Friday, March 31, 2023

TANESCO YATAKIWA KUWEKA KITENGO CHA KERO KININSIA

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) limetakiwa kuweka kitengo maalumu kitakachoshughulika na kusikiliza kero za kijinsia ili kuweka usawa wa kijinsia katika shirika hilo.

Hayo yamesemwa Jijini hapa na Naibu Waziri wa Nishati,Stephen Byabato katika uzinduzi wa Programu ya Mpango wa Jinsia wa miaka minne(2023-2027)wa TANESCO kwa kusirikiana na Benki ya Dunia kupitia mradi wa umeme wa Tanzania hadi Zambia(Tanzania-Zambia Transmission Interconnector Project-TAZA).

Naibu Waziri Byabato amesema kuwa Shirika hilo limekuwa likishughulikia masuala ya jinsia kwa namna mbalimbali hivyo kwasasa ni wakati muafaka wa kuwa na kitengo kitakachokuwa na bajeti,uongozi wa kitengo chenye uelewa na uweledi wa kusikiliza kero za kijinsia mbalimbali zitakazojitokeza.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO,Maharage Chande amesema kuwa lengo la programu hiyo kuwa ni kutatua changamoto wanazokutana nazo wanafunzi wanawake katika maeneo yao ya kazi kwa lengo la kukuza ajira zao ili kuongeza idadi ya wanawake wanaoajiriwa.

Mkurugenzi Chande ametaja maeneo ya kimkakati yatakayopewa kipaumbele kuwa ni kuiboresha sera ya Shirika na kujenga uwezo ili sera iende sambamba na masuala ya kijinsia,kuwepo na taarifa sahihi zinazohusu masuala ya unyanyasaji wa kijinsia kwenye Taasisi,kuruhusu fursa ya ukuzaji wa taaluma kwa wafanyakazi wanawake hasa wanaofanyakazi kwenye miradi na kuwepo kwa nafasi ya mafunzo kwa vitengo kwa wafanyakazi wanawake waliopo kazini ili kuwajengea uwezo kuelekea kwenye ajira kamili.

Aidha  kuhusu mradi wa kusafirisha umeme wa Tanzania hadi Zambia (TAZA),Chande ameeleza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Nishati na TANESCO wanatekeleza ujenzi wa mradi wa upanuzi wa njia ya kusafirisha umeme mkubwa wa kilovoti 400 kutoka katika kituo cha kupokea,Kupoza na kusafirisha umeme mkubwa cha Tagamenda Iringa kwenda kwenye nchi zilizopo kusini mwa Tanzania(Southern African Power Pool)kupitia Kisada Iringa,Iganjo Mbeya na Nkangamo Tunduma Songwe.

Chande amekitaja kituo hicho cha Tagamenda kuwa ni kitovu cha kusafirisha umeme mkubwa wa kilovoti 220 kwenda kwenye mikoa takribani 18 nchini.

Na kwa upande mwingine kituo hiki kimeunganishwa na kituo cha umeme cha zuzu Dodoma ili kusafirisha umeme mkubwa kwenda kwenye nchi zilizopo Mashariki mwa Tanzania ambazo ni Kenya,Uganda na Ethiopia kupitia mradi wa kuunganisha umeme baina ya Kenya na Tanzania(Kenya-Tanzania Power Interconnection Project-KTPIP)

Thursday, March 30, 2023

DK SAMIA ANA LENGO LA KUBORESHA AFYA KISARAWE.

RAIS DR SAMIA ANA LENGO LA KUIFANYA SEKTA YA AFYA  KUWA YA MFANO ZAIDI KISARAWE -DR JAFO

Na Mwandishi Wetu, Kisarawe 

WAZIRI wa nchi ofisi ya makamu wa Rais muungano na mazingira (Mb) Jimbo la Kisarawe Mhe Dkt. Selemani Said Jafo amekabidhi vifaa mbalimbali vya afya katika Hospitali ya Wilaya ya Kisarawe kwa lengo la kuboresha huduma za afya katika wilaya hiyo kwa Vijiji 66 Fedha ikiwa ni kutoka kwa Mhe Rais Samia na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi CCM katika Kutekeleza ilani ya 2020-2025.

Katika makabidhiano ya vifaa hivyo Mhe Dr Jafo amewapongeza watendaji wa Idara ya  afya katika hospitali hiyo kwa kazi kubwa wanayofanya katika kuwahudumia wagongwa na pia ameahidi kuwa nao karibu ili kutatua baadhi ya changamoto wanazokutana nazo katika utoaji wa huduma kwa ujenzi wagonjwa.

Aidha wananchi wameishukuru serikali kwa kuwasaidia upatikanaji wa vifaa hivyo kwani vita saidia kupunguza usumbufu wa upatikanaji wa huduma ya matibabu hospitalini hapo

Aliipongeza Serikali ya Awamu ya Sita Kwa kupendelea zaidi Kisarawe katika Upatikanaji wa Huduma ya Afya Kwa kuipatia Vifaa Tiba na fedha mbalimbali kwa Ajili ya Afya ambayo inaifanya Halmashauri ya Wilaya Kisarawe kuwa Nzuri katika Huduma za Afya.

Wednesday, March 29, 2023

NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora ametembelea mradi wa Nyumba Za Watumishi Magomeni

NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora  ametembelea mradi wa Nyumba Za Watumishi Magomeni na kuongea na watendaji wa Shirika la Nyumba la Watumishi( WATUMISHI HOUSING INVESTMENT), na kuwakumbusha kuendelea kusimamia msingi wa uwanzishwaji wa shirika hilo pasi kusahau kuendelea kujenga nyumba za Watumishi sehemu zenye uhitaji mkubwa kimkakati. #KaziInaendelea #WHI

Tuesday, March 28, 2023

KIKWETE AKUTANA NA TAASISI YA UONGOZI

NAIBU Waziri Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora Ndg. Ridhiwani Kikwete, amezunumza na Watendaji wa Taasisi ya @UONGOZI mapema leo na kuwaasa kuendelea na kazi nzuri wanayoifanya bila kusahau msingi wa kuanzishwa kwa taasisi hiyo. #KaziInaendelea #UongoziBora

Sunday, March 26, 2023

WAZIRI UMMY AFIKA KWENYE VIJIJI UGONJWA WA MARBURG ULIPOANZIA


WAZIRI UMMY AFIKA KWENYE VIJIJI UGONJWA WA MARBURG ULIPOANZIA

Na. WAF - Bukoba, Kagera

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amefanya ziara ya kutembelea vijiji vya Kata ya Maruku na Kanyangele vilivyopo Wilaya ya Bukoba Mkoani Kagera kwa lengo la kujionea hali inavyoendelea baada ya kutangazwa kutokea kwa mlipuko wa ugonjwa wa Marburg Mkoani humo. 

Katika Ziara hiyo, Waziri Ummy ameambatana na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania Dkt. Zabron Yoti pamoja na Mwakilishi wa Shirika la UNICEF Tanzania Bi. Shalini Bahuguna ili nao wajionee hali ya ugonjwa huo inavyoendelea kudhibitiwa nchini Tanzania. 

Aidha, Waziri Ummy amesema kwa sasa hali ni salama na kuwataka Wananchi wa vijiji hivyo, wana Kagera na watanzania kwa ujumla kuondoa hofu na kuendelea na shughuli zao kwa kuwa Serikali inawajali Wananchi wake.

“Niwatoe hofu Watanzania tuendelee kufanya kazi zetu lakini tuzingatie maelekezo ya Serikali ya kujikinga na ugonjwa huu kwa kuepuka kushikana mikono hususan kipindi hiki lakini pia tujitahidi kunawa mikono mara kwa mara na maji tiririka kwa sabuni.” amesema Waziri Ummy

Hata hivyo, Waziri Ummy amesema kuwa Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea na juhudi za kuhakikisha ugonjwa huo unamalizika kwa haraka na hautatokea tena katika maeneo hayo. 

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Kanyangele Bw. Hamim Hassan ameishukuru Serikali kwa kufanya juhudi kubwa ambapo hadi sasa hakuna mgonjwa yeyote aliyeongezeka kuwa na ugonjwa huo. 

“Hatua za haraka za Serikali kupitia Wizara ya Afya zilizochukuliwa za kuwaweka sehemu maalumu waliokuwa karibu na wagonjwa imesaidia sana kutoendeleza maambukizi kwengine na hali ni shwari kwa sasa.” amesema Bw. Hassan

WAZIRI UMMY ATEMBELEA WATUMISHI WALIOWEKWA KARANTINI

WAZIRI UMMY ATEMBELEA WATUMISHI WALIOWEKWA KARANTINI

Na. WAF - Bukoba, Kagera

WAZIRI wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amewatembelea watumishi wa afya waliowekwa sehemu maalumu ya uangalizi baada ya kuwahudumia wagonjwa wa Marburg walioripotiwa katila Wilaya ya Bukoba Mkoani Kagera.

Ziara hiyo ameifanya leo akiambatana na Wawakilishi kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) Dkt. Zabron Yoti na Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani (UNICEF) Bi. Shalini Bahuguna baada ya kutembelea katika Vijiji vya Kata ya Maluku na Kanyangele ambapo ugonjwa huo umeanzia

Waziri Ummy amewatia moyo watumishi hao kwakuwa Serikali ipo pamoja nao na lengo ni kuendelea kuwalinda wao na wanaowazunguka ikiwemo familia zao. 

“Niwatie moyo ndugu zangu huu ugonjwa utaisha kwakuwa Serikali imedhamiria kuendelea kupambana ili kutokomeza kabisa na hali itarudi kama zamani.

Mwisho, Waziri Ummy amewataka watumishi hao wa Afya kuzingatia Kanuni na Taratibu za Udhibiti wa Maambukizi (Infection Prevention and Control) wakati wote wanapowahudumia wagonjwa.


Wednesday, March 22, 2023

CHAVITA YAIPONGEZA eGA KWA HUDUMA ZA SERIKALI MTANDAO JUMUISHI KWA WATU WENYE ULEMAVU

 

MWENYEKITI  wa Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA) Wilaya ya Rufiji Mkoa wa Pwani Suleiman Zalala ameipongeza Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kwa huduma jumuishi za utekelezaji wa jitihada za Serikali Mtandao kwa watu wenye ulemavu.

Zalala ametoa pongezi hizo wakati wa kilele cha kikao kazi cha Serikali Mtandao kilichofanyika hivi karibuni katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa (AICC) Jijini Arusha.

Zalala ameishukuru Mamlaka kwa kuthamini na kuona mchango wa kundi maalumu la watu wenye ulemavu kushiriki katika mafunzo hayo ili kuboresha huduma jumuishi za Serikali Mtandao kwa watu wenye walemavu.

"CHAVITA imekuwa na ushirikiano wa muda mrefu na eGA katika mipango mbalimbali ya mafunzo inayoandaliwa na Mamlaka kwa watu wenye ulemavu na kwamba mafunzo hayo yamekuwa yakiwajengea uwezo na uelewa mkubwa wa utekelezaji wa jitahada za Serikali Mtandao katika utoaji wa huduma mbalimbali kwa wananchi,"amesema Zalala.

Amesema kubwa wameweza kujifunza na kupata uelewa juu ya mabadiliko mbalimbali ya teknolojia katika utoaji wa huduma na huduma mbalimbali zinazowezeshwa na eGA kwa wananchi kama vile ununuzi wa Luku, kata za maji n.k

Aidha ameomba mafunzo hayo yawe chachu kwa Taasisi nyingine za Umma kuiga mfano wa kile kilichofanywa na Mamlaka kwa kuwashirikisha makundi maalum kwenye uandaaji wa mafunzo na mipango mbalimbali inayotekelezwa na taasisi zao .

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) Mhandisi Benedict Ndomba amewashukuru wadau wote waliohudhuria kikao kazi hicho na kwa michango yao itakayosaidia kufanikisha na kuimarisha utekelezaji wa jitihada za Serikali Mtandao kwa ajili ya kuboresha utendaji kazi wa Taasisi za umma, pamoja na utoaji wa huduma kwa umma.

“Naimani kuwa kikao hiki kimewajengea uwezo zaidi washiriki wote kuhusu Serikali Mtandao na kila mdau ametambua namna ambavyo anaweza kufanikisha jitihada za Serikali Mtandao kupitia sekta yake,"amesema Mhandisi Ndomba

Mhandisi Ndomba ameongeza kuwa washiriki zaidi ya 1624 wamehudhuria kikao hicho na mada 22 ziliwasilishwa na wadau kutoka katika taasisi mbalimbali za Umma zilizolenga kutathmini na kuimarisha nguzo kuu Nne (4) za Serikali Mtandao.

Amesema kuwa katika kikao hicho wadau wamepata fursa ya kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano katika kutekeleza jitihada za Serikali Mtandao nchini pamoja na kutafuta ufumbuzi wa changamoto za serikali mtandao zilizopo nchini ili kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii .

Amebainisha kuwa washiriki wametoa maoni mbalimbali ya namna ya kukuza jitihada za Serikali Mtandao ikiwa ni pamoja na kushauri uboreshaji wa Mifumo mbalimbali inayotoa huduma kwa umma pamoja na kupanua wigo wa utoaji wa huduma za Serikali Mtandao katika maeneo mbalimbali nchini.


Mkurugenzi amesema Menejimenti ya Mamlaka imeyapokea maoni na ushauri uliotolewa na kwamba eGA ipo tayari kufanyia kazi maoni hayo yanayolenga kuboresha na kukuza jitihada za Serikali Mtandao nchini.