Tuesday, February 28, 2023

IRUWASA YAONGOZA KUFUNGA MITA ZA MAJI KABLA YA MALIPO

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

MAMLAKA ya Maji na Usafi wa Mazingira Iringa (IRUWASA) imevunja rekodi kwa kuongoza nchini kwa kufunga mita 6,752 za malipo ya Maji Kabla ambazo zimekuwa suluhisho na kupunguza idadi ya wadaiwa sugu wa ankra za maji.

Akizungumza Jijini Dodoma Mkurugenzi Mtendaji wa IRUWASA, David Pallangyo amesema, Mamlaka hiyo iliyoanza daraja C hadi sasa ipo daraja A na inajitegemea gharama za matengenezo na uendeshaji na sehemu ya uwekezaji, imefanikiwa katika eneo la TEHAMA kwa kufunga mita za malipo kabla kwa wateja hao.

Pallangyo amesema kuwa kutokana na kufunga mita za malipo kabla kwa viongozi wa serikali na taasisi mbalimbali, kumepunguza ongezeko la madeni ya watumiaji maji bila kulipa na kubaki deni la shilingi bilioni mbili ambalo wadaiwa wengi ni watu wa kawaida.

Amesema kuwa mamlaka hiyo pia imevuka lengo la Sera ya Maji ya 2002 na Ilani ya CCM ya kutoa huduma ya usambazaji maji kwa mji wa Iringa na maeneo ya pembezoni kwa kuunganisha wateja 40,459 sawa na asiimia 97 ya wakazi ambazo ni zaidi ya asilimia 95 zinazoelekezwa kwenye sera na Ilani.

Aidha amesema kuwa katika mpango wa muda mrefu, Serikali kupitia IRUWASA inakusudia kutekeleza mradi mkubwa wa uboreshaji huduma ya majisafi na majitaka katika manispaa ya Iringa, miji ya Kilolo pamoja na baadhi ya vijiji kando ya bomba la maji litakapopita.

"Mradi huu unalenga kuanzisha chanzo kipya katika mto Mtitu uliopo Wilaya ya Kilolo utaongeza upatianaji wa maji ya kutosha kwa miaka 20 ijayo na utaongeza utoaji wa majitaka zaidi ya asilimia 30 ya wakazi wa Iringa kutoka asilimia 6.8 za sasa,"amesema Pallangyo.

Ameongeza kuwa mradi huo utekelezwa kwa ushirikiano wa serikali kupitia mkopo wenye masharti nafuu kutoka serikali ya Korea wa dola za Kimarekani milioni 88.4 utaanza kutekelezwa Mei 2023 na ujenzi utaanza Aprili 2024 na utakamilika 2027.

Amesisitiza kuwa mradi utakapokamilika huduma za maji safi na salama kwa miji ya Iringa, Kilolo na Ilula zitafikia asiimia 100 kwa saa 24 kwa siku saba.

Jumla ya wananchi 456,010 watanufaika na huduma ya majisafi hadi mwaka 2045, huku wananchi 141,543 watanufaika na huduma ya uondoaji majitaka na Watanzania 6,455 watanufaika na kazi za mikataba na utachangia uchumi na ustawi wa jamii. 


Thursday, February 23, 2023

MAMLAKA YA SERIKALI MTANDAO KUONGEZA UWEZO WA MAWASILIANO


Na Mwandishi Wetu, Dodoma

MAMLAKA ya serikali Mtandao (eGA) imepanga kupanua uwezo wa Mtandao wa mawasiliano serikalini ( Government Network) na kuufikisha wilaya zote nchini Ili kurahisisha utekelezaji wa jitihada za serikali Mtandao na kuwafikishia huduma wananchi wote popote walipo.

Hayo yamesemwa na Mkurugezi mkuu wa mamlaka ya serikali mtandao Mhandisi Benedict Ndomba wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa mamlaka hiyo.

Ndomba amesema kuwa mfumo wa ubadilishaji taarifa serikalini imewezesha zaidi ya taasisi 50 kubadilishana taarifa kupitia mfumo huo na amezitaka taasisi za umma ambazo hazijaunganishwa katika mfumo huo ziunganishwe Ili ziweze kubadilishana taarifa na taasisi nyingine pale inapohitajika.

"Jumla ya taasisi 200 zinatumia mfumo wa ofisi Mtandao kwa ajili ya kurahisisha utendaji kazi katika taasisi za umma pia umesaidia kupunguza matumizi ya karatasi kutunza mazingira na kuokoa fedha za serikali,"alisema Ndomba.

Serikali mtandao ni matumizi ya Teknolojia ya habari na mawasiliano ( TEHAMA) Katika utendaji kazi wa taasisi za umma na utoaji wa huduma kwa wananchi wenye lengo la kuongeza ufanisi wa utendaji kazi Katika taasisi ya umma pamoja na kuboresha utoaji huduma kwa umma Ili huduma hizo zipatikane kwa urahisi haraka na gharama nafuu. 

WASIOENDELEZA ARDHI KUNYANGANYWA

NAIBU Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Ridhiwani Kikwete amezitaka Serikali za Vijiji kuorodhesha majina ya wawekezaji ambao wamehodhi ardhi bila kuiendeleza ili irudishwe kwa ajili ya matumizi mengine.

Aliyasema hayo alipokuwa kwenye ziara ya kwenye Kata ya Lugoba Halmashauri ya Chalinze kuzungumza na wananchi kutatua kero na changamoto kwenye Jimbo la Chalinze ambapo yeye ndiyo Mbunge wa Jimbo hilo.

Ridhiwani alisema kuwa maeneo mengi aliyopita kikiwemo Kijiji cha Makombe  kumekuwa na malalamiko mengi toka kwa wananchi juu ya baadhi ya maeneo yaliyoombwa na wawekezaji hayajaendelezwa na kuwa mapori.

"Vijiji na Vitongoji orodhesheni majina ya wawekezaji wote walio katika maeneo yenu ambao hawajaendeleza ardhi waliyoiomba kufanya uwekezaji lakini wameiacha bila kuiendeleza kwani huo siyo utaratibu ni vema wakanyanganywa na kupewa watu wengine ili kuyatumia kuleta maendeleo,"alisema Ridhiwani.

Alisema kama kuna maeneo mnaona yametelekezwa na wawekezaji wasipate shida wanachotakiwa viongozi kupitia mikutano mikuu ni kutoa hoja na kuandikwa muhutasari kisha upelekwe Halmashauri na kupelekwa Wizarani ili kubadilishwa matumizi na kurudishwa Kijijini na kupangiwa shughuli nyingine.

"Tena kuna baadhi ya wawekezaji wanapokwenda kuomba maeneo wanatoa ahadi nyingi kuwa wakipewa watasaidia huduma za jamii au kutoa ajira kwa Vijana wa eneo husika lakini hawafanyi hivyo ni vema wakaachia ardhi waliyopewa,"alisema Ridhiwani.

Naye Diwani wa Lugoba Rehema Mwene alisema kuwa Kijiji cha Makombe kinakabiliwa na changamoto ya ubovu wa barabara, ukosefu wa maji, uchakavu wa Zahanati na baadhi ya maeneo kukosa umeme.

Mwene alisema kuwa changamoto nyingine ni baadhi ya wawekezaji kuchukua maeneo na kutoyaendeleza hivyo kufanya kuwe na mapori makubwa ambayo yanahatarisha usalama wa watu.

Kwa upande wake kaimu Mtendaji wa Kijiji cha Makombe Godfrey Nyange akisoma risala ya Kijiji alisema kuwa kuna migogoro ya mipaka baina ya Kijiji hicho na Vijiji vya Kinzagu na Mindutulieni.

Nyange alisema kuwa changamoto nyingine ni wanufaika wa Mfuko ya Maendeleo ya Jamii (TASAF) kuondolewa kwenye mfumo na wengine kutolipwa fedha zao za kila mwezi. Naibu Waziri alitembelea Vijiji vya Makombe, Mindutulieni na Lunga kwenye Kata ya Lugoba.



TANESCO KUONGEZA UZALISHAJI UMEME


Na Mwandishi Wetu Dodoma

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) linatarajia kuzalisha megawati 5,000 kupitia miradi mbalimbali ifikapo kwa mwaka 2025 hivyo kuongeza uzalishaji umeme kupitia gridi ya Taifa.

Hayo yamesemwa na kaimu Mkurugezi wa huduma kwa wateja wa shirika la umeme Tanzania ( TANESCO) Martin Mwambene wakati akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali ya shirika hilo na uelekeo wake kwa mwaka wa 2023 .

Mwambene amesema kuwa kwa sasa shirika hilo lina uwezo wa kuzalisha umeme wa megawati 1,820 wakati mitambo iliyopo ina uwezo wa kuzalisha megawati 1,300 pekee. 

Amesema kuwa TANESCO kwa kutambua matatizo ya umeme yaliyopo nchini imekuja na mradi wa Gridi Imara ambapo katika bajeti ya mwaka huu imetengewa shilingi bilioni 500 kwa ajili ya kuanza utekelezaji wake.

"Katika mradi wa Grid Imara utajumuisha ununuzi wa mashine umba 6000, mita 700,000 za umeme, nguzo 380,000 ununuzi na ufungaji wa nyaya zenye urefu wa km 40,000, ujenzi wa njia za kusafirisha umeme mkubwa takribani kilomita 948 na ujenzi wa vituo 14 vya kupooza umeme,"amesema Mwambene. 

Aidha amezungumzia pia maendeleo ya ujenzi katika Bwawa la Mwalimu NYerere kuwa upo katika asilimia 88 na zoezi la uwekaji maji limefikia mita za ujazo 133 kutoka usawa wa bahari

TCU KUTHIBITI UBORA


Na Mwandishi Wetu Dodoma

TUME ya vyuo vikuu Tanzania (TCU) imeendelea kuimarisha mifumo yake ya uthibiti ubora na mifumo ya ndani ya vyuo vikuu Ili kuhakikisha vinaendana na mwelekeo wa nchi pamoja na kuandaa na kuratibu mafunzo kwa viongozi wahadhiri na maofisa wa vyuo vikuu vya umma na binafsi hapa nchini kwa lengo la kuwajengea uwezo katika usimamizi wa uendeshaji wa taasisi zao.

Hayo yamesemwa na katibu mtendaji tume ya vyuo vikuu Tanzania Prof. Charles Kihampa wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa shughuli mbalimbali za tume hiyo kwa kipindi Cha Miaka miwili ya uongozi wa serikali ya awamu ya sita.

Kihampa amesema kuwa Katika kuhakiki ubora tume imeimarisha mifumo yake ya ushauri na ukaguzi wa mara kwa mara wa kawaida na wa kushtukiza kwa mujibu wa Sheria na utaratibu zilizopo kwa lengo la kuhakikisha kuwa Elimu itolewayo na vyuo vikuu hapa nchini inakidhi viwango vya ubora kikanda, kitaifa na kimataifa.

Amesema kuwa nafasi za masomo Katika vyuo vya Elimu ya juu Katika program za shahada ya kwanza zimeongezeka kutoka 157,770 Mwaka 2020/2021 Hadi 172,168 Mwaka 2022/2023 sawa na ongezeko la nafasi 14,398 ya asilimia 9.1.

Aidha amesema mwaka 2022/2023 serikali imetenga kiasi Cha shilingi bilion 6.4 kupitia mradi wa Elimu ya juu kwa mageuzi ya kiuchumi ( higher Education for Economic Transformation- HEET) kwa ajili ya kuimarisha uthibiti ubora na uhuishaji wa mitaala ya vyuo vikuu ambapo zaidi ya mitaala 300 ya vyuo hivyo vinafanyiwa mapitio Ili kuhuishwa kwa kizingatia maoni ya wadau mbalimbal

Thursday, February 16, 2023

WAKULIMA WATAKIWA KUTUMIA MFUMO WA STAKABADHI GHALANI



Na Mwandishi Wetu Dodoma

BODI ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imetoa wito kwa wakulima kutokubali kurubuniwa na madalali badala yake waingie kwenye mfumo wa Stakabadhi ghalani ili kuuza mazao yao kulingana na bei iliyopo sokoni.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi hiyo Asangye Bangu Jijini Dodoma wakati akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za bodi hiyo.

Bangu amesema kuwa kumekuwa na wimbi la madalali kwenda mashambani kwa wakulima na kuwarubuni na kununua kwa bei ya chini hali ambayo inawakandamiza wakulima.

"Tangu kuanzishwa kwa mfumo huo mwaka 2007/2008 hadi 2020/2021 ukuaji wa uzalishaji umekuwa ukiongezeka kwa wastani wa asilimia 12 kwa mwaka ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 2 kwa mwaka kabla ya kuanzishwa kwa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala,"amesema Bangu.

Amesema bodi imeendalea na juhudi za kuboresha mfumo uliokuwepo wa kizamani wa usimamizi wa ghala ambapo kwa kushirikiana na bodi inakuja na mfumo mpya wenye kuweza kurahisisha kazi za maandalizi ya taarifa utoaji stakabadhi na udhibiti wa matukio ghalani hivyo kupunguza muda wa michakato na kuongeza ufanisi na usalama wa mzigo.

Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) ni taasisi chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara iliyoundwa kwa Sheria namba 10 ya 2005 na Marekebisho Kifungu 4 Sura 339 mwaka 2016 iliyopewa majukumu ikiwemo kutoa leseni kwa waendesha ghala, meneja dhamana na wakaguzi wa ghala.

Majukumu mengine ni kuchapa na kuidhinisha vitabu vya Stakabadhi za Ghala, kusajili na kuingiza taarifa za wadau muhimu wa mfumo, kuwakilisha nchi katika masuala ya taifa na kimataifa yahusuyo Mfumo wa Stakabadhi za Ghala pamoja na majukumu mengine kama taasisi itakavyoelekezwa na Waziri wa Viwanda na Biashara.

Wednesday, February 15, 2023

KAMATI ZA MAGONJWA YA MLIPUKO KUTOA ELIMU KWA JAMII

IMEELEZWA kuwa uanzishwaji wa kamati za magonjwa ya milipuko kutasaidia kuielimisha jamii kukabili magonjwa ili yasisambae kwa kasi na kutoleta athari.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson John alipokuwa akifungua mkutano wa kamati hiyo inayoundwa na wanajamii, wataalamu wa afya, viongozi wa dini na kamati ya usalama ya Wilaya.

John amesema kuwa kwa kuzingatia hilo itasaidia kukabili magonjwa ya mlipuko kwa kutoa elimu juu ya kukabiliana na magonjwa hayo.

Amezitaka kamati ya magonjwa ya milipuko kutoa elimu juu ya magonjwa kulingana na mila desturi na tamaduni za eneo husika.

Kwa upande wake Johnson Mndeme kutoka Wizara ya Afya Idara ya Kinga sehemu ya afya kwa Umma amesema kuwa malengo ya kuanzishwa kamati hizo ni kutoa elimu juu ya magonjwa ya mlipuko ili kuepukana na dhana potofu.

Kwa upande wake maganga mkuu wa Halmashauri ya Mji Kibaha Peter Nsanya amesema kuwa wanakamati wanapaswa kutoa elimu ya kupambana na magonjwa mbalimbali ndani ya jamii.


TBA YAENDELEA NA MIPANGO YA UJENZI KWA NYUMBA WATUMISHI



Na Mwandishi Wetu Dodoma

WAKALA wa Majengo Tanzania (TBA) wamefanikiwa kuendelea kutekeleza Malengo waliyojiwekea kwenye mpango mkakati wa mwaka 2021/22 hadi 2025/2026 pamoja na kutekeleza ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020 ikiwa ni pamoja na kusimamia na kuhakikisha utengenezaji wa makazi bora kwa watumishi.

Hayo yamebainishwa na katibu mkuu mtendaji (TBA) Daudi Kondoro wakati akizungumza na wandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa majukumu wa wakala huo katika kipindi cha miaka miwili ya serikali ya awamu ya sita.

Kondoro amesema wakala wameendelea kutoa huduma ya uhakika ya makazi kwa serikali na kwa watumishi wa umma kwa kutoa huduma ya uhakika ya makazi na nyumba ambapo mpaka sasa kuna nyumba 1,622 zilizopangishwa kwa watumishi wa umma na pamoja na nyumba 7,700 zilizouzwa kwa watumishi wa umma Tanzania Bara Bara.

"TBA imetengeneza fursa za ajira na kutoa mafunzo kwa vitendo ambapo imetengeneza ajira takribani 100,000 kwa vijana walio na ujuzi na ambao hawana ujuzi kupitia miradi ambayo imekua ikitekelezwa,"alisema Kondoro.

Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) imeishukuru serikali ya Rais Dkt. Samia kwa kukuendelea kuwawezesha kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ikiwemo kupewa fedha bilioni 54.2 kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya ujenzi.

WANANCHI WATAKIWA KUKOPA KWA MALENGO

Na Mwandishi Wetu Dodoma

KATIBU Mtendaji Mkuu wa Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Beng'i Issa amewataka wananchi kuacha kukopa fedha bila malengo badala yake watumie mikopo kama fursa kujiletea maendeleo.

Issa ameyasema  hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa majukumu ya baraza la uwezeshaji wananchi kiuchumi Katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita.

Amesema kupitia Baraza la Uwezeshaji kiuchumi wameunda njia mbalimbali ambazo zitawasaidia wananch kunufaika na Baraza hilo la kuwezesha wananchi kiuchumi ikiwemo mifuko ya mikopo ya jamii ambayo kwa sasa kuna jumla ya mifuko 72 ili kuwanufaisha wanchi wote walio katika mifuko hiyo ya jamii.

"Hadi sasa imewezesha kuwapatia ya zaidi ya shilingi bilioni 3.5 wafanyabiashara wenye viwanda vya kati na vidogo katika miradi 62 kwenye mikoa 12 nchini na inasimamia majukwaa ya uwezeshaji wanawake kiuchumi katika mikoa yote 26 na Halmashauri zote nchini.

Aidha amesema kuwa  Watanzania zaidi ya 83,000 wamepata ajira za kimkakati na Baraza huandaa makongamano kwa ajili ya maonesho kwa lengo la kuendelea kutoa elimu kwa wananchi.

Tuesday, February 14, 2023

MFUKO WA MAWASILIANO KWA WOTE KUPELEKA VIFAA VYA TEHAMA SHULE MAHITAJI MAALUM



Na Mwandishi Wetu Dodoma

MFUKO wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) unatarajia kutumia shilingi milioni 575 kwa ajili ya mradi wa kupeleka vifaa maalum vya TEHAMA vya kujifunzia kwa Shule 16 zenye watoto wenye mahitaji maalum hapa nchini.

Hayo yamesemwa na Mtendaji mkuu wa mfuko wa mawasiliano kwa wote ( UCSAF) Justina Mashimba leo Februari 13,2023 Jijini Dodoma, wakati akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za mfuko huo.

Mashimba amesema kuwa vifaa vitakavyopelekwa katika shule hizo ni pamoja na TV, mashine ya (Nukta Nundu) Orbit reader (Machine za Kisasa), Laptops, (Printa ya nukta nundu).

"Jumla ya shule 811 zimefikishiwa vifaa vya TEHAMA ambapo kwa wastani kila shule imepewa Kompyuta 5, Printa 1 na Projekta 1 kwa mwaka wa fedha wa 2022/23 ambapo Shule 150 zitafikishiwa vifaa vya TEHAMA bajeti yake ikiwa ni shilingi 1.9 na vifaa hivyo vitasaidia wanafunzi kusoma katika shule hizo,"amesema Mashimba

Amezitaka Shule hizo zitakazonufaika ni pamoja na Shule ya Sekondari ya Mpwapwa (Mpwapwa-Dodoma), Sekondari ya Mkolani (Mwanza), Sekondari ya Kashaulili (Mpanda-Katavi), Sekondari ya Morogoro (Morogoro), Sekondari ya Shinyanga (Kishapu-Shinyanga), Sekondari ya Wavulana Songea (Songea), Sekondari ya Kazima (Tabora) na Sekondari ya Haile Selassie (Mjini Magharibi)

Aidha akizungumzia hali ya mawasiliano nchini amesema kuwa mwaka 2009 Huduma za Simu ilikuwa asilimia 45 wakati kwa sasa imeongezeka hadi kufikia asilimia 96,Teknolojia ya 2G ni asilimia 96,3G ni asilimia 72,4G ni asilimia 55 na Geographical Coverage ya 2G ni asilimia 69; 3G ni asilimia 55 na 4G ni asilimia 36.

Amesema kuwa upande wa ujenzi wa minara Vijiji UCSAF imeingia mikataba kufikisha huduma katika kata 1,242 zenye Vijiji 3,654, Wakazi 15,130,250 ambapo Minara 1,087 yenye Vijiji 3,378 na wakazi 13,320,750 na Utekelezaji unaendelea katika Minara 155 yenye Vijiji 276 na wakazi 1.8 kwa ruzuku iliyotolewa ya shilingi bilioni 199 ikiwemo pia mradi wa kimkakati wa Zanzibar Minara 42, Shehia 38 ruzuku bilioni 6.9


BARAZA LA TAIFA LA UJENZI LATATUA MIGOGORO YA MIRADÍ YA UJENZI



Na Mwandishi Wetu Dodoma

BARAZA la Taifa la ujenzi limeendesha mafunzo ya kusimamia mikataba ya ujenzi na utatuzi wa migogoro katika miradi ya ujenzi kwa wadau 155 kutoka Tanzania Bara na Visiwani.

Hayo yasemwa Mtendaji Mkuu wa baraza la taifa la ujenzi Dkt.Matiko Mturi wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa baraza hilo katika serikali ya awamu ya sita.

Dkt Mturi amesema wameandaa rasimu ya mapendekezo ya gharama za msingi za ujenzi wa barabara kwa kila mkoa wa Tanzania Bara na kuwakilisha katika kikao cha wadau wa ndani ya serikali ili kupata maoni na ushauri wao.

"Baraza limefanikiwa kuratibu ,kuandaa na kuwasilisha Wizara ya ujenzi na uchukuzi(sekta ya ujenzi) andiko dhana lenye mapendekezo ya kuboreshwa kwa mfumo wa sheria zinazosimamia ujenzi wa nyumba na majengo nchini,"amesema Mturi.

Amesema mwelekeo wa taasisi katika kutekeleza majukumu ni pamoja na kufuatilia utekelezaji wa sera ya ujenzi nchini,kuandaa na kutekeleza mpango mkakati wa maendeleo wa sekta ya ujenzi,kutoa miongozo mbalimbali ya kitaalam ya maeneo mbalimbali ya ujenzi.

Aidha amesema Taasisi inaendelea kutoa mafunzo kwa wadau wa ujenzi kuhusu maadili na utekelezaji wa miradi ya ujenzi, sanifu jenga na usimamizi wa mikataba ya ujenzi kwa wadau mbalimbali pamoja na kutoa mafunzo yanayolenga kukuza na kujenga wataalam mahiri katika sekta ya ujenzi.

Monday, February 13, 2023

REDIO ZITANGAZE HABARI ZA VIJIJINI

Na Mwandishi Wetu Dodoma

NAIBU Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew amevitaka vyombo vya habari kuhakikisha vinaendelea kutangaza na kuanda makala na vipindi vinavyolenga Maeneo ya Vijijini ambako kumekuwa na usikivu mkubwa wa Redio.

Methew amesema hayo Jijini Dodoma katika Maadhimisho ya Siku ya Redio Duniani ambapo kumefanyika Mkutano Mkuu wa mwaka wa watoa huduma wa sekta ya utangazaji Tanzania.

Amesema kuwa mchango wa vyombo vya habari ni mkubwa sana hasa Redio vimekuwa vikitoa taarifa nzuri hivyo kwa sasa Redio za FM zihakikishe zinakuwa na vipindi na makala nyingi zinazogusa Jamii na Utekelezaji wa Miradi ya serikali ya awamu ya sita.

"Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt  Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuhakikisha inasimamia na kuboresha upatikanaji wa habari serikalini na Taasisi zake kwa umakini na haraka hivyo vyombo vya habari vina haki ya kutumia fursa hiyo viweze kuitangaza nchi iliko toka na ilipo sasa ambapo kuna Utekelezaji wa miradi mingi inayowagusa Wananchi ikiwemo afya, Elimu,maji,nishati na miundonbinu,"amesema Methew.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule amepongeza vyombo vya Habari hasa Redio za Dodoma kwa kuendelea kuitangaza Dodoma ambako ndio Makao Makuu ya nchi huku akiwataka wamiliki, wahariri na Waandishi wa habari katika siku mbili wapate fursa ya kuizunguka Dodoma kuona ujenzi unaoendelea kwenye mji wa kiserikali Mtumba kunaendelea ujenzi wa majengo ya wizara na Taasisi mbalimbali za serikali ambapo watakuwa wamefanya utalii wa ndani  ambako serikali imetoa fedha nyingi katika Ujenzi huo.

Kwa Upande wake Mkurugenzi wa kituo cha Redio cha Wapo Fm Edina Malisa ameishauri mamlaka ya Mawasiliano TCRA kuhakikisha inakuwa inavitembelea vyombo vya habari na kujadiliana changamoto mbalimbali ambazo wanazipata ili kuweza kushirikiana na serikali ili kuweza kupatia ufumbuzi na kuendana na sheria na kanuni za vyombo vya habari.

Mkutano Mkuu wa mwaka wa watoa huduma wa sekta ya utangazaji Tanzania umewashirikisha wamiliki wa vyombo vya habari, wakurugenzi, wahariri na Waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali hapa nchini ambapo Mkutano huo ni wa siku mbili.

Friday, February 10, 2023

12 WAFA 63 WAJERUHIWA AJALINI

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

WATU 12 wamefariki dunia na wengine 63 kujeruhiwa katika ajali ya gari iliyotokea usiku wa kuamkia Alhamisi Februari 9, 2023 Wilayani Kongwa mkoani Dodoma.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amesema kuwa ajali hiyo imehusisha magari mawili na kusababisha vifo vya watu 12 (wanaume nane , wanawake wanne) na majeruhi 63 (wanaume 40 wanawake 23).

Senyamule amesema ajali hiyo imetokea usiku Kata ya Pandambili Kijiji cha Silwa wilayani Kongwa, barabara ya Dodoma - Morogoro.

"Majeruhi wanaendelea na matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Kongwa na Kituo cha Afya Gairo na miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mkoa wa Morogoro na majeruhi wawili wamehamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma,"amesema Senyamule.

Amesema ajali hiyo imetokea majira ya saa  6 usiku na imehusisha lori la mizigo lenye namba za usajili T 677 DVX na basi la abiria  la Kampuni ya Frester lenye namba za usajili T 415 DPP lililokuwa likitokea Bukoba kwenda Dar es Salaam.

Akizungumza na wakazi wa Pandambili eneo ambapo ajali ilipotokea Senyamule ametoa rai kwa jamii kutii sheria bila shuruti ili kuepuka ajali. 

"Serikali ilikuwa na nia njema ya kuruhusu vyombo vya usafiri kutembea usiku, lakini sasa baadhi ya madereva wanaanza kutozingatia Sheria za usalama barabarani, tutaendelea kuwachukulia hatua kali,"amesema Senyamule.a

Pia mewatembelea majeruhi katika Hospitali ya Kongwa na Kituo cha Afya Gairo na kutoa pole na kuwatakia uponyaji wa haraka.

Naye Mkuu wa Operesheni na Mafunzo  wa Jeshi la Polisi Kamishna Awadh Haji ametaja chanzo cha ajali hiyo kuwa ni mwendo kasi na uzembe wa dereva wa basi kutaka kulipita gari la mbele yake bila ya kuchukua tahadhari na kugongana na lori hilo  lililokuwa limebeba saruji.


WATUMISHI HOUSING A YAJENGA NYUMBA KWA WATUMISHI

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

WATUMISHI Housing Investment (WHI) imeweza kujenga nyumba 983 kwa ajili ya watumishi wa umma katika mikoa mbalimbali nchini.

Aidha kupitia kampuni yake ya ujenzi imeshiriki katika ujenzi wa mji wa serikali Jijini Dodoma pomoja na majengo ya taasisi za serikali ikiwa ni pamoja na ujenzi wa chuo Cha utumishi wa umma katika mkoa wa Singida.

Hayo yamesemwa na Mkurugezi mtendaji wa WHI Dkt Fred Msemwa wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu mwenendo wa taasisi hiyo ambapo kumekuwa na ongezeko la kushuka kwa bei ya nyumba kutoka asilimia 10 hadi asilimia 30.

Amesema kuwa wanategemea kuwa na miradi mipya ya ujenzi katika mwaka wa fedha 2022/2023 ambayo ni Kawe, Dodoma, Gezaulole, mradi wa viwanda Arusha pamoja na nyumba za watumishi Halmashauri mpya.

"Yapo baadhi ya mafanikio ambayo taasisi imefanikiwa ikiwa ni pamoja na kupata vifaa vya upimaji wa ardhi vyenye thamani ya shilingi bilioni 1.5 kutoka serikalini kupitia mkopo wa benki ya dunia unaoratibiwa na benki kuu ya Tanzania,"amesema Msemwa.

Watumishi Housing Investment ni taasisi ya umma iliyo chini ya ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora (OR-MUUUB) iliyoanzishwa Mwaka 2014 na ilianzishwa na serikali kupitia mifuko ya hifadhi ya jamii ikiwemo mfuko wa pensheni kwa watumishi wa umma (PSSSF), mfuko wa hifadhi ya jamii ( NSSF) pamoja na shirika la nyumba la Taifa na mfuko wa bima ya Afya (NHIF)

Wednesday, February 8, 2023

NSSF YAKUSANYA BILIONI 165.7

Na Mwandishi Wetu Dodoma

MKURUGENZI Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Masha Mshomba amesema kuwa katika nusu ya mwaka wa fedha iliyoishia Desemba 2022 umekusanya shilingi bilioni 165.7 kutokana na mapato ya uwekezaji na vitega uchumi vya Mfuko. 

Hayo yamebainishwa leo Februari 8,2023 Jijini Dodoma katika mkutano na waandishi wa habari wakati akielezea utekelezaji wa majukumu ya Mfuko huo katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mshomba amesema kiasi hicho cha mapato hakijajumuisha ongezeko la thamani ya vitega uchumi vya Mfuko huo na kuongeza kuwa katika kipindi husika thamani ya vitega uchumi vya Mfuko ilikua na kufikia shilingi trilioni 5.8 ikiwa ni ongezeko la asilimia 7 ikilinganishwa na thamani ya shilingi trilioni 5.4 iliyofikiwa katika mwaka wa fedha ulioishia mwezi Juni 2022.

"NSSF wana fursa za nyumba za makazi salama kupitia mfuko huo mwananchi anaweza kumiliki nyumba ya ndoto yake kwa kulipa gharama ya nyumba kwa mkupuo mmoja au kulipa kidogo kidogo wakati wakiendelea kuishi katika nyumba husika na nyumba hizo zipo Dungu, Mtoni Kijichi na Toangoma Jijini Dar es Salaam,"amesema Mshomba.

Amesema serikali imetekeleza mikakakati mbalimbali ya kuvutia wawekezaji wakubwa ikiwa ni pamoja na kupitia maonesho ya filamu ya The Royal Tour.

"Miradi hiyo pekee imechangia takribani wanachama wapya 33,066 na kwa ujumla mkakati huo wa Serikali umechangia katika ongezeko la wanachama na michango inayokusanywa na Mfuko,"amesema Msomba.

Ameongeza kuwa kutokana na juhudi mbalimbali za Serikali kuvutia uwekezaji na kufungua fursa mpya za biashara, wastani wa makusanyo ya michango kwa mwezi yameongezeka na kufikia shilingi bilioni 134 kutoka wastani wa shilingi bilioni 118 kwa mwezi katika mwaka wa fedha ulioishia Juni 2022 ikiwa ni sawa na asilimia 14.

MAMLAKA YA USIMAMIZI BAHARI KUU KUJENGA KIWANDA KUCHAKATA SAMAKI

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

MAMLAKA ya kusimamia uvuvi wa Bahari Kuu inatarajia Kujenga Kiwanda kikubwa cha kuchakata Samaki Mkoani Tanga ambacho kitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani zaidi ya 100 kwa siku ambacho kitagharimu Dola Milioni 10 na kutoa fursa ya ajira kwa Watanzania.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo,Dk Emanuel Sweke wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Mamlaka ya usimamizi wa Bahari Kuu. 

Sweke amesema kuwa katika kudhibiti uvuvi haramu  Mamlaka hiyo imeweza kuweka mifumo madhubuti ambayo inaendana na Teknolojia kwakufanya doria mbalimbali kwa ajili ya kukomesha uvuvi haramu.

"Kutokana na shughuli zake Mamlaka hiyo imeweza kuvunja rekodi ya kukusanya mapato mengi kwa kipindi cha mwaka 2022 hadi kufikia shilingi bilioni 4.1 na wametoa jumla ya leseni za uvuvi 5336,"alisema Sweke.

Mamlaka ya kusimamia uvuvi wa Bahari Kuu imeanzishwa rasmi Mwaka 2010 lengo lake likiwa ni kusimamia shughuli zote za uvuvi wa Bahari Kuu na ufuatiliaji.

WACHIMBA VISIMA VYA MAJI WATAKIWA KUWA NA VIBALI

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

BODI ya Maji ya Bonde la Wami-Ruvu imewataka wadau wa maji nchini kuzingatia na kufuata taratibu za uchimbaji wa visima vya maji ikiwemo kupata vibali halali ili kupata maji yenye ubora na kuondokana na malalamiko mengi ya maji yasiyo na viwango.

Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Wami Ruvu Mhandisi Elibariki Mmasi ameeleza hayo  wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa miradi ya maji chini ya bodi hiyo.

Mmasi amesema wadau wa maji wanapaswa kufahamu madhara ya kuchimba visima bila vibali na kupelekea changamoto ya ubora wa maji kwenye maeneo mengi jambo linaloweza kuleta madhara kiafya.

"Baadhi ya hatua zinazopaswa kuchukuliwa ili kutumia maji yasiyo na madhara kuwa ni pamoja na kuhakikisha maji yanayopatikana baada ya kuchimbwa yanapelekwa maabara kuchunguzwa iwapo yanafaa kwa matumizi au la,"amesema Mmasi

Aidha amesema kuwa bodi hiyo imejipanga kuhakikisha inamaliza changamoto ya tatizo la maji katika mikoa ya Dar es salaam,Pwani na Morogoro kwa kuchimba visima vya maji 

HUDUMA MTANDAO KUBORESHWA

 

Na Wellu Mtaki, Dodoma

MAMLAKA ya Serikali Mtandao ( EGA ) kuandaa na kutelekeza mikakati madhubuti ili huduma za Mtandao zote kupatikana ili kudhibiti matishio ya usalama mtandaoni na kurahisisha utoaji wa huduma kwa umma.

Hayo yamesemwa na Mkurugezi mkuu wa mamlaka ya serikali Mhandisi Benedict Benny Ndomba wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu kikao kazi cha tatu cha serikali Mtandao kinachotarajiwa kufanyika Februari 8 hadi 10 mwaka huu katika ukumbi wa AICC Jijini Arusha ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama ( mb).

