Sunday, September 13, 2015

MBUNGE KUTOA M 700 KUSAIDIA WAJASIRIAMALI

Na John Gagarini, Kibaha
MGOMBEA Ubunge wa Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Silvestry Koka ameunga mkono mpango wa kukipatia kila kijiji hapa nchini shilingi milioni 50 za uwezeshaji wajasiriamali kwa kuahidi kutoa kiasi cha shilingi milioni 700 kwa Jimbo hilo kwenye mpango huo.
Alitoa ahadi hiyo  wakati wa uzinduzi wa kampeni kwenye Jimbo hilo zilizofanyika kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja Kibaha mbele ya Mgombea Mwenza wa CCM Samia Suluhu Hassan ambaye alikuwa mgeni rasmi na kusema kuwa mpango huo ni mzuri na unapaswa kuungwa mkono na wadau wa maendeleo.
Koka ambaye alikuwa Mbunge wa Jimbo hilo anatetea kiti chake alisema kuwa tangu achaguliwe amekuwa akiwawezesha wajasiriamali wa Jimbo lote la Kibaha kwa kuwapatia fedha za kuwezesha vikundi vyao pamoja na mafunzo.
“Nimefurahishwa na mapango huo ambao ndiyo ilikuwa ajenda yangu ya kutaka wajasirimali waweze kuendeleza shughuli zao hivyo naipongeza serikali kwa kuona kuwa kuna haja ya kutoa fedha kwa ajili kuongeza pato la wananchi,” alisema Koka.
Alisema kuwa katika muda wake wa Ubunge miaka mitano iliyopita alitoa zaidi ya shilingi zaidi ya milioni 500 kwa wajasiriamali pamoja na kuwapatia elimu ya ujasirimali kupitia vikundi alivyohamasisha kuanzishwa.
“Nitatoa fedha hizo kwa kuiunga mkono serikali ili kuwaletea maendeleo wananchi wa Jimbo la Kibaha Mjini ambao wengi wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa mitaji kwa ajili ya kuendeshea shughuli zao,” alisema Koka.
Naye Mgombea Mwenza Samia Suluhu alisema kuwa mpango huo utawezesha wajasiriamali kukuza mitaji yao na  serikali itasimamia ipasavyo fedha hizo ili zisiweze kutumika vibaya ili ziweze kuleta manufaa kwa wananchi.
Samia alisema kuwa wenyeviti wa Vijiji ambao watazinyemelea fedha hizo kwa manufaa yao binafsi wajiandae kwani wale watakaozitumia kinyume cha taratibu watachukuliwa hatua kali ikiwa ni pamoja na kuwashtaki. Pia fedha kwa akinamama na vijana asilimia 10 kwenye halmashauri atasimamia na kuhakikisha zinatolewa kama taratibu zinavyoonyesha.

Mwisho.  

No comments:

Post a Comment