Saturday, December 26, 2015

KATIBU TFF AWATAKA WABUNGE WAIBUE VIPAJI VYA SOKA VIJIJINI

Na John Gagarini, Bagamoyo

KATIBU Mkuu wa Shirikisho la Soka Nchini (TFF) Selestine Mwesigwa amewaomba wabunge kwenye Majimbo mbalimbali kuendeleza soka ngazi za chini ili kuibua wachezaji watakaokuwa wachezaji wa vilabu vikubwa pamoja na timu ya Taifa kwa siku za baadaye.

Aliyasema hivi karibuni wakati akikabidhi zawadi za washindi wa kombe la Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Dk Shukuru Kawambwa (Kawambwa Cup) ambapo timu ya Jitegemee iliibuka mabingwa baada ya kuichapa Buma 2-0 kwenye uwanja wa Mwanakalenge wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.

Mwesigwa alisema kuwa wachezaji wengi walianzia ngazi za chini hivyo wabunge wana nafasi kubwa ya kuibua vipaji ambavyo vimejificha huko Vijijini na mashindano kama hayo ndiyo yenye uwezo wa kuwaibua vijana.

“Wabunge wengine wanapaswa kuiga mfano wa mashindano hayo ya Kawawmbwa Cup ni jambo la busara kwani linainua vipaji vya vijana, kujenga afya zao pia nakuomba usiishie hapa anzisha na mashindano ya mpira wa wanawake na sisi TFF tutakuunga mkono kwa hilo”, alisema Mwesigwa.

Aliwataka wachezaji wanaopata nafasi ya kwenda kucheza kwenye timu kubwa kujenga nidhamu na kuzingatia mafunzo ya makocha ili waweze kufikia mafanikio makubwa.

 Kwa upande wake Dk Kawambwa aliwashukuru wadau wote walioshirikiana nae kufanikisha mashindano hayo na kusema kuwa mashindano hayo yamedumu kwa miaka 10 mfululizo ambapo ameahidi kuyaboresha na kuyaendeleza katika kipindi kingine cha miaka mitano ijayo.

Dk.Kawambwa alisema lengo la kuanzisha mashindano hayo ni kuibua vipaji vya vijana kuanzia vijiji, kata na wilaya pamoja na kuwaepusha kukaa vijiweni bila shughuli yoyote.
Timu ya Jitegemee Fc kata ya Magomeni iliibuka Kidedea katika mashindano hayo ya 2015 nakujinyakulia zawadi ya kombe, seti ya jezi, mipira miwili, pikipiki na medali ya dhahabu.

Mshindi wa pili alikuwa ni Buma waliopata seti ya jezi na mipira, na mshindi wa tatu timu ya Mwambao ilikabidhiwa seti ya jezi na mipira na  timu yenye nidhamu pamoja na kipa bora walipatiwa zawadi ya ngao. Mashindano ya Kawambwa Cup yalishirikisha vilabu 73 kutoka kata Saba za Jimbo la Bagamoyo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment