Saturday, January 19, 2013

WAAGONJWA WAAATIBIWA KWA VIBATARI


Na John Gagarini, Kisarawe
KUTOKANA na kukosa umeme zahanati ya Vikumburu tarafa ya Chole wilayani Kisarawe mkoa Pwani inatumia vibatari kutoa matibabu kwa wagonjwa nyakati za usiku.
Pia vibatari hivyo hutumika hata kuzalisha mama wajawazito wanaokwenda kujifungua nyakati hizo.
Hayo yalibainishwa na baadhi ya wakazi wa kata ya Vikumburu wakati wa ziara ya siku tatu kwenye wilaya ya Kisarawe iliyofanywa na Katibu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa Bi  Amina Makilagi
Wakazi hao walibainisha kuwa ukosefu wa uememe kwenye kata hiyo pamoja na maeneo mengine imekuwa ni changamoto kubwa kwao wanapokwenda kupata matibabu hasa nyakati za usiku.
Kwa upande wake ofisa mtendaji wa kata ya Vikumburu Mohamed Lusonzo alikiri kuwepo tatizo hilo na kudai kero hiyo ianatokana na kutokuwepo kwa umeme.
Aidha alisema kuna tatizo la ukosefu wa gari la kubeba wagonjwa la kuwapeleka kwenye hospitali ya wilaya na endapo wakihitaji gari la wagonjwa hutakiwa kutoa kiasi cha shilingi 20,000 ya mafuta na 10,000 kwa ajili ya muuguzi.
“Mgonjwa akizidiwa akihitaji gari la wagonjwa hutakiwa kutoa kiasi cha shilingi 30,000 ambazo ni kwa ajili ya mafuta shilingi 20,000 na shilingi 10,000 kwa ajili ya muuguzi jambo ambalo linawapa wakati mgumu kupata fedha hizo,” alisema Bw Lusonzo.
Kutokana na malalamiko hayo Bi Makilagi alitaka apelekewe majina ya watumishi wanaowatoza fedha hizo wagonjwa kwani ni kinyume cha taratibu.
“Ningependa nipewe majina ya watu hao wanaotoza fedha hizo ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao kwani ni kinyume cha taratibu wagonjwa kulipishwa hela ya mafuta,” alisema Bi Makilagi.
Bi Makilagi alilaani tabia hiyo inayofanywa na baadhi ya watumishi hao kutoza fedha wagonjwa ikizingatiwa hali ya maisha ni ngumu vijijini ambako kipato chao ni kidogo.
Pia zahanati hiyo ya Vikumburu inakabiliwa na ukosefu wa nyumba za watumishi ambapo watumishi wanne wamepanga chumba kimoja hali iliyosababisha kuhamisha familia zao.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment