Saturday, December 5, 2015

WAWILI WAFA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MLINZI wa kampuni ya Ulinzi ya Optima inayolinda kwenye jengo la Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani Primc Bararwirwa amekutwa amekufa jirani na na kituo kikuu cha Mabasi cha Maili Moja Wilayani Kibaha.
Tukio hilo lilitokea Desemba 4 mwaka huu majira ya asubuhi jirani na Grosari ya Kilimani ambapo mwandishi wa habari hizi aliushuhudia mwili wa marehemu ukiwa chali na kufunikwa na shuka huku ukiwa hauna viatu.
Baadhi ya watu waliomshuhudia marehemu kabla ya kifo chake walisema kuwa usiku wake walimwona marehemu akiwa na wenzake huku wakiongea lakini walishangaa asubuhi kuona akiwa amekufa na hakuwa na jeraha lolote mwilini mwake.
Polisi walifika kwenye eneo hilo na kuuchukua mwili wa marehemu kisha kuupeleka Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani kwa ajili ya kuchunguza kifo chake na kusubiri ndugu kwa ajili ya taratibu za mazishi.
Kamanda wa polisi mkoani Pwnai Jafary Mohamed alithibitisha kutokea tukio hilo ambapo wanaendelea na uchunguzi kujua chanzo cha kifo hicho ambacho kimewashtua wakazi wengi wa Maili Moja waliokuwa wanamfahamu marehemu.
Katika tukio lingine mkulima wa Kijiji cha Zogowale kata ya Misugusugu Aloyce Chuma (54) amefariki dunia huku watu wengine watatu wakijeruhiwa  baada ya kupigwa na radi ambayo iliambatana na upepo mkali.
Akizungumza na gazeti hili mwenyekiti wa Mtaa wa Zogowale Rajab Mhanyige alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 10 jioni wakati marehemu akiwa amekaa kwenye gogo na wenzake hao waliojeruhiwa wakati wamepumzika baada ya shughuli za kilimo.
Mhanyige alisema kuwa radi hiyo ilipiga sehemu walipokuwa wamekaa watu hao na kumwua marehemu na kuwajeruhi wenzake huku yeye akifia eneo la tukio na hakuwa na jeraha lolote mwilini mwake.
“Siku hiyo ilipiga radi kali iliyoambatana na upepo mkali ambayo mimi sijawahi kusikia tangu kuzaliwa kwangu ilikuwa na kishindo kikubwa sana na niliamini kuwa itakuwa imeleta matatizo na kweli kwani baada ya muda nilletewa taarifa kuwa kuna mtu kafa kutokana na radi hiyo ambapo baadaye mvua kubwa ilinyesha,” alisema Mhanyige.  
Alisema mara baada ya tukio hilo waliuchukua mwili wa marehemu pamoja na majeruhi na kuwapeleka kwenye kituo cha Afya cha Mlandizi kwa ajili ya kuhifadhi mwili na majeruhi kwa ajili ya matibabu ambao nao hawakuwa na majeraha yoyote.
Aidha aliwataja majeruhi ambao baadaye waliruhusiwa kurudi nyumbani kuwa ni Cosmas Bandula (54), Sultan Kigumu ambaye alirushw aumbali wa mita 10 na mtu aliyetambuliwa kwa jina moja la Kamugisha (48). Polisi walithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment