Sunday, February 14, 2016

MAMA AMFANYIA UKATILI MWANAE WA KAMBO AMVUTA SEHEMU ZA SIRI


Na John Gagarini, Kibaha
SHEILA Husein mkazi wa Janga Kata ya Janga Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani amejikuta matatani baada ya kumpiga mtoto wake wa kambo wa kiume mwenye umri wa miaka (2) na kumjeruhi sehemu mbalimbali za mwili ikiwa ni pamoja na kumvuta sehemu zake za siri.
Akizungumza na waandishi wa habari mwenyekiti wa Mtaa wa Janga na Diwani wa kata hiyo Chande Mwalika alisema kuwa mtoto huyo amekuwa akipigwa kila siku kwa fimbo hali ambayo imemfanya awe na makovu mengi mwilini.
Mwalika alisema kuwa moja ya majirani ambaye alishindwa kuvumilia vitendo hivyo Adinani Mkupa nakutoa taarifa hiyo alisema kuwa vitendo vilivyokuwa vikifanywa na mtuhumiwa huyo ni vya kikatili na haviwezi kuvumilika.
“Amekuwa akimchapa mwanae kwa fimbo bila ya kumuonea huruma hali ambayo imemfanya mtoto huyo aharibike mwili mzima kutokana na vipigo hivyo na kibaya zaidi ni pale alipofikia hatua ya kumvuta sehemu zake za siri na hakuna sababu maalumu inayomfanya amwazibu mtoto huyo kwani bado ni mdogo sana na hana uwezo wa kuongea,” alisema Mwalika.
Alisema kuwa kutokana na hali hiyo ilibidi watoe ripoti kwa kwenye uongozi wa kata kwa ajili ya hatua zaidi kwa mtuhumiwa ambaye ni mama wa nyumbani huku mumewe aliyetajwa kwa jina moja la Abdul akiwa ni mfanyabiashara kwenye magulio.
Kwa upande wake ofisa mtendaji wa kata ya Janga Michael Mwakamo alisema kuwa baada ya kupata taarifa hiyo ilibidi mgambo wapelekwe nyumbani kwa mtuhumiwa kwa ajili ya kumchukua kwa ajili ya kutoa maelezo ni kwanini anamtesa mtoto huyo.
Mwakamo alisema kuwa mtuhumiwa huyo alichukuliwa na kwenda ofisini hapo na baada ya mahojiano ilibidi apelekwe polisi kwa hatua zaidi na baada ya mahojiano kukamilika alipelekwa Mahakama ya Mwanzo ya Mlandizi.
“Tulimuuliza ni kwani ni anamfanyia vitendo vya ukatili mtoto wake huyo wa kambo alijibu kuwa hata mumewe humpiga mtoto huyo hivyo nay eye akaona afanye hivyo lakini hakuna sababu nyingine ya yeye kumchapa kupita kiwango mtoto huyo;” alisema Mwakamo.
Hakimu wa mahakama ya Mwanzo ya Mlandizi Sharifa Mtumuya alimsomea mashitaka ya shambulio ambapo mtuhumiwa alikana shitaka hilo na kupelekwa mahabusu baada ya taratibu za dhamana kushindikana na kesi hiyo itasikilizwa tena Februari 16 mwaka huu.
Mahakama iliamuru mtoto huyo akae kwa ofisa kilimo wa kata ya Janga Neema Sonje hadi itakapoamuliwa vingine wakati kesi hiyo ikiwa inaendelea kwani haitawezekana kuendelea kukaa kwenye nyumba aliyokuwa akiishi.
Mwisho.      
Na Mwandishi Wetu, Kibaha

MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amewaonya baadhi ya  madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuacha mara moja tabia ya kumtishia kumfukuza kazi  Mkurugenzi  Mtendaji wa Mji huo pamoja na Mweka Hazina wake kwa madai kwamba amekataa kulipa deni la shilingi milioni 231 la mkandarasi mmoja  anayayetoa huduma mbalimbali ndani ya Halmashauri hiyo.

Akizungumza katika kikao cha baraza la madiwani wa mji huo mkuu huyo wa mkoa aalisema kuwa anasikitishwa na kitendo cha baadhi ya madiwani hao wa kusimamia halmashauri ili iweze kufanya kazi kwa makini na kutekeleza miradi ya maendeleo kwa ufanisi na  badala  yake wanafanya kazi ya kuihujumu halmashauri kwa maslahi yao binafsi.

Ndikilo alisema kuwa madiwani hao badala ya kushinikiza Halmashauri kutekeleza miradi ya maendeleo lakini wamekuwa wakiwapigia debe watoa huduma na kuwatisha watendaji.

“Shutuma ya baadhi ya madiwani kuhujumu halmashauri hiyo kwa kuwatishia kuwaazimia watendahi  wakuu wa mji huo kuwafukuza kazi kwa madai kwamba wamekataa  kulipa deni la shilingi milioni 231 ambazo halmashauri hiyo inadaiwa na mkandarasi mmoja anayetoa huduma ndani ya mji wa Kibaha haipendezi na wanapaswa kuangalia wajibu wao wa kuwatumikia wananchi;” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa si vema kuegemea kwa mtoa huduma wanapaswa kuacha mara moja tabia ya kuwatishia watendaji ambao wamekataa kulipa deni la mzabuni huyo
na kuacha kuingiza maslahi binafisi katika utendeji wa kazi na badala yake watimize wajibu wao wa kuisimamia halmashauri.
Kwa upande wake mwenyekiti wa halmashauri ya mji huo Leonard Mloe alikiri kuwepo kwa taarifa za baadhi ya madiwani kutaka waungwe mkono kuweka maazimio ya kumfukuza kazi mweka hazina wa mji wa kibaha kwa kukataa kuizinisha malipo hayo.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM mkoa wa Pwani kimempongeza Rais wa awamu ya Tano Dk John Pombe Magufuli kwa kuweza kuzuia mianya ya upotevu wa mapato kwa kuwabana wakwepa kodi na kuliingizia Taifa mapato yanayozidi kiasi cha trilioni tatu kwa kipindi chake cha siku 100 madarakani.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha wakati wa kikao cha Halmashauri Kuu cha mkoa huo katibu mwenezi wa CCM mkoa Dk Zainab Gama akisoma tamko la mkoa kuhusu utendaji kazi wa Rais Magufuli alisema kuwa ni wa kutukuka.

Dk Gama alisema kuwa Rais ameweza kubana matumizi ya serikali na kufanikisha nchi kupata fedha nyingi ikiwa ni pamoja na kupunguza safari za nje kwa viongozi hivyo kuiwezesha serikali kubana matumizi yasiyo ya lazima ya shilingi bilioni 7 ambazo zitatumika kwenye miradi ya maendeleo.

“Jambo linguine ni kubadilisha mfumo wa sherehe za Kitaifa uliyokuwa unatumia gharama kubwa na badala yake siku za sherehe hizo ni kufanya usafi wa mazingira kote nchini;” alisema Dk Gama.

Alisema kuwa katika kuonyesha dhamira yake ya dhati ya kuwatumikia wananchi aliteua baraza dogo la mawaziri ambao ni makini na hata baada ya kuteuliwa tayari wameanza kazi kwa kasi kubwa inayoendana na kauli Mbiu yake ya Hapa Kazi Tu.

“Tunaunga mkono dhamira yake ya dhati ya kuinua uchumi kuwa wa kati kwa kusisitiza kujenga viwanda na pia kuboresha mtandao wa barabara za juu katika Jiji la Dar es Salaam Fly Overs pamoja na barabara za njia sita kutoka Dar es Salaam hadi Chalinze,” alisema Dk Gama.

Aidha alisema kuwa katika kipindi hicho aliweza kuwachukulia hatua kali za kinidhamu watendaji wabovu katika taasisi mbalimbali za serikali ambazo walisababisha wananchi kuichukia serikali yao/
Awali akifungua kikao hicho mwenyekiti wa CCM mkoa wa Pwani Mwinshehe Mlao alisema kuwa katika uchaguzi ujao wa Chama utakaofanyika mwakani viongozi wanaoteua wagombea wanapaaswa kuwa makini ili kupata viongozi bora.

Mlao alisema kuwa viongozi wanaoteuliwa kukisimamia chama wanapaswa kuwa na uwezo na si mradi tu ambao baadaye wanakuja kufanya chama kinapata wakati mgumu wakati wa uchaguzi mkuu.

Mwisho.

