Sunday, December 27, 2015

WATAKA TAFSIRI YA UPANUZI WA BARABARA WAPATE HAKI ZAO

Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Kijiji cha Kiluvya B wilaya ya Kisarawe mkoa wa Pwani wameiomba Wizara ya Ujenzi na Makazi iangalie upya tafsiri ya upanuzi wa barabara kuu kwani upanuzi uliofanyika ni urefu wa mita 120 upande mmoja wakati sheria inasema kila upande wa barabara itapanuliwa kwa urefu wa mita 60 kwa 60 kutoka katikati ya barabara kuu.
Kutokana na sheria hiyo kutafsiriwa mita 120 nyumba zilizojengwa kando ya Barabara ya Morogoro baadhi zimebomolewa na nyingine zimeekewa alama ya X zikitakiwa kubomolewa baada ya muda usiozidi zaidi ya wiki moja na kupelekea kilio kikubwa kwa wakazi hao.
Wakizungumza waandishi wa habari waliotembelea kijiji hicho moja ya wakazi hao aliyejitambulisha kwa jina la Abubakary Yusuph alisema kuwa athari ya kubomolewa nyumba hizo ni kubwa sana hivyo kuomba suala hilo liangaliwe upya.
Yusuph alisema kuwa wao hawana tatizo la kuondoka kwenye eneo hilo kwa ajili ya kupisha shughuli za maendeleo bali wameomba sheria ifuatwe ili wasinyimwe haki zao kwani wao wako hapo tangu vilipoanzishwa vijiji vya ujamaa miaka ya 70.
“Tunaomba wizara na serikali kuliangalia upya suala hili kwani sisi hatuna shida kwa wale waliojenga ndani ya mita 60 kwani tunajua suala hilo ni la kisheria lakini mita 120 tunaona kuwa hatujatendewa haki ni vema wanapotekeleza suala hilo wakazingatia sheria ya barabara na kama wanataka eneo zaidi ni vema wakatulipa ndipo waendelee na zoezi hilo,” alisema Yusuph.
Alisema kuwa watu wengi walijenga umbali zaidi ya mita 60 kwani walikuwa wakijua kuwa kama watakuwa ndani ya mita hizo basi bomobomoa ikija wangebomolewa nyumba zao lakini walikojenga walijua wako salama wanashangaa kuona nyumba zao zinabomolewa.
Naye Alfonce Kejo alisema kuwa baadhi yao ni wastaafu na hawana kipato chochote na waliwekeza kwenye nyumba zao kwa ajili ya makazi mara baada ya kustaafu kazi hivyo wanaomba suala lao lishughulikiwe ili wapate haki yao.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Kijiji hicho Julius Bukoli ambaye naye amekumbwa na bomoa bomoa hiyo alisema kuwa nyumba yake aliijenga kabla ya mwaka 2000 na iko umbali wa karibu mita 100 toka barabara kuu lakini ametakiwa kubomoa.
Bukoli alisema kuwa hata wanaohusika katika kubomoa nyumba hizo hawafuati taratibu za kutoa taarifa kwenye uongozi wa Kijiji bali wanakuja nyakati za jioni na kubomoa au kuweka alama za X kisha kuondoka.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA Cha Kuweka na Kukopa Cha TCCIA Saccos mkoa wa Pwani kimeweza kukopesha mikopo inayofikia zaidi ya shilingi milioni 398 kwa wanachama wake.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha, Meneja wa chama hicho Arestide Temu alisema kuwa fedha hizo zimetolewa kwa  wanachama waliofuata taratibu za mikopo kwa lengo la kukuza mitaji yao ya biashara.

Temu alisema kuwa hata hivyo biashara nyingi kwenye mkoa huo zinashindwa kukua vizuri kutokana na kutokuwa na mzunguko mkubwa wa fedha kwa sababu ya kuwa na shughuli chache za kiuchumi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa viwanda.

“Sababu nyingine ya wafanyabiashara kushindwa kufikia malengo ni kutokana na kufanya biashara zinazofanana na kusababisha kushindwa kufikia malengo hata hivyo tumepata mafanikio tumeweza kupata faida ya shilingi milioni 26 tofauti na lengo la kupata faida ya shilingi milioni 20 tulizokuwa tumejipangia kwa mwaka huu ambapo faida hiyo ni hadi mwezi Novemba mwaka huu,” alisema Temu.

Alisema kuwa maendeleo ya chama yanakwenda vizuri ambapo kwa sasa wamanachama wanaweza kukopa mara tatu ya fedha walaizojiwekea kama akiba na wanaweza kukopa hadi shilingi milioni 15 kwa mara moja.

“Riba ni asilimia 15 ya mkopo wowote anaoomba mwanachama ambapo hisa moja inauzwa kiasi cha shilingi 10,000 huku mwanachama akitakiwa kununua hisa kuanzia 10 na kuendelea,” alisema Temu.
Aidha alisema kuwa chama hicho cha kuweka na kukopa kilianzishwa mwaka 2001 kikiwa na wanachama 600 ambapo kwa sasa kina wanachama 227 huku wengine wakiwa wameondolewa kwa kushindwa kufuata taratibu za chama.   

Mwisho.




No comments:

Post a Comment