Ndomba amesema kuwa takribani wadau 1,000 wa serikali Mtandao kutoka katika mashirika na taasisi za umma wakiwemo maafisa masuuli, wajumbe wa bodi, Wakuu wa vitengo vya tehama, maofisa tehama, rasilimali watu, mipango, mawasiliano, wahasibu pamoja na watumishi wote wa mifumo ya tehama serikali wanatatarajiwa kushiriki kikao hicho.

"Lengo la kikao hicho ni kijadiliana juu ya mafanikio, changamoto pamoja na kuweka mikakati mbalimbali ya kukuza serikali Mtandao nchin Ili kuhakikisha matumizi sahihi na salama ya tehama katika taasisi za umma,"alisema Ndomba.

Aidha alisema kuwa Mamlaka ya serikali Mtandao( (e-GA) ni taasisi iliyopewa jukumu la kuratibu, kusimamia na kukuza juhudi za serikali Mtandao pamoja na kuhimiza uzingatiwaji wa sera, Sheria, kanuni, viwango na miongozo ya serikali Mtandao katika taasisi za umma ili kuhakikisha matumizi sahihi na salama ya tehama yanazingatiwa katika taasisi hizo.

Monday, February 6, 2023

NJOMBE YATEKETEZA ILANI YA CCM KWA VITENDO



NJOMBE YATEKELEZA ILANI YA UCHAGUZI YA (CCM) KWA VITENDO

Na Elizabeth Paulo, Njombe

MKOA wa Njombe umeendelea na utekelezaji wa  Miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwa ni ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika mkoa huo.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe Antony Mtaka amebainisha Utekelezaji wa miradi hiyo katika taarifa ya utekelezaji wa Ilani kwa Mkoa wa Njombe katika kipindi cha mwaka mmoja Julai 2021 hadi Disemba 2022.

Mtaka amesema Mkoa wa Njombe unaendelea kutekeleza mipango ya maendeleo kwa kuzingatia Ilani ya Chama ambapo na Dira ya Taifa ya maendeleo 2025 na malengo ya maendeleo endelevu ya Milenia yenye lengo la kuendelea kuwatumikia wananchi na kuboresha maisha ya wananchi wote.

"Kama ilani ya chama tawala inavyoelekeza Mkoa umekusudia kusimamia na kuelekeza rasilimali zake katika kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za Afya, Elimu, Maji, Umeme na Makazi vijijini na Mijini pamoja na kuleta mageuzi ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika kujitegema kwa chakula wakati wote na kuchangia kikamilifu kwa maendeleo ya kiuchumi,"alisema Mtaka.

Amesema serikali ya Mkoa itajikita katika mambo matatu muhimu yatakayogusa maisha ya wananchi ikiwa ni pamoja na kusikiliza na kutatua kero za wananchi, kufuatilia wanafunzi ambao bado hawajaripoti mashuleni huku asilimia 90 ya wanafunzi kidato cha kwanza wameripoti katika shule mbalimbali ambapo awali ilikuwa asilimia12.

"Mkoa umeanzisha mkakati wa kuwaondoa wanufaika wa Tasaf baadaya miaka mitatu hadi miaka mitano kwa kuanza na Halmashauri ya Makambako ambapo katika ziara ya Waziri wa Kilimo Bashe alitoa miche ya parachichi 20,000 yenye thamani ya shilingi millioni 100 kwa wanufaika wa Tasaf hao ambapo kila kaya imepewa miche 10,"amesema Mtaka.

Aidha amesema kuwa kutokana na kero kubwa na changamoto inayowakabili wananchi na wakazi wa mkoa huo kutozwa ushuru mara mbili kuingia stendi kuu ametoa wito kwa viongozi na wakusanyaji wa mapato ya ndani ya Halmashauri kutafuta vyanzo vya mapato na kuacha mapato kero kwa wananchi.

Awali akizungumza Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Njombe Deo Sanga ameupongeza uongozi wa chama tawala chini ya Mwenyekiti wake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutenga fedha nyingi za ujenzi wa miradi ya maendeleo katika mkoa wa Njombe. 

Katika kuwainua kiuchumi Halmashauri ya Mkoa imeendelea kutoa mikopo kwa Vikundi vya akina mama, Vijana na watu wenye ulemavu ambapo jumla ya shilingi bilioni 10.6 zimekopeshwa ambapo vikundi vya wanawake ni 382 vyenye wanufaika 4,062, Vijana vikundi 237 vyenye wanufaika 1,564 pamoja na watu wenye ulemavu kwa vikundi 72 vyenye wanufaika 207.

Maadhimisho ya Miaka 46 ya kuzaliwa kwa Chama cha mapinduzi kwa Mkoa wa Njombe imehudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Chama, akiwemo Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt Pindi Chana, Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tamisemi anayeshughulikia Elimu na Afya Dkt Festo John Dugange, Wabunge, wenyeviti wa Halmashauri, Wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya, pamoja na wananchi wa Mkoa huo.


Saturday, February 4, 2023

RAIS DK SAMIA APONGEZWA MIRADI YA MAENDELEO



RAIS APONGEZWA KUHAMASISHA MAENDELEO KUINUA UCHUMI.                

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM NEC) Taifa Hamoud Jumaa amempongeza Rais Dk Samia Suluhu Hassan kuhamasisha maendeleo na kukuza uchumi wa nchi.

Jumaa aliaysema hayo alipowaongoza wana CCM na wananchi kuadhimisha miaka 46 ya CCM Kibaha Vijijini na kuwa Tanzania ilipofikia kwa kipindi hicho kuna mengi ya kujivunia.

Alisema kuwa wumuunge mkono Rais na kuacha maneno kwani sekta zote zikiwemo afya, elimu kujengwa, vikundi vya ujasiliamali na machinga wanawezeshwa mikopo na miradi mikubwa ya kimkakati haijasimama ikiwa ni pamoja na reli ya mwendo Kasi SGR, Bandari kavu ya Kwala, Daraja la kisasa la Wami.

Jumaa aliwataka wana CCM kuwa wamoja kuimarisha ushirikiano ili kuiletea ushindi CCM uchaguzi wa Serikali za mitaa 2024 na uchaguzi mkuu 2025 pia aliweka jiwe la msingi ujenzi wa ofisi ya kata Mtongani ambao ulianza tangu mwaka 2017 kwa njia ya kujitolea ambapo amechangia 500,000 na rafiki yake 500,000 kwa ajili ya ujenzi huo.

Naye Mwenyekiti wa CCM Kibaha Vijijini Mkali Kanusu alieleza kuwa Rais Samia apewe ushirikiano na kuyaeleza yale aliyoyatekeleza nchini na alisisitiza kwa wana CCM kuwa na umoja na mshikamano na pasipo kutengana ili chama kiweze kusonga mbele.

Katibu wa CCM Kibaha Vijijini Safina Nchimbi alieleza kuwa maadhimisho hayo yameambatana na tukio la kuchangia damu kupanda miti kufanya usafi kituo cha afya Mlandizi na zahanati

Kwa upande wake Katibu wa CCM Mtongani Gloria Kirei alisema ujenzi huo mbali ya wanaCCM kujitolea pia wabunge viti maalum Hawa Mchafu ,Subira Mgalu, wilaya na Mwenyekiti wa UWT mkoa Zainabu Vullu nao walichangia vifaa mbalimbali.


Friday, February 3, 2023

MIAKA 46 CCM JUMUIYA YA WAZAZI BAGAMOYO YAPANDA MITI SHULENI

WAKAZI wa Chalinze wilayani Bagamoyo wametakiwa kupanda miti ili kutunza mazingira kuzuia upepo wa mara kwa mara unaoezua mapaa katika majengo yao.

Akizungumza wakati wa zoezi la upandaji wa miti katika shule ya msingi Bwilingu Kata ya Bwilingu Chalinze Mwenyekiti wa Wazazi wilaya ya Bagamoyo Aboubakary Mlawa alisema kuwa wananchi wanapaswa kuwa na utamaduni wa kupanda miti mara kwa mara na si kusubiri wakati wa sherehe ama ugeni.

Mlawa alisema kuwa kwa eneo la chalinze eneo kubwa lipo wazi kwa kutokuwa na miti kutoka na ujenzi hivyo ni muhimu sasa kila mkazi awe na utamaduni wa kupanda miti.

"Kumekuwa na matukio mengi ya upepo kuezua mapaa katika majengo ya watu binafsi sambamba na majengo ya taasisi zikiwemo shule dawa pekee kuzuia hali hii ni kupanda miti kwa wingi,"alisema Mlawa.

Alisema kuwa kama kila mtu akipanda mti mmoja katika maeneo yanayomzunguka ana hakika mazingira ya majengo yao yatakuwa na usalama.

"Wao kama Jumuiya ya Wazazi jukumu mojawapo walilopewa na Chma cha Mapinduzi ambalo pia katika dhumuni la kuwepo kwa jumuiya hiyo ni utunzaji wa nazingira hivyo ni muhimu kusimamia na kuhakikisha upandaji wa miti unakuwa endelevu,"alisema Mlawa.

Aidha alisema anaomba upandaji wa miti usiwe wakati wa ujio wa wageni ama wakati wa sherehe,zoezi la upandaji miti liwe la kila siku.

Awali Diwani wa kata ya Bwilingu Nasser Karama alisema kama Diwani alihakikisha kuwa maeneo mbalimbali ya Taasisi yanapata huduma ya maji kwa kuchimba visima vya kisasa. 

Karama alisema kuwepo kwa visima hivyo kutachochea utunzaji wa miti hiyo na uboreshaji wa mazingira.

Jumuiya wa Wazazi wilaya ya Bagamoyo katika kusherekea miaka 46 ya kuzaliwa kwake ilifanya shughuli mbalimbali ikiwemo utoaji misaada mbalimbali, upandaji miti na uchangiaji wa damu. 


MTAA WA BAMBA KUJENGA SEKONDARI

MTAA wa Bamba Kata ya Kongowe Wilayani Kibaha imesafisha eneo kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Sekondari kwa wanafunzi wanaotoka Mtaa huo ambapo hutembea umbali wa kilometa 16 kwenda Shule ya Sekondari Mwambisi.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo kwenye eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi huo Mwenyekiti wa Mtaa huo Majid Kavuta amesema kuwa tayari wana vifaa kwa ajili ya kuanza ujenzi huo kwa awali madarasa manne.

Kavuta ametaja vifaa hivyo kuwa ni tofali 3,600, saruji mifuko 50, mchanga lori tatu, kokoto lori mbili na wanatafuta mdau ili awapatie nondo ambapo kila kaya inatakiwa kutoa tofali 10.

"Kutokana na wanafunzi hao kusoma mbali kunasababisha utoro na wanafunzi wa kike kurubuniwa na kujiingiza kwenye mapenzi na wale wa kiume kujiingiza kwenye matumizi ya dawa za kulevya na uvutaji wa bhangi,"amesema Kavuta.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Kata ya Kongowe Simon Mbelea amesema ujenzi huo ni kutekeleza ilani ya chama kuhakikisha watoto wanapata elimu kwenye mazingira rafiki.

Mbelwa amesema pia ni kuunga mkono jitihada za Rais DK Samia Suluhu Hassan kuboresha sekta ya elimu ambapo ametoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya elimu nchini.

RC ATAKA WANAOSUBIRIA MABADILIKO KUCHAPA KAZI



MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakari Kunenge amewataka Wakurugenzi na viongozi ambao nafasi zao zinatokana na uteuzi wa Rais kutofanya kazi zao kwa hofu ya kutochaguliwa kwani hiyo ni mipango ya Mungu.

Kunenge aliyasema hayo Mjini Kibaha alipokuwa akiwaapisha wakuu wapya wa Wilaya na kuwakaribisha waleo waliohamishiwa vituo vyao vya kazi na kuja kwenye mkoa huo.

Alisema kuwa hakuna sababu kwa viongozi hao kutofanya kazi kwa ufanisi kuhofia uteuzi kwani hiyo itasababisha shughuli za maendeleo kutofanyika kikamilifu.

"Wakurugenzi na wale ambao nafasi zao bado hazijafanyiwa mabadiliko na Rais fanyeni kazi mambo mengine mwachieni Mungu mbona mimi nafanya kazi zangu kama taratibu zilivyo mengine tumuachie Mungu yeye ndiye anayejua,"alisema Kunenge.

Aidha alisema kuwa kuchaguliwa hiyo ni mipango ya Mungu hivyo kila mtu afanye kazi kwa mujibu wa sheria msihofie uteuzi kwani kazi za mtu ndiye zitakazomfanya achaguliwe tena.

"Yawezekana unaangaliwa hivyo ukifanya kazi chini ya kiwango unaweza ukajiharibia ni vema ukaendekea kuwajibika bila kujali mbele kutakuwa na nini kwani hayo ni majaaliwa,"alisema Kunenge.

Aliwataka viongozi hao ambao nafasi zao zinatokana na uteuzi wa Rais kutatua changamoto za wananchi kwani ndiyo wajibu wao na wamewekwa hapo kutokana na uwezo wao.

"NIKI WA PILI" AKABIDHIWA KIJITI NA SARA MSAFIRI KUONGOZA WILAYA YA KIBAHA BAADA YA MABADILIKO YA WAKUU WA WILAYA.

MKUU mpya wa Wilaya ya Kibaha Nickson John ambaye amehamishiwa hapa kutoka Wilaya ya Kisarawe amesema kuwa ili kufikia ndoto za Rais DK Samia Suluhu Hassan na matarajio ya wananchi ni kujenga timu ya pamoja.

John aliyasema hayo alipokuwa akikaribishwa Wilayani hapo na viongozi na watendaji wa taasisi na wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha na Halmashauri ya Mji Kibaha na kumuaga aliyekuwa mkuu wa Wilaya hiyo Sara Msafiri.

Alisema kuwa wananchi wana matarajio makubwa ya kupata maendeleo kutoka kwa viongozi hivyo anachohitaji ni ushirikiano ili kuwa na timu itakayofanya kazi kwa pamoja.

"Ndoto yangu ni kuhakikisha tunashirikiana na Rais ili ndoto za kuleta maendeleo zitimie kwa ushirikiano wetu sisi tukiwa ni viongozi,"alisema John.

Aidha alisema kuwa wananchi wanamatumaini makubwa makubwa na viongozi hivyo watazingatia vipaumbele vya Rais na vya wananchi ili kuleta maendeleo.

"Ili tufanye kazi vizuri napenda uwazi na utu ambacho ni kitu kikubwa pamoja na nidhamu na uwajibikaji haya yatatusaidia katika kufikia malengo tuliyojiwekea,"alisema John.

Kwa upande wake mkuu wa zamani wa Wilaya ya Kibaha Sara Msafiri aliwashukuru viongozi na watendaji wa Wilaya hiyo kwa ushirikiano waliompa alipokuwa hapo na kuwatakia heri wanaoendelea na utumishi kushirikiana.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Erasto Makala alisema kuwa watahakikisha wanashirikiana na Mkuu wa Wilaya ili kutoa huduma bora kwa wananchi.

Makala alisema kuwa kwa kushirikiana na Mkuu huyo wa Wilaya wanaamini watakuwa na ushirikiano kufikia ndoto za wananchi.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kibaha Musa Ndomba alisema kuwa watamapa ushirikiano mkuu mpya wa Wilaya ili kuwatumikia wananchi.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mhandisi Mshamu Munde alisema kuwa watashirikiana naye ili kufikia pale wanapopataka.


WAKAMATWA NA SILAHA MMOJA ATUHUMIWA MAUAJI

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani linamshikilia mtu mmoja mwanaume (53) ambaye jina limehifadhiwa mkulima mkazi wa Kijiji cha Ruvu Stesheni Wilaya ya Kibaha akiwa na silaha aina ya Shortgun Greener yenye namba za usajli 729 na maganda sita ya Risasi za Shortgun na unga wa baruti.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani ACP Pius Lutumo alisema kuwa mtuhumiwa huyo anashikiliwa kwa kukutwa na silaha hiyo.

Lutumo alisema kuwa mtuhumiwa huyo alishafanya tukio la mauaji huko Kisarawe na kutorokea katika kijiji cha Ruvu Stesheni Wilaya ya Kibaha.

"Mtuhumiwa huyo atafikishwa mahakamani mara upelelezi utakapokamilika na kuwataka watu waache kutumia silaha hizo kinyume cha sheria,"alisema Lutumo.

Katika tukio lingine ambalo lilitokea mnamo Januari 8 mwaka huu majira ya saa 06:45 mchana huko maeneo ya Msanga Sokoni Kata ya Msanga, Tarafa ya Maneromango Wilaya ya Kisarawe mtu mmoja mwanaume (47) ambaye jina lake limehifadhiwa mfanyabiashara mkazi wa Msanga Sokoni alikamatwa kwa kukutwa na Bunduki aina ya Riffle yenye namba za usajili zilizofutika.

Lutumo alisema kuwa mtuhumiwa huyo hakuwa na vibali vya umiliki wa silaha hiyo ambapo ilikamatwa wakati Polisi wakiwa kwenye misako ambayo imefanyika ndani ya kipindi cha mwezi mmoja.

Aidha alisema kuwa pia risasi sita zilikamatwa baada ya kufanya misako katika wilaya za mkoa huo kwa lengo la kudhibiti makosa ya uvunjaji, unyang’anyi wa kutumia nguvu, wizi, wizi wa mifugo, utumiaji wa dawa za kulevya pamoja na matumizi ya pombe harammu ya moshi (gongo).

"Jeshi la Polisi mkoa wa Pwani limefanya misako na operesheni mbalimbali kuanzia tarehe 1 Januari hadi tarehe  31 Januari mwaka huu ambapo Jumla ya watuhumiwa 19 wanaume wamekamatwa,"alisema Lutumo.

Aliongeza kuwa katika misako hiyo walifanikiwa kukamata pikipiki mbili za aina tofauti, Televisheni Spika, deki, feni na meza ya Tv vyote kimoja kimoja
Viti 13 waya ya Fensi rola tatu, Gongo (Pombe ya Moshi) lita 140 na Bhangi gunia 12, Puli 57 na kete 157.

"Upelelzi wa matukio haya bado unaendelea na utakapokamilika watuhumiwa hawa wote watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowahusu,"alisema Lutumo.

Alibainisha kuwa Jeshi la Polisi linaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa kutoa taarifa zozote zinazo husiana na uhalifu na wahalifu kwa wakati kwa kuwatumia wakaguzi kata waliopo kwenye maeneo yao yote ndani ya Mkoa wa Pwani nao watazifanyia kazi kwa wakati na haraka.


Thursday, February 2, 2023

WATAKIWA KUPIMA VIWANJA VIWANJA


MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakari Kunenge ametoa mwezi mmoja kwa wananchi wa mitaa ya Lumumba na Mkombozi Kata ya Pangani Wilayani Kibaha kupima viwanja vyao ambavyo serikali ilitoa baada ya kuvamia eneo lililokuwa la Kituo cha Mitamba Kibaha.

Aidha amewataka wananchi waliovamia sehemu ya Shamba hilo kuondoka kwani wako hapo kinyume cha sheria kwani eneo hilo lilikabidhiwa kwa Halmashauri ya Mji Kibaha kwa ajili ya kuliendeleza.

Kunenge aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na wananchi wa mitaa hiyo kutatua migogoro ya ardhi baada ya wananchi wa mitaa hiyo kugomea zoezi upimaji ardhi wakitaka warasimishiwe eneo ambalo walipewa baada ya kulivamia.

Alisema mtu anayerasimishiwa ni yule ambaye anamiliki ardhi kihalali lakini wao walipewa tu hivyo wanapaswa kupimiwa kwa gharama ya mita za mraba shilingi kwa shilingi 1,5000.

"Natoa mwezi mmoja kwa wananchi wote kwenye mitaa hiyo kupima ardhi yao ili wamiliki kihalali na malipo yalipunguzwa kutoka 2,500 hadi 1,500 kwa mita za mraba baada ya wengi kulalamika kuwa hawana uwezo,"alisema Kunenge.

Alibainisha kuwa eneo hilo lilikuwa likimilikiwa na iliyokuwa Wizara ya Kilimo na Mifugo wakati huo ambapo watu walilivamia na Wizara ilibidi ilimege na kuwaachia wananchi sehemu mwaka 2012.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mhandisi Mshamu Munde alisema kuwa walitoa matangazo ya wananchi kupima viwanja lakini mwitikio ukawa ni mdogo.

Munde alisema kuwa kutokana na hali ya ugumu wa kupima maeneo hayo wakitaka wayarasimishe hivyo kwa mwezi huo mmoja wanaamini watu watajitokeza kupima maeneo yao 

Shamba hilo la Mitamba lilianzishwa mwaka 1982 na 1983 na Wizara ya Kilimo na Mifugo wakati huo kwa lengo la kutoa mafunzo na uzalishaji wa ngombe bora Mitamba lilikuwa na ukubwa wa hekari 4,000 ambapo ilitoa fidia milioni 20 kwa wananchi waliokuwa wakikaa kwenye eneo hilo wapatao 1,557.