WATAFUTA MILIONI 50 UJENZI WA MADARASA YA SEKONDARI

NA John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Mtaa wa Mbwate kata ya Msangani wilayani Kibaha mkoani Pwani wanahitaji kiasi cha Shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa manne ya shule ya sekondari kwenye mtaa huo.
Mtaa huo una wanafunzi zaidi ya 500 wanaotoka kwenye mtaa huo kwenda kusoma kwenye shule ya sekondari ya Nyumbu ambayo iko umbali wa kilometa zaidi ya 10 hali ambayo inawapa wakati mgumu wanafunzi hao kutokana na umbali.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwenye eneo ambalo wanalifanyia usafi kwa ajili ya ujenzi wa shule hiyo mwenyekiti wa mtaa huo Abdala Mtandio alisema kuwa walikuwa wamelenga kuanza ujenzi mwakani lakini kutokana na wanafunzi wengi wanaotoka kwenye mtaa huo kusoma mbali wameona afadhali waanze na madarasa machache ili kuwasaidia watoto wao ili wasome karibu na wanakoishi.
“Tunaomba wadau watusaidie kupata fedha hizo ili tuanze ujenzi kwani kwa sasa shule ya sekondari ya Kata ya Nyumbu  imeelemewa na wanafunzi hivyo tunaiomba Halmashauri iwapunguzie wanafunzi hao kwenye shule tutakayojenga kwani kwenye mtaa wetu kuna eneo kubwa kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari wakati kule hawana eneo la kuongeza madarasa,” alisema Mtandio.
Mtandio alisema kuwa kutokana na serikali kutaka shule kuongeza madarasa kwa zile ambazo zina wanafunzi wengi ni vema Hlamashauri ikaongeza nguvu kwenye ujenzi wa shule ambayo wanataka kujenga ili kupunguza mlundikano wa wanafunzi kwenye shule hiyo ya Nyumbu.
“Tunaomba wadau watusaidie kwani kwa sasa eneo limepatikana kwa ajili ya ujenzi ambalo lina ukubwa wa hekari 10 tumeanza kwa kujitolea kufyeka vichaka na sasa tunajitolea kungoa visiki ambapo pia tunaomba Halmashauri itusaidie greda kwa ajili ya kungoa visiki tuliomba muda mrefu ambapo tathmini ilifanyika na kuonekana kuwa zinahitajika kiasi cha shilingi milioni nane kwa ajili ya greda,” alisema Mtandio.
Kwa upande wake mmoja wa wakazi wa mtaa huo Steven Mwita alisema kuwa malengo ya mtaa wetu ni kuanza ujenzi kuanzia mwezi wanne hivyo wanawaomba serikali na wadau wengine wa maendeleo wawasaidie kwa kuwachangia kwa hali na mali ili wafikie lengo la kujenga shule ya sekondari.
Mwita alisema kuwa matarajio yao ni kufanya ujenzi wa kisasa wa ghorofa ili baadaye wawe na elimu ya juu yaani kidato cha tano na cha sita kwa lengo la kuinua sekta ya elimu kwenye mtaa pamoja na wilaya nzima ya Kibaha

Mwisho.

Saturday, February 13, 2016

WAATHIRIKA WA MAFURIKO WAPATIWA MAHINDI YA MSAADA

Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula Nchini (NFRA)  imeupatia mkoa wa pwani tani 1,283 za mahindi kwa ajili ya wahanga wa mafuriko wilayani Rufiji.
Mahindi hayo yatasagwa kwa ajili ya kuwapatia unga bure  wananchi 53,446 kwenye tarafa za Mkongo,Ikwiriri na muhoro wilayani humo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini kibaha mkuu wa mkoa wa pwani injinia evarist ndikilo alisema kuwa mahindi hayo yaliwasili juzi wilayani humo.
"Tunatarajia mahindi hayo yatawawasaidia waathirika hao, kisha yatasagwa na wananchi walioathirika watapewa bure," alisema ndikilo.
Ndikilo alisema kuwa tayari magari ya kubeba mahindi hayo kutoka halmashauri yameshachukua mahindi hayo ya msaada kwa kipindi cha mwezi Februari na Machi
" Pia tumeteua wafanyabiashara sita ambao watanunua mahindi kwa wakala hao kisha kuyauza kwa bei ndogo ili kila mwananchi amudu kununua," alisema ndikilo.
Aidha alisema mkakati uliopo kwa sasa wa kiwasaidia wananchi hao ni kuhamasisha wafanyabiashara kupeleka bidhaa kama Michele,unga na maharage, kufanya tathmini ya mafuriko, kuhamasisha kulima mazao ya muda mfupi Mtama, viazi, kunde na muhogo.
"Hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya kifo kilichotokana na mafuriko hayo ambayo yameathiri watu ambao wanalima kandokando ya Mto rufiji ambapo Daraja la mto muhoro limefunikwa na maji," alisema ndikilo.
Aliwaomba wadau mbalimbali kujitokeza kutoa misaada ya kiutu kwa waathirika wa mafuriko hayo yaliyoathiri hekta 8,133 za mpunga na hekta 7,171 za Mahindi.
Chanzo cha mafuriko hayo yalianza kuingia kijiji cha mloka tarehe 31 januari hadi februari 6 ambapo maji hayo yametokea mto rufiji unaopokea maji ya mvua kutoka mikoa Iringa, Mbeya na Morogoro.
Mwisho.

RC AWAPA MWEZI MAWAKALA MWEZI MMOJA KUWASILISHA MAPATO WANAYODAIWA NA HALMASHAURI

Na John Gagarini, Kibaha
MAWAKALA wote wanaokusanya mapato ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani wametakiwa walipe makusanyo yao yote wanayodaiwa na Halmashauri ndani ya mwezi mmoja.
Agizo hilo lilitolewa jana na mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo wakati akifungua baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo nakusema kuwa ucheleweshaji wa fedha hizo unasababisha Halmashauri kushindwa kufanya mipango yake ya maendeleo.
Alisema kuwa baadhi ya mawakala wamekuwa wakichelewesha makusanyo na tozo mbalimbali wanazozitoza toka kwa wananchi kwa niaba ya Halamashauri hivyo wanapaswa kupeleka malipo hayo kwa wakati.
“Moja ya hoja ambazo zimekuwa zikiwasilishwa na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) ni kushindwa kukusanya mapato ya ndani ya mawakala kwa wakati na kukosa mikakati ya kuongeza mapato ya Halmashauri,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa suala lingine ni mikataba inayoingiwa inakuwa si mizuri na inatoa mwanya kwa wakala kuacha kuwasilisha mapato bila ya kuchukuliwa sheria kutokana na kuchelesha mapato hayo.
“Pia nashauri madiwani wajiepushe na kuomba zabuni mbalimbali katika Halamashauri ili kuepuka migongano ya kimaslahi na muweze kuisimamia vizuri kwani endapo mtakuwa na maslahi hamtaweza kuisimamia hivyo kushindwa kuleta maendeleo,” alisema Ndikilo.
Aliwataka Madiwani kusimamia fedha za makusanyo ya ndani zianarudi kwa wananchi kwa kugaramia huduma mbalimbali na miradi ya maendeleo kwa ustawi wa wananchi.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Halmashauri Leonard Mlowe alisema kuwa watendaji wa halmashauri wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kuwa waadilifu ili kufanikisha maendeleo kwa wananchi yanapatikana.
Mlowe amewataka watendaji hao kuwasimamia mawakala ili wahakikishe wanawasilisha fedha za makusanyo mbalimbali zinafika kwa wakati ili kuwaletea maendeleo wananchi.

Mwisho.    

