Tuesday, December 16, 2014

TATIZO LA MAJI CHALINZE KUWA HISTORIA NA KIBAHA YAENDELEA KUKIMBIZANA NA MAABARA

Na John Gagarini, Kibaha
CHANGAMOTO ya maji wilayani Bagamoyo mkoani Pwani huenda ikawa historia baada ya serikali ya India kutoa kiasi cha bilioni 800 kwa ajili ya mradi wa maji wa Wami Chalinze.
Akizungumza na waandishi wa habari mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa fedha hizo zitasaidia kukabiliana na tatizo hilo ambalo limekuwa likiwasumbua wananchi wa wilaya hiyo.
Ridhiwani alisema kuwa fedha hizo ambazo ni sehemu ya mkopo baada ya ziara ya Waziri Mkuu wa nchi ya India alipotembelea nchini hivi karibuni.
“Fedha hizi zitasaidia kwa kiasi kikubwa kukamilisha mradi huo ambao umekwama kwa baadhi ya maeneo kutokana na mkandarasi aliyepewa kazi hiyo kutotengeneza miundombinu kwa kiwango kinachotakiwa,” alisema Ridhiwani.
Alisema mbali ya kujenga miuondombinu ya kufika kwenye vijiji mbalimbali pia fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kujenga mabwawa ya muda kwa ajili ya kuhifadhi maji na kuchujia maji.
“Wakati mwingine maji yamekuwa yakitoka machafu kutokana na maji kuingiwa na tope hasa pale mvua inaponyesha hivyo tunatarajia kuwe na matanki ambayo yatachuja maji kwani yaliyopo ni machache,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisema pia kutajengwa vioski na matenki kwenye vitongoji na vijiji 20 kwani baadhi viko umbali mdogo  kwenye baadhi ya matenki lakini havipati maji.
Alibainisha kuwa Jimbo la Chalinze baada ya muda mfupi itaepukana na adha ya maji kwani watakuwa na uhakika wa kupata maji safi na salama kupitia mradi huo kama baadhi ya maeneo.
Na John Gagarini, Kibaha
WILAYA ya Kibaha mkoani Pwani imefikia asilimia 80 ya ujenzi wa maabara kwenye shule za sekondari na inatarajia kukamilisha ujenzi huo mwishoni mwa mwezi huu.
Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba alisema kuwa wilaya hiyo imeweza kujenga maabara 53 katika kipindi cha miezi miwili cha agizo la Rais Dk Jakaya Kikwete.
Kihemba alisema kuwa kulikuwa na changamoto kubwa ambazo zimechangia ujenzi huo kushindwa kukamilika kwa asilimia 100 ambapo kwa sasa zimebakia maabara 10.
“Changamoto kubwa ilikuwa ni wenyeviti wa mitaa na viji kujiuzulu kabla ya uchaguzi kwani wao ndiyo wahamasishaji wakuu wa kukusanya michango pia mwitikio wa wananchi kuchangia kuwa mdogo na suala la akaunti ya Tegeta Escrow kushusha uchangiaji kutokana na wapinzani kutumia sababu ya wananchi wasichangie,” alisema Kihemba.
Alisema kuwa wilaya yetu ina jumla ya shule 21 ambapo kila shule inatakiwa kujenga maabara 3 hivyo kufanya wilaya kuhitaji maabara 63 na thamani ya kila maabara ni shilingi milioni 60.
“Tunawashukuru wadau wetu mbalimbali wa maendeleo na wananchi ambao walitusaidia fedha kwa ajili ya kufanikisha ujenzi wa maabara hizi na tunaendelea kuwaomba watusaidie ili tuweze kukamilisha ujenzi huo kama tulivyopanga,” alisema Kihemba.
Mkuu huyo wa wilaya ya Kibaha alisema kuwa anamshukuru Rais kwa kuwapa msukumo wa ujenzi wa maabara kwani kwa kipindi kifupi maabara nyingi zimejengwa ambazo zitakuwa na manufaa makubwa kwa wanafunzi.

Mwisho.

