maporomoko ya tope, mawe na miti kutoka mlima Hanang’ yaliyotokea tarehe 3 Disemba 2024 mkoani Manyara.

Akipokea misaada iliyotolewa na shule hiyo tarehe 23 Februari, 2024 kwaniaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi,  Kaimu Mkurugenzi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bi. Jane Kikunya amesema Ofisi inatambua mchango mkubwa wa Taasisi zinazoendelea kushiriki katika kurejesha hali kwa waathirika wa maafa hayo kwa namna wanavyoendelea kutoa misaada mbalimbali ili kusaidia hatua ya urejeshaji hali inayoendelea.

"kipekee kwa niaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu naomba kuwashukuru kwa moyo mliouonesha na nia katika kuchangia na kutoa msaada kwaajili ya waathirika wa maafa, tunashukuru kwa Shule yenu kwa kujitokeza na kuchangia misaada muhimu kwaajili ya waathirika wa Hanang, misaada iliyotolewa itawafikia waathirika wote kwa utaratibu uliowekwa na Ofisi."alisema Bi. Jane Kikunya.

Alieleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wameendelea kurejesha hali za waathirika wa maafa hayo yaliyosababisha vifo, uharibifu wa makazi, miundombinu ya barabara, umeme na mashamba, huku akitoa wito kwa wadau kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kufanikisha hatua zilizopo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shule hiyo  Bi. Juliana Kallinga amesema uongozi wa shule na wafanyakazi wa shule hiyo wameandaa baadhi ya vitu ambavyo ni ishara ya kuwafariji waathirika hao.

"Kama familia ya El-Shaddai tunapenda kuwafariji Watanzanaia wenzetu walioathirika kwa kuwapatia msaada wa vitu mbalimbali ikiwemo mchele, unga, maharagwe, nguo mbalimbali kwa wakubwa na wadogo, dawa za meno na vyombo mbalimbali vya kupikia,lakini pia tunamuomba Mungu aendelee kuwapa mfaraja na nguvu kila aliyepotelewa na ndugu jamaa na marafiki, hakika shule yetu iliguswa na changamoto hii."alisema Bi. Juliana.




CAPTIONS


P 1.

Kaimu Mkurugenzi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bi. Jane Kikunya akizungumza mara baada ya kupokea msaada ya kibinadamu kutoka kwa uongozi pamoja na walimu wa shule ya Msingi El-shaddai Februari 23, 2024 Jijini Dodoma.



P 2.

Mkurugenzi wa Shule ya Msingi  El-shaddai Bi. Juliana Kallinga akisoma taarifa ya msaada waliyoitoa kwa waathirika wa maporomoko ya tope, mawe na miti Wilaya ya Hanang’ mkoani Manyara.



P 3.

Mkurugenzi Idara ya Uwezeshaji Kiuchumi na Maendeleo ya Sekta Binafsi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bw. Condrad Millinga akipokea taarifa msaada iliyosomwa na Mkurugenzi wa Shule ya Msingi  El-shadai Bi. Juliana Kallinga.


P 4.

Baadhi ya vitu vilivyopokelewa ikiwemo mchele, unga, maharagwe, nguo, dawa za meno na vyombo mbalimbali vya kupikia kwa ajili ya waathirika wa maafa ya maporomoko ya tope, mawe na miti kutoka mlima Hanang’.


(PICHA ZOTE NA OFISI YA WAZIRI MKUU)

Friday, February 23, 2024

KIJANA WA KITANZANIA AGUNDUA MFUMO WA KITAALUMA KWA WANAFUNZI WA ELIMU YA MSINGI HADI CHUO KIKUU

NA WELLU MTAKI Dodoma.

KIJANA wa Kitanzania Alpha Mbennah mwenye taaluma ya Uhandisi amegundua Mfumo wa Uchakataji,Uhifadhi na Uandaaji wa Taarifa za Kitaaluma za wanafunzi kuanzia ngazi ya Elimu msingi mpaka Vyuo Vikuu uitwao "SPIN-ED Academic Performance Management System utakaowezesha kuleta ufanisi katika kazi.

Akizindua mfumo huo  Jijini Dodoma katika Mkutano wake na Wanahabari Mhandisi Mbennah amesema kuwa mfumo huo unamruhusu mwalimu katika ngazi tajwa kuweza kukusanya na kuingiza alama za mwanafunzi aliyesajiliwa katika mfumo kisha huchukua alama hizo na kuzichakata kwa kutengeneza wastani uliopimwa au usiopimwa kubaini gredi ya alama hizo, yaani A, B, C, n.k.

“Pia huu mfumo unaweza kubaini wastani wa darasa husika, nafasi aliyoshika kila mwanafunzi katika somo husika na katika darasa kwa ujumla pamoja na kutengenza ripoti ya maendeleo ya kitaalamu kwa kila mwanafunzi aliyesajiliwa kwenye mfumo, katika darasa husika, kutoa maoni ama comments zinazohusiana na ufaulu wa mwanafunzi na kuchora grafu ya maendeleo ya kitaaluma kwa kila mwanafunzi".

Mbenah amesema kuwa vyote hivyo hufanywa moja kwa moja huku akisema kuwa hivo ni baadhi ya vipengele vilivyopo katika mfumo wa SPIN-ED.

“Niseme tu kwamba vina umuhimu mkubwa sana katika uchakataji wa taarifa za kitaaluma za wanafunzi kwani huwasaidia walimu na wadau mbalimbali wa elimu kufanya maamuzi mbalimbali na hatimae kuongeza ufanisi katika mbinu za ufundishaji na ujifunzaji".

Aidha amesema sababu kubwa ya yeye kufanya ugunduzi wa mfumo huu wa SPIN-ED ni kutokana na changamoto alizoziona wakati akiwa mwalimu wa kujitolea katika moja ya shule hapa nchini, hususan katika uandaaji wa ripoti za maendeleo ya kitaaluma ya wanafunzi.

wakati mwingine huchukua muda mrefu kwa Walimu kuandaa na hata wakati mwingine Walimu kukosa hamasa ya kutoa majaribio ya mitihani ya Mara kwa Mara ya kuwapima wanafunzi wakihofia kuchukua muda kwa uandaaji wa ripoti na Maendeleo yao.

Mfumo huu wa SPIN-ED ameugundua mwaka 2021 na kuanza kufanya kazi mwaka huohuo ambapo mpaka kufika sasa zipo shule 3 zinazotumia mfumo huu.

SERIKALI KUENDELEA KUDHIBITI DAWA ZA KULEVYA NA RUSHWA



NA WELLU MTAKI , DODOMA.

SERIKALI inaendelea kukabiliana na masuala ya  biashara ya dawa za kulevya na rushwa nchini  ili kuhakikisha wanajenga taifa lililo imara kwa kutoa Elimu kuanzia shule za msingi mpaka vyuo vikuu.

Kauli hiyo imetolewa na Kamishna wa Kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya  Aretas Lyimo Jijini Dodoma   wakati  akifunga mafunzo kuhusu mkakati  wa habari , Elimu , mawasiliano  na programu ya TAKUKURU rafiki pamoja na  tatizo za dawa za kulevya , mapambano dhidi ya rushwa kwa maafisa wanaohusika na uelimishaji umma na mawasiliano.    

Lyimo amesema kupitia mafunzo waliopewa maafisa wanaohusika na uelimishaji umma na mawasiliano yatasaidia kuleta matokeo chanya ya  kukabiliana na biashara ya dawa za kulevya na Rushwa kwani ni vitu vinavyofanana.

“Naamini kupitia muunganiko wetu na klabu ambazo tayari tumeshanzianzisha huko mashuleni itasaidia kuwafikia kwa uharaka zaidi watu katika ngazi za mitaa hadi huko kwenye Halmashauri  wanafunzi wengi wanatokea kwani huko,”amesema. Lyimo

Amesema matunda ya ushirikiano kati ya TAKUKURU na taasisi ya kupambana dawa za kulevya tayari yameanza kuonekana kwani vitu hivyo vimekuwa vikiisumbua serikali katika kuhakikisha wote wanao husika wanatiwa mbaroni na kuchukuliwa hatua za kisheria.

“Nitoe wito kwa wadau kuwa nyenzo pekee ya kuepusha watu kujiingiza kwenye Rushwa na dawa za kulevya ni kutoa elimu hata tukiendelea kukamata kwa namna gani lazima tuhakikishe tunatoa elimu pamoja na kushirikiana na vyombo vya habari ili watusaidie kuwafikia watu wengi kwa wakati mmoja,”amesema.

Kwa upande wake Naibu Mkurugenzi Mkuu TAKUKURU Bi. Neema Mwakalile amesema kilichotokea kwenye mafunzo hayo kinadhihirisha ushirikiano  uliopo kati ya TAKUKURU na Mamlaka ya Kupambana na dawa za Kulevya ni mkubwa kwani vitu hivyo vinafanana na mapambano yanapaswa kuimarishwa zaidi.

Mwakalile amesema kuwa washiriki wamejifunza juu ya tatizo la dawa za kulevya, sababu za matumizi ya dawa hizo pamoja na kutambua dawa tiba ambapo vijana wengi wameonekana kujiingizia kwa kiasi kikubwa katika janga hilo huku akiongeza kuwa elimu waliyo wapatia washiriki katika mkutano huo itaenda kuumarisha zaidi mapambano na hatimaye kufikia hazma ya Serikali.

“Washiriki walipitishwa kwenye mkakati wa kupambana na Rushwa ili kuelewa zaidi na namna ya kwenda kuelimisha wanafunzi pia mafunzo haya yatasaidia jamii kuichukia Rushwa na kuepukana na Dawa za kulevya,”amesema.Mwakalile

Pia ameongeza kuwa katika mambo mengi waliyowafundisha wataenda kutoa elimu hasa kwa wanafunzi kwani swala hilo limekuwa mtambuka. 

