Saturday, December 26, 2015

WAVAMIZI WA VIWANJA VYA MICHEZO WAONYWA NA WAZIRI

Na John Gagarini, Kibaha
NAIBU Waziri wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Anastazia Wambura amewataka watu wanaovamia maeneo ya viwanja vya michezo kukomesha tabia hiyo kwani inawanyima fursa vijana kushiriki kwenye michezo.
Aliyasema hayo hivi karibu mjini Kibaha wakati akifunga michuano ya kombe la Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka (Koka Cup) kwenye uwanja wa Mwendapole wilayani humo na kusema kuwa watu hao hawapaswi kuungwa mkono kwani wanawanyima ajira vijana.
Wambura alisema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakivamia maeneo ya michezo na kujenga jambo ambalao linakwenda kinyume na matumizi yaliyopangwa na serikali hivyo vijana kushindwa kuendeleza vipaji vyao.
“Watu wenye tabia hii inabidi waiache kwani inadumaza azma ya serikali kuendeleza michezo mbalimbali hapa nchini hasa ikizingatiwa licha ya michezo kuwa ni burudani lakini pia inatoa fursa ya ajira hasa kwa vijana,” alisema Wambura.
Alisema kuwa serikali imekuwa na mipango mbalimbali ya kuendeleza michezo ikiwa ni pamoja na kuwa na viwanja ambavyo vitawawezesha vijana kushiriki michezo hivyo watu wanaovamia na kujenga ni dhahiri wanakwamisha juhudi hizo.
“Tunaomba wadau wa michezo wahamasishe ujengwaji wa viwanja vya kisasa ambapo baadhi ya watu wameonyesha uzalendo kwa kujenga viwanja ambavyo vinaendeleza jitihada za serikali kuendeleza michezo,” alisema Wambura.
Kwa upande wake Koka alisema kuwa lengo la kuandaa mashindano hayo ni kuwahamasisha vijana kushiriki michezo kwenye Jimbo lake ambapo alizipatia timu zote vifaa vya michezo kwa ajili ya kushiriki ligi hiyo.
Koka alisema kuwa jumla ya timu 168 katika Jimbo hilo zilishiriki ligi hiyo iliyoanzia ngazi ya mitaa hadi kata na baadaye kupata mshindi wa Jimbo ambapo jumla ya wachezaji zaidi ya 4,000 walishiriki michuano hiyo na bingwa alikuwa ni Home City toka kata ya pangani baada ya kuifunga Lisborn kutoka kata ya Kongowe kwa Penati 6-5.
Mshindi wa tatu ni Phata Farm ya Mkuza iliyoifunga Visiga  3-0, Bingwa alijinyakulia kiasi cha shilingi 500,000 na kombe huku mshindi wa pili akijinyakulia 500,000 na medali na mshindi wa tatu akijinyakulia 200,000 ngao na medali 

Mwisho.

No comments:

Post a Comment