Thursday, December 17, 2015

MAKANDARASI WANAWAKE WATAKIWA KUJENGA VIWANJA VYA NDEGE

Na John Gagarini, Kibaha
WAKANDARASI wanawake nchini wametakiwa kuomba kandarasi kubwa zikiwemo za ujenzi wa barabara kubwa pamoja na viwanja vya ndege kupitia kampuni zao za ujenzi ili kujiongezea kipato na kuiletea nchi maendeleo.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Mkurugenzi wa iliyokuwa Wizara Ujenzi Kegora wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo makandarasi wanawake katika maandalizi ya zabuni na manunuzi kwa kazi za ujenzi wa barabara yaliyoandaliwa na wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano.
Kegora alisema kuwa wanawake wameonyesha uwezo mkubwa kwa kufanya kazi za ujenzi wa barabara kwa viwnago vinavyokubalika hivyo ni vema wakaomba kandarasi za ujenzi mkubwa ambao zinatarajiwa kufanyika.
“Kwa sasa ombeni kazi za ujenzi mkubwa kama vile wa viwanja vya ndege, bandari, madaraja na reli ili muonyeshe umahiri wenu katika kazi za ujenzi na mnapaswa kuacha woga kwani uwezo mnao na mmeonyesha kuwa manaweza,” alisema Kegora.
Alisema wanawake wakandarasi wanapaswa sasa kuacha kubaki nyuma kwa kujenga miradi midogo midogo ya ujenzi bali wafanye miradi mikubwa ili wapate mafanikio kama walivyofanikiwa kupitia ujenzi.
“Jiendelezeni kitaaluma mfikie madaraja ya juu ili mpate kuimarika kitaaluma muwe juu pia muongeze idadi ya wakandarasi wanawake kwani mmeonyesha kazi nzuri na ndiyo maana mnapewa mafunzo haya,” alisema Kegora.
Kwa upande wake mratibu wa mafunzo hayo Mhandisi Rehema Myeya alisema kuwa mafunzo hayo yana lengo la kuwawezesha wakandarasi hao wanawake kujua namna ya ujazaji wa zabuni na mikata wakati wa kuomba kandarasi.
Myeya alisema kuwa makandarasi wanawake wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kushindwa kujaza vizuri zabuni hizo hivyo kusababisha kukosa kandarasi za ujenzi wa barabara hapa nchini hasa ikizingatiwa kuwa wengi wao hawana elimu kubwa.
Jumla ya wakandarasi wanawake 26 kutoka mikoa Dar es Salaam, Morogoro, Tanga, Singida, Kilimanjaro na Arusha ambapo hadi sasa tayari wamewapatia mafunzo makandarasi zaidi ya 200 kwenye mikoa yote hapa nchini.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment