Tuesday, December 15, 2015

ASOTA NDANI MIAKA MITANO AOMBA MSAADA

Na John Gagarini, Kibaha
MARIAMU Mpembenwe (85) mkazi wa Mkoani A kata ya Tumbi wilayani Kibaha mkoani Pwani anakabiliwa na tatizo la maumivu ya viungo mbalimbali vya mwili ikiwemo mguu na mkono hali iliyomfanya ashindwe kutoka nje kwa kipindi cha miaka mitano.
Aidha anaomba kupatiwa baiskeli ya watu wenye ulemavu ili iweze kumsaidia kuweza kutembelea kwenda kupata huduma muhimu ikiwemo za matibabu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha waliomtembelea nyumbani kwa mwanae alisema kuwa hali yake kiafya ni mbaya kutokana na kukosa matibabu pamoja na chakula kwani mwanae ambaye anamtegemea hana kipato chochote cha kujikimu zaidi ya kuomba misaada.
Mpembenwe alisema kuwa anakabiliwa na matatizo mengi ikiwa ni pamoja na kutoona huku nyumba anayoishi kuvuja kipindi cha mvua.
“Nawaomba watu mbalimbali weneye uwezo ikiwemo serikali ili niweze kukabiliana na changamoto zinazonikabili kwani sipati huduma bora za afya, chakula, hata sehemu ninayolala kitanda hakina godoro na huduma za haja napata hapa hapa mazingira ni mabaya naomba msaada wa fedha kwa ajili ya kujikimu,” alisema Mpembenwe.
Kwa upande wake mtoto wa mama huyo Iddy Mtegya (65) alisema kuwa ni kweli mama yake anakabiliwa na matatizo mengi likiwemo la kiafya licha ya kwamba amekuwa akipatiwa matibabu hapo hapo nyumbani.
Mtegya alisema kuwa ni kweli hajatoka nje kwa kipindi hicho kwani ana matatizo ya mguu wa kulia na mkono wa kulia hivyo kushindwa kutemebea na kutokana na hali yake ya unene wanashindwa kumbeba kumtoa nje au kumpeleka sehemu nyingine.
“Naomba msaada kwa watu wenye uwezo watusaidie kiti cha magurudumu ili tuweze kumsaidia mama ili tuweze kumtoa mama nje pia kumpeleka sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na hospitali licha ya kwamba yeye mwenyewe hataki kwenda hospitali,” alisema Mtegya.
Naye diwani wa kata ya Tumbi Hemed Chanyika alisema kuwa suala hilo linasikitisha kwani licha ya hali aliyokuwa nayo mama huyo anapaswa kupatiwa huduma zote za kibinaadamu kwani kumnyima huduma hizo ni kumuongezea matatizo.
Chanyika alisema kuwa hata baadhi ya watendaji wa mtaa walipaswa kulieleza tukio hilo sehemu husika ili aweze kusaidiwa kupitia vitengo mbalimbali vya misaada kwani wameonekana kutoliweka wazi suala hilo kwa kipindi hicho cha miaka mitano.
Mwenyekiti wa mtaa wa Mkoani A Titus Kabora alisema kuwa wanataarifa ya mama huyo na familia hiyo ilianza kuhudumiwa kupitia mfuko wa maendeleo ya jamii TASAF lakini tatizo misaada hiyo ni midogo na haitoshelezi mahitaji.
Mwisho.  




No comments:

Post a Comment