Sunday, September 6, 2015

BAKWATA WAASA UCHAGUZI MKUU

Na John Gagarini, Kibaha
KAIMU Mufti Mkuu wa Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Abubakari Zuberi amesema kuwa wanasiasa wanaokosa nafasi za uongozi wasiwe chanzo cha kuvunja amani ya nchi katika kipindi cha uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Aliyasema hayo juzi mjini Kibaha wakati wa maombi maalumu ya kuombea amani ya nchi yailiyoandaliwa na BAKWATA mkoa wa Pwani na kuwashirikisha viongozi na waumini wa kiislamu wa mkoa huo pamoja na waumini wa dini mbalimbali.
Mufti Zuberi alisema kuwa kuna baadhi ya viongozi walioshindwa na watakaoshindwa kwenye kuwania nafasi za uongozi wa kisiasa wanaonesha viashiria vya kutaka kuvunja amani iliyopo kutokana na kutokubali kushindwa.
“Kwa sasa tunaona viashiria mbalimbali vya kutaka kuvunja amani ya nchi     kutoka kwa baadhi ya wanasiasa hapa nchini na kutokana na hali hiyo tumeona ni vema tukafanya maombi haya kwa ajili ya kumwomba Mungu atunusuru na hali hiyo ili isije ikajitokeza,” alisema Mufti Zuberi.
Alisema kuwa Tanzania ni kama chumvi ya amani ambayo ikitumika vizuri itaongeza ladha lakini ikitumika vibaya itaharibu kila kitu hivyo ni vema Watanzania wakaendelea kuilinda amani iliyopo kwa sasa kwani baadhi ya majirani zetu wameathiriwa na vita na wanakimbilia kwetu.
“Tumwombe Mungu aendelee kutudumishia amani iliyopo kwa muda mrefu na tusikubali kuivunja amani yetu kwa tama ya baadhi ya watu wenye uroho wa madaraka kwani endapo amani itavunjika tutakuwa hatuna pa kukimbilia kwani majirani zetu wanakuja kwetu je sisi tutaenda wapi endapo amani itatoweka,” alisema Mufti Zuberi.
Kwa  upande wake mkuu wa Wilaya ya Kibaha Halima Kihemba ambaye alimwakilisha mkuu wa mkoa wa Pwani alisema kuwa tayari serikali imeweka mazingira ya uchaguzi kufanyika kwa njia ya amani na utulivu.
Kihemba alisema kuwa viongozi wa dini wanapaswa kuhakikisha amani inaendelea kudumu na kuwataka wawaelekeze waumini wao kufuta taratibu zilizopangwa katika kushiriki uchaguzi na wale wote waliojiandikisha watapiga kura na watakaokwenda kinyume cha sheria hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.
Naye Kadhi mkuu wa mkoa wa Pwani Abbas Mtupa alisema kuwa tayari wametoa maagizo kwa Maimamu na Masheikh wa misikiti yote kufanya maombi maalumu kila Ijumaa kuiombea amani ya nchi ili uchaguzi uwe wa amani.
Mtupa alisema kuwa maombi hayo maalumu ya kumwomba Mungu kwa wale wenye nia mbaya ya kuleta vurugu washindwe na maombi hayo yatakuwa endelevu hadi uchaguzi mkuu utakapoisha ili hali ya amani iendelee kudumu.
Mwisho.

  

     
 









Picha 1914 Kadhi wa mkoa wa Pwani Abbas Mtupa akizungumza kwenye maombi maalumu kuliombea taifa amani lilofanyika kwenye viwanja vya Bwawani Maili Moja Kibaha.

1918 Baadhi ya wakinamama waliohudhuria maombi maalumu ya kuliombea Taifa kuwa na amani katika uchaguzi mkuu wakiewasikiliza viongozi wao
1922 Mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba akihutubia kwenye maombi maalumu ya kuombea amani kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
1923 Sheikh Mtonda akiongea kwenye maombi maalumu kuliombea Taifa kuwa na amani kwenye kipindi cha uchaguzi.
1925 Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Pwani Said Lipambila akiwahutubia waumini wa Kiislamu waliohudhuria maombi maalumu kuiombea nchi kuwa na amani kipindi cha uchaguzi
1933 Kaimu Mufti mkuu wa Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Abubakari Zuberi akiwahutubia waumini wa dini ya kiislamu waliohudhuria maombi maalumu kuliombea Taifa kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja wilayani Kibaha
1936 Baadhi ya wamini wa dini ya Kiislamu wakiwasikiliza viongozi wao wakati wa maombi ya kuliombea Taifa kwenye uwanja wa Bwawani maili Moja Kibaha
1940 baadhi ya waumini wakisikiliza viongozi wao wakati wa maombi maalumu ya kuliombea Taifa
1947 Kaimu Mufti Mkuu Abubakari Zuberi kulia akizungumza na Kadhi wa mkoa wa Pwani Abbas Mtupa wakati wa maombi maalumu ya kuliombea Taifa kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja Kibaha


No comments:

Post a Comment