Monday, December 15, 2014

SOKA WANAWAKE PWANI WAINGIA KAMBINI KUJIANDAA TAIFA CUP

Na John Gagarini, Kibaha
TIMU ya soka ya wanawake ya mkoa wa Pwani imeingia kambini kwenye shule ya sekondari ya Baden Powell iliyopo wilayani Bagamoyo kujiandaa na mchezo wake na timu ya mkoa wa Morogoro utakaochezwa Desemba 28 mwaka huu.
Mchezo huo ambao utapigwa kwenye uwanja wa Mabatini Mlandizi wilayani Kibaha wa kuwania kombe la Taifa kwa wanawake.
Akizungumza na gazeti hili mjini Kibaha, katibu wa chama cha soka la Wanawake (TWFA) mkoa wa Pwani Florence Ambonisye alisema kuwa maandalizi ya mchezo huo yanaendelea vizuri.
Ambonisye alisema kuwa timu hiyo inanolewa na mchezaji wa timu ya Taifa ya Wanawake Hilda Masanche iliingia kambini wiki iliyopita.
“Timu inatarajiwa kurejea Desemba 26 wilayani Kibaha ambapo itaingia kambini kwenye kambi ya Ruvu JKT Mlandizi siku mbili kabla ya mchezo huo,” alisema Ambonisye.
Aidha alisema kuwa timu hiyo itaongezewa wachezaji wanne mara itakaporudi Kibaha ili kuipa nguvu timu hiyo inayoundwa na wachezaji wengi vijana ambao ni wanafunzi shule za sekondari.
“Changamoto kubwa inayoikabili timu hiyo ni ukosefu wa vifaa kwani wachezaji wanatumia vifaa vyao binafsi walivyoendanavyo kambini,” alisema Ambonisye.
Alibainisha kuwa wanatarajia kushinda mchezo huo kwani timu yao imejiandaa vyema na mchezo huo licha ya kuwa wapinzani wao nao wako vizuri na wana uhakika wa kuingia 16 bora.
Mwisho.

CCM YAONGOZA MATOKEO YA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA, VITONGOJI NA VIJIJI

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Pwani kimeonyesha kufanya vizuri kwenye uchaguzi wa serikali za Mitaa, Vitongoji na Vijiji ambapo kwenye matokeo ya awali kimeonekana kushinda maeneo mengi.
Katika Jimbo la Mafia CCM ilishinda vitongoji  96 kati ya 136 sawa na asilimia 70 Chama Cha Wananchi CUF asilimia 40 sawa na asilimia 29,katika vijiji  CCM ilishinda vijiji 19 kati ya 23 sawa na asilimia 82.6 CUF vijiji 4 sawa na asilimia 17.3.
Katika Jimbo la Kibaha Mjini kati ya mitaa iliyopo 73 ,CCM imeshinda mitaa 62 sawa na asilimia 84.9, huku wapinzani wao Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wakishinda kwenye mitaa 10 sawa na asimilia 13.7.
Katika Jimbo Kibaha  Vijijini kwenye Vijini 32 CCM ilishinda mitaa 31 , ambapo kwenye mitaa 10 ilishinda bila kupingwa sawa na asimilia 96.9 ,upinzani ilishinda kijiji kimoja sawa na asimilia 13.1, kati ya vitongoji 106 CCM ilishinda vitongoji 98 sawa na asilimia 92.5,upinzani vitongoji 4 sawa na asilimia 3.8.
Katika Wilaya ya Bagamoyo vijiji vilivyopo ni 75 CCM ilishinda vijiji 67 sawa na asilimia 90.5 na vijiji 8 havijafanya uchaguzi, kati ya vitongoji  610 CCM ilishinda 540 sawa na asilimia 88.5 na vitongoji 45 havijafanya uchaguzi ambapo wapinzani walishinda vitongoji sawa na  asilimia 4.1.
Wilaya ya Bagamoyo haijafanya uchaguzi katika vijiji 8 na vitongoji 45 kutokana na uhaba wa vifaa ikiwemo katasi husika za viti maalum na kuchanga majina ya wananchi na nembo za vyama vya siasa.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Bagamoyo Ibrahim Matovu alithibitisha kutokea kwa mabadiliko ya uchaguzi katika maeneo hayo ambapo alisema uchaguzi huo baadhi ya maeneo ulifanyika jana na kwingine utafanyika leo desemba 16.

