Monday, December 21, 2015

WANAFUNZI 204 HAWAKUFANYA MTIHANI WA DARASA LA SABA

Na John Gagarini, Kibaha

WANAFUNZI 204 mkoani Pwani hawakufanya mtihani  wa kumaliza elimu ya Msingi kwa mwaka 2015 kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoro.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Katibu Tawala wa mkoa huo Mgeni Baruan wakati wa kutangaza matokeo ya wanafunzi waliofanya mtihani wa darasa la saba kwa mwaka 2015 na kusema kuwa jumla ya wanafunzi waliofanya mtihani huo walikuwa 22,191 sawa na asilimia 99.1.

Baruan alisema kuwa wanafunzi ambao hawakufanya mtihani kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoro 185, vifo watano, ugonjwa wanane, huku sababu nyingine wakiwa ni wawili.

“Ukiachilia mbali wanafunzi hao ambao hawakufanya mtihani  na ufaulu wa wanafunzi kwa mkoa huo umefikia asilimia 63.1 ikilinganishwa na mwaka 2014 sawa na asilimia 56.2.,” alisema Baruan.

Alisema kuwa wanafunzi 14,010 wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2016 kati ya wanafunzi baada kufaulu mtihani wao wa kumaliza elimu ya Msingi ambapo wanafunzi wote waliofaulu wamepata nafasi na hakuna aliyekosa nafasi.

“Kati ya idadi ya wanafunzi waliofanya mtihani ni wavulana ni 10,024 na wasichana ni 12,167 huku ikionyesha kuwa mkoa haukupata tuhuma za udanganyifu katika zoezi la ufanyaji mtihani,” alisema Baruan.

“Mkoa umeshika nafasi ya 14 kitaifa hata hivyo ufaulu huo hauridhishi kwani haujafikia kiwango cha asilimia 80 kwa mujibu wa mwelekeo wa Matokeo Makubwa Sasa Big Results Now (BRN) hivyo zinahitajika jitihada zaidi ili kufikia kiwango hicho,” alisema Baruan.

Kwa upande wake ofisa elimu mkoa Yusuph Kipengele alisema kuwa agizo la Rais la Dk John Pombe Magufuli la kuondolewa kwa ada na michango mbalimbali kuanzia shule ya msingi na sekondari liko palepale.

Kipengele alisema kuwa baadhi ya michango iliyoondolewa ikiwa ni pamoja na ada ni vitambulisho, mawadati, majengo,  vifaa vya michezo mlinzi haitakuwepo na mwalimu atakayechangisha mchango wowote atakuwa anakiuka agizo la Rais.

Hata hivyo alisema kuwa jukumu la wazazi ni kumnunulia vifaa vya shule mwanae ikiwa ni pamoja sare za shule, madaftari, kalamu, chakula, nauli na vifaa vingine vidogovidogo ambavyo siyo mzigo kwa mzazi yoyote.

Mwisho.

Friday, December 18, 2015

PWANI WAONGEZA UFAULU DARASA LA SABA

Na John Gagarini, Kibaha
JUMLA ya Wanafunzi 14,010 wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2016 kati ya wanafunzi baada kufaulu mtihani wao wa kumaliza elimu ya Msingi ambapo wanafunzi wote waliofaulu wamepata nafasi na hakuna aliyekosa nafasi.
Akitangaza matokeo hayo jana mjini Kibaha kwa wanafunzi waliofanya mtihani wa darasa la saba kwa mwaka 2015 katibu Tawala wa mkoa wa Pwani Mgeni Baruan alisema kuwa jumla ya wanafunzi waliofanya mtihani huo walikuwa 22,191 sawa na asilimia 99.1.
Baruan alisema kuwa waliotarajiwa kufanya mtihani walitarajiwa kuwa ni 22,191 ambapo wanafunzi 204 hawakufanya mtihani huo na ufaulu wa wanafunzi kwa mkoa huo umefikia asilimia 63.1 ikilinganishwa na mwaka 2014 sawa na asilimia 56.2.
“Mkoa umeshika nafasi ya 14 kitaifa hata hivyo ufaulu huo hauridhishi kwani haujafikia kiwango cha asilimia 80 kwa mujibu wa mwelekeo wa Matokeo Makubwa Sasa Big Results Now (BRN) hivyo zinahitajika jitihada zaidi ili kufikia kiwango hicho,” alisema Baruan.
Alisema kuwa alisema kuwa kati ya idadi ya wanafunzi waliofanya mtihani ni wavulana ni 10,024 na wasichana ni 12,167 huku ikionyesha kuwa mkoa haukupata tuhuma za udanganyifu katika zoezi la ufanyaji mtihani.
“Wanafunzi ambao hawakufanya mtihani ni 204 ni kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoro 185, vifo watano, ugonjwa wanane, huku sababu nyingine wakiwa ni wawili,” alisema Baruan.
Kwa upande wake ofisa elimu mkoa Yusuph Kipengele alisema kuwa agizo la Rais la Dk John Pombe Magufuli la kuondolewa kwa ada na michango mbalimbali kuanzia shule ya msingi na sekondari liko palepale.
Kipengele alisema kuwa baadhi ya michango iliyoondolewa ikiwa ni pamoja na ada ni vitambulisho, mawadati, majengo,  vifaa vya michezo mlinzi haitakuwepo na mwalimu atakayechangisha mchango wowote atakuwa anakiuka agizo la Rais.
Hata hivyo alisema kuwa jukumu la wazazi ni kumnunulia vifaa vya shule mwanae ikiwa ni pamoja sare za shule, madaftari, kalamu, chakula, nauli na vifaa vingine vidogovidogo ambavyo siyo mzigo kwa mzazi yoyote.
Mwisho.

WATATU WAFA AJALINI PWANI

Na John Gagarini,Kibaha

WATU watatu wamefariki dunia leo katika matukio mawili ya ajali yaliyotokea mkoani Pwani.

Kamanda wa polisi mkoani Pwani,Boniventura Mushongi amethibitisha kutokea kwa matukio hayo, ambapo amesema katika tukio la kwanza watu wawili walifariki dunia kwenye ajali iyotokea huko Mbala Kijiweni wilaya ya Kipolisi Chalinze .

Amesema katika tukio hilo gari lenye namba za usajili T.743 BTV aina ya scania Lori likiendeshwa na Hashim Sadick(30) mkazi wa Gairo ikitokea Dar es salam kuelekea chalinze iligongana uso kwa uso na gari yenye namba za usajiliT.846 BXU aina ya Fuso ikiendeshwa na Cosmas Mwaifule.

Kamanda Mushongi amesema,madereva wa magari hayo walikufa baada ya ajali hiyo kutokea.
Amesema ajali nyingine imetokea  baada ya gari lenye namba za usajili T.290 DFS aina ya Isuzu mali ya kampuni ya magazeti ya Mwananchi ikiendeshwa na Elisha Mmari ikitokea Dar es salaam kwenda Mbeya ilimgonga mwendesha pikipiki na kumsababishia kifo.
Kamanda Mushongi amesema jina la dereva huyo wa pikipiki halikufahamika  na ajali imetokea eneo la Visiga  wilaya ya Kibaha.

Chanzo cha ajali hizo kinadaiwa kuwa ni kupishana bila tahadhari(overtaking) pasipo uangalifu.

Miili ya marehemu wote watatu imehifadhiwa katika hospitali ya Rufaa ya Tumbi ikisubiri uchunguzi wa daktari.

Mwisho

Thursday, December 17, 2015

MAKANDARASI WANAWAKE WATAKIWA KUJENGA VIWANJA VYA NDEGE

Na John Gagarini, Kibaha
WAKANDARASI wanawake nchini wametakiwa kuomba kandarasi kubwa zikiwemo za ujenzi wa barabara kubwa pamoja na viwanja vya ndege kupitia kampuni zao za ujenzi ili kujiongezea kipato na kuiletea nchi maendeleo.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Mkurugenzi wa iliyokuwa Wizara Ujenzi Kegora wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo makandarasi wanawake katika maandalizi ya zabuni na manunuzi kwa kazi za ujenzi wa barabara yaliyoandaliwa na wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano.
Kegora alisema kuwa wanawake wameonyesha uwezo mkubwa kwa kufanya kazi za ujenzi wa barabara kwa viwnago vinavyokubalika hivyo ni vema wakaomba kandarasi za ujenzi mkubwa ambao zinatarajiwa kufanyika.
“Kwa sasa ombeni kazi za ujenzi mkubwa kama vile wa viwanja vya ndege, bandari, madaraja na reli ili muonyeshe umahiri wenu katika kazi za ujenzi na mnapaswa kuacha woga kwani uwezo mnao na mmeonyesha kuwa manaweza,” alisema Kegora.
Alisema wanawake wakandarasi wanapaswa sasa kuacha kubaki nyuma kwa kujenga miradi midogo midogo ya ujenzi bali wafanye miradi mikubwa ili wapate mafanikio kama walivyofanikiwa kupitia ujenzi.
“Jiendelezeni kitaaluma mfikie madaraja ya juu ili mpate kuimarika kitaaluma muwe juu pia muongeze idadi ya wakandarasi wanawake kwani mmeonyesha kazi nzuri na ndiyo maana mnapewa mafunzo haya,” alisema Kegora.
Kwa upande wake mratibu wa mafunzo hayo Mhandisi Rehema Myeya alisema kuwa mafunzo hayo yana lengo la kuwawezesha wakandarasi hao wanawake kujua namna ya ujazaji wa zabuni na mikata wakati wa kuomba kandarasi.
Myeya alisema kuwa makandarasi wanawake wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kushindwa kujaza vizuri zabuni hizo hivyo kusababisha kukosa kandarasi za ujenzi wa barabara hapa nchini hasa ikizingatiwa kuwa wengi wao hawana elimu kubwa.
Jumla ya wakandarasi wanawake 26 kutoka mikoa Dar es Salaam, Morogoro, Tanga, Singida, Kilimanjaro na Arusha ambapo hadi sasa tayari wamewapatia mafunzo makandarasi zaidi ya 200 kwenye mikoa yote hapa nchini.
Mwisho.

Tuesday, December 15, 2015

ASOTA NDANI MIAKA MITANO AOMBA MSAADA

Na John Gagarini, Kibaha
MARIAMU Mpembenwe (85) mkazi wa Mkoani A kata ya Tumbi wilayani Kibaha mkoani Pwani anakabiliwa na tatizo la maumivu ya viungo mbalimbali vya mwili ikiwemo mguu na mkono hali iliyomfanya ashindwe kutoka nje kwa kipindi cha miaka mitano.
Aidha anaomba kupatiwa baiskeli ya watu wenye ulemavu ili iweze kumsaidia kuweza kutembelea kwenda kupata huduma muhimu ikiwemo za matibabu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha waliomtembelea nyumbani kwa mwanae alisema kuwa hali yake kiafya ni mbaya kutokana na kukosa matibabu pamoja na chakula kwani mwanae ambaye anamtegemea hana kipato chochote cha kujikimu zaidi ya kuomba misaada.
Mpembenwe alisema kuwa anakabiliwa na matatizo mengi ikiwa ni pamoja na kutoona huku nyumba anayoishi kuvuja kipindi cha mvua.
“Nawaomba watu mbalimbali weneye uwezo ikiwemo serikali ili niweze kukabiliana na changamoto zinazonikabili kwani sipati huduma bora za afya, chakula, hata sehemu ninayolala kitanda hakina godoro na huduma za haja napata hapa hapa mazingira ni mabaya naomba msaada wa fedha kwa ajili ya kujikimu,” alisema Mpembenwe.
Kwa upande wake mtoto wa mama huyo Iddy Mtegya (65) alisema kuwa ni kweli mama yake anakabiliwa na matatizo mengi likiwemo la kiafya licha ya kwamba amekuwa akipatiwa matibabu hapo hapo nyumbani.
Mtegya alisema kuwa ni kweli hajatoka nje kwa kipindi hicho kwani ana matatizo ya mguu wa kulia na mkono wa kulia hivyo kushindwa kutemebea na kutokana na hali yake ya unene wanashindwa kumbeba kumtoa nje au kumpeleka sehemu nyingine.
“Naomba msaada kwa watu wenye uwezo watusaidie kiti cha magurudumu ili tuweze kumsaidia mama ili tuweze kumtoa mama nje pia kumpeleka sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na hospitali licha ya kwamba yeye mwenyewe hataki kwenda hospitali,” alisema Mtegya.
Naye diwani wa kata ya Tumbi Hemed Chanyika alisema kuwa suala hilo linasikitisha kwani licha ya hali aliyokuwa nayo mama huyo anapaswa kupatiwa huduma zote za kibinaadamu kwani kumnyima huduma hizo ni kumuongezea matatizo.
Chanyika alisema kuwa hata baadhi ya watendaji wa mtaa walipaswa kulieleza tukio hilo sehemu husika ili aweze kusaidiwa kupitia vitengo mbalimbali vya misaada kwani wameonekana kutoliweka wazi suala hilo kwa kipindi hicho cha miaka mitano.
Mwenyekiti wa mtaa wa Mkoani A Titus Kabora alisema kuwa wanataarifa ya mama huyo na familia hiyo ilianza kuhudumiwa kupitia mfuko wa maendeleo ya jamii TASAF lakini tatizo misaada hiyo ni midogo na haitoshelezi mahitaji.
Mwisho.  




