Tuesday, January 27, 2015

ZAKIA MEGHJI SHEREHE ZA CCM PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MLEZI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Pwani Zakia Meghji anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye sherehe za (CCM) kutimiza miaka 38 zitakazofanyika Kata ya Visiga wilayani Kibaha.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana mjini Kibaha katibu wa CCM Kibaha Mjini Abdala Mdimu alisema kuwa sherehe hizo zitaadhimishwa kwa shughuli mbalimbali za kuimarisha chama ambazo tayari zilishaanza tangu Januari 26 kwenye kata ya Mkuza.
Mdimu alisema kuwa Meghji ambaye ni Mbunge na Mjumbe wa Halmashauri Kuu (MNEC) atahitimisha sherehe hizo Februari Mosi kwenye kata hiyo ambayo imepewa upendeleo kutokana na chama hicho kuchukua mitaa yote saba kwenye uchaguzi wa wenyeviti wa Mitaa uliofanyika hivi karibuni.
“Wakati wa sherehe hizi kutakuwa na shughuli mbalimbali kama vile kukagua uhai wa chama ngazi ya mashina, matawi, kata wilaya pamoja na uhakiki wa daftari la uanachama ili kuwa na takwimu sahihi za wanachama,” alisema Mdimu.
Aidha alisema kuwa kazi nyingine ni kufanya mikutano ya kuhamasisha wanachama kujitokeza kujiandikisha katika daftarai la wapiga kura msisitizo ukiwa ni kwa wananchi wote wenye sifa kujiandikisha upya hata wale wenye vitambulisho vya kupiga kura miaka iliyopita.
“Tunatarajia Halmashauri kuu za kata zitafanyika kwenye kata hizo za Kibaha Mjini ambazo ni 14 ambapo wajumbe wa mkoa watasambaa kwenye kata hizo kabla ya mkutano mkubwa wa hadhara wa kuhitimisha sherehe hizo ambapo Meghji ndiye atakayefunga akiwa ndiyo mgeni rasmi,” alisema Mdimu.
Aliwataka wanaccm kujitokeza kwa wingi siku hiyo ili kwenda kumsikiliza mlezi wa chama siku hiyo ili waweze kuimarisha chama katika maeneo yao pia kujiandaa na uchaguzi mkuu wa mwaka huu ili kuhakikisha chama kinapata ushindi mkubwa wa kishindo huku kaulimbiu ya mwaka huu ikisema Umoja ni Ushindi (Katiba Yetu, Taifa Letu).
Mwisho.

  

WANASIASA WASIMWAGE DAMU WAKATI WA UCHAGUZI

Na John Gagarini, Kibaha
WANASIASIA nchini wametakiwa kuwa na hofu ya Mungu na kuacha kutumia lugha za kusema kuwa watamwaga damu wakati wa kipindi cha uchaguzi.
Hayo yalisemwa na Mchungaji wa kanisa la Gosheni Inland Church lililopo kitongoji cha Chamakweza wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Jackson Bukelebe, wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa shule ya awali kituo cha kuhudumia watoto wa wafugaji inayomilikiwa na kanisa hilo.
Mch Bukelebe alisema wao kama kanisa wanataka uchaguzi wa amani na utulivu na hawataki wanasiasa watakaotuvunjia hali ya amani iliyopo na kutuletea vurugu kwani hao hawafai na hawastahili kuwa viongozi na wanapaswa kutumia lugha za ustaarabu na siyo zile zitakazosababisha uvunjifu wa amani ambayo imedumu kwa kipindi kirefu tangu nchi imepata uhuru,
“Viongozi hawa wanapaswa kuwa na hofu ya Mungu na si kuwa na roho ya uharibifu na wakiwa na hofu ya Mungu watakuwa na upendo wa kuwapenda wengine na wataachana na mambo binafsi bali wataangalia mambo ya watu kwa ujumla,” alisema Mch Bukelebe.
Kwa upande wake mgeni rasmi kwenye harambee hiyo mwenyekiti wa CHADEMA Jimbo la Chalinze Mathayo Torongey alisema kuwa muda wa siasa umekishwa kinachotakiwa ni kuhakikisha shughuli za maendeleo zinafanyika ili kuwaondolea wananchi changamoto mbalimbali zinazowakabili.

“Kuhusu uchangiaji wa fedha kwa ajili ya elimu ni muhimu lakini kuna baadhi ya jamii ya wafugaji inaona kama elimu siyo jambo la muhimu hivyo kuwa wagumu kuchangia maendeleo ya elimu,” alisema Torongey.

Torongey ambaye alikuwa mgombe kwenye uchaguzi mdogo wa Jimbo la Chalinze aliwataka wanajamii ya kifugaji kutokuwa wagumu kuchangia elimu na kuacha tabia ya kuwaozesha watoto wao wakike badala yake wawapleke shule.

Awali akisoma risala kwa mgeni rasmi moja ya wanafunzi wanaosoma kwenye shule hiyo Amina Simbilwa alisema kuwa wamekuwa wakipata changamoto ya kukosa elimu kutokana na baadhi ya wazazi wao kuhamahama kutafuta malisho.

Shule hiyo ilianzishwa mwaka 2014 kwa lengo la kuwapatia elimu ya awali watoto hao kwani iliyopo iko mbali na wao ambao Kijiji chao ni cha Wafugaji na ina jumla ya wanafunzi 72.


Mwisho.   

Monday, January 26, 2015

MAJAMBAZI WALIOUA ASKARI BADO KUKAMATWA MSAKO WAENDELEA

Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la polisi mkoani Pwani,linaendelea na msako mkali wa kuwatafuta watu waliohusika kufanya mauaji ya askari wawili wa jeshi hilo pamoja na kuiba silaha mbalimbali kwenye kituo cha polisi Ikwiriri,wilayani Rufiji .

Pia limekanusha uvumi wa kuwa siku ya tukio hilo kuliwa na askari wengine ambao walikimbia kwa lengo la kujihami baada suala ambalo si la ukweli. 

Kamanda wa polisi mkoani humo kamishna msaidizi mwandamizi Ulrich Matei alisema kuwa hakuna hadi sasa hakuna mtu aliyekamtwa na msako  unafanywa usiku na mchana ili kuhakikisha wanawapata wahusika na kuwachukulia hatua za kisheria.

Aidha Matei aliitaka jamii kuacha tabia ya kuvumisha mambo yasiyo ya ukweli ama kuibua hoja zisizokuwa za ukweli baada ya matukio mbalimbali kutokea na badala yake anaetaka ukweli anatakiwa kuuliza kwa wahusika ili kupata taarifa za ukweli na si vinginevyo.