Monday, February 8, 2016

WATU 53,000 WAKUMBWA NA MAFURIKO PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
WATU 53,446 wilayani Rufiji mkoani Pwani wamekumbwa  na mafuriko hali iliyowafanya wazungukwe na maji na kuhitaji msaada kufuatia mvua za Vuli zinazoendelea hapa nchini.
Aidha tayari boti mbili za uokozi tayari zimepelekwa kwenye maeneo hayo kwa ajili ya kuwaondoa watu hao waliozungukwa na maji na kuwapeleka sehemu salama.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu toka kwenye eneo la tukio, Mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa maji hayo ambayo yametoka maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mkoa wa Morogoro.
“Vijiji vingi wilayani humo vimezingirwa na maji na watu wengi waliokumbwa na kadhia hiyo ni wale waliohamia mashambani kwa ajili ya kilimo na kukutwa na maji hayo pamoja na nyumba ambazo ziko mabondeni,” alisema Ndikilo.  
Alisema kuwa mvua hizo ambazo zilizoanza kidogo kidogo tangu Januari 31 mwaka huu zimeathiri zaidi kwenye maeneo ya kata za Mwaseni, Tarafa ya Mkongo, Tarafa ya Ikwiriri na kata ya Muhoro.
“Kutokana na athari za mvua hizo hekta zaidi ya 7,000 za Mahindi na hekta zaidi ya 8,000 za Mpunga  zimesombwa na maji na tayari mkoa umewasiliana na Waziri Mkuu kwenye kitengo cha Wakala wa mazao kuomba msaada wa chakula tani 1,280 za mahindi,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa wameteua wafanyabiashara sita kwa ajili ya kununua mahindi na kuyasaga kwa ajili ya chakula ikiwa ni njia ya kuwasaidia wananchi pia kukabili mfumuko wa bei ambao unaweza kujitokeza kutokana na hali hiyo.
Katika hatua nyingine mkoa umeomba tani 10 za mbegu za mahindi na tani tano za mbegu za Mtama kwa ajili ya kupanda kukabiliana na athari ya mazao ambayo yamesombwa na maji ya mvua za Vuli ambazo wiki ijayo zitaanza mvua za Masika.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI imeombwa kuipatia Idara ya Ziamamoto mkoani Pwani vifaa kwa ajili ya kukabiliana na majanga ya moto na kuokoa watu wanaokumbwa na majanga mbalimbali.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha Kamanda wa Kikosi cha Zimamoto mkoani Pwani Goodluck Zelote alisema kuwa kutokana na uhaba wa vifaa baadhi ya wilaya hazina vituo vya zimamoto.
Zelote alisema kuwa kwenye mkoa wa Pwani kati ya wilaya sita ni wilaya tatu tu za Kibaha, Bagamoyo na Mafia ndiyo zenye vikosi hivyo huku wilaya za Kisarawe, Rufiji na Mkuranga zikiwa hazina huduma hiyo.
“Ingependeza angalau kila wilaya kuwa japo na kikosi cha Zimamoto na uokoaji japo hakitaweza kutoa huduma kwenye eneo lote lakini angalau zingesaidia ambapo kwa sasa utendaji kazi unakuwa mgumu,” alisema Zelote.
Alisema kuwa vifaa hivyo ni magari pamoja na vifaa vya uokoaji ambapo alitoa mfano wa ajali ya moto ambayo ilitokea hivi karibuni Chalinze walifika na kunusuru nyumba yote kuteketea kwa moto lakini kutokana na umbali uliopo walinusuru vyumba kadhaa.
“Kwa sasa tunachokifanya ni kutoa elimu zaidi ya kujikinga na kuzuia moto kwa kutumia vifaa vya kuzimia moto ambavyo kila mtu anapaswa kuwa navyo kuanzia kwenye maeneo ya huduma hadi majumbani,” alisema Zelote.
Aidha alisema kuwa moja ya changamoto wanayoipata ni ujenzi holela ambao hauzingatii mipango miji hali ambayo inasababisha magari ya kuzimia moto kushindwa kufika kwenye nyumba ambazo zinawaka moto na kuwataka watu wazingatie kanuni za ujenzi.
Mwisho.  



Sunday, February 7, 2016

WANANCHI WATAKIWA KUTOWAHIFADHI WAGENI

Na John Gagarini, Kibaha
IDARA ya Uhamiaji Mkoani Pwani imewataka  wananchi kutokubali kukaa na wageni ambao si raia Watanzania kwani ni kinyume cha taratibu na endapo watabainika watachukulia hatua za kisheria kwa kuwatunza wageni.
Hayo yalisemwa na Naibu Kamishna wa Idara hiyo Grace Hokororo alipozungumza na mwandishi wa habari hizi ofisni kwake mjini Kibaha na kusema kuwa kuna watu wanaishi na wageni jambo ambalo ni kosa kisheria.
Hokororo alisema kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa wakiishi na wageni majumbani mwao wengine wakiwa wamewapangisha, wamewaajiri au kuwapangisha kwenye nyumba zao kama Raia wa Tanzania bila ya kufuata taratibu.
“Mgeni yoyote anapoingia nchini anapaswa kufuata taratibu na lazima serikali au idara hivyo watu wanaokaa nao au kufanya nao shughuli yoyote bila ya kufuata taratuibu za nchi ni kosa na endapo wanagundua kuwa siyo raia wanapaswa kutoa taarifa ili hatua zichukuliwe kwa mhamiaji haramu,” alisema Hokororo.
Alisema kuwa changamoto inayowakabili ni uchache wa watumishi hali ambayo inawafanya washindwe kuwadhibiti wahamiaji haramu hao ambao wamekuwa wakileta athari nyingi kwa raia  endapo atakaa kinyemela bila ya kufuata taratibu.
“Kuna athari mbalimbali zinazotokana na Raia wa nje kuishi bila ya kibali ikiwa ni pamoja na kunyakua rasilimali kama vile mashamba na vitu vingine lakini akiishi kwa kufuata taratibu kuna namna ya kupewa rasilimali bila ya kumwathiri mwenyeji,” alisema Hokororo.
Aidha alisema kuwa changamoto nyingine ni mkoa kutawanyika na njia za kuingilia ni nyingi kwa kupitia kwenye Bahari ambako hakuna vyombo vya kufanya doria kwenye bandari ambazo nyingine ni bubu ambazo zinatumika kama milango ya kuingilia.

Mwisho.

Monday, February 1, 2016

UWAMAMI WATAKA SULUHU NA HALMASHAURI KISARAWE

Na John Gagarini, Kisarawe

UMOJA wa Wafanyabiashara wa Mazao ya Misitu Wilayani Kisarawe mkoani Pwani (UWAMAMI) wameomba suluhu na Halmashauri ya Wilaya ili waache mgomo wa kufanya biashara hiyo kwa kurejeshewa fedha zao za faini ambazo walitozwa kimakosa.

Wafanyabiashara hao walisema kuwa wataachana na mgomo huo endapo Halmashauri hiyo hiyo itawarudishia fedha zao kiasi cha zaidi ya shilingi milioni nne ambazo wafanyabiashara hao walipigwa kinyume cha taratibu.

Akizungumza na waandishi wa habari Makamu Mwenyekiti wa umoja huo Mohamed Dikata alisema kuwa mgomo huo utaendelea hadi pale Halmashauri itakapowarejeshea fedha zao kwani hali hiyo imeathiri biashara zao hasa ikizingatiwa walikiri kuwa walifanya makosa katika upigaji fani huo kwa wafanyabiashara ambao walizidisha mzigo wa mazao ya misitu walipokuwa wakiitoa mashambani.

“Sisi tunatoa huduma kwa wananchi hivyo tunaomba Halmashauri warudishe fedha hizo ambazo ni sehemu ya mitaji yetu na tumejaribu kukaa mara kadhaa bila ya kufikia muafaka kwani wao wanataka kutulipa kidogo kidogo fedha zetu jambo ambalo hatujaliafiki tulipigwa faini ambapo wengine walipigwa faini na kufikia zaidi ya milioni moja na kutoa fedha taslimu kwani nini  wao warejeshe kwa mafungu kwani sehemu ya fedha tulizotoa ni za biashara hivyo kuyumbishwa katika shughuli zetu za kibiashara," alisema Dikata.

Aidha alisema kuwa wanataka watumishi wa Halmashauri waliohusika waondolewe kwani wamekiuka taratibu za kazi zao kwa kuwalipisha faini zisizostahili kwani si mara yao ya kwanza hivyo wanapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria.

“Walitupiga faini ya shilingi 16,000 kwa kila gunia badala ya shilingi 1,600 kwa gunia ambalo linakuwa limezidi na sisi hatukatai kulipa faini ambayo ni halali tunachopinga ni kuzidishiwa mara 10 zaidi ya faini halali,” alisema Dikata.

Jitihada za kumpata mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe hazikufanikiwa kwani alikuwa nje ya ofisi kikazi ambapo kaimu wake naye hakupatikana hata hivyo ofisa Mipango wa Patrick Alute alikiri kuwa na tatizo hilo na kusema kuwa mazungumzo yanaendelea baina ya wafanyabiashara hao.

Alute alisema kuwa Halmashauri inaendelea na mazungumzo ili kufikia muafaka, umoja huo hujihusisha na biashara ya uuzaji wa mkaa pamoja na kuni ambapo gunia moja hulipiwa kiasi cha shilingi 20,000 kama ushuru wa Halmashauri.

Mwisho.