Tuesday, January 5, 2016

HALMASHAURI KUTOA HUDUMA KADRI YA UWEZO WAKE

Na John Gagarini, KibahaKATIKA kukabiliana na changamoto mbalimbali za utoaji huduma kwa wananchi Halmashauri ya Mji wa Kibaha imesema kuwa itatatua kero hizo kadiri ya uwezo wa fedha za miradi ya maenedeleo zinavyopatikana.
Hayo yalisemwa na mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Gladys Dyamvunye alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake na kusema kuwa kuna changamoto za utoaji huduma kwani kila mwananchi anataka maendeleo.
Dyamvunye alisema kuwa changamoto ni nyingi kwani ili kuondoa kero lazima huduma ziboreke lakini kutokana na mahitaji ya huduma kuongezeka kutokana na ongezeko la idadi ya watu kila wakati.
“Kadiri maendeleo yanavyokuja mahitaji ya huduma nayo yanaongezeka hivyo kuonekana kama huduma ni kidogo lakini tutaendelea kutoa huduma kadiri ya uwezo wetu ili kuwaondolea changamoto wananchi,” alisema Dyamvunye.
Alisema kuwa halmashuri itahakikisha huduma zinazotolewa kwa wananchi zinaboreshwa ili kuondoa malalamiko yasiyo ya msingi kwani lengo ni kuboresha utoaji huduma ambayo ndiyo kazi ya Halmashauri.
“Bajeti ya fedha inaweza kuwa ni tatizo hivyo baadhi ya huduma zinaonekana kama hazitolewi kiufasaha lakini si lengo la Halmashauri yetu kwani matazamio yetu ni huduma bora kwa wananchi ili waipende serikali yao,” alisema Dyamvunye.
Aliwataka wananchi kushirikiana na halmashauri yao ili iweze kutoa huduma ambazo zitakabili changamoto zilizopo kwa wananchi na kusema wataendelea kuhudumia wananchi kadiri ya uwezo wao.

Mwisho.      

HALMASHAURI YASAKA MILIONI 16 KUKARABATI TAA ZA STENDI AMBAZO HAZIWAKI MIEZI 10 ILIYOPITA

Na John Gagarini, KibahaHUKU watumiaji wa stendi kuu ya mabasi ya Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wakilalamika kukosekana kwa taa kwenye stendi hiyo kwa kipindi cha miezi 10 Halmashauri ya Mji wa Kibaha imesema kuwa iko katika harakati za kutafuta fedha kiasi cha shilingi milioni 16 kwa ajili ya kukarabati taa hizo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha Mhandisi wa Halmashauri ya Mji huo Dismas Marango alisema kuwa baadhi ya taa kwenye stendi hiyo zimeungua hali inayofanya stendi hiyo kuwa gizani kwa kipindi chote hicho.
Marango alisema kuwa mara baada ya baadhi ya taa hizo kuungua waliwasiliana na Temesa ambao ndiyo wanaohusika na ukarabati wa umeme na magari ya serikali walifuatilia juu ya tataizo hilo na kugundua kuungua kwa baadhi ya taa hizo ambazo ziko zaidi ya 10.
“Waligundua kuungua kwa taa hizo huku nyingine zikiwa hazina mwanga mkali ambapo gharama ya kukarabati ni shilingi milioni 16 ili huduma hiyo iweze kurejea katika hali yake ya kawaida na kuondoa adha ya watumiaji wa stendi hiyo kuwa gizani,” alisema Marango.
Alisema kuwa gharama hizo ni kubwa sana hali ambayo inawafanya washindwe kurejesha huduma ahiyo ya taa kwa muda sasa lakini hata hivyo wanaendelea na michakato ya kutafuta fedha hizo ili kurejesha huduma hiyo.
“Suala hili ni la ghafla hivyo hata bajeti yake haikuwepo lakini tunaendelea na michakato mbalimbali ili kupata fedha hizo ili kuhakikisha taa zinawaka na kuondoa usumbufu kwa watumiaji wa stendi wakiwemo abiria na wale wanaofanyabiashara kwenye stendi yetu,” alisema Marango.
Aliwataka watumiaji wa stendi hiyo kuwa na uvumilivu wakati Halmashauri ikihangaika kupata fedha kwa ajili ya kurudisha huduma ya taa kwani hata wao wanachukizwa na hali hiyo lakini mipango inafanywa kurudisha hali ya kawaida.
Mwisho.

WALIOTELEKEZA VIWANJA VYA KITOVU CHA MJI WAPEWA MIEZI SITA KUVIENDELEZA

Na John Gagarini, Kibaha
HALMASHAURI ya Mji wa Kibaha imetoa muda wa miezi sita kwa watu walionunua viwanja kwenye kitovu cha mji kujenga kama sheria za ujenzi vinavyoonyesha na kwa sasa hawatakuwa tena na majadiliano kwa watakaoshindwa kujenga watanyanganywa viuwanja hivyo.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na hatua ambazo watachukua kwa watu walioshndwa kuendeleza viwanja hivyo tangu walipovinunua mwaka 2010 ofisa ardhi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Edward Mbala alisema kuwa watu hao walipew ahadi mwaka 2015 wawe wamejenga.
Mbala alisema kuwa licha ya kupewa muda wote huo lakini watu hao wameshindwa kujenga hadi sasa licha ya kuwa na maongezi ya mara kwa mara kati ya Halmashauri na wawekezaji hao mara kwa mara lakini hadi sasa wameshindwa kuyaendeleza maeneo hayo.
“Mara ya mwisho tuliwaita Aprili mwaka jana lakini walisema kuwa tatizo kubwa lililowafanya washindwe kuanza ujenzi kwenye viwanja hivyo ni hadi pale Halmashauri itakapokuwa imefanya ujenzi wa Stendi na Soko jambao ambalo tuliwaambia kuwa wao waendelee na ujenzi huku sisi tukitafuta wabia kwa ajili ya ujenzi wa vitu hivyo,” alisema Mbala.
Alisema tayari wameshapata benki ambayo itawakopesha kwa ajili ya ujenzi wa soko pamoja na stendi ambapo zaidi ya bilioni 20 zinatarajiwa kutumika kujenga miuondombinu hiyo hivyo wale walionunua viwanja waanze ujenzi.
“Tumesha waambia wayaendeleze maeneo hayo na tayari tumewapa miezi  sita kuhakikisha wanakamilisha ujenzi huo na endapo watashindwa kujenga sheria itachukua mkondo wake kwa kuwanyanganya na kuwapa wengine,” alisema Mbala.
Aidha alisema kuwa tayari wameshatoa matangazo sehemu mbalimbali na kwa wamiliki hao ili waendeleze maeneo yao ambayo ndiyo yanaonyesha sura ya mji  wa Kibaha lakini kwa sasa maeneo hayo bado ni vichaka.
Mwisho.

Sunday, January 3, 2016

KIBAHA KUJENGA STENDI NA SOKO

Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unatarajia kujenga Kituo Kikubwa cha Mabasi pamoja na Soko baada ya kupata mkopo wa zaidi ya shilingi bilioni 20 toka Benki ya Uwekezaji ya (TIB) na kuufanya mji wa Kibaha kuwa wakisasa.

Hayo yalisemwa na mkuu wa mkoa wa Pwani alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo na kusema kuwa kwa sasa taratibu zinaendelea baina ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha na benki hiyo.

Ndikilo alisema kuwa ujenzi huo unatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa mara taratibu za kitaalamu zitakapokamilika ambapo kwa sasa bado zinaendelea ikiwa ni pamoja na kupata kibali .

“Tunatarajia kuwa na stendi ya kisasa ambayo thamani yake itakuwa ni shilingi bilioni 20 pamoja na soko litakalokuwa na thamani ya shilingi bilioni 9 hasa ikizingatiwa mkoa ulikuwa hauna soko kubwa bali lililopo ni dogo na halina uwezo wa kuchukua bidhaa nyingi,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa wafanyabiashara wa mkoa wa Pwani hususani wale wa makao makuu ya mkoa Maili Moja na vitongoji vyake huwalazimu kwenda kununua bidhaa Kariakoo au kwenye masoko mengine Jijini Dar es Salaam jambo ambalo linafanya bei za bidhaa kuwa juu.

“Kibaha ambako ndiyo makao makuu ya mkoa ni kama malango wa Jiji la Dar es Salaam lakini bidhaa zimekuwa zikipita hapa na kwenda huko kisha wafanyabiashara kwenda kununua na kuzirudisha hapa hivyo kupandisha bei kutokana na gharama kuwa kubwa,” alisema Ndikilo.

Aidha alisema kuwa soko hilo ambalo litajengwa sambamba na stendi litakuwa la kisasa ambapo magari yatakuwa na uwezo wa kuingia na kushusha bidhaa na si kama ilivyo sasa ambapo kutokana na udogo wa soko lililopo hubidi magari ya bidhaa yashindwe kuingia.

Mwisho.
  

   


Saturday, January 2, 2016

MKULIMA AOKOTA BOMU LA KUTUPWA KWA MKONO

Na John Gagarini, Kibaha
MKULIMA wa Mtaa wa Sagare wilayani Kibaha mkoani Pwani Hassan Omary ameokota bomu la kutupwa kwa mkono  ambalo lilisahaulika wakati wa Operesheni Tokomeza iliyofanyika nchini Julai mwaka 2015.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha kamanda wa polisi mkoani Pwani Bonventura Mushongi alisema bomu hilo lilisahaulika wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo la kukamata wahalifu mbalimbali waliokuwa wakiiba Maliasili za nchi.
Mushongi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Desemba 31 mwaka 2015 majira ya saa 5 asubuhi wakati mke wa Omary alipokuwa akilima aligonga kitu kigumu cha chuma na alipokitoa aliona kitu kama bomu na kumwita mumewe aliye waita watu wakiwemo viongozi wa mtaa huo.
“Baada ya kuona hivyo Omary alitoa taarifa polisi na kusema kuwa wameona bomu ndipo polisi walipofika na kubaini kuwa ni bomu la kutupwa kwa mkono ambalo fuse yake ili haribika,” alisema Mushongi.
“Halikuweza kulipuka lakini endapo lingepata joto kali mfano joto la moto lingeweza kulipuka lakini hata hivyo tumeshukuru Mungu kuwa halikuweza kulipuka kwa muda wote huo kwnai endapo lingelipuka lingeweza kuleta madhara,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa baadaye ilibainika kuwa inawezekana bomu hilo la kutupwa kwa mkono liliachwa kwa bahati mbaya  wakati wa Operesheni Tokomeza iliyofanyika Julai mwaka jana.
“Kwa kushirikiana na jeshi letu tutalipelekwa kwa wataalamu wa mabomu ambao ni Jeshi la wananchi (JWTZ) kwa ajili ya kujua zaidi kuhusiana na bomu hilo ikiwa ni pamoja na kuliharibu ili lisiweze kuleta madhara,” alisema Mushongi.
Awali mwenyekiti wa mtaa wa Sagale Bernego alisema kuwa mama huyo alikuwa akisafisha shamba kwenye eneo la Omary ambalo limekuwa likichimbwa vitu vilivyoachwa zamani na watawala wa Kijerumani na Kiarabu maarufu kama Tunu.
Bernego alisema kuwa machimbo hayo ya Tunu yalikuwa yakifanywa na mmiliki huyo ambapo eneo hilo lilizua utata miaka michache iliyopita kwani kumekuwa na mambo ya miujiza yamekuwa yakitokea kwenye machimbo hayo.
Mwisho.        


DEREVA BODABODA ACHOMWA KISU AFA WALIKUWA WAKIGOMBEA MWANAMKE

Na John Gagarini, Kibaha
DEREVA Bodaboda Ally Kasimu (23) mkazi wa Kilimahewa wilayani Kibaha mkoani Pwani amefariki dunia kwa kuchomwa kisu na waendesha pikipiki wenzake wakati wakigombea mwakanamke.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa wa Mtakuja kata ya Pangani, Ramadhan Mwaya alisema kuwa marehemu alikufa wakati wa mkesha wa kukaribisha mwaka mpaya wa 2016 na kuaga mwaka 2015.
Mwaya alisema kuwa marehemu alikutwa na umauti huo akiwa amekaa pembeni na pikipiki yake huku wenzake wakimgombea mwanamke kisha kumchoma yeye kutokana na ugomvi wa wenzake waliokuwa wakigombana.
“Madereva hao pamoja na watu wengine walikuwa kwenye sherehe hizo ambazo ziliandaliwa na Halima Kitwana ambazo ziliambatana na muziki maarufu Kigodoro ulianza majira ya saa 2 usiku na baada ya muziki kwisha baada ya saa sita kamili waliondoka lakini baadaye walionekana kumgombea mwanamke ndipo walipomchoma mwenzao,” alisema Mwaya.
Alisema kuwa marehemu alichomwa kisu sehemu ya tumboni na kujeruhiwa vibaya ambapo walijaribu kumkimbiza hospitali ya Rufaa ya Mkoa  ya Tumbi kwa ajili ya matibabu lakini alifariki wakiwa njiani.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoani Pwani Bonventura Mushongi alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa watu waliohusika na tukio hilo walikimbia na wanaendelea kutafutwa kujibu tuhuma za mauaji.
Mushongi aliwataka wananchi wa mkoa huo kuwa makini katika kipindi hichi cha sherehe za kusherehekea kuukaribisha mwaka mpya kwa kutotumia vilevi kupita kiasi ili kuepukana na matukio ya uvunjifu wa amani.

Mwisho.

Sunday, December 27, 2015

HABARI MBALIMBALI ZA MKOA WA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unatarajiwa kuwa moja ya mikoa ambayo itakuwa kwa kasi kutokana na kuongezeka kwa shughuli nyingi za uwekezaji za kiuchumi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa bandari wilayani Bagamoyo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa mkoa una fursa nyingi za uwekezaji na watu binafsi pamoja na makampuni yameonyesha nia ya kuwekeza.

Ndikilo alisema kuwa uwekezaji umeanza kuchukua nafasi yake baada ya Jiji la Dar es Salaam kuonekana kuwa limejaa hivyo fursa iliyopo ni mkoa huo ambao uko jirani na Dar es Salaam.

“Kwa sasa tunajivunia na mojawapo ya uwekezaji mkubwa ni ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo ambayo itaongeza pato la mkoa huo kwani utazalisha ajira nyingi na wageni wengi wataingia kwa ajili ya shughuli nyingi za kibiashara,” alisema Ndikilo.

Alisema uwekezaji mwingine ni pale Kisarawe ambapo kimejengwa kiwanda cha saruji, Kibaha kuna viwanda vya Jipsam, Nondo na uwekezaji sehemu nyingine mbalimbali za wilaya zinazounda mkoa huo.

“Tukija kwenye zao kuu la biashara la Korosho nalo limezidi kunufaisha wakulima ambapo kwa sasa kilo ya korosho imepanda na kwa mnada sasa inauzwa kati ya 2,600 na 2,700 kutoka chini ya shilingi 1,000 na hii ni kutokana na mfumo wa stakabadhi ghalani,” alisema Ndikilo.

Aidha alisema kuwa kwa kipindi kirefu mkoa huo haukuwa na fursa nyingi hali ambayo ilisababisha uonekane kama uko nyuma kiuchumi tofauti na ilivyo sasa fursa zimekuwa nyingi sana hivyo mafanikio ya kiuchumi yatakuwa makubwa.

Aliwataka watu wa mkoa huo hususani vijana kutumia fursa hizo zilizopo ambazo zimejitokeza kwa sasa ili kujikwamua na hali ngumu ya kimaisha pia watumie fursa za kilimo ambazo ni nyingi.

Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unaendelea na uhakiki wa watu walioweka mashamba pori ili taarifa zipelekwe kwa Waziri husika na baadaye kwa Rais ili kutengua umiliki wao endapo watashindwa kuyaendeleza hususani wale walionunua kwenye kitovu cha Mji wa Kibaha.

Kwa mujibu wa Mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa kuna mashamba pori mengi makubwa ambayo hayajaendelezwa kwenye wilaya zote za mkoa huo ikiwa ni pamoja na Kibaha, Kisarawe, Rufiji, Bagamoyo na Mkuranga.

Ndikilo alisema kuwa tayari wameshaanza kuyafanyia kazi mashambapori hayo kwa kushirikiana na wakurugenzi wa Halmashauri kwa mashamba yasiyoendelezwa.

“Tayari tumeshawapelekea notisi baadhi yao ili wajieleze ni kwanini wameshindwa kuyaendeleza mashamba hayo na kwanini wasinyanganywe kutokana na kushindwa kuyaendeleza,” alisema Ndikilo.

Kwa upande wa kitovu cha Mji wa Kibaha ambako ndiyo makao makuu ya mkoa huo alisema kuwa wamiliki binafsi pamoja na taasisi ambazo ni nyingi wameshapewa barua kujieleza kwanini hawakuviendeleza viwanja hivyo.

“Tunawashangaa ni kwa nini wameshindwa kuendeleza viwanja hivyo ambavyo endapo vingejengwa vingeweka suraa nzuri ya mji kwani hapo ndiyo kwenye mandari ya uso wa mji,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa licha ya kutakiwa kujieleza kwa nini hawakuviendeleza viwanja hivyo pia waeleze kuwa watavijenga lini na muda watakaokubaliana hawapaswi kuupitisha tena.

“Kwa watakaoshindwa kuviendeleza baada ya makubaliano watanyanganywa viwanja hivyo ili wapewe wengine watakaoweza kuviendeleza kwa kujenga kwa wakati ukaoakuwa umepangwa,” alisema Ndikilo.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

JUMUIYA ya Wazazi kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kibaha Mjini kimezigawia Jumuiya za Kata ardhi yenye ukubwa wa hekari moja kwa lengo la kuziendeleza kiuchumi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha baada ya zoezi hilo la kuwagawia ardhi hiyo ambalo lilifanyika kwenye sherehe za siku ya Uhuru, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Kibaha Mjini Dk Athuman Mokiwa alisema kuwa eneo hilo litakuwa kitovu cha uchumi wa Jumuiya hiyo.

Mokiwa alisema kuwa eneo hilo lenye ukubwa wa hekari 15 wameligawa kwa kata 14 za kichama ambapo kila kata inapaswa kuziendeleza kwa kulima na baadaye kufanya ujenzi.

“Kipindi cha nyuma tulishindwa kuliendeleza kutokana na kukosa fedha kwa ajili ya kulipima lakini baada ya kulipima sasa tumegawa kila kata wawe na eneo lao kwa ajili ya shughuli za kiuchumi,”alisema Dk Mokiwa.

Alisema kuwa shamba hilo lilikuwa likivamiwa na watu kutokana na kutokuwa na hati za umiliki lakini kwa sasa wameshalimiliki kisheria hivyo hakuna mtu atakayeweza kuvamia tena.

Naye katibu wa Wazazi kata ya Kibaha lilipo shamba hilo Rehema Ally alisema kuwa wanaushukuru uongozi kwa kuwapatia eneo ambapo wanatarajia kuliendeleza na hiyo ni rasilimali yao kiuchumi.

Ally alisema kuwa baada ya kupatikana hati watawakaribisha wawekezaji kwa ajili ya kujenga taasisi zikiwemo za shule au zaahanati na huduma nyingine za kijamii.

Viongozi wa Jumuiya hizo za kata wamekubaliana kufanya usafi kila baada ya wiki mbili ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Rais Dk John Magufuli juu ya usafi kukabiliana na magonjwa ya milipuko pia kuweka maeneo mbalimbali katika hali ya usafi.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

KUFUATIA dereva wa Pikipiki wa Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani Ally Rashid (35) kuuwawa kwa kupigwa risasi na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kisha kumpora pikipiki aliyokuwa akiieendesha madereva wenzake wameomba uchunguzi wa kina ufanyike kuhusiana na tukio hilo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha katibu wa Chama Cha Madereva Pikipiki Kibaha (CHAWAMAPIKI) Shaban Kambi alisema tukio hilo ni la kushangaza kwa watu kutumia bunduki kwa ajili ya kupora pikipiki likiwa ni tukio la pili.
Kambi alisema kuwa kumekuwa na matukio ya wizi wa pikipiki lakini kwa kutumia bunduki si hali ya kawaida hivyo tunaomba polisi wafuatilie tukio hilo la kusikitisha kwa mwenzetu kuuwawa.

“Matukio ya kutumia silaha ni matatu ambapo mtu mmoja alivamiwa nyumbani kwake na kupigwa risasi na kufa la pili ni mwenzetu mwingine alipigwa risasi ya mguuni na kuporwa pikipiki lakini hakufa huku mwenzetu wa juzi naye alipigwa risasi na kufa ambapo cha kushangaza matukio yote yametokea upande mmoja,” alisema Kambi.

Alisema matukio yote hayo yametokea maeneo ya machinjioni hali ambayo inawapa hofu wakazi wa Maili Moja kwa kuona kuwa maisha yao sasa yako hatarini kwa watu hao kufanya uahalifu kwa kutumia bunduki.

“Tumesha waambia madereva pikipiki kuwa makini kwani kuna baadhi ya maeneo kwa sasa ni hatarishi pia wakiwa na wasiwasi wasiwabebe watu wasiowafahamu hasa nyakati za usiku hasa katika kipindi hichi cha mwisho wa mwaka,” alisema Kambi.

Aidha alisema kuwa wao wako tayari kushirikiana na jeshi la polisi katika kufuatilia watu wanaojihusisha na matukio hayo ya uporaji wa pikipiki pamoja na mali za watu.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unatarajia kujenga Kituo Kikubwa cha Mabasi pamoja na Soko baada ya kupata mkopo toka Benki ya Uwekezaji ya (TIB) na kuufanya mji wa Kibaha kuwa wakisasa.

Hayo yalisemwa na mkuu wa mkoa wa Pwani alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo na kusema kuwa kwa sasa taratibu zinaendelea baina ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha na benki hiyo.

Ndikilo alisema kuwa ujenzi huo unatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa mara taratibu za kitaalamu zitakapokamilika ambapo kwa sasa bado zinaendelea.

“Tunatarajia kuwa na stendi ya kisasa pamoja na soko hasa ikizingatiwa mkoa ulikuwa hauna soko kubwa bali lililopo ni dogo na halina uwezo wa kuchukua bidhaa nyingi,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa wafanyabiashara wa mkoa wa Pwani hususani wale wa makao makuu ya mkoa Maili Moja na vitongoji vyake huwalazimu kwenda kununua bidhaa Kariakoo au kwenye masoko mengine Jijini Dar es Salaam jambo ambalo linafanya bei za bidhaa kuwa juu.

“Kibaha ambako ndiyo makao makuu ya mkoa ni kama malango wa Jiji la Dar es Salaam lakini bidhaa zimekuwa zikipita hapa na kwenda huko kisha wafanyabiashara kwenda kununua na kuzirudisha hapa hivyo kupandisha bei kutokana na gharama kuwa kubwa,” alisema Ndikilo.

Aidha alisema kuwa soko hilo ambalo litajengwa sambamba na stendi litakuwa la kisasa ambapo magari yatakuwa na uwezo wa kuingia na kushusha bidhaa na si kama ilivyo sasa ambapo kutokana na udogo wa soko lililopo hubidi magari ya bidhaa yashindwe kuingia.

Mwisho.