Wakati huo huo Mkuu wa wilaya ya rufiji Nurdin Babu amesema emesikitishwa na mauaji ya polisi wawili kwenye kituo cha ikwiriri wilayani humo juzi.
Akizungumza na gazeti hili Babu alisema kuwa tukio hilo ni la kusikitsha na halistahili kuungwa mkono na jamii iliyostaarabika.
"Inasikitisha sana na jambo hili ni ukatili na tunalilaani kwa nguvu zote na tutahakikisha tunawasaka watu waliohusika na tukio hili," alisema Babu.
Babu alisema kuwa wanaendelea kufuatilia na kufanya misako kwenye maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo ili kubaini waliohusika na tukio hilo la kikatili.
"Kuwaua watu wanaolinda usalama wa raia ni jambo la kusikitisha kwani linakatisha tamaa sana," alisema Babu.
Babu ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya alisema kuwa wananchi wanapaswa kutoa ushirikiano kuhakilisha watu hao wanatiwa mikononi mwa vyombo vya sheria na jeshi la polisi bado linaendelea na uchunguzi kubaini watu waliohusika na tukio hilo.
Mwisho.

HALMASHAURI YA MJI KUJENGA SOKO NA STENDI VYA KISASA

Na John Gagarini, Kibaha
HALMASHAURI ya Mji wa Kibaha inatarajia kuanza mradi mkubwa wa ujenzi wa Soko la kisasa pamoja na Stendi utakaogharimu kiasi zaidi ya shilingi bilioni 20 kuanzia Februari mwaka huu.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Adhu Mkomambo alipozungumza na mwandishi wa habari hizi na kusema kuwa taratibu za mwisho zinakamilika kuanza ujenzi huo.
Mkomambo alisema kuwa ujenzi huo wa soko na setndi vitakuwa mkombozi kwa wananchi wa Kibaha na mkoa mzima wa Pwani kutokana na kukosa vitu hivyo kwa muda mrefu.
“Pale kuna soko na stendi lakini havina hadhi ya Mji hivyo kupitia benki ya uwekezaji (TIB) tutajenga vitu hivi kwa lengo la kuboresha mji na kuleta maendeleo kwa wananchi wa wilaya ya Kibaha,” alisema Mkomambo.
Aidha alisema kuwa vitu hivyo ni moja ya vyanzo vya mapato ya Halmashauri hivyo ujenzi wake utazingatia ubora na viwango ili kuwa na hadhi kwani soko lililopo halina ubora kulingana na mji wa Kibaha
“Mbali ya miradi hiyo ambayo itaanza kwa pamoja pia Halmashauri itaendelea na miradi yake ya ujenzi wa barabara na uboreshaji wa sekta mbalimbali za jamii ili huduma ziweze kuwa bora,” alisema Mkomambo.
Alibainisha kuwa wataendeleza ushirikiano kati ya Halmashauri yake wananchi pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kuendelea kuuboresha mji huo unaoelekea kuwa Manispaa.
Mwisho.  




  

Friday, January 23, 2015

ASKARI ALIYEUAWA AAGWA

Na John Gagarini, Kibaha
KONSTEBO wa Polisi aliyeuwawa na majambazi waliovamia kituo cha Polisi cha Ikwiriri wilayani Rufiji mkoani Pwani Judith Timoth (32) juzi aliagwa mjini Kibaha na mamia ya watu wakiwemo askari wenzake aliowahi kufanya nao kazi kabla ya kuhamia Rufiji.
Mwili huo uliagwa kwenye hospitali ya Polisi mkoa na kuongozwa na ofisa wa jeshi hilo Thabita Makaranga, kwa safari ya kuelekea mkoani Mbeya kwa ajili ya mazishi  na kuliibua simanzi kubwa kwa watu waliohudhuria tukio hilo na kuvuta hisia na vilio kutoka kwa waombolezaji.
Akiongoza kwenye ibaada ya kumwaga marehemu mwinjilisti wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Maili Moja alikokuwa akisali kabla ya kuhamia wilayani Rufiji, Josephine Urio alisema kuwa watu wanapaswa kujiandaa kwa kusali muda wote kwani hawajui siku wala wakati watatwaliwa.
“Wanadamu wanapaswa kuacha roho za mauaji kama hao waliofanya mauaji hayo kwani hawako salama kama wanavofikiri Mungu atawapa pigo kama walivyotoa roho za watu wasiokuwa na hatia na watu wenye uovu waache njia hizo,” alisema Urio.
Akisoma wasifu wa marehemu moja ya wafanyakazi wenzake Robert Munisi alisema kuwa jeshi hilo litapambana na watu wote waliohusika na tukio hilo na kuliomba kanisa lilisaidie polisi kukabiliana na wahalifu hao na watasimamia amri kumi za Mungu.
Munisi alisema marehemu alizaliwa mkoani Mbeya na kupata elimu ya Msingi na Sekondari na kupata mafunzo ya sheria mkoani Mbeya kisha kujiunga na Chuo cha Mafunzo ya Polisi huko Moshi kuanzia Oktoba 30 mwaka 2004 na kuhitimu Fabruari 25 mwaka 2005 pia alipata mafunzo mbalimbali yakiwemo ya Upelelezi.
Aidha amesema marehemu kabla ya umauti alikuwa akisoma masomo ya Sociology mwaka wa pili Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) ameacha mtoto mmoja wa kiume aitwaye Bryan.Marehemu alivamiwa juzi akiwa kazini na mwenzake majira ya saa 8 usiku na kushambuliwa na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi waliokuwa na silaha na kufariki dunia yeye na mwenzake Koplo Edger Milinga.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAZAZI wa shule ya Msingi Juhudi kata ya Visiga wilayani Kibaha wameulalamikia uongozi wa shule hiyo kwa kuwarudisha watoto wao wanaojiunga darasa la kwanza kwa kushindwa kulipa kiasi cha shilingi 15,000 kwa ajili ya kuwaandikisha.
Moja ya wazazi hao Mabeka Mabeka akizungumza kwenye kikao cha wazazi alisema kuwa wanashangazwa na taratibu za kuwatoza kiasi hicho licha ya kuwa serikali imekataza michango hiyo na kusababisha wazazi kuwa kwenye wakati mgumu kupata fedha hizo.
Mabeka alisema kuwa wanaushangaa uongozi wa shule hiyo kwa  kuwaandikisha wanafunzi wa darasa la kwanza kwa kututoza fedha hizo jambo ambalo ni kinyume cha sheria kwani serikali ilitamka kuondoa michango kwa wanafunzi wanaoanza ili kuondoa kero kwa wazazi.
“Michango hii ni kikwazo kwa wazazi kuwapeleka watoto shule huku serikali ikitaka watoto wote waliofikia umri wa kwenda shule waandikishwe ili waweze kupata elimu ya msingi,” alisema Mabeka.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo Theobad Rwegalulila alikiri kuwepo kwa jambo hilo na kusema kuwa limekuwa changamoto kubwa kwa wazazi ambao wamekuwa wakilalamika kupinga malipo hayo ili watoto waweze kupata fursa ya kujiunga na darasa la kwanza.
Naye mwalimu mkuu wa shule hiyo Hawa Mgogolo alikiri kuwepo kwa michango hiyo na kusema kuwa walikubaliana na wazazi kwenye kikao cha wazazi mwaka 2012 lakini anashangaa wazazi hao kuanza kulalamika wakati wao wenyewe walikubali mchango huo.
Mgololo alisema kuwa ni kweli walikuwa wakiwatoza fedha hizo kwa ajili ya matumizi mbalimbali na fedha hizo zinatumika kununulia vitu mbalimbali kama vile chaki, madaftari ya maendeleo na vifaa mbalimbali kwa ajili ya wanafunzi hao.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SHULE ya Msingi ya Maili Moja iliyopo wilayani Kibaha inakabiliwa na ubovu wa madarasa ambayo yanaweza kuanguka wakati wowote hali ambayo inahatarisha usalama wa wanafunzi na walimu kwenye shule hiyo.
Kutokana na ubovu huo madarasa matano kati ya 11 ndiyo yanayotumika ambapo wanafunzi wanasoma zaidi ya wanafunzi 150 hadi 200 kwenye darasa moja.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kikoa cha dharura cha wazazi kuzungumzia ubovu wa madarasa hayo, mwalimu mkuu wa shule hiyo Reginald Fanuel alisema kuwa madarasa hayo yamebomoka vibaya.
“Madarasa hayo yako kwenye hali mbaya na wakati wowote yanaweza kuanguka na kusababisha maafa kwa wanafunzi na walimu endapo hazitachukuliwa hatua za haraka za kunusuru hali hiyo ambayo sasa imefikia hatu mbaya,” alisema Fanuel.
Fanuel alisema kuwa kutokana na hali hiyo wanaomba msaada wa kusaidiwa ujenzi ili kunusuru hali hiyo ambayo ni hatari kwa wanafunzi na walimu wanaotumia madarasa hayo pia mlundikano kwenye madarasa mazima ni mkubwa sana.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya shule Said Chitenje alisema kuwa tatizo hilo lilianza muda mrefu ambapo wamekuwa wakiakabiliana na hali hiyo kwa kuchangisha michango wazazi lakini michango imekuwa ikisusua.
“Kweli hali ni mbaya na kutokanana hali kuzidi kuwa mbaya tumekubaliana na wazazi kuwa kila mzazi ambaye ana mwanafunzi shuleni hapa atoe kiasi cha shilingi 5,000 kwa ajili ya kufanya ujenzi wa madarasa hayo,” alisema Chitenje.
Naye diwani wa kata ya Maili Moja Andrew Lugano alisema kuwa kwa sasa wanaendelea na mchakato wa kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya ujenzi wa madarasa hayo yaliyoharibika ili kuwanusuru wanafunzi hao.
Lugano alisema kuwa wazazi hao waliomba wakutane na mkurugenzi wa halmashauri ya Mji ili wazungumzie suala hilo na namna ya kuwez akukabiliana na tatizo hilo na kuwaomba watu na wafadhilimbalimbali kujitokeza kusaidia ujenzi wa majengo hayo.

Mwisho.  

Wednesday, January 21, 2015

MAJAMBAZI YAUA ASKARI WAWILI

Na John Gagarini, Kibaha

ASKARI wawili wa Jeshi la Polisi Kituo cha Ikwiriri wilayani Rufiji mkoani Pwani wamekufa baada ya watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kuwashambulia kwa silaha baada ya kuvamia kituo hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari kwa njia ya simu toka eneo la tukio Ikwiri wilayani Rufiji Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alisema kuwa majambazi hao walitumia silha kuwaua askari hao.

Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 8 kwenye kituo hicho cha Polisi cha Ikwiriri. Aliwataja askari waliokufa kuwa ni usiku Askari waliokufa ni namba E 8732 CPL Edger Milinga na WP 5558 PC Judith Timoth.

Alisema kuwa licha ya kufanya mauaji hayo pia walifanikiwa kupora silaha aina mbalimbali zikiwemo SMG 2, SAR 3, Ant Riot 1, mali ya serikali na S/Gun Protector mali ya kampuni ya Sigara Tanzania.

Aidha alisema kuwa pia watu hao waliharibu kwa kulipiga risasi gari la polisi la kituo  hicho lenye namba za usajili PT 1965.


Mwisho.

Wednesday, January 14, 2015

MRADI WAMI CHALINZE KUNUFAISHA 271,000

Na John Gagarini, Chalinze

MRADI wa Maji wa Wami Chalinze awamu ya tatu  mara utakapokamilika unaratajia kuwafikia wananchi 271,000 wa Jimbo la Chalinze wilaya ya Bagamoyo mkoa wa Pwani.

 Aidha mradi huo wenye thamani ya shilingi bilioni 60 unatarajia kuanza mwezi Machi mwaka huu utapunguza tatizo la upatikanaji wa maji kwa wakazi wa Chalinze ambao wanahudumiwa na mradi huo.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Meneja wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) Mhandisi Christer Mchomba alisema katika awamu hiyo itaongeza mitandao ya maji kwenye vitongoji 210 kutoka kwenye vijiji 47 ambavyo vilifikiwa kwenye utekelezaji wa awamu ya pili iliyoanza mwaka 2008.

 “Katika awamu ya tatu ya mradi huu yatajengwa pia matenki ya kuhifadhia maji kwenye vijiji 20 vya awamu ya kwanza kikiwamo kijiji cha Bwiringu, Msata, Lugoba, Msoga, Mandela na vingine ambavyo havikujengewa matenki,” alisema Mhandisi Mchomba.

Mhandisi Mchomba alisema kwa sasa awamu ya pili ,wizara inakamilisha ujenzi wa nyongeza ya chujio la maji ambalo litaongeza wingi wa maji yanayosafishwa na kuzalishwa.

Alisema kuwa watajenga tanki kubwa eneo la Mazizi lenye uwezo wa kuhifadhi maji yenye ujazo wa lita 200,000 pamoja na vituo vya maji kwenye vijiji na vitongoji vyote kwenye Jimbo hilo.

