WAKALA WA HUDUMA ZA
MISITU (TFS) WILAYANI BAGAMOYO NA MIKAKATI YA KUNUSURU MIKOKO KUMALIZWA
Na John Gagarini
KATIKA kuhakikisha misitu inalindwa hivi karibuni serikali
ilianzisha Wakala wa Huduma za Misitu kwenye wilaya zote hapa nchini ili
kuboresha usimamizi.
Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imechukua baadhi ya
majukumu kutoka idara ya misitu.
TFS imepewa jukumu la kutunza misitu ya hifadhi ya Taifa
(Misitu ya Asili na Mashamba ya Miti), Hifadhi za nyuki na mazao yatokanayo na
nyuki.
Majukumu ambayo TFS
imeyachukua ni pamoja na kuanzisha na kusimamia hifadhi za misitu ya asili na
hifadhi za nyuki zinazomilikiwa na serikali kuu, kuanzisha na kusimamia
mashamba ya miti na mashamba ya nyuki yanayomilikiwa na serikali kuu.
Majukumu mengeine ni kusimamia rasilimali za misitu na nyuki
katika misitu ya wazi, kusimamia utekelezaji wa sheria na kanuni katika maeneo
yanayoihusu, kuendeleza watumishi, ukusanyaji wa maduhuli ya serikali kutokana
na mazao ya misitu na nyuki, kutunza mali na rasilimali na kutafuta masoko ya
mazo na huduma ya misitu na nyuki.
TFS imegawanyika kwenye kanda mbalimbali ambapo moja ya Kanda
ni ile ya Mashariki ambapo misitu ya serikali kuu wilayani Bagamoyo inaangukia
kwenye kanda hiyo.
Meneja wa TFS wilayani humo Bw Charles Mwamfute anaelezea
changamoto zinazokabili wilaya hiyo katika misitu ambapo ina eneo la misitu ya
hifadhi lenye ukubwa wa hekta 3,883 huku misitu ya hifadhi ya Mikoko ikiwa na
ukubwa wa Hekta 5,636.
Bw Mwamfute akizungumzia hifadhi ya Mikoko ambayo iko
pembezoni mwa Bahari ya Hindi kuanzia Kusini mwa Mto Mpiji hadi Kasakazini mwa
mto Mlingani ambapo upande wa Mashariki ni Bahari ya Hindi na Magharibi ni
bamvua (yanapoishia maji ya Bahari baada ya kujaa) kubwa la maji chumvi ya
Bahari.
Alisema misitu ya hifadhi ya Mikoko ni muhimu katika uhifadhi
wa viumbe hai wa baharini ikiwemo mazalia ya samaki na kuzuia mmomonyoko
wa kingo za bahari na utunzaji wa
mazingira kwa ujumla.
Alisema kuwa ndani ya
eneo hilo kuna
Visiwa vyenye miti isiyo ya Mikoko na maeneo hayo maji ya bamvua hayafiki
ambapo misitu imezungukwa na Vijiji tisa na maeneo hayo huvamivamiwa mara kwa
mara kwa kuwa si mikoko.
“Maeneo mengi yenye Mikoko yameharibiwa sana ambapo kwenye majangwa ya chumvi yana
migogoro mingi ambapo wanaotumia maeno hayo hawafuati taratibu ndani ya hifadhi
pia hawana hata hati miliki na kuweka Bikoni kinyume na matumizi ya hifadhi
ambpo hujiongezea maeneo na kuharibu Mikoko,” alisema Bw Mwamfute.
Alisema baadhi ya athari zilizotokana na kuvunwa miti ya
Mikoko ni pamoja na kukosekana mazalio ya samaki jambo ambalo linafanya samaki
washindwe kuzaliana na kusababisha kitoweo hicho kuwa adimu.
Alisema baadhi ya maeneo ya hifadhi za Mikoko imekatwa na
watu hao, kuchimba chumvi, kuanzisha mabwawa ya kuvua samaki huku wengine
wakiifyeka misitu hiyo kwa ajili ya kuona mandhari ya bahari ikiwa baadhi ya
wamiliki wa hoteli na watu binafsi.
Aliendelea kusema athari za kufyekwa misitu hiyo ya mikoko
kumeanza kuonekana kwani maji yamekuwa yakifika hadi kwenye hoteli na nyumba
hizo ambazo zinaonekana kuliwa na maji ya bahari kwa zilizojengwa pembeni ya
Bahari.
Alisema kuwa zaidi ya hekta 70 za hifadhi ya misitu ya Mikoko
imeharibiwa na watu hao wengine wakiwa ni wawekezaji ambapo katika kukabiliana
na uharibifu huo wameshaanza kuchukua hatua kwa kuwapeleka mahakamani
waharibifu hao pia kuanza kupanda upya miti hiyo muhimu kwa viumbe hai ambapo
moja ya adhabu watakazo zipata watu hao ni pamoja na kupanda miti ya Mikoko na
kuwajibika endapo miti hiyo itakatwa.
“Pia tumeanzisha kamati za utunzaji wa misitu hiyo kwenye
vijiji ambavyo vinazunguka hifadhi hizo ambapo hutuletea taarifa za waharibifu
hao ambao wengine huharibu misitu hiyo nyakati za usiku na kufanya ufuatiliaji
kuwa mgumu,” alisema Bw Mwamfute.
Hata hivyo alibanisha changamoto kubwa inayowakabili ni idara
ya ardhi kuwapatia watu ardhi kwenye maeneo ya hifadhi jambo ambalo limekuwa
likisababisha uharibifu kuendelea kwani watu hao wanabainisha kuwa wanapewa
maeneo hayo kihalali.
Aliongeza kuwa ramani za hifadhi hizo ziliwekwa tangu enzi za
mkoloni miaka ya 50 kabla hata nchi haijapata uhuru ambapo wakoloni waliilinda
misitu hiyo bila ya kuiharibu kinyume na ilivyo sasa ambapo watu wanaiharibu
bila ya kuangalia athari zinazoweza kujitokeza.
“Changamoto kubwa tuliyonayo ni ushirikiano mdogo na baadhi
ya taasisi ikiwemo ardhi kwenye halmashauri kwani sheria ya misitu inasema
mwisho wa hifadhi ya Mikoko ni pale Bamvua linapoishia lakini watu wa ardhi
wanagawa ardhi ndani ya eneo hilo
ambalo liko ndani ya hifadhi,” alisema Bw Mwamfute.
Alisema changamoto nyingine ni kuwa na watumishi wachache
ambapo ni watumishi wawili tu ndiyo wanaofuatilia eneo hilo lenye ukubwa wa zaidi ya hekta 5,000 ya
hifadhi ya Misitu ya Mikoko.
Aidha Bw Mwamfute alisema kuwa kutokana na wakala kupewa
majukumu ya kusimamia msitu watatumia sheria kuwadhibiti watu wanaoharibu
misitu hiyo kwa kuwachukulia hatua kali za kisheria.
Kwa upande wake ofisa misitu wa wilaya ya Bagamoyo Bw Joseph
Msaki alisema kuwa kikubwa kinachotakiwa ni watu kupewa mafunzo juu ya utunzaji
wa misitu hiyo.
“Kitu kingine tutahakikisha tunapata ramani ya eneo la
hifadhi ili kuondoa utata uliopo na kisha kuunda kamati mpya za mazingira za
kila kijiji kisha kuweka sheria ndogo ndogo na kuwa na ushirikiano na sekta
zingine,” alisema Bw Msaki.
Kwa upande wake
mwenyekiti wa kamati ya ya Mikoko katika Kijiji cha Kiharaka Bw Msafiri Kiponda
alisema kuwa baaadhi ya wawekezaji wamefanya uharibifu mkubwa wa kukata mikoko
wakidai kuwa wamepewa vibali na watu wa ardhi.
Bw Kiponda alisema kuwa kutokana na mitkoko kufyekwa na
wawekezaji hao mazalio ya samaki hakuna hali inayowafanya wakose samaki hivyo
kukosa miradi ya uhifadhi wa viumbe hai na hawatoi asilimia yoyote kwenye
Kijiji kama sheria inavyowataka.
Kutokana na uharibifu mkubwa wa hifadhi ya Misitu ya mikoko
na ile mingine kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Bagamoyo ikongozwa na
mkuu wa wilaya hiyo Bw Ahmed Kipozi ilitembelea misitu hiyo na kujionea hali
mbaya ya misitu.
Mkuu wa wilaya hiyo alitaka apewe majina ya watu waliojenga
kwenye hifadhi ya misitu ya Mikoko kwani wamesababisha uharibifu mkubwa ambo
hautaweza kuvumiliwa kwani athari za kuharibu misitu hiyo ni kubwa
ikilinganishwa na faida itakayopatikana ni kwa watu wachache huku wengi
wakiathirika kwa kuharibiwa mazingira.
Bw Kipozi alisema kuwa mbali ya kupewa majina ya watu
waliojenga na kuharibu mikoko pia apewe majina ya maofisa wa ardhi toka
halmashauri ambao waliwapatia watu ardhi kwenye maeneo ya hifadhi ya Mikoko na
kusababisha uharibifu huo mkubwa kwa wilaya ya Bagamoyo.
Aliwataka watendaji wa halmashauri kushirikiana na wakala hao
ili kuepusha kuvunwa misitu hiyo ya Mikoko kwani kugawa maeneo hayo ya hifadhi
ni kuchangia kuendeleza uharibifu ndani ya hifadhi hiyo.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment