Wednesday, January 9, 2013

WANAWAKE WATAKIWA KUIMARISHA VICOBA


Na John Gagarini, Kibaha

MWENYEKITI wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) mkoa wa Pwani Bi Zainabu Vullu amewataka wanawake Mkoani humo kuimarisha vyama vyao vya kuweka na kukopa (SACCOS) ili ziweze kuwakomboa kiuchumi.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati wa baraza la umoja huo lililoambatana na uchaguzi viongozi wa kamati ya utekezaji ya mkoa wa Pwani.
Bi Vullu alisema kuwa wanawake kwa kiasi kikubwa ndiyo wanaoendesha familia hivyo ni vema wakaviimarisha vyama vyao vya kuweka na kukopa ili waweze kuboresha maisha yao na familia zao.
“Vyama hivi maarufu kama Vicoba vimekuwa mkombozi kwa wanawake wengi kwani zamani walikuwa na wakati mgumu kutokana na taasisi za kifedha kuwa na masharti magumu,” alisema Bi Vullu.
Bi Vullu ambaye ni Mbunge wa Viti Maalumu kutoka mkoani Pwani alisema kuwa Vicoba vimewasaidia wanawake na kuwafanya waweze kuwa na maisha bora na familia zao.
“Baadhi ya mafanikio waliyoyapata wanawake kupitia vyama hivi ni pamoja kujenga nyumba, kusomesha watoto, kuanzisha vitega uchumi na kuendesha familia zao,” alisema Bi Vullu.
Alizipongeza baadhi ya wilaya kwa kuweza kujiwekea akiba ambapo wilaya ya Bagamoyo imejiwekea kiasi cha shilingi milioni 11 huku wilaya ya Kisarawe wakiwa wamejiwekea kiasi cha shilingi milioni 5.
Aidha aliwataka wanawake katika mkoa huo kuanzisha miradi mbalimbali ya kimaenedeleo kwa kutumia fedha hizo za Vicoba pia wajitokeze kuwania nafasi za uongozi ndani ya chama.
Mwisho.  

No comments:

Post a Comment