“Kwa sasa wanazalisha maji kwa asilimia 85 tu kutokana na mashine kushindwa kufanya kazi kikamilifu ambapo kwa siku ni mita za ujazo 2,000 badala ya 5,000 kwa siku,” alisema Mhandisi Mchomba.  

Kwa upande wake ofisa maabara wa mradi huo Riziki Kacheche alisema  kuwa maji ghafi yanapokuwa machafu zaidi tope huziba na kuzuia maji kuchukuliwa katika kiwango kinachotakiwa kwenda kusafishwa na hivyo kusabababisha uwezo wa kuzalisha maji na kuyasafisha kuwa mdogo.

Mwisho

Tuesday, January 13, 2015

VIONGOZI WA SERIKALI ZA MITAA NA VIJIJI WAASWA NA WANANCHI WAHAKIKISHIWA KUPATA UMEME


 Na John Gagarini, Bagamoyo
VIONGOZI wa serikali za mitaa na vijiji wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani waliochaguliwa hivi karibuni wametakiwa kusoma mapato na matumizi ili kuepuka kuenguliwa kwenye nafasi zao kama baadhi yao waliopita kukataliwa na wananchi.
Moja ya changamoto zilizosababisha viongozi hao waliopita baadhi yao walienguliwa na wananchi huku wengine wakishindwa kurudishwa kwenye kura za kuteuliwa kuwani uongozi kwenye uchaguzi uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana.
Hayo yalisemwa Bagamoyo na katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kombo Kamoto alipozungumza na wananchi wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo Ridhiwani Kikwete kwenye  vijiji vya kata za Kibindu, Mbwewe, Mdaula, Bwiringu, Fukayosi, Miono na Kiwangwa.
Kamote alisema kuwa viongozi hao waliochaguliwa na wananchi hasa wale wanaotoka chama hicho kwani hawana budi kuwatumikia wananchi ipasavyo kwa lengo la kuwatatulia changamoto ambazo zinawakabili katika nyanja mbalimbali kwenye huduma za kijamii.
“Mmechaguliwa na wananchi kwa heshima ya chama chetu, hususani kusoma mapato na matumizi hivyo niwasihi mchape kazi kama sheria na taratibu zinavyowaongoza, sitopenda kusikia wananchi wakilalamikia kuhusu utendaji wenu, mtambue mwaka huu mmeapishwa na mahakimu tofauti na miaka yote, hivyo yeyote atayekiuka kiapo hicho ataondolewa kwenye nafasi yake,” alisema Kamote.
Alisema kuwa viongozi hao watatakiwa kuitisha mikutano na kusoma mapato na matumizi kwa wananchi ili waweze kujua yanayofanyika kwenye maeneo yao.
Viongozi hao pia waliaswa kutokuwa madalali wa kuuza ardhi kiholela na kuwakandamiza wananchi ambao wakati mwingine hawajui haki zao za msingi.
“Baadhi waliondolewa kutokana na kushindwa kuitisha mikutano ikiwa ni pamoja na kushindwa kusoma mapato na matumizi hali iliyowafanya waondolewa madarakani au kushindwa kwenye uteuzi wa kuwania nafasi hizo, alisema Kamote.
Aidha alisema kuwa inashangaza kuona baadhi ya viongozi wanakuwa vinara wa kuuza maeneo na kama yupo kiongozi aliyekuwa anafanya hivyo wanapaswa kuacha na kuwa waadilifu ili kulinda nafasi walizopata.
“Viongozi huu si muda wa kuanza majigambo ama kujivunia nafasi mlizoshika  bali mnatakiwa kutimiza wajibu wenu kwa kusimamia ilani ya chama cha mapinduzi ili kuleta maendeleo kwa wananchi,” alisema Kamote.
Kwa upande wake Ridhiwani Kikwete aliwaomba viongozi hao kufanya kazi kwa bidii ili chama kiendelee kuaminika na kushika dola .
“Fanyeni kazi bila kubagua watu ,watumikieni pasipo kujali itikadi za kisiasa na hiyo ndio sifa pekee ya kiongozi wa sasa asiyejali udini,ukabila wala chama alichopo,”alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alisema kuwa yeye akiwa mbunge ataendelea kuwatumika ipasavyo katika kuwaondolea changamoto zinazowakabili.
mwisho.
Na John Gagarini,Chalinze
KILIO cha baadhi ya wananchi wa Jimbo la Chalinze kukosa umeme huenda kikaisha baada ya kuhakikishiwa kuwa watapata huduma hiyo kuanzia m,waka huu kupitia miradi ya umeme vijijini kupitia wakala wa umeme Vijijini (REA).
Changamoto hiyo itapungua kwenye maeneo mbalimbali ya Jimbo hilo katika vijiji ambavyo vipo kwenye awamu ya awamu ya tatu inayotarajiwa kuanza mwezi Juni mwaka huu kupitia miradi hiyo ya REA.
Akiwahutubia wananchi wa vijiji vya Kibindu, Mbwewe, Mdaula, Bwilingu, Fukayosi, Kiwangwa na Chalinze mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa serikali ya CCM imejipanga kuikabilia changamoto hiyo.
“Kila maeneo niliyopita nimekutana na malalamiko  kutoka kwa wananchi juu ya kukosa umeme wakati vijiji vingine vya kata hizo vikiwa vimepata umeme na kuhoji huku wao wakiona kwa macho umeme umepita juu na kwenda maeneo jirani,” alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alise kuwa anatambua umuhimu wa umeme hivyo amekuwa akifanya jitihada za kufuatilia na ndio maana amelazimika kufuatana na meneja wa miradi ya umemem mkoani Pwani Leo Mwakatobe ambaye anatolea ufafanuzi suala hilo.
“Mfano eneo la Kiwangwa halikuwepo katika umeme unaosambazwa na REA lakini baada ya kufanya juhudi hizo fedha zimepatikana hivyo utakuwa wa REA ambapo tanesco imetoa sh.milioni 420 na REA sh.milioni 800,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisema kuwa fedha hizo tayari ziko na kazi ya kuanza kusambaza umeme itaanza wakati wowote, kwani anajua umuhimu wa umeme lakini wananchi na kuwaomba wananchi wafahamu juhudi za serikali.
Kwa upande wake  mhandisi wa Tanesco mkoa wa Pwani, Mhandisi Leo Mwakatobe, alisema wanaendelea kumalizia utekelezaji wa awamu ya pili wa mradi wa REA na kazi iliyobaki ni mkandarasi kuanza kazi wakati wowote kuanzia mwezi huu.
Mwakatobe fedha kwa ajili ya mradi wa kusambaza umeme zimepatikana, hivyo wananchi wenye kuhitaji waanze kuchukua fomu.kinachotakiwa wawe na picha mbili na kitambulisho cha aina yoyote.
Mwisho




Monday, January 12, 2015

CHALIWASA YAKANUSHA MASHINE KUUZWA KENYA NA MAGAREZA YAPONGEZWA

Na John Gagarini, Wami
MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) imekanusha uvumi kuwa mashine za uzalishaji wa maji zimeuzwa nchini Kenya hali ambayo imesababisha maji kukatika mwezi mzima.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake    Meneja wa mamlaka hiyo Injinia Christer Mchomba alisema kuwa uvumi huo si wa kweli kwani mashine zote zipo na zinatumika kama kawaida.
Injinia Mchomba alisema kuwa uvumi huo umekuja kutokana na maji kutokutoka kwa sababu ya mashine hizo kuvuta uchafu ambao umesababisha kuziba na kushindwa kupitisha maji.
“Tatizo la maji kushindwa kutoka hakutokani na mashine kuuzwa bali ni kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha kwenye mkoa wa Morogoro ambapo ndiyo chanzo cha mto Wami na kusababisha uchafu kuwa mwingi na mashine kuziba na kuharibika hivyo maji kushindwa kutoka,” alisema Injinia Mchomba.
Alisema kuwa tatizo ni tekeo ambapo kwa sasa linawekwa ambalo likikamilika litasaidia kuchuja uchafu tofauti na ilivyokuwa mwanzo kwani maji zamani yalikuwa masafi na yalikuwa hayana uchafu.
“Uchafu huo unatokana na uharibifu mkubwa wa mazingira unaofanywa na watu wanaojihusisha na uchimbaji wa madini, kuingiza mifugo kwenye vyanzo vya maji na uchafuzi wa mazingira hivyo kusababisha uchafu mwingi kuja na maji,” alisema Injinia Mchomba.
Alisema kuwa ukarabati wa mashine hizo unaendelea ambapo umefikia asilimia 85 na baada ya miezi miwili au mitatu tatizo la ukosefu wa maji Chalinze litakuwa ni historia
“Tuna mitambo 30 na mingine mipya hata hatujaifungua iweje watu waseme kuwa imeuzwa wakitaka ukweli waje hapa ili waione kuliko kusema tu bila ya kujua ukweli na waache kuvumisha vitu ambavyo havina ukweli,” alisema Injinia Mchomba.
Aidha alisema kuwa kwa sasa kuna mradi unaotekelezwa ambao utavifikia vitongoji vyote vya Jimbo la Chalinze ambapo awamu ya tatu utatumia bilioni 60 hadi kukamilika.
Mwisho.   
Na John Gagarini, Ubena
MBUNGE wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete amelipongeza Jeshi la Magereza mkoani Pwani kwa ujenzi wa madarasa mawili ya shule ya Sekondari ya Bwawani kwa gharama nafuu.
Aliyasema hayo wakati akizindua madarasa hayo kwa ajili ya wanafunzi wa kutwa wa shule hiyo ambayo inamilikiwa na Jeshi hilo la Magereza eno la Ubena.
Ridhiwani alisema kuwa Jeshi hilo limeonyesha uzalendo wa hali ya juu na kutumia vizuri rasilimali fedha kwa kujenga madarasa hayo yenye mawili thamani ya shilingi milioni 31.8.
“Haya ndiyo mambo tunayoyataka kwa kufanya ujenzi wa vitu vya umma kwa matumizi mazuri ya fedha na ujenzi bora hivyo taasisi nyingine za serikali zinapaswa kuzingatia ujenzi kama huu,” alisema Ridhiwani.
Alisema baadhi ya taasisi za umma zimekuwa zikifanya ujenzi wa kawaida kwa gharama kubwa huku ukiwa haujazingatia ubora wa ujenzi wa majengo ambayo hutumiwa kwa muda mrefu.
Aidha alizitaka halmashauri kuwatumia wataalamu wa Magereza katika ujenzi wa majengo mbalimbali ambapo ujenzi wao unazingatia ubora matumizi bora ya rasilimali fedha.
Awali akimkaribisha mbunge huyo mkuu wa Magereza mkoa wa Morogoro  Kato Lugainunula ambaye alimwakilisha mkuu wa Magereza nchini John Minja, alisema kuwa lengo la Magereza ni kuihudumia jamii katika nyanja mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoaji wa elimu.
Lugainunula alisema kuwa awali shule hiyo ilitumika kutoa elimu ya sekondari kwa watumishi wa Magereza ambao walikuwa hawajapata elimu ya sekondari lakini waliondoa utaratibu huo na kutoa elimu kwa wanafunzi kutoka sehemu mbalimbali.
Naye kaimu mkuu wa shule hiyo ya Bwawani Emanuel Lwinga alisema kuwa madarasa hayo ni kwa ajili ya wanafunzi wa kutwa ujenzi wake ulitumia muda wa miezi mitano hadi kukamilika kwake.
Lwainga alisema kuwa kila darasa lina uwezo wa kuchukua wanafunzi kati ya 40 na 45 ambapo shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 396 wakiwemo wale wa kidato cha tano na shule hiyo ni moja ya shule zinazofanya vizuri kwenye matokeo ya kidato cha nne kimkoa.

  Mwisho.

Thursday, January 8, 2015

CHANGAMOTO YA MAJI NA VIONGOZI WAUZA KIJIJI

Na John Gagarini, Chalinze
UONGOZI wa Mradi wa maji wa Wami Chalinze wilayani Bagamoyo umetakiwa kutoa taarifa juu ya ukosefu wa maji ambao kwa sasa umedumu takribani mwezi mzima ambapo baadhi ya wanasiasa wa vyama vya upinzani wapotosha ukweli kuhusu tatizo hilo.
Hayo yalisemwa na diwani wa kata ya Bwilingu Nassa Karama katika viwanja vya Masoko wakati mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alipokwenda kusikiliza kero za wananchi wa kata hiyo.
Karama alisema kuwa maji kwa sasa ni kilio kikubwa kwa wakazi wa mjin huo  huku wao wakiwa hawana utaalamu wa kujua tatizo la ukosefu wa maji linatokana na nini hivyo kushindwa kuwapa majibu sahihi wananchi ambapo hali hiyo imesababishwa ndoo kuuzwa kwa shilingi 700 kutoka shilingi 200.
“Suala la kutotoka kwa maji ni la kitaalamu na wahusika wa mradi wa maji wa Wami Chalinze wanapaswa kutoa taarifa juu ya changamoto zinazosababisha ukosefu wa maji ili majibu yasitolewe na wanasissa ambao wanatumia fursa hiyo kupotosha ukweli wa tatazi hilo,” alisema Karama.
Alisema kuwa wananchi wanapata usumbufu mkubwa kwani kwa sasa wananunua maji kwa baadhi ya watu wenye magari ya kuuza maji ambapo kabla ya tatizo hilo walikuwa walikuwa wakinunua kwa sh.200 na sasa ni sh.700 hali inayosababisha kuwapa wakati mgumu baadhi ya wananchi  ambao baadhi yao kipato chao ni cha chini.
“Baadhi ya wanasiasa hao wanapotosha kwa wananchi kuwa kuna mashine mbalimbali za kukamilisha mradi huo zimeuzwa Nairobi nchini Kenya jambo ambalo linachanganya wananchi na kuleta tafsiri tofauti  kutokana na tatizo hilo,” alisema Karama.
Aliutaka uongozi wa maradi kuo kutoa taarifa juu ya ukosefu wa maji ili kutowapa mwanya wanasiasa  wenye nia ya kutumia jambo hilo kama mtaji wao wa kisiasa.
Naye Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akijibu kuhusiana na maswali hayo alisema anafanya taratibu ya kumpeleka waziri wa maji ili aweze kwenda kutembelea maeneo yenye kero kubwa jimboni humo kujionea hali halisi ya ukosefu wa maji.
Ridhiwani alisema kuwa tatizo kubwa la ukosefu wa maji linatokana na tope linaloingia katika mitambo hali inayosababisha maji kushindwa kutokana ambapo kwa sasa wamenunua chujio kwa ajili ya kuchuja uchafu ambao umekuwa ukiziba na maji kushindwa kutoka.
Aliwataka wanasiasa kuacha kupotosha ukweli kwani si jambo zuri kupotosha wananchi  na kuwataka wataalamu kujenga tabia ya kutoa taarifa ya vikwazo vilivyopo ili wananchi wajue.
Mwisho.
Na John Gagarini, Fukayosi
BAADHI ya  viongozi wa Kijiji cha Kidomole wilayani Bagamoyo mkoani Pwani waliohusika kuuza ardhi ya Kijiji hicho kinyume cha sheria wametakiwa kujiandaa kusimama kwenye vyombo vya sheria kujibu tuhuma hizo.
Viongozi hao kwa wameuza eneo kubwa la Kijiji ambapo wananchi wa maeneo hayo wanatakiwa kuondoka na kumpisha mununzi huyo ambaye amechukua eneo kubwa la kijiji.
Akizungumza na wananchi wa Kijiji hicho Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete, wakati wa ziara ya kutembelea na kukagua shughuli za maendeleo alisema viongozi hao lazima wachukuliwe hatua za kisheria kwa ukiukaji wa maadili ya uongozi.
“Inashangaza kuona mtu anakuja na risiti na kusema kuwa kanunua eneo lote la Kijiji na wananchi wanatakiwa kuondoka kumpisha eti mwekezaji jambo kama hili haliwezekani kwani taratibu haziruhusu na viongozi waliofanya hivi wajiandae kwa kukimbilia tutapambana nao ili haki ya wananchi ipatikane,” alisema Ridhiwani.

Alisema kuwa hatakuwa tayari kuona wananchi hao wanaondolewa kwani sheria za ardhi haziruhusu kuuza eneo la Kijiji zaidi ya hekari 50 zaidi ya hapo lazima suala hilo lipelekwe kwa kamishana wa ardhi.

“Inashangaza kusikia kiongozi kauza hekari zaidi ya 100 kwa mwekezaji sheria haisemi hivyo hata hizo hekari 50 lazima wanakijiji waridhie kwa kufanya mkutano mkuu ili kumpitisha muombaji lakini siyo watu wawili au watatu wanakaa huko ofisini na kuuuziana eneo kinyemela utaratibu huu haupo kisheria,” alisema Ridhiwani.

Akizungumzia kuhusiana na baadhi ya maeneo ya Kijiji kuwemo kwenye eneo la ranchi ya Taifa (NARCO) alisema kuwa uongozi wa halmashauri unapaswa kuonyesha mipaka kwani wananchi walioko kwenye eneo hilo walianza kuishi kabla ya ranchi hiyo.

Aidha alisema maeneo yote yanayomilikiwa na ranchi ya Taifa yaliwekewa mipaka na inajulikana rasmi kisheria tofauti na hapo ambapo ranchi hiyo ndo inaanza kuonyesha mipaka huku kukiwa hakuna alama yoyote na kuutaka uongozi wa ranchi kushirikiana na wananchi hao ili kuondoa malalamiko kwani wanapaswa kuondolewa kwenye maeneo hayo.
Mwisho.



Wednesday, January 7, 2015

WAKAZI CHALINZE WALALAMIKA UKOSEFU WA DAWA KITUO CHA AFYA

Na John Gagarini, Chalinze
WAKAZI wa Chalinze Mjini wameiomba Wizara ya Afya kuangalia upya mgawanyo wa dawa kwenye kituo cha Afya cha Chalinze kwani dawa zinazopelekwa kituoni hapo hazikidhi mahitaji.
Wagonjwa wengi wanaokwenda kuhudumiwa kituoni hapo licha ya kuandikiwa dawa hazipatikani na hutakiwa kununua kwenye maduka ya dawa.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara mbele ya Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete ambaye yuko kwenye ziara ya kukagua masuala ya maendeleo, moja ya wakazi wa Chalinze kitongoji cha Bwiringu aliyejitambulisha kwa jina la Athuman Rashid alisema huduma ya dawa hakuna kabisa.
“Kila ukienda kupata huduma kwenye kituo cha afya Chalinze utahudumiwa vizuri lakini dawa ni mtihani kwani utaambiwa dawa hakuna nenda kanunue kwenye maduka ya dawa,” alisema Rashid.
Rashid alisema kuwa mgawanyo wa dawa kwenye kituo hicho ni mdogo licha ya kuwa kituo hicho kinahudumia wagonjwa wengi lakini kinakuwa na upungufu mkubwa wa dawa.
“Ombi letu sisi kwa Wizara ya Afya ni kuangalia namna gani ya kukiwezesha kituo hichi kuwa na mgao mkubwa wa dawa kwani suala la dawa ni tataizo kubwa sana na linatuathiri kwani maduka ya madawa yanauza kwa bei za juu,” alisema Rashid.
Naye Mbunge wa Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa ni kweli changamoto hiyo ni kubwa sana kwenye kituo hicho na ni vema kituo hicho kikaangaliwa upya.
“Wagonjwa wamekuwa wakilalamika sana juu ya upatikanaji wa dawa kwani kituo hichi kinapewa dawa sawa na vituo vingine vya afya ambavyo havina wagonjwa wengi,” alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alisema tayari wameshaongea na Wizara hiyo na stoo ya madawa MSD juu ya kuomba kuongezewa mgao wa dawa kutokana na ukubwa wa kituo kwani mahitaji ni makubwa sana.

Mwisho.    w

Tuesday, January 6, 2015

MBUNGE WA JIMBO LA CHALINZE RIDHIWANI KIKWETE AENDELEA NA ZIARA JIMBONI

Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo Ridhiwani Kikwete akiwahutubia wakazi wa Kijiji cha Pera kweny kata ya Kibindu wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wakati wa ziara ya kutembela shughuli za maendeleo

 Ridhiwani Kikwete Mbunge wa Jimbo la Chalinze akikabidhi mpira kwa moja ya Wazee kwenye Kijiji cha Pera Kata Kibindu wakati wa zaiara yake kwenye jimbo hilo

 Hili ni darasa la shule ya msingi ya Kibindu ambayo iliezuliwa paa baada ya kutokea mvua kubwa iliyonyesha mwishoni mwa mwaka jana

 Diwani wa Kata ya Kibindu Mawazo Mkufya akiongea na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete mwenye kofia alipotembelea shule hiyo kuangalia uharibifu uliotokana na mvua kubw ailiyonyesha na kuharibu baadhi ya madarasa na ofisi ya mwalimu mkuu wa shule hiyo

 Moja ya Madarasa ya shule ya Msingi Kibindu yaliyoharibiwa na mvua kubw ailiyonyesha mwaishoni mwa mwaka jana 

 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kulia akiongea na waandishi wa habari hawapo kushoto ni diwani wa kata ya Kibindu Mawazo Mkufya. 

 Baadhi ya akinamama wa Kijiji cha Kibindu wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete hayupo pichani wakati wa ziara yake kwenye jimbo hilo

 Choo cha shule ya Msingi Maluiwi kikiwa kimebomoka hali ambayo inawafanya wanafunzi wa shule hiyo kujisaidia porini kwa zaidi ya miaka miwili sasa.

 Hichi ni choo cha nyasi ambacho kinatumiwa na walimu wa shule ya Msingi Maluiwi

 Mbunge wa Chalinze Ridhiwani Kikwete akiongea na wananchi wa Kitongoji cha Mdaula alipotembelea kwenye ziara yake ya kuangalia shughuli za maendeleo kwenye jimbo hilo.

Monday, January 5, 2015

MCHAKATO WA MAMLAKA YA MJI MDOGO CHALINZE CHANGAMOTO KUBWA, MAJAMBAZI WATUMIA MSITU WA MWIDU

Na John Gagarini, Ubena
MCHAKATO wa kuifanya Chalinze kuwa mamlaka ya Mji Mdogo umekumbwa na changamoto kubwa baada ya makundi mawili ya wakulima na wafugaji kupinga mpango huo.
Makundi hayo ambayo ndiyo makubwa katika Jimbo la Chalinze yameonekana kutoupokea mpango huo kwa madai kuwa utawasababisha kushindwa kufanya shughuli za ambazo ndizo zinazowafanya waweze kuishi.
Changamoto za kupinga mchakato huo zimebainika wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete kutembelea shughuli za maendeleo.
Akizungumzia changamoto hizo Ridhiwani alisema Jimbo hilo lilitenga maeneo kwa ajili ya wafugaji na wakulima katika mpango bora wa matumizi ya ardhi ambapo kila kundi linakaa kwenye eneo lake.
“Changamoto hizi zinakuja kutokana na hali halisi kuwa endapo mamlaka hiyo itakubalika ina maana kutakuwa na sheria ya kuzuia ufugaji wa mifugo pamoja na kuzuia kilimo huku makundi hayo yakitegemea shughuli hizo kuendeshea maisha yao,” alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alitoa mfano kwenye maeneo ya wafugaji ya Vijiji vya Chamakweza ambao wana mifugo zaidi ya 18,000, Lukenge wana mifugo zaidi ya 10,000 na Matuli mifugo zaidi ya 8,000.
“Wafugaji wamesema kuwa endapo Mamlaka hiyo itapitishwa mifugo yao wataipeleka wapi na wao ufugaji ndiyo maisha yao kwa ajili ya chakula pamoja na uchumi,” alisema Ridhiwani.
Alisema pia kwa wakulima nao hawataruhusiwa kulima je wataishije wakati kilimo ndiyo shughuli yao ya kuendeshea maisha yao ikiwa ni pamoja na uchumi wao na hawana kitu kingine wanachoweza kukifanya.
“Changamoto hizi katika kueleka Mji Mdogo zimekuwa ni kubwa na ukiangalia zina uzito hivyo mchakato huu umesitishwa huku serikali ikiwa inaangalia namna bora ya kufanya ili kutoathiri maisha ya wananchi,” alisema Ridhiwani.
Aliongeza hata hivyo wananchi wanapaswa kujiandaa na mabadiliko kwani kila jambo lina wakati wake ambapo mipango kama hiyo ina lengo la kuwasogezea huduma karibu wananchi.
Mwisho.
Na John Gagarini, Ubena
WANANCHI wa Kata ya Ubena Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani wameuomba uongozi wa Gereza la Ubena kuwaruhusu kulitumia eneo la pori la Mwidu kwenye barabara ya Morogoro Chalinze ambalo limekuwa likitumiwa na majambazi kujificha kwa ajili ya kuteka magari nyakati za usiku.
Ombi hilo lilitolewa na diwani wa kata hiyo Mrisho Choka mbele ya Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete ambaye yuko kwenye ziara kutembelea Jimbo hilo kukagua shughuli za maendeleo.
Choka alisema kuwa kuwa pori hilo limekuwa likitumiwa na majambazi ambao hujificha kisha kutega magogo barabarani na kusababisha ajali kisha kufanya uhalifu kwa kutumia silaha mbalimbali.
“Eneo hili limekuwa hatarishi kwa magari hasa nyakati za usiku ambapo kumekuwa na matukio mengi ya utekwaji wa magari ambayo kabla ya kutekwa husababishiwa ajali kwa kuwekewa magogo hivyo tunauomba uongozi wa gereza kuturuhusu tutumie eneo hilo ili kuzuia vitendo hivyo,” alisema Choka.
Alisema kuwa endapo wananchi watalitumia eneo hilo itasaidia kupunguza vitendo hivyo kwani kwa ambapo kwa sasa majambazi hao wanafanya wanavyotaka kutokana na eneo hilo kuwa pori.
Aidha alisema kuwa wiki iliyopita magari manne yalitekwa na katika kukabiliana na uhalifu katika eneo hilo wamekuwa wakifanya doria na askari polisi lakini hata hivyo majambazi hao wamekuwa wakiwategea na kutekeleza uhalifu.
Kwa upande wake Ridhiwani Kikwete alisema kuwa ombi lao atalipeleka kwenye vyombo husika ili lifanyiwe kazi ili kuondokana na vitendo hivyo ambavyo vimekithiri katika eneo hilo.

Mwisho.

Sunday, January 4, 2015

WALILIA WODI YA WAZAZI

Na John Gagarini, Chalinze
WANANCHI wa Kijiji cha Kwaruhombo kwenye Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wametoa kilio cha kujengewa wodi ya wazazi kwenye kituo cha afya cha Kwaruhombo ili wanawake wajawazito wasijifungue kwenye wodi za kawaida.
Akizungumza kijijini hapo wakati wa ziara ya maendeleo ya mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete, Hadija Stambuli alisema kuwa akinamama wamekuwa wakijifungulia kwenye wodi hivyo kutokuwa na usiri.
Stambuli alisema kuwa hiyo imekuwa changamoto kubwa kwa akinamama wanapokwenda kujifungua wamekuwa wanashindwa kusitiriwa wakati wa uzazi.
“Tunakuomba Mbunge wetu utusaidie wakinamama ili tunapokwenda kujifungua kwani hakuna usiri hivyo tungepata jengo maalumu kwa ajili ya kujifungungulia ingekuwa vizuri,” alisema Stambuli
Akijibu malalamiko hayo mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa kujifungua ni jambo jema na linahitaji usiri.
Ridhiwani alisema kuwa kwa kushirikiana na halmashauri ili kuhakikisha kunakuwa na jengo kwa ajili ya kinamama kujifungulia.
“Tutakaa na uongozi wa Halmashauri ili kuhakikisha kunakuwa na jengo maalumu kwa ajili ya kujifungulia ili kuwaondolea fadhaa akinamama wakati wakijifungua,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisikitishwa na matumizi mabaya ya mafuta kwa ajili ya gari la wagonjwa wanaopata rufaa na kuutaka uongozi wa kituo hicho kuhakikisha kinadhibiti matumizi hayo.

Mwisho.

WANANCHI WAMLALAMIKIA MWEKEZAJI

Na John Gagarini, Chalinze
WAWEKEZAJI kwenye Kijiji cha Changarikwa wametakiwa kufuata taratibu za kisheria ili kuondoa migogoro baina yao na wananchi.
Hayo yalisemwa na mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete, wakati akizungumza na wananchi wa Kijiji hicho kwenye ziara yake ya maendeleo jimboni humo.
Ridhiwani alitoa ushauri huo kufuatia wananchi hao kulalamika dhidi ya moja ya wawekezaji kwenye kijiji hicho kuchukua eneo lenye ukubwa wa hekari 500 na kutotimiza ahadi za kuwasaidia kwenye huduma za kijamii.
Moja ya wananchi wa Kijiji hicho Bakary Hatibu alisema kuwa mwekezaji huyo wakati anaomba ardhi hiyo moja ya masharti waliyokubaliana naye ni kuwajengea shule, zahanati na trekta lakini sasa ni miaka 15 hakuna hata kimoja alichotekeleza.
“Tumekuwa tukipata tabu kwani wakati mwingine tnazuiwa kupita kwenye maeneo amabayo yanamilikiwa na mwekezaji,” alisema Hatibu.
Kwa upande wake Mbunge huyo alisema kuwa kumekuwa na malalamiko mengi dhidi ya wawekezaji kujipatia maeneo pasipo kutimiza masharti ya maombi ya ardhi.
“Jambo la kushangaza ni mwekezaji kupewa hekari 500 na kijiji jambo ambalo ni kinyume cha sheria ya ardhi namba 5 ya mwaka 1999 inayosema kuwa kijiji kinauwezo wa kumpa mwekezaji si zaidi ya hekari 50,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa kama wameona mwekezaji hafai kwani wao ndiyo waliompa ardhi wanauwezo wa kumnyanganya kwa kufuata taratibu za kisheria endapo wataona ameshindwa kutekeleza ahadi wakati anaomba ardhi.
“Mnauwezo wa kumuondolea umiliki endapo atakiuka masharti kwani huo ni mkataba na endapo atakiuka masharti unaweza kuvunjika na ardhi ikarudishwa kwa wanakijiji,” alisema Ridhiwani.
Alisema ni vema wawekezaji wakatekeleza tatatibu ili kuwa na ushirikiano na wananchi ambao wanatoa ardhi yao ili nao wanufaike nayo.
Mwisho.


Saturday, January 3, 2015

SHULE HATARIN I KUWAANGUKIA WANAFUNZI

 Baadhi ya wananchi na wafanyabiashara wa Kijiji cha Kibindu wilayani Bagamoyo wakimsikiliza Mbunge wao wa Jimbo la Chalinze mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete alipotembelea Kijiji hicho wakati wa ziara yake ya kushukuru wananchi baada ya kumchagua kuwa mbunge miezi kadhaa iliyopita

 Akinamama wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete hayupo pichani baada ya kutembelea kijiji cha Kibindu kutoa shukrani kwa wananchi kumchagua kwenye nafasi hiyo miezi kadhaa iliyopita.

 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Kibindu wilayani Bagamoyo mkoani Pwani

 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akizungumza na waandishi wa Habari mbele ya jengo la shule ya Msingi Kibindu ambalo lilianguka kufuatia mvua kubwa ziulizonyesha mwishoni mwa mwaka jana kushoto ni diwani wa kata ya Kibindu Mawazo Mkufya.


 Moja ya madarasa ya shule ya msingi Kibindu likiwa limebomoka kufuatia mvua kubwa zilizonyesha mwishoni mwa mwaka jana.

 Diwani wa kata ya Kibindu Mawazo Mkufya aliyenyanyua mikono juu akitoa maelezo kwa Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kulia aliyevaa kofia ya kijani kufuatia mvua kubwa kubomoa madarasa ya shule ya Msingi Kibindu

 Moja ya Madarasa ya shule ya Msingi Kibindu likiwa limeezuliwa paa kufuatia mvua kubwa zilizonyesha mwishoni mwa mwaka jana na kusababisha madarasa mawili na ofisi ya mwalimu mkuu kuharibika.

 Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete akikabidhi mpira kwa baadhi ya viongozi wa timu za soka za Kijiji cha Kibindu

 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akionge na wananchi wa Kijiji cha Kibindu alipofanya ziara ya kushukuru wananchi wa Jimbo hilo kwa kumchagua kushika nafasi hiyo miezi kadhaa iliyopita.