Tuesday, December 8, 2015

TUMIENI MISITU KUJIONGTEZEA KIPATO TOKA WATALII

Na John Gagarini, Kibaha
WANANCHI wanaoishi jirani na Hifadhi ya Msitu wa Ruvu Kusini wametakiwa kuacha kufanya uharibifu wa msitu huo badala yake wautumie kama chanzo cha mapato kwa njia ya Utalii.
Hayo yalisemwa kwenye Kijiji cha Kipangege wilayani Kibaha mkoani Pwani na ofisa miradi wa Shirika lisilo la Kiserikali la Usimamizi wa Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) Yahaya Mtonda wakati wa tamasha la Kimataifa la Utalii wa kutumia Baiskeli.
Mtonda alisema kuwa kutokana na umuhimu wa misitu ukiwemo msituo ambao unatumika kuchuja hewa safi ukiwa ni mapafu ya kupumulia hewa ya Jiji la Dar e s Salaam wananchi wanapaswa kuulinda na kuondokana na dhana kukata miti kwa ajili ya kujiongezea kipato.
“Kwa sasa tumeshaweka mazingira ya kuufanya msitu huu kuwa wakitalii tofauti na ilivyokuwa mwanzo kwani kwa sasa watalii watakuja kuutembelea na kufanya utalii kujionea miti mbalimbali ya asili ambayo inapatikana hapa Tanzania na hakuna sehemu nyingine inakopatikana hivyo ni wakati sasa wa wananchi kutumia fursa hii kujiongezea kipato kupitia utalii badala ya kukata miti kwa ajili ya mbao na kuni au mkaa,” alisema Mtonda.
Alisema kuwa endapo wananchi watatumia fursa hiyo watapata mapato huku wakienedelea kutunza msitu huo pamoja na kuhifadhi mazingira na kukabilian na changamoto ya tatizo la Tabianchi ambayo inasababisha kukosekana mvua na kusababisha hali ya hewa kuwa mbaya hususani kuwa na joto kali.
Kwa upande wake Mshauri wa Ufundi wa (TFCG) Andrew Perkin lengo la tamasha hilo ni kuwapa uelewa wananchi juu ya umuhimu wa kulinda misitu ili waweze kufurahia mazingira mazuri ambayo uoto wake wa asili unasababisha hali ya hewa kuwa safi.
Perkin alisema kuwa misitu hiyo ilikuwa ikiharibiwa sana na wananchi kutokana na kukata miti kwa ajili ya shughuli za kibinadamu zikiwa ni pamoja na uvunaji wa misitu ambapo kwa sasa tayari wameshawaondoa watu waliokuwa kwenye msitu huo na hali yake inaanza kurudi kama ilivyokuwa mwanzo.
Naye mwenyekiti wa Umoja wa Wapanda Baiskeli (UWABA) Meja Mbuya alisema kuwa wamekuwa wakihamasisha watu kupanda baiskeli kwani matumizi ya magari yamekuwa yakiharibu mazingira kutokana na moshi unaotokanan na magari hayo.
Mbuya alisema kuwa mbali ya kupanda baiskeli wamekuwa wakitoa elimu mbalimbali ya juu ya utunzaji wa misitu na kushauri matumizi ya nishati ya jua na upepo katika baadhi ya matumizi ili kutoharibu mazingira. Jumla ya watu zaidi ya 100 toka mataifa mbalimbali walishiriki tamasha hilo ambapo walitembea umbali wa kilometa 30.

Mwisho. 

Saturday, December 5, 2015

WAWILI WAFA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MLINZI wa kampuni ya Ulinzi ya Optima inayolinda kwenye jengo la Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani Primc Bararwirwa amekutwa amekufa jirani na na kituo kikuu cha Mabasi cha Maili Moja Wilayani Kibaha.
Tukio hilo lilitokea Desemba 4 mwaka huu majira ya asubuhi jirani na Grosari ya Kilimani ambapo mwandishi wa habari hizi aliushuhudia mwili wa marehemu ukiwa chali na kufunikwa na shuka huku ukiwa hauna viatu.
Baadhi ya watu waliomshuhudia marehemu kabla ya kifo chake walisema kuwa usiku wake walimwona marehemu akiwa na wenzake huku wakiongea lakini walishangaa asubuhi kuona akiwa amekufa na hakuwa na jeraha lolote mwilini mwake.
Polisi walifika kwenye eneo hilo na kuuchukua mwili wa marehemu kisha kuupeleka Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani kwa ajili ya kuchunguza kifo chake na kusubiri ndugu kwa ajili ya taratibu za mazishi.
Kamanda wa polisi mkoani Pwnai Jafary Mohamed alithibitisha kutokea tukio hilo ambapo wanaendelea na uchunguzi kujua chanzo cha kifo hicho ambacho kimewashtua wakazi wengi wa Maili Moja waliokuwa wanamfahamu marehemu.
Katika tukio lingine mkulima wa Kijiji cha Zogowale kata ya Misugusugu Aloyce Chuma (54) amefariki dunia huku watu wengine watatu wakijeruhiwa  baada ya kupigwa na radi ambayo iliambatana na upepo mkali.
Akizungumza na gazeti hili mwenyekiti wa Mtaa wa Zogowale Rajab Mhanyige alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 10 jioni wakati marehemu akiwa amekaa kwenye gogo na wenzake hao waliojeruhiwa wakati wamepumzika baada ya shughuli za kilimo.
Mhanyige alisema kuwa radi hiyo ilipiga sehemu walipokuwa wamekaa watu hao na kumwua marehemu na kuwajeruhi wenzake huku yeye akifia eneo la tukio na hakuwa na jeraha lolote mwilini mwake.
“Siku hiyo ilipiga radi kali iliyoambatana na upepo mkali ambayo mimi sijawahi kusikia tangu kuzaliwa kwangu ilikuwa na kishindo kikubwa sana na niliamini kuwa itakuwa imeleta matatizo na kweli kwani baada ya muda nilletewa taarifa kuwa kuna mtu kafa kutokana na radi hiyo ambapo baadaye mvua kubwa ilinyesha,” alisema Mhanyige.  
Alisema mara baada ya tukio hilo waliuchukua mwili wa marehemu pamoja na majeruhi na kuwapeleka kwenye kituo cha Afya cha Mlandizi kwa ajili ya kuhifadhi mwili na majeruhi kwa ajili ya matibabu ambao nao hawakuwa na majeraha yoyote.
Aidha aliwataja majeruhi ambao baadaye waliruhusiwa kurudi nyumbani kuwa ni Cosmas Bandula (54), Sultan Kigumu ambaye alirushw aumbali wa mita 10 na mtu aliyetambuliwa kwa jina moja la Kamugisha (48). Polisi walithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Mwisho.