 “Ni lazima kuanza kuwajenga wanafunzi wa shule msingi na sekondari kwani wao ndio watakuwa msingi mzuri kwenda kupinga na kukataa dawa za kulevya pia  Rushwa na dawa za kulevya vina madhara makubwa kwenye nyanja zote elimu na uchumi,”ameongeza.

Taasisi ya kupambana na Rushwa na TAKUKURU waliingia makubaliano 20/5 2023 kwaajili ya kutoa elimu kuhusu rushwa na dawa za kulevya.

Thursday, February 22, 2024

CHESTMOKA MABINGWA KIBAHA VIJANA CUP

TIMU ya soka ya Chestmoka imetwaa ubingwa wa Kibaha Vijana Cup kwa kuifunga Muharakani kwa penati 6-5 na kujinyakulia kiasi cha shilingi milioni 1.

Mchezo huo wa fainali ulichezwa kwenye uwanja wa Mwendapole Wilayani Kibaha Muharakani walijinyakulia kiasi cha shilingi 500,000 na washindi watatu Tp Pwani wakijinyakulia seti ya jezi.

Mgeni rasmi Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Mussa Ndomba ambaye alimwakilisha mdhamini wa ligi hiyo Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka amesema michezo ni afya na ajira.

Ndomba amesema kuwa Halmashauri itaendelea kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya michezo ili vijana waweze kucheza na kujipatia ajira.

Awali akimkaribisha mgeni rasmi Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Soka Mkoa wa Pwani COREFA Mohamed Lacha amesema kuwa malengo ni kutaka soka lichezwe ndani ya mkoa huo.

Lacha amesema ili soka likue ni kuwa na michezo mingi ili kuibua vipaji vingi na kuviendeleza ili kuwa na timu nzuri.

Naye meneja wa mashindano hayo Walter Mwemezi amesema jumla ya timu 16 zilichuana kwenye mashindano hayo.

Mwemezi amesema kuwa matarajio yao kwa mwakani ni kushirikisha timu nyingi ili mashindano hayo yawe na msisimko zaidi.

Kwa upande wake mwakilishi wa Koka Said Mbecha amesema kuwa Mbunge ameahidi kuendelea kusaidia michezo ili vijana wengi wapate fursa mbalimbali zilizopo kwenye michezo.

Tuesday, February 20, 2024

MAMLAKA YA KUDHIBITI NA KUPAMBANA NA DAWA ZA KULEVYA KUENDELEA KUWEZESHWA

 


NA WELLU MTAKI, DODOMA

Serikali inaendelea kuiwezesha Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ikiwa ni pamoja na kuboresha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ili kuongeza kasi ya mapambano na hatimaye kumaliza kabisa tatizo la dawa za kulevya nchini. 

Hayo yamesemwa na waziri wa nchi ofisi ya waziri mkuu sera bunge na uratibu Mhe. Jenista Mhagama wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya serikali Katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya kwa Mwaka 2023

Amesema Serikali imepata mafanikio makubwa ambapo kuanzia mwezi Januari hadi Disemba 2023 Zaidi kilogramu milioni 1 za aina mbalimbali za dawa za kulevya zilikamatwa katika maeneo mbalimbali nchini huku Watuhumiwa 10,522 ambao kati yao wanaume ni 9,701 na wananwake ni 821 walikamatwa kuhusika na dawa hizo.

"Serikali kupitia Mamlaka ya Kudhibiti Kupambana na Dawa za Kulevya imepata mafanikio makubwa ambapo kuanzia mwezi Januari hadi Disemba 2023 kilogramu 1,965,340.52 za aina mbalimbali za dawa za kulevya zilikamatwa katika maeneo mbalimbali nchini. Watuhumiwa 10,522 ambao kati yao wanaume ni 9,701 na wananwake ni 821 walikamatwa kuhusika na dawa hizo. Aidha, jumla ya hekari 2,924 za mashamba ya bangi na mirungi ziliteketezwa" amesema Mhagama.

Aidha amesema kuwa Serikali imefanikiwa kuzuia uingizaji wa zaidi kilogramu milioni 15 za kemikali bashirifu ambazo zingeweza kutumika kutengenezea dawa za kulevya kinyume cha sheria.

"Kiasi cha dawa za kulevya kilichokamatwa katika kipindi cha mwaka mmoja pekee ni kikubwa zaidi kuwahi kukamatwa hapa nchini kwani kinazidi kiasi cha kilogramu 660,465 zilichokamatwa katika kipindi cha miaka 11. Aidha, Serikali imefanikiwa kuzuia uingizaji wa kilogramu 157,738.55 za kemikali bashirifu ambazo zingeweza kutumika kutengenezea dawa za kulevya kinyume cha sheria" amesema Mhagama.

Pia ameeleza kuwa kumekuwepo na ongezeko la waraibu wanaojiunga na tiba katika kliniki mbalimbali zilizopo nchini ongezeko hilo ni sababu ya kuadimika kwa dawa za kulevya mtaani baada ya kuvunja baadhi ya mitandao mikubwa ya wauzaji wa dawa za kulevya.

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za  Kulevya imesaini hati ya makubaliano ya ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa kutoa elimu ya dawa za kulevya na rushwa kupitia klabu za kupinga rushwa nchini ambapo sasa zitaitwa  klabu za kupinga rushwa na dawa za kulevya. 




KOKA ATOA FEDHA NA JEZI KWA WASHINDI KIBAHA VIJANA CUP





MBUNGE wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka ametoa fedha na vifaa vya michezo vyenye thamani ya shilingi milioni 1.7 kwa ajili ya washindi wa Kombe la Kibaha Vijana Cup.

Akikabidhi vifaa hivyo kwa uongozi wa Chama Cha Soka Kibaha (KIBAFA) ofisini kwake kwa niaba ya Mbunge huyo Katibu wa Mbunge Method Mselewa amesema fedha hizo na vifaa hivyo vitatolewa kwenye hatua ya fainali itakayochezwa Februari 21 kwenye uwanja wa Mwendapole.

Koka akizungumza kwa njia ya simu amesema kuwa ameamua kujitolea ili kuinua vipaji vya vijana wa Kibaha kwani michezo ni ajira kubwa kwa vijana na wengi wamenufaika kupitia soka na kuwa ni sehemu ya maendeleo.

Amesema kuwa ataendelea kusaidia michezo mbalimbali ili vijana wapate fursa kwenye timu kubwa ambapo chimbuko huanzia chini ambako ndiyo kwenye msingi.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa KIBAFA David Mramba amesema kuwa wanamshukuru mbunge huyo kwa kuchochea sekta ya michezo kwenye Jimbo hilo na kuwafanya vijana kushiriki michezo.

Naye Mjumbe wa soka la wanawake kupitia chama hicho Jesca Sihha amesema kutolewa zawadi hizo ni chachu kwa wanasoka na kuomba na soka la wanawake nalo lipewe kipaumbele.

Monday, February 12, 2024

UJENZI MADARASA, USHIRIKIANO WAZAZI, WALIMU NA WADAU KICHOCHEO UFAULU MZURI BUNDIKANI


MTAA wa Uyaoni Kata ya Maili Moja Wilayani Kibaha umeishukuru serikali kwa kujenga madarasa saba yenye thamani ya shilingi milioni 140 kwenye Shule ya Sekondari ya Kata ya Maili Moja Bundikani kwa kipindi cha miaka mitatu na kuifanya iwe na miundombinu mizuri na kuongeza ufaulu.

Aidha serikali ilitoa fedha ambazo zimejenga vyoo matundu 18 pamoja ujenzi wa darasa moja ambalo kwa sasa liko hatua ya umaliziaji na mwaka huu imefuta daraja sifuri kwa kidato cha nne ambapo mtaa huo ni mlezi wa shule hiyo.

Mwenyekiti wa Mtaa huo Fadhil Kindamba amesema kuwa ufaulu mwaka huu wanafunzi 22 wamefaulu daraja la kwanza, 73 daraja la pili 144 daraja la tatu na 130 daraja la nne.

Kindamba amesema ufaulu huo umetokana ushirikiano uliopo baina ya walimu, wazazi na wadau wengine wa elimu na kuboreshwa kwa miundombinu ya shule.

Katika hatua nyingine mtaa huo unatarajia kujenga vibanda viwili vya biashara kwa ajili ya kuvipangisha ili kujiongezea mapato na tayari wana matofali 500 kwa ajili ya kuanzia ujenzi utakaoanza hivi karibuni.

Amesema pia wanatarajia kuanzisha mnada ambapo tayari eneo limeshapatikana baada ya mwananchi mmoja kwenye mtaa huo kujitolea eneo kwa ajilo hiyo.

Tuesday, February 6, 2024

JINSI SERIKALI ILIVYOBORESHA SHULE YA SEKONDARI MWANALUGALI YAPELEKA MAMILIONI

MTAA wa Mwanalugali B Wilaya ya Kibaha umepokea kiasi cha shilingi milioni 452.6 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni mawili madarasa saba na bwalo la chakula kwenye Shule ya Sekondari ya Mwanalugali.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake Mwenyekiti wa Mtaa huo ilipo shule hiyo Deodatus Rwekaza amesema kuwa wanaishukuru serikali kwa kutoa fedha hizo ili wanafunzi wasome kwenye mazingira mazuri.

Rwekaza amesema kuwa fedha kiasi cha shilingi milioni 240 kwa ajili ya bweni moja ilitolewa na limekamilika linatumika, bweni la pili ilitolewa fedha kiasi cha shilingi milioni 120 zimetolewa na ujenzi umefikia hatua ya kupaua.

"Fedha nyingine ni kiasi cha shilingi milioni 88 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa saba ambapo sita yamekamilika moja likiwa bado tunaishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wetu Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha sekta ya elimu,"amesema Rwekaza.

Amesema kuwa fedha kiasi cha shilingi milioni 100 zometolewa kwa ajili ya ujenzi wa bwalo la wanafunzi ambalo ujenzi wake umefikia hatua ya linta.

"Shule hii pia imechimbiwa kisima kirefu kutoka kwa wafadhili kutoka taasisi ya Ishik Education and Medical Foundation ya nchi ya Uturuki tunawashukuru sana kwa msaada huo ili kukabiliana na changamoto ya maji,"amesema Rwekaza.

Monday, February 5, 2024

NYUMBU YAITAMBIA AFRICAN LYON

Ofisa Michezo Mkoa wa Pwani katika aliyevaa tisheti ya bluu Grace Bureta akiwa na baadhi ya viongozi wa Chama Cha Soka Mkoa wa Pwani (COREFA)  wakifuatilia mchezo wa First League Nyumbu 3-2 African Lyon Fc.

MWENDAPOLE B KUJENGA SHULE YA MSINGI


MTAA wa Mwendapole B Wilayani Kibaha uko kwenye hatua za mwisho katika kupata eneo kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Msingi ili kuwapunguzia changamoto watoto wa mtaa huo kugongwa na magari wakivuka kwenda shule iliyoko mtaa jirani.

Aidha wanafunzi wanaotoka mtaa huo hutembea umbali wa kilometa mbili kwenda na kurudi hivyo kuwa na uhitaji wa shule ili kuwapunguzia umbali mrefu kwenda shule.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha Mwenyekiti wa Mtaa huo Abubakary Matumla amesema kuwa mtaa huo una shule za msingi na sekondari za watu binafsi ambazo ni wazazi wachache wenye uwezo wa kuwapeleka watoto wao kusoma hapo.

"Tayari eneo limepatikana lina ukubwa wa hekari nne ambalo ni la mtu binafsi ambaye inabidi alipwe ndipo aliachie hivyo kuna makubaliano na Halmashauri ya Mji wampatie eneo lingine ili apishe hapo tuko hatua za mwisho za mabadilishano,"amesema Matumla.

Matumla amesema kuwa tayari wana tofali zaidi ya 4,000 kwa ajili ya ujenzi huo hivyo wanasubiri tu Halmashauri wampatie eneo lingine ili waanze ujenzi wa shule hiyo ambayo itawaondolea changamoto ya kugongwa au kusoma mbali.

"Wananchi wameshachanga fedha kiasi cha shilingi milioni 1.6 ambapo tunashirikiana na diwani ili kufanikisha kupata eneo hilo na matumaini ni makubwa,"amesema Matumla.

LATRA YACHUKUA HATUA KWA DALADALA ZINAZOKIUKA TARATIBU ZA USAFIRISHAJI/KUKATISHA RUTI

MAMLAKA ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) Mkoa wa Pwani imeyachukulia hatua za kisheria mabasi madogo Daladala 53 kutokana na makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na kukatisha safari.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na ofisa leseni na usajili wa Mamlaka hiyo Geofrey Mashishi alipozungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake.

Mashishi amesema kuwa hatua hizo zimechukuliwa kwa kipindi cha miezi miwili iliyopita Desemba mwaka jana na Januari mwaka huu kwa Daladala zinazofanya safari ndani ya Mkoa huo.

"Hatua hizo tumezichukuwa kwa wasafirishaji hao kwa sababu ya kukiuka masharti ya leseni zao kwa makosa mbalimbali mengine yakiwa ni kutotoa tiketi, kuzidisha nauli na mengine ambayo ni kinyume na taratibu za usafirishaji,"amesema Mashishi.

Amesema kuwa ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa wasafirishaji wanaokiuka masharti ya leseni zao kunahitajika ushirikiano baina yao na wadau wakiwemo abiria.

"Sekta ya usafirishaji ina changamoto nyingi na tumekuwa tukifanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa kwashirikiana na Jeshi la Polisi ili kuhakikisha wasafirishaji wanafuata kanuni, sheria na taratibu za usafirishaji ili kuondoa malalamiko,"amesema Mashishi.

Aidha amesema kuwa wamekuwa wakitoa elimu kwa abiria ili kujua haki zao na wasafirishaji kujua wajibu wao wanapotekeleza majukumu yao kupitia vyombo vya habari.

"Ukaguzi wa kufuatilia ni endelevu hivyo ni vema wasafirishaji wakazingatia masharti ya leseni zao ili kuondoa changamoto zisizo za lazima kwa wadau wa usafiri,"amesema Mashishi.




Sunday, February 4, 2024

LIKUNJA CUP ROBO FAINALI KUTIMUA VUMBI FEBRUARI 7


 MAashindano ya Likunja Cup hatua ya Robo Fainali yataanza kutimua vumbi Februari 7 uwanja wa Shule ya Msingi Zegereni kwa kuzikutanisha Misugusugu Fc na Veterani Fc kwa mujibu wa Rashid Likunja 

ATAKA MIKOPO ASILIMIA 10 YA HALMASHAURI IKOPESHE VIJANA WALIOACHA MATUMIZI DAWA ZA KULEVYA

HUKU Serikali ikiendelea na mchakato wa namna ya utoaji mikopo ya asilimia 10 za Halmashauri imeombwa kuangalia namna ya kuvikopesha vikundi vya waraibu wa dawa za kulevya ili wafanye shughuli za ujasiriamali.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Yohana Kilonzo Mkurugenzi wa Taasisi ya (OYARB) inayowahudumia watu waliokuwa wakitumia dawa za kulevya na kuacha na sasa wanatumia dawa za Methadoni zinazosaidia kuwarudisha katika hali yao ya kawaida ambapo kituo hicho kina vijana 500.

Kilonzo amesema kuwa watumiaji hao wanapokuwa hawana shughuli ya kufanya ni rahisi kurudia kutumia dawa za kulevya hivyo kuna haja ya kuwapatia shughuli za kufanya ili waweze kujipatia kipato.

"Wakati wakiendelea na tiba tunawafundisha shughuli za ujasiriamali ambapo wana mradi wa uuzaji wa sabuni za maji lengo wakitoka hatua hii wawe na uwezo wa kujitegemea ndiyo sababu tunaona nao wafikiriwe kwenye hiyo mikopo wapewe upendeleo,"amesema Kilonzo

Amesema kuwa kwa baadhi ya waliofuzu tiba hiyo baada ya kutumia Methadoni kwa kipindi cha miaka miwili ambazo wanapewa Hospitali ya Mkoa ya Rufaa ya Tumbi wamewachukua na kazi yao ni kufundisha juu ya athari na kuachana na matumizi ya dawa hizo. 

"Na hawa wana kikundi chao wanafanya shughuli zao hivyo hata wakikopeshwa wana uwezo mzuri wa kurudisha kwani kikundi chao kiko makini na wanajitambua kwani baadhi yao ni wasomi wazuri na wana uwezo mkubwa wanashindwa kukopesheka kama vijana kwani wengi wana umri mkubwa,"amesema Kilonzo.


HOSPITALI YA BENJAMIN MKAPA YAIKOSHA KAMATI YA BUNGE KWA UBORA WA HUDUMA

 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Maswala ya UKIMWI imeipongeza menejimenti na uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamin Mkapa kwa ubora wa Huduma na kuwatia moyo kwa  kuendelea kuwahudumia wananchi .

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Afya na Maswala ya UKIMWI, Mhe. Stanslaus Nyongo baada ya kupokea taarifa ya Huduma za kibingwa na bingwa bobezi zinazotolewa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamin Mkapa iliyopo Jijini Dodoma.

Mhe. Nyongo amesema kuwa Hospitali hiyo imekuwa ya mfano katika utoaji wa Huduma bora na  usafi wa mazingira na kuleta ufanisi sahihi wa uwekezaji mkubwa ulofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Sluhu Hassan.

“Hongereni kwa kazi nzuri mnayofanya ya kuwahudumia watanzania lakini pia Mkurugenzi husisite kutuma kutuma vijana wako kuendelea kujifunza ili Tanzania tuzidi kuwa kivutio cha tiba Utalii Afrika mashariki na Afrika nzima kwa ujumla”, Amesema Mhe. Nyongo.

Vile vile ametoa wito kwa uongozi huo kwendelea kuwa wabunifu katika kuongeza mapato ya hospitali hiyo ili kujiimarisha zaidi kiuchumi na kuacha kuwa tegemezi kwa serikali kuu.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamin Mkapa, Dkt. Alphonce Chandika ameishukuru serikali chini ya uongozi imara wa Rais Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa alioufanya katika Hospitali hiyo hususani katika vifaa tiba na vitendanishi, kusomesha wataalamu na upatikanaji wa dawa kwa wakati.

Saturday, February 3, 2024

TAASISI YA KUMBUKUMBU YA MWALIMU NYERERE YATEMBELEA BUNGENI




Taasisi ya kumbukumbu ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Mkoa wa Pwani yatembelea Bungeni Tarehe 2.2.2024 Kwa Mwaliko wa Mhe Subira Mgalu Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Pwani Kwa lengo la Kujifunza Shughuli za Bungeni.

Katibu wa Taasisi hiyo Mkoa wa Pwani Ndugu Omary Punzi Kwa niaba ya Taasisi alitoa Shukrani Kwa Mbunge Subira Mgalu Kwa namna alivyoipokea Taasisi na kuheshimu sambamba na hilo alipongeza Juhudi za Serikalini ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Daktari Samia Suluhu Hassani namna Bunge lilivyokuwa linafanya kazi Vizuri Kwa uchangamfu sana na Kujibu hoja vizuri

Thursday, February 1, 2024

AMEND TANZANIA LATOA MAFUNZO KWA MAOFISA USAFIRISHAJI.



Shirika la AMEND Tanzania ambalo linajihusisha na masuala ya kutoa elimu kwa wananchi kuhusu usalama barabarani limeweza kutoa elimu na mafunzo kwa maafisa wasafirishaji wa vituo tofauti katika jiji la Dodoma.

Shirika hilo ambalo lipo chini ya ufadhili wa Ubalozi wa Uswisi nchini Tanzania limeweza kutoa elimu na mafunzo kwa maafisa wasafirishaji maarufu kwa jina la bodaboda kwa malengo ya kudhibiti wigo ajali barabarani pamoja na kuwapa mafunzo mbali mbali pamoja na utumiaji wa alama za barabarani ambazo zimekuwa zikipuuzwa na maafisa wasafirishaji hao.

Nuhu Toyi ambaye ni balozi wa mafunzo na afisa msafirishaji kutoka kituo cha UDOM  jijini Dodoma amesema alibaatika kupata mafunzo ambayo yametolewa na shirika la AMEND Tanzania na kupitia mafunzo hayo yameweza kumsaidia kuendesha chombo chake kwa kujihamini bila kusababisha ajali.

“Pongezi za dhati ziende kwa Ubalozi wa Uswisi nchini Tanzania hususan kitengo cha afya kinachofadhiliwa na miss Vivian kwa kutambua umuhimu wa kundi hili la vijana wa bodaboda wengi ni vijana ambao tupo kati ya umri wa miaka 25. Kazi hii wengi tumekuwa tukiifanya kwa mazoea na hatuna elimu kwaio wengi tumekuwa ni wahanga wa kusababisha au kusababishiwa ajari kwasababu ya kukosa elimu barabarani lakini Ubalozi wa Uswisi nchini Tanzania umeona itakuwa ni vyema kama vijana hawa ambao ni taifa la kesho na nguvu kazi ya taifa wasiweze kudhuulika na ajali” alisema Toyi.

Kwa upande wake afisa usafirishaji, Laurenti Mayowa amesema alikuwa haelewi alama za barabarani lakini kupitia mafunzo hayo wamepokea kutoka shirika la AMEND Tanzania kwani limekuja kitofauti katika kutoa mafunzo yao kwani wamefundishwa kwa nadharia pamoja na vitendo.

“Tulipata mafunzo mazuri sana kwenye swala la uendeshaji wa pikipiki lakini pia tumeweza kufundishwa namna ya kutumia barabara lakini pia namba ya kutumi vyombo vyetu, kwa kweli mafunzo yalikuwa mazuri nimejifunza mambo mengi na mazuri na kabla ya mafunzo nilikuwa sielewi kwamba barabarani nilikuwa naendesha hovyo hovyo tu na baada ya mafunzo nashukuru mpaka sasaivi nime elewa na tulikuwa wengi sana tukifundishwa awamu kwa awamu nafikiri bodaboda takriban 230 au 250 kwa Dodoma hapa na sasahivi wame elimika”, alisema Mayowa.

Alisema alama za barabarani ilikuwa ni changamoto kwa madereva wengi , walikuwa wanaziona lakini wanashindwa kuzitumia kama ipasavyo na walidhani ni michoro tu lakini baada ya mafunzo waliweza kuelewa aina za michoro na alama zinazotumiwa barabarani.

“Tulifundishwa kuna alama za onyo, alama za amri, kuna alama za maelekezo kwaio hayo yote tumefundishwa lakini pia nimefundishwa alama nyengine ambazo nilikuwa sizielewi vizuri kama alama za michoro juu ya sakafu ya barabara hizo nazo nilikuwa sizielewi nilikuwa naona tu michoro na sielewi maana yake lakini baada ya elimu nimevielewa vizuri” alisema Mayowa

Aidha alisisitiza kwa maafisa usafirishaji kubadilika  na kuwa na mahudhurio mazuri ya mafunzo yanayotolewa na shirika la AMEND Tanzania kwasababu yanafundishwa kwa vitendo pamoja na kutii sheria za barabarani.

“Tumefundishwa dereva kujihami kwaio wale ambao hawajapata mafunzo hawezi kuelewa na kutii sheria akiwa yupo barabarani na anaweza kusababisha ajali kwasababu anakuwa hana uelewa wowote na vigumu kujilinda anapotumia chombo chake”,Mayowa.

Naye afisa usafirishaji kutoka kituo cha Ndasha,Bw. Ally Rashid Ally alisema kuwa bodaboda ni ajira kama zilivyo ajira nyengine na imeteka soko kubwa la ajira kwa vijana kwenye upataji wa kipato na awali haikupewa thamani kama zilivyo biashara nyengine.

Amesema wamekuwa na madereva usafirishaji wengi lakini baadhi yao kwenye kundi hilo hawana elimu ya kutosha ya barabarani na kutambua alama zilizomo.

Aidha Bw. Ally amesema elimu iliyotewa ni msaada mkubwa kwa maafisa usafirishaji mkoani Dodoma kwani wengi wao wamekuwa na nidhamu iwapo wanatumia vyombo vyao barabarani na changamoto za ajali na vifo vimeweza kuepukika kutokana na maarifa waliopokea kutoka kwa wakufunzi kupitia shirika la AMEND Tanzania.

WIZARA YA KATIBA NA SHERIA KUENDELEA KUWEKA MIUNDOMBINU YA TEHAMA

Wizara ya katiba na Sheria imeendelea kusimamia uwekaji wa mifumo na miundombinu ya TEHAMA thabiti ili kuhakikisha wananchi wote wanafanikiwa na huduma za kisheria na wanafikiwa vizuri ikiwemo kupata elimu ya masuala ya sheria.

Hayo yameelezwa leo Januari 30,2024 jijini Dodoma na Waziri wa Katiba na Sheria Balozi Dkt.Pindi Chana wakati akikabidhi vifaa vya TEHAMA kwa taasisi za haki jinai.

"Masuala ya sheria ni vizuri wananchi nao wakayajua, uendeshaji wa kesi,upatikanaji wa nyaraka za kesi na ushahidi hukumu na maamuzi ya kesi na uwepo wa vyombo vya utoaji haki katika ngazi za jamii"Amesema 

Aidha amesema serikali imejidhatiti katika kuimarisha masuala ya utoaji na upatikanaji wa haki nchini

"Kama alivosema katibu Mkuu unapochelewesha haki ni kama mtu ananyimwa haki,nisingependa tuwe wacheleweshaji wa haki hizo"

Hata hivyo ameongeza kuwa taasisi za haki jinai zimejenga mifumo mizuri ya TEHAMA ambayo inarahisisha upatikanaji wa taarifa na huduma za kisheria kwa wananchi,kwa Wakati bila urasimu na kuepusha rushwa.

"Uwepo wa mifumo ya TEHAMA na matumizi ya teknologia utawapunguzia wananchi muda na gharama za kushughulikia masuala ya kisheria na badala yake watajikita zaidi katika shughuli za Kiuchumi na maendeleo"

Awali akimkaribisha Waziri wa Katiba na Sheria Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Bi.Mary Makondo ameeleza Kuwa mradi huu umelenga kuimarisha matumizi na fursa za TEHAMA nchini ili kurahisisha upatikanaji wa haki

Pia kuimarika kwa matumizi ya TEHAMA kunawezesha kuziunganisha taasisi za haki jinai katika mfumo mmoja wa kielectronic katika kuwasiliana kiutendaji na hivyo kuimarisha ubora na upatikanaji wa huduma za kisheria zinazotolewa na taasisi hizi 

"Tangu kuanziashwa kwa mfumo huu Kazi zifuatazo zimetekelezwa ikiwa ni pamoja na upembuzi yakinifu wa mahitaji ya sekta ya sheria pamoja na haki jinai kuelekea haki mtandao,vile vile ujenzi wa miundombinu ya TEHAMA kwenye jengo la Wizara"Amesema

Aidha ameeleza Kuwa Wizara inaendelea kutumia fursa ya TEHAMA kwa kushirikiana na taasisi za serikali pamoja na wadau katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kwa wakati.



Kwa upande wake Mkurugenzi mkuu wa Mashitaka nchini(DPP) Sylvester Mwakitalu akitoa salaam fupi za ofisi yake amesema ofisi ya Mashitaka imefarijika kupokea vifaa hivyo na vitawasaidia katika kuboresha utendaji wao wa kazi na katika kuwahudumia watanzania 


Aidha tunaamini vifaa hivi vitatusaidia katika kuhakikisha kwamba haki za wananchi tunaowahudumia zinapatikana kwa wakati

 

Naye Mkuu wa Gereza la Msalato SSP Flavian Justine ameeleza Kuwa vifaa hivyo kwao ni muhimu kwa kuhifadhi taarifa za wahalifu,lakini pia kwa kurahisisha taarifa za mawasiliano kati ya magereza na mahakama na kuipunguzia serikali gharama za kusafirisha wahalifu kuhudhuria mahakamani.

WANANCHI WAJITOLEA KUJENGA OFISI YA MTAA ZEGERENI





WAKAZI wa Mtaa wa Zegereni Wilayani Kibaha Mkoani Pwani wamejitolea kujenga ofisi ya kisasa ya Mtaa ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye eneo la ujenzi Mwenyekiti wa Mtaa huo Rashid Likunja amesema ofisi iliyopo ni ya zamani ambapo imejengwa miaka 20 iliyopita.

Naye Mtendaji wa Mtaa huo Femida Ayubu amesema kuwa wameweka utaratibu wa kila kaya kuchangia ujenzi huo ambao hufanywa kila Jumatano.

Kwa upande wake moja ya wananchi Leah Chambo amesema kuwa wanashirikiana na mtaa kwa kujitolea shughuli mbalimbali za maendeleo kwenye mtaa wao ili huduma ziwe bora.