Mwisho

ZAIDI YA 500 WASHINDWA KUPIGA KURA UCHAGUZI WAHAIRISHWA

Na John Gagarini, Bagamoyo
HUKU uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji ukiwa umefanyika juzi na matokeo yakiendelea kutoka wananchi 514 wa Kijiji cha Mwetemo Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo wameshindwa kupiga kura kutokana na uhaba wa karatasi za kupigia kura.
Uchaguzi huo ulishindwa kufanyika kutokana na karatasi za kupigia kura kuwa chache hivyo watu wengine kushindwa kupiga kura ambapo watafanya uchaguzi huo Desemba 19.
Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kitongoji hicho kuangalia zoezi hilo la upigaji kura wa kuchagua viongozi akiwemo mwenyekiti na wajumbe watano msimamizi msaidizi wa uchaguzi Thomas Madega alisema kuwa wamekubaliana uchaguzi huo kufanyika siku hiyo.
“Karatasi za kupigia kura kwanza zilichelewa kwani zilifika kituoni saa 10 kasoro jioni na pia zilikuwa chache hivyo watu wachache walipiga kura na wengine walishindwa kupiga kabisa,” alisema Madega.
Madega alisema kuwa walikaa na viongozi wa vyama vyote na kukubaliana kusogezwa mbele zoezi la upigaji kura.
“Tumekubaliana na vyama vyote kusogeza uchaguzi huo hadi Ijumaa na wamekubali tumewaambia wawatangazie wafuasi wao juu ya hili,” alisema Madega.
Juu ya kuahirisha kwa muda mrefu tofauti na maeneo mengine ambayo yalikuwa na matatizo na uchaguzi kufanyika jana alisema kuwa wametoa muda mrefu ili waandaliwe vifaa vya upigaji kura kwa uhakika.
Kwa upande wake mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete alisema kuwa muda huo ni mrefu sana kwani maeneo mengine yalifanya uchaguzi kesho yake.
“Nadhani suala la siku ya kupiga kura lirudishwe nyuma kwani Ijumaa ni mbali sana hivyo kuna haja ya wahusika kuliangalia hilo ili wasipishane na wengine,” alisema Ridhiwani.
Ridhiwani alishauri zoezi la namna ya kupiga kura washirikishwe zaidi wananchi kwani wale wanaowachagua ni viongozi wao hivyo wao ndiyo wenye nafasi kubwa ya kushauri na si viongozi wa vyama vya siasa.
Baadhi ya vijiji na vitongoji ambavyo vilifanya uchaguzi wao jana Jumatatu badala ya Jumapili ni Kijiji cha Changarikwa, Vitongoji vya Kwamkula, Mkambala A na B, Kwaluguru A na B, Pugwe, Migola na Kwadivumo kwenye kata ya Mbwewe.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo Ibrahim Matovu alipoulizwa juu ya baadhi ya maeneo kushindwa kupiga kura alisema kuwa bado hajapata takwimu sahihi ndiyo anafuatilia kujua changamoto hizo.
Uchuguzi mdogo uliofanywa na mwandishi wa habari hizi ulibaini zoezi la upigaji kura ulikumbwa na changamoto kadhaa ikiwemo ukosefu wa vifaa vya upigaji kura kama vile upungufu wa karatasi, picha za wagombea kuwekwa kwenye nembo ya chama kisichohusika na kukosekana kwa  fomu za wagombea wa nafasi ya ujumbe.

Mwisho.


Picha no 3942 msimamizi msaidizi wa kituo cha kupigia kura Kitongoji cha Mkwajuni kwenye Kijiji cha Miono wilaya ya Bagamoyo Faustina Oforo  akisubiria wapiga kura wa uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa. 


Picha no 3940 Msimamizi msaidizi wa uchaguzi kitongoji cha Msikitini kwenye Kijiji cha Mbwewe wilaya ya Bagamoyo Said Mlinde kulia akiongea na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kushoto alipotembela kituo hicho kushuhudia zoezi la upigaji kura.
 

Monday, December 8, 2014

CHADEMA WATISHIA KUANDAMANA

CHAMA Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani kimetoa siku mbili hadi Desemba 10 kwa Katibu Tawala wa Wilaya (DAS) Kibaha kuwarejesha wagombea wa nafasi mbalimbali kupitia chama hicho na endapo hatawarejesha watafanya maandamano kushinikiza warudishwe kuwania nafasi hizo.
Jumla ya wagombea 16 wa chama hicho wameondolewa kwenye kinyanganyiro cha kuwania nafasi za uongozi kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Deemba 14 mwaka huu, wakiwemo wenyeviti na wajumbe, kutokana na sababu mbalimbali za kukiuka sheria za uchaguzi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha mwenyekiti wa chama hicho Jimbo la Kibaha Mjini Mohamed Mnembwe alisema kuwa wametoa siku mbili Jumatatu na Jumanne ambapo Jumatano wataandamana kama endapo DAS hatawarejesha wagombea hao kwenye kinyanganyiro hicho.
Mnembwe alisema kuwa maandamano hayo watayafanya kuanzia kwenye ofisi za chama kwenda kwa DAS kudai haki za wagombea wao.
“Kuandamana ni haki ya kikatiba na si kuvunja sheria ni kutaka wagombea wetu warejeshwe kwani wameondolewa kwa uonevu na hawakutendewa haki kwani sababu zenyewe za kuwaengua si za halali,” alisema Mnembwe.
Alisema wagombea wao hawakupewa nafasi ya kupeleka ushahidi kwani wengi walienguliwa kwa madai kuwa si wakazi wa maeneo waliyoomba uongozi na kukosea kujaza fomu ikiwa ni pamoja na mtaa na mahali wanapoishi.
“Wengi waliwekewa pingamizi kuwa si wakazi wa maeneo hayo lakini wangethibitisha kwa kuwaita wahusika wakiwemo wenye nyumba kwani kusema kuwa balozi hamtambui si sawa kwani sisi pia tuna mabalozi wetu kikubwa wangepata ushahidi kama kweli si wakazi wa maeneo hayo, kwa upande wa ujazaji wa fomu ni mahali unapoishi na mtaa ndiyo walivyokosea na majina yao kuondolewa,” alisema Mnembwe.
Aidha alisema kuwa wao wanachotaka ni wagombea wao kurejeshwa kwenye nafasi za kuwania nafasi hizo na endapo DAS atafanya hivyo hawatafanya maandamano kwani wanataka uchaguzi huo ufanyike kwa amani na utulivu.
“Tunajua muda umeisha ila wakirejeshwa tunauhakika wa kushinda kwenye uchaguzi huo na tutatoa taarifa polisi ili kuomba ulinzi kwani maandamano yetu ni ya amani na hatuna nia ya kufanya vurugu kikubwa tunachotaka ni haki kutendeka,” alisema Mnembwe.
Mwenyekiti huyo wa CHADEMA Jimbo la Kibaha alitaja maeneo ambako wagombea wake wameondolewa kuwa ni Maili Moja 2, Kongowe 6, Visiga 3, Vikawe Shuleni 1,Miswe Chini 1 na Miwaleni 3.
Hivi karibuni DAS Sozi Ngate alipoulizwa kuhusiana na malalamiko hayo alisema kuwa kama wanaona wameonewa waende mahakamani kudai haki yao.
Mwisho.


















AFA KWA KUCHOMWA KISU NA WATU WASIOFAHAMIKA

Na John Gagarini, Kibaha
MTU mmoja aliyefahamika kwa jina la Juma Abdala (65) mkulima wa Kitongoji cha Kwa Mwaleni kijiji cha Mbwewe kata ya Mbwewe wilayani Bagamoyo mkoani Pwani amekufa kwa kuchomwa kwa visu na watu wasiofahamika.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo walisema kuwa mzee huyo aliitwa na vijana wawili waliofika nyumbani kwake na kumwita pembezoni mwa nyumba yake kisha kumshambulia na kumwua.
Akizungumza kwa njia ya simu na mwandishi wa habari hizi ofisa mtendaji wa kijiji cha Mbwewe Ramadhan Mwanaagonile alisema kuwa tukio hilo lilitokea Novemba 6 mwaka huu majira ya saa 1:30 usiku Kitongojini hapo.
Mwanaagonile alisema kuwa siku ya tukio vijana hao ambao hawafahamiki walifika nyumbani kwa marehemu na kumtaka waongee naye wakati huo marehemu alikwenda kwenye kibanda jirani kwa ajili ya kunywa kahawa.
“Watu hao walipomuulizia marehemu walijibiwa kuwa hayupo walitaka aitwe ili waongee naye ndipo alipoitwa na kumtaka wakazungumze pembeni na ndipo walipokwenda kwenye ua wa nyumba yake na kuanza kuongea,” alisema Mwanaagonile.
Alisema baada ya muda walisikia marehemu akipiga kelele kuomba msaada huku akisema kuwa anakufa na walipokwenda walikutwa kachomwa kisu kitovuni na kifuani na mkononi.
“Marehemu alijaribu kukimbia kwenda waliko watu lakini alishindwa na kuanguka na watu walipofika walimkuta akiwa anatokwa na damu nyingi ambazo zilisababisha kifo chake huku wale watu wakiwa hawaonekani kwani walikimbia kusikojulikana,” alisema Mwanaagonile.
Aidha alisema taarifa zilitolewa kituo cha Polisi cha Mbwewe ambao walifika na kuuchukua mwili wa marehemu na baadaye mwili ulichunguzwa na daktari kisha kukabidhiwa ndugu kwa ajili ya mazishi.
“Tulijaribu kuwatafuta vijana hao bila ya mafanikio na hatukukuta chochote pale palikotokea tukio watu hao hawakumchukulia kitu chochote kwnai alikuwa na simu na vitu vingine lakini waliviacha,” alisema Mwanaagonile.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo alisema bado halijafikishwa ofisini kwake na kusema kuwa atafuatilia na kulitolea taarifa.
Mwisho.



Sunday, December 7, 2014

OUT KUTUMIA MAMILIONI KUFUNDISHA WALIMU WA MASOMO YA SAYANSI



Na John Gagarini, Kibaha
CHUO Kikuu Huria Tanzania (OUT) kimepata fedha kiasi cha dola za Kimarekani milioni 50 kutoka benki ya dunia kwa ajili ya kuwajengea uwezo walimu wa masomo ya Sayansi na Hisabati hapa nchini.
Aidha fedha hizo pia zitatumika kwa ajili ya kujenga maabara mchanganyiko, mabweni na ofisi za walimu kwa lengo la kuboresha ufundishaji wa masomo chuoni hapo.
Hayo yalibainishwa na mgeni rasmi kwenye mahafali ya kwanza ya OUT kituo cha mkoa wa Pwani, Naibu Makamu Mkuu wa chuo hicho kitengo cha Teknolojia za Kujifunzia na Huduma za Mikoa Profesa Modest Varisanga.
Prof. Varisanga alisema kuwa kuna uhaba mkubwa wa walimu wa masomo hayo hivyo wameamua kuwekeza kwenye masomo hayo kwani ndiyo msingi wa kupata wataalamu mbalimbali.
“Chuo kinaendelea kujiimarisha kwenye maeneo mbalimbali pamoja na kuhakikisha tunazalisha wataalamu na msingi ni masomo ya Sayansi ndiyo sababu ya kuweka mkakati wa makusudi wa kuwawezesha na kuwajengea uwezo walimu hao wanaosoma kwenye chuo chetu,” alisema Prof Varisanga.
Alisema kuwa fedha hizo pia zitatumika kujenga maabara mabweni na ofisi za walimu ili kuboresha utoaji elimu kwa wanachuo ambao hupata masomo yao kwa elimu ya masafa.
Katika hatua nyingine alisema kuwa wameiomba serikali kuvibadili vyuo hivyo kutoka vituo hadi kuwa vyuo vya mikoa ambapo maombi hayo yamefikishwa kwenye baraza la Mawaziri na yamekubaliwa huku kwa sasa mchakato ukiwa unaendelea.
Kwa upande wake mkurugenzi wa kituo cha mkoa wa Pwani Abdala Alli alisema kuwa elimu ya masafa ambayo inatolewa na chuo hicho imekuwa suluhisho la elimu hapa nchini wakiwemo wanawake.
Alli alisema kuwa elimu ya masafa ndiyo elimu bora kwa sasa kwani inatolewa huku kwa wale watumishi wakiendelea kufanyakazi bila ya kuathiri utendaji kazi tofauti na elimu ya moja kwa moja ambayo humtaka mwanachuo kukaa darasani pamoja na kuwa kwenye bweni ambapo gharama zake ni kubwa.
Akisoma risala ya wahitimu Stella Mapunda alisema kuwa kituo chao kinakabiliwa na uhaba wa walimu pamoja na kumbi za mikutano na mihadhara kwa ajili ywa wanachuo kujadiliana na kujifunzia.
Mapunda alisema kwa sasa wanatumia majengo ya Shirika la Elimu Kibaha ambayo hayatoshelezi mahitaji ya wanachuo ambapo kumekuwa na ongezeko la udahili wa wanachuo wapya kila mwaka.
Jumla ya wahitimu 98 toka kituo cha mkoa wa Pwani walihitimu na kutunukiwa vyeti ngazi mbalimbali kwenye mahafali ya Kitaifa yaliyofanyika kwenye makao makuu ya chuo hicho yaliyopo Bungo wilayani Kibaha wiki iliyopita.
Mwisho.