Tuesday, September 22, 2015

KAMPENI ZAENDELEA JIMBO LA CHALINZE

Na John Gagarini, Mandela
MGOMBEA Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi Ridhiwani Kikwete amesema kuwa endapo atafanikiwa kuchaguliwa kwenye nafasi hiyo atahakikisha zahanati inajengwa kwenye Kijiji cha Kibaoni ili kuwaondolea adha wananchi wa kijiji hicho.
Aliyasema hayo jana kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika Kijijini hapo kata ya Mandela na kusema kuwa ilani ya chama anasema kila kijiji lazima kiwe na zahanati huku kila kata ikitakiwa kuwa na kituo cha afya ili kurahishisha upatikanaji wa huduma za afya karibu.
Ridhiwani alisema kuwa hicho kitakuwa moja ya vipaumbele vyake ambavyo atahakikisha kuwa katika kipindi cha miaka mitano ujenzi huo unakamilika na wanakijiji wanapata huduma za afya karibu tofauti na sasa ambapo huwalazimu kwenda kijiji jirani cha Mandela.
“Ilani ya chama inasema kuwa kila kijiji lazima kiwe na zahanati hivyo endapo nikichaguliwa kwenye nafasi hii ya ubunge kwa kushirikiana na wananchi hivyo nitahakikisha zahanati inajengwa ili huduma zipatikane karibu,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa hata kata ya Mandela haina Kituo cha afya ambapo kata hiyo ni mpya ambayo imezaliwa kutoka kata ya Miono na kutaka ujenzi wa kituo hicho cha afya kujengwa kwenye kijiji hicho.
“Katika kipindi cha uongozi wangu wa mwaka mmoja na miezi miwili tumeweza kukarabati zahanati 24 huku nane zikiwa zimejengwa pia tumeweza kufanikisha kujngwa nyumba za waganga pamoja na upatikanaji wa vifaa tiba na dawa,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisema kuwa bado kuna changamoto ya baadhi ya vijiji kukosa zahanati hata hivyo mikakati ni kuhakikisha zinajengwa ambapo mipango inaendelea kwa kushirikiana na wananchi.
Kwa upande wake mgombea udiwani wa kata ya Mandela Madaraka Mbode alisema kuwa tayari kata imetenga eneo lenye ukubwa wa hekari 10 kwa ajili ya ujenzi wa zahanati kwenye kijiji cha Kibaoni.
Mbode alisema kuwa ujenzi wa zahanati hiyo utafanikiwa endapo wananchi watawachagua wgombea kutoka CCM lakini endapo wakiwachagua viongozi wa vyama vya upinzani hawataweza kupata maendeleo.
Naye mkazi wa Kibaoni Ally Athuman alisema kuwa changamoto kubwa inayowakumba wananchi kwenye zahanati wanazokwenda kupata matibabu ni ukosefu wa dawa.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mandela
MGOMBEA Udiwani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Mandela wilaya ya Bagamoyo Madaraka Mbode amemwomba mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kusimamia ujengwaji wa tenki kubwa la maji ili kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa maji.
Mbode aliyasema hayo kwenye Kijiji cha Lupungwi wakati wa mkutano wa kampeni za Ubunge nakusema kuwa Ridhiwani ndiye aliyeanzisha mchakato wa ujengwaji wa matenki kwenye baadhi ya vijiji.
Alisema kuwa awamu ya pili imevifanya vijiji vingi kwenye Jimbo hilo kuwa na maji lakini baadhi bado havijapata huduma hiyo ambapo awamu ya tatu ya mradi wa maji utavifikia vijiji na vitngoji ambavyo havikubahatika kupata maji.
“Wananchi nawaombeni mchagueni Ridhiwani kwani anauwezo wa kutufanikishia kupata maji ambapo kwa sasa maji yanatoka lakini endapo kunatokea tatizo kwenye mtambo maji hayapatikani ndiyo maana ujenzi wa matenki makubwa unaanza ili kuhakikisha maji yanapatikana muda wote,” alisema Mbode.
Aidha alisema kuwa anaomba na yeye achaguliwe kwenye nafasi ya udiwani ili ashirikiane na mbunge huyo kuwaletea maendeleo ambapo kwa sasa kijiji hicho kimewekewa nguzo kwa ajili ya kuwasambaziwa umeme.
Naye Ridhiwani Kikwete alisema kuwa tayari tathmini imeshaanza kufanywa ambapo wataalamu wameshachukua udongo kwa ajili ya kupima kabla ya kujenga tenki hilo ambalo litakuwa na uwezo wa kuhifadhi maji mengi.
Ridhiwani alisema kuwa awamu hii ya tatu ya mradi wa maji wa wami chalinze utavifikia vijiji na vitongoji vyote sambamba na ujengaji wa matenki makubwa kwa ajili ya kuhifadhia maji.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mandela
BAADHI ya waangalizi wa uchaguzi wamesema kuwa Tanzania imeweka historia kwa kuwa na waangalizi wengi kwenye uchaguzi wa mwaka huu hali ambayo itafanya uchaguzi kuwa huru na wa haki.
Hayo yalisemwa jana na mwangalizi wa ndani kutoka (TEMCO) Renatus Mkinga kwenye kijiji cha Lupungwi kata ya Mandela wilayani Bagamoyo wakati wa mkutano wa kampeni wa mgombea ubunge wa Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete.
Mkinga alisema kuwa kwa waangalizi wa ndani ni zaidi ya 6,000 huku wale wa kutoka nje wakiwa ni 600 ambao ni wengi na haijawahi kutokea katika chaguzi zilizopita.
“Sisi hatuna vyama tunachokifanya ni kuangalia ,mwenendo mzima wa uchaguzi kuanzia hatua ya kampeni hadi utakapofanyika uchaguzi Oktoba 25 mwaka huu,” alisema Mkinga.
Alisema kuwa kazi ya wasimamizi ni kuangalia mienendo ya uchaguzi katika kampeni na anaamini kuwa utakuwa huru na haki kwani hadi sasa kampeni zinaendele vizuri.
“Tunahudhuria kwenye mikutano ya vyama mbalimbali ili kuangalia wanapiga kampeni vipi na kuangalia wananchi wanajitokeza vipi kusikiliza sera za vyama husika,” alisema Mkinga.
Aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kusikiliza sera za vyama mbalimbali ili waweze kuangalia ni mgombea gani ambaye anawafaa ili mwisho wa siku waweze kumchagua kiongozi bora na si bora kiongozi.
Mwisho.
   

        

No comments:

Post a Comment