Monday, September 21, 2015

WENGI WAMUAGA MTOTO WA ALIKUWA KIONGOZI WA WAFUGAJI, RAIS DK JAKAYA KIKWETE ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI

Na John Gagarini, Lugoba
WAGOMBEA wanaowania nafasi za uongozi hapa nchini wametakiwa kukubali matokeo mara uchaguzi utakapofanyika Oktoba 25 mwaka huu kwani kuna maisha mengine baada ya uchaguzi  kuendelea kufanya kampeni zao huku wakiendelea kuhubiri na kulinda amani iliyopo kwani wana nafasi kubwa ya kuwashawishi wafuasi wao wasifanye vurugu au kufanya vitendo vinavyosababisha uvunjifu wa amani.
Pia wagombea watakaoshindwa kwenye uchaguzi mkuu wakubali matokeo kwani kwenye washindani lazima kuwe na washindwa ili kuondoa hali ya mafarakano kwani kwa wale watakaoshindwa wasipokubali matokeo wanaweza kuleta uvunjifu wa amani.
Hayo yalisemwa juzi Kijiji cha Maviayangombe kata ya Lugoba wilayani Bagamoyo mkoani Pwani na Askofu mkuu wa Dayosisi ya Morogoro ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Jacob Mameo Ole Paulo wa Dayosisi ya Morogoro wakati wa mazishi ya mtoto wa aliyekuwa kiongozi wa wafugaji Laban Moreto, Karokya Moreto (33) ambaye alikuwa mwanajeshi wa kikosi cha 04/691 cha Mtwara.
Askofu Ole Paulo alisema kuwa wagombea hao wanauwezo wa kudumisha amani kwa kuhubiri au kuingiza nchi kwenye machafuko endapo watayatumia vibaya majukwaa wakati wa kipindi hichi cha kampeni za uchaguzi.
“Wanapaswa kuhubiri amani na kuacha kutumia maneno yatakayo haribu amani ya nchi iliyopo ambayo imedumu kwa kipindi kirefu tangu nchi ilipopata uhuru miaka zaidi ya 50 hivyo itakuwa ajabu ivunjwe kisa kuwania uongozi tu,” alisema Askofu Ole Paulo.
Aidha alisema kuwa vyama vya siasa vinapaswa kupingana kwa hoja na kwa malumbano ambayo hayana maana bali yanaweza kuleta mitafaruku isiyokuwa ya lazima hasa kwa wale wanaoshindwa kwani wanapaswa kukubali matokeo.
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa amesikitishwa na kifo cha marehemu ambaye alikuwa ni ndugu kwani wamekuwa wakiishi kama familia moja na walikuwa na ushirikiano mkubwa baina ya familia zao.
Ridhiwani alisema kuwa kifo hicho ni pigo kwa familia hiyo pia kwa Taifa kwani alikuwa ni mtumishi wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na alikuwa mtaalamu wa rada hivyo pengo lake haliwezi kuzibika kikubwa ni kumwombea marehemu.
Kufuatia msiba huo Rais Dk Jakaya Kikwete alituma salamu za pole kwa familia hiyo kupitia kwa Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete na kusema kuwa anatoa pole na Mungu awape nguvu katika kipindi hichi kigumu cha maombolezo na yuko pamoja nao.
Alisema kuwa Rais alishindwa kuhudhuria msiba huo kwani kwa sasa yuko nje ya nchi lakini pindi atakaporudi ataitembelea familia hiyo kwa ajili ya kuifariji kufuatia kifo cha mtoto wa aliyekuwa kiongozi wa kabila wafugaji
Naye mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mathayo Torongei alisema ili amani iendelee kuwepo ni vema dola ikatenda haki badala ya kupendelea upande mmoja.
Marehemu alifariki kwa ajali baada ya gari alilokuwa akiendesha kupasuka tairi la mbele na kusababisha ajali iliyopelekea kifo chake siku ya Septemba 16 mwaka huu  huko Mtwara ameacha mke na watoto watatu.
Mwisho. 







Mgombea Ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete kulia akifurahia jambo na mkuu wa wilaya ya Nachingwea mkoani Lindi Pololet Mgema wakati wa mazishi ya Karokya Moreto (33) mtoto wa alikuwa kiongozi wa wafugaji Laban Moreto huko Kijiji cha Maviyangombe kata ya Lugoba. 

 Baadhi ya Wazee wakiwa wamekaa kwenye msiba huo huko kijiji cha Maviyangombe Lugoba wilayani Bagamoyo. 

Kulia ni Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Morogoro  Jacob mameo Ole Paulo akiwa na mgombea Ubunge jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete. 

Kulia Ridhiwani Kikwete mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia CCM akifuatiwa na mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga, mkuu wa wilaya ya Nachingwea Pololet Mgema na mgombea ubunge Jimbo hilo kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Matayo Torongei wakiwa kwenye msiba huo. 

 Askofu Jacob Mameo Ole Paulo akizungumza wakati wa msiba huo. 

Baadhi ya ndugu wa wakilia kuomboleza kifo cha ndugu yao. 

 baadhi ya ndugu wa wakilia kuomboleza kifo cha ndugu yao.

Akinamama ndugu wa karibu wa marehemu wakilia kuomboleza kifo hicho. 

Baadhi ya askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania JWTZ wakiwa wamebeba jeneza lilokuwa na mwili wa marehemu kuelekea makaburini kwa ajili ya mazishi. 

Baadhi ya waombolezaji wakiaga mwili wa marehemu kabla ya mazishi  

Sehemu ya waombolezaji wa msiba huo. 

No comments:

Post a Comment