Tuesday, December 8, 2015

TUMIENI MISITU KUJIONGTEZEA KIPATO TOKA WATALII

Na John Gagarini, Kibaha
WANANCHI wanaoishi jirani na Hifadhi ya Msitu wa Ruvu Kusini wametakiwa kuacha kufanya uharibifu wa msitu huo badala yake wautumie kama chanzo cha mapato kwa njia ya Utalii.
Hayo yalisemwa kwenye Kijiji cha Kipangege wilayani Kibaha mkoani Pwani na ofisa miradi wa Shirika lisilo la Kiserikali la Usimamizi wa Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) Yahaya Mtonda wakati wa tamasha la Kimataifa la Utalii wa kutumia Baiskeli.
Mtonda alisema kuwa kutokana na umuhimu wa misitu ukiwemo msituo ambao unatumika kuchuja hewa safi ukiwa ni mapafu ya kupumulia hewa ya Jiji la Dar e s Salaam wananchi wanapaswa kuulinda na kuondokana na dhana kukata miti kwa ajili ya kujiongezea kipato.
“Kwa sasa tumeshaweka mazingira ya kuufanya msitu huu kuwa wakitalii tofauti na ilivyokuwa mwanzo kwani kwa sasa watalii watakuja kuutembelea na kufanya utalii kujionea miti mbalimbali ya asili ambayo inapatikana hapa Tanzania na hakuna sehemu nyingine inakopatikana hivyo ni wakati sasa wa wananchi kutumia fursa hii kujiongezea kipato kupitia utalii badala ya kukata miti kwa ajili ya mbao na kuni au mkaa,” alisema Mtonda.
Alisema kuwa endapo wananchi watatumia fursa hiyo watapata mapato huku wakienedelea kutunza msitu huo pamoja na kuhifadhi mazingira na kukabilian na changamoto ya tatizo la Tabianchi ambayo inasababisha kukosekana mvua na kusababisha hali ya hewa kuwa mbaya hususani kuwa na joto kali.
Kwa upande wake Mshauri wa Ufundi wa (TFCG) Andrew Perkin lengo la tamasha hilo ni kuwapa uelewa wananchi juu ya umuhimu wa kulinda misitu ili waweze kufurahia mazingira mazuri ambayo uoto wake wa asili unasababisha hali ya hewa kuwa safi.
Perkin alisema kuwa misitu hiyo ilikuwa ikiharibiwa sana na wananchi kutokana na kukata miti kwa ajili ya shughuli za kibinadamu zikiwa ni pamoja na uvunaji wa misitu ambapo kwa sasa tayari wameshawaondoa watu waliokuwa kwenye msitu huo na hali yake inaanza kurudi kama ilivyokuwa mwanzo.
Naye mwenyekiti wa Umoja wa Wapanda Baiskeli (UWABA) Meja Mbuya alisema kuwa wamekuwa wakihamasisha watu kupanda baiskeli kwani matumizi ya magari yamekuwa yakiharibu mazingira kutokana na moshi unaotokanan na magari hayo.
Mbuya alisema kuwa mbali ya kupanda baiskeli wamekuwa wakitoa elimu mbalimbali ya juu ya utunzaji wa misitu na kushauri matumizi ya nishati ya jua na upepo katika baadhi ya matumizi ili kutoharibu mazingira. Jumla ya watu zaidi ya 100 toka mataifa mbalimbali walishiriki tamasha hilo ambapo walitembea umbali wa kilometa 30.

Mwisho. 

No comments:

Post a Comment