Sunday, January 27, 2013

WANANCHI NA KATIBA MPYA


John Gagarini, Mkuranga
WANANCHI wametaka katiba mpya iwe na kipengele cha wafanyakazi wa serikali kufanya kazi kwa mkataba wa miaka 10 ili aweze kuwajibishwa endapo utendaji kazi wake hautaridhisha.
Hayo yalisemwa jana Mkuranga na Bw Mohamed Abdul wakati wa Mdahalo wa Katiba kwa wakazi wa Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani uliandaliwa na Mtandao wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali wilayani Mkuranga (MKUNGONET).
Alisema kuwa baadhi ya wafanyakazi wa serikali wamekuwa hawatekelezi vema majukumu yao hali inayofanya washindwe kuwaletea maenedeleo wananchi ambao wanaamini kuwa elimu walizonazo hawazitumii kikamilifu.
“Tungetaka katiba iwe na kipengele cha wafanyakazi wa serikali kuwa na mkataba wa miaka 10 ili akifanya vema aongezewe mkataba na kama akifanya vibaya asiongezewe mkataba wa kazi,” alisema Bw Abdul.
Alisema kuwa endapo kutakuwa na mikataba ya muda wa kufanya kazi kutaleta uwajibikaji sehemu za kazi tofauti na ilivyo sasa baadhi ya wafanyakazi kutowajibika kwa kuamini kuwa hawawezi kuondolewa kazini hata kama wameboronga.
Aidha alisema kuwa pia sifa za wataalamu  mbalimbali ziwekwe kwenye mbao za matangazo ili wananchi waweze kujua uwezo wa wataalamu hao.
“Hii itasaidia kuwawajibisha wataalamu hao ambao wataonekana uwezo wao ni mdogo kwani baadhi hawana uwezo,” alisema Bw Abdul.
Kwa upande wake mratibu wa MKUNGONET Bw Mohamed Katundu alisema kuwa lengo la mdahalo huo ni kuwaelekeza namna ya kutoa maoni yao juu ya marekebisho ya katiba mpya.
Bw Katundu alisema kuwa mdahalo huo uliofadhiliwa na The Foundation for Civil Society ulihudhuriwa na madiwani, wataalamu toka wilayani, mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali na wananchi.
Mwisho.     
Na Mwandishi Wetu, Mkuranga
WATU wenye ulemavu wametaka kuwe na mchakato wa kuwapata wabunge wanaowakilisha kundi hilo ili kila moja liwe na mwakilishi wake tofauti na sasa kuwa na mwakilishi mmoja ambaye hawezi kutoa mawazo ya makundi mengine.
Akizungumza wilayani Mkuranga kwenye mdahalo wa katiba ulioandaliwa na mtandao wa mashirika yasiyo ya kiserikali wilayani Mkuranga (MKUNGONET) Ester Waziri alisema kuwa wabunge wanaochaguliwa kwa ajili ya uwakilishi watu wenye ulemavu uwakilishi wake bado unalegalega.
Waziri alisema kuwa kuna karibu iana tano za watu wenye ulemavu lakini uwkailishi unakuwa wa kundi moja huku mengine yakiwa yamesahauliwa.
“Tungependa katiba ionyeshe kila kundui kuwa na uwakilishi bungeni kwani kila moja lina mahitaji yake na vipaumbele vyake,” alisema Waziri.
Alitaja baadhi ya makundi hayo ni kama vile walemavu wa viungo, ngozi, wasioona, viziwi, bubu na wengineo ambao kila mmoja ana mahitaji yake.
“Kila kundi ni vema lingekuwa na mwakilsihi wake bungeni kuliko mmoja kuwakilisha makundi yote hivyo mengine kushindwa kuwekewa mazingira mazuri ya kupata fursa mbalimbali za kimaendeleo,” alisema Waziri.
Mratibu wa shirika hilo Mohamed Katundu alisema kuwa waliamua kuandaa mdahalo huo ili wananchi wajue namna ya kutoa maoni yao juu marekebisho ya katiba mpya kwenye mchakato unaoendelea.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
KATIKA kuihamsisha jamii wilayani Kibaha mkoani Pwani kushiriki kwenye michezo wadau wa michezo wameanzisha klabu ya mazoezi ijulikanayo kama Kongowe Jogging Club.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini hapa moja ya waanzilishia wa klabu hiyo Simon Mbelwa alisema kuwa lengo la kuanzisha klabu hiyo ni kuwahamasisha watu kushiriki michezo kwani mbali ya kutoa burudani pia ni ajira.
Mbelwa ambaye pia ni mwamuzi wa ligi Kuu ya Voda Com alisema kuwa tayari wana wanachama 18 na tayari wameshaanza mazoezi ambayo hufanyika kila siku ya Jumamosi na Jumapili.
“Michezo hapa bado haijahamasishwa vya kutosha hivyo wao kama wadau wameona njia mojawapo ni kuanzisha klabu hiyo ambayo itayahusisha michezo mingi kama vile soka, mpira wa pete, riadha na michezo mingine,” alisema Mbelwa.
Alisema kuwa jamii imekuwa haina mwamko wa michezo hivyo wao watashirikiana na wadau wengine kuhakikisha michezo inakuwa kwenye wilaya ya Kibaha
“Wataalamu wa michezo hiyo wapo nikiwemo mimi mwenyewe ambapo nitafundisha michezo mingi kama soka na mingne pia walimu wa michezo mbalimbali tayari tumeshwapata hivyo wapenda michezo wajitokeze kutuunga mkono,” alisema Mbelwa.
Alisema changamoto kubwa ni ukosefu wa vifaa kwa wanamichezo wa klabu yao na kuwataka wafadhili mbalimbali kujitokeza kuwasaidia ili waweze kufanikisha michezo.
Aliwataka wazazi kuwaruhusu watoto wao kujitokeza kushiriki michezo kwani ni moja ya njia za kupata ajira na kuboresha afya zao na kuondokana na magonjwa madogomadogo.
Mwisho.  

No comments